Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 6/11 kur. 6-9
  • Je, Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Usio na Ugaidi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Usio na Ugaidi?
  • Amkeni!—2011
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kitabu Kinachoweza Kubadili Moyo
  • Undugu Unaochochewa na Upendo
  • Kufuata Mafundisho ya Yesu
  • Faida za Kufuata Mafundisho ya Biblia
  • Kutakuwa na Wakati Ujao Wenye Usalama
  • Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?
    Amkeni!—2011
  • “Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”
    Amkeni!—2011
  • Young People Ask—What Will I Do With My Life? (Sehemu ya 1)
    Huduma Yetu ya Ufalme—2012
  • Nilipata Upendo na Amani ya Kweli
    Amkeni!—2012
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2011
g 6/11 kur. 6-9

Je, Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Usio na Ugaidi?

“TUNAHITAJI kujitahidi sana . . . ili tuiguse mioyo na akili.” Huo ndio mkataa uliofikiwa baada ya miaka 20 ya kuchunguza nyutu za watu waliosemekana kuwa magaidi.

Lakini ni nini kinachoweza kubadili mioyo na akili za watu ambao wamehusika sana katika matendo ya jeuri na kulipiza kisasi?

Kitabu Kinachoweza Kubadili Moyo

Katika miaka ya 1990, Hafeni, alianza kuchunguza mafundisho yake ya kidini na akaamua kutafuta Biblia. Anasema hivi: “Nilianza kwa kuchunguza Injili [vitabu vya Biblia vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana], ambavyo vilikuwa na masimulizi ya maisha ya Yesu. Nilipokuwa nikisoma, nilipendezwa upesi na utu wa Yesu na njia yake ya kushughulika na watu kwa fadhili na bila ubaguzi. Hilo liligusa sana moyo wangu.”

Hafeni anasema kwamba alipoendelea kusoma, “andiko moja la Biblia lilinisaidia kabisa kuelewa jinsi Mungu anavyohisi—Matendo 10:34 na 35.” Linasema hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”

Hafeni anasema hivi: “Nilifikia mkataa kwamba wanadamu ndio wanaosababisha ubaguzi wa kikabila, kitaifa, na kijamii. Nilikuja kutambua kwamba ujumbe wa Biblia unaweza kubadili jinsi watu wanavyofikiri na kwamba jambo muhimu zaidi maishani ni kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Hilo ni muhimu zaidi kuliko kupigana kwa niaba ya watu wa kabila, jamii, au rangi fulani.”

Joseba, aliyenukuliwa katika habari iliyotangulia, alikuwa anasimamia kikundi kidogo cha kikosi maalumu kilichopanga kulipua kituo kimoja cha polisi. “Lakini kabla ya kutekeleza shambulizi hilo,” anaeleza Joseba, “nilikamatwa na nikafungwa gerezani kwa miaka miwili.” Baadaye, mke wake, Luci, akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Mwishowe, Joseba alianza kushiriki katika mazungumzo hayo.

Joseba anasema hivi: “Kadiri nilivyojifunza mengi zaidi kumhusu Yesu, ndivyo alivyokuja kuwa kielelezo changu. Nilipendezwa hasa na maneno haya yake: ‘Wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.’ Nilijua kwamba maneno hayo yalikuwa ya kweli.” (Mathayo 26:52) Joseba alisema hivi: “Kumwua mtu kunawachochea watu wa familia yake wawe na chuki na tamaa ya kulipiza kisasi. Jeuri inasababisha maumivu tu, haitokezi ulimwengu bora.” Joseba alianza kufanya mabadiliko katika kufikiri kwake.

Hafeni na Joseba walijionea kwamba mafundisho ya Biblia yanaweza kubadili maisha ya mtu. Biblia inasema kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu” na kwamba linaweza kutambua “fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Nguvu za Neno la Mungu zimewasaidia watu wengi kubadili njia yao ya kufikiri na matendo yao. Lakini je, kuna uthibitisho kwamba kuna umoja ulimwenguni pote kati ya wale ambao kwa kweli wanafuata mafundisho ya Biblia?

Undugu Unaochochewa na Upendo

Hafeni alipoanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, alichochewa sana kuona jinsi watu wa jamii tofauti-tofauti walivyoshirikiana kwa upatano. “Ilisisimua sana kuketi kando ya wazungu,” anasema. “Sikuwahi kufikiri kwamba katika maisha yangu ningewahi kumwita mzungu ndugu yangu. Hilo lilinisadikisha kabisa kwamba lazima Mashahidi wawe ndio wenye dini ya kweli, kwa kuwa walikuwa na umoja kati yao ambao nilitamani na walikuwa na upendo kati yao licha ya tofauti za kijamii.”

Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa sababu wana ‘upendo kati yao wenyewe.’ (Yohana 13:34, 35) Pia alikataa kujihusisha katika mizozo ya kisiasa na akawaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 6:15; 15:19; Mathayo 22:15-22) Wakati huo Wakristo wa kweli walitambuliwa kwa upendo na msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, kama tu ilivyo leo.

Kufuata Mafundisho ya Yesu

Lakini ni kwa njia gani upendo unaweza kuwavutia watu kukiwa na mambo mengi yanayochochea ugaidi ulimwenguni? Masuala ya kisiasa yanapotokeza chuki, mara nyingi uaminifu kwa jamii, taifa, au kabila hutokeza mzozo kati ya watu wawili au kati ya mataifa.

Kwa mfano, kule nyuma katika mwaka wa 1914, utukuzo wa kikabila ulimfanya Gavrilo Princip amwue Dyuki Mkuu Francis Ferdinand, aliyepaswa kurithi kiti cha ufalme cha Austria-Hungaria. Princip alikuwa mshiriki wa kikundi kilichojiita Mkono Mweusi, ambacho kulingana na katiba yake, kilipendelea kujihusisha katika “mapambano ya kuleta mapinduzi badala ya . . . utendaji wa kitamaduni” ili kufikia malengo yake. Mauaji hayo yalianzisha vita kati ya mataifa yanayodai kuwa ya Kikristo, na hilo likaanzisha Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilivyosababisha vifo vya mamilioni ya watu waliodai kuwa wafuasi wa Yesu, yule “Mkuu wa Amani.”—Isaya 9:6.

Baada ya vita hivyo kwisha, kasisi fulani mashuhuri, Harry Emerson Fosdick, aliwakashifu viongozi wanaodai kuwa wa Kikristo kwa kutowafundisha washiriki wa makanisa yao kuiga mfano wa Yesu. “Tumewazoeza watu kwa ajili ya vita,” akaandika. “Tumewafanya askari kuwa mashujaa wetu na hata ndani ya makanisa yetu tumeziweka bendera za vita.” Fosdick alimalizia kwa kusema: “Kwa pembe moja ya mdomo wetu tumemsifu Mkuu wa Amani na kwa pembe ile nyingine tukatukuza vita.”

Tofauti na hilo, uchunguzi mmoja kuhusu mambo ya kijamii uliochapishwa mnamo 1975 ulisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wamedumisha daima msimamo wao usio na jeuri wa ‘kutokuwamo kwa Kikristo’ wakati wa vile vita viwili vikubwa vya ulimwengu na mizozo ya kijeshi iliyofuata wakati wa kile kipindi cha ‘Vita Baridi.’” Ingawa Mashahidi walitendewa vibaya na kufungwa, “hawakuwahi kulipiza kisasi.” Uchunguzi huo ulifikia mkataa huu: “Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yanatokana na usadikisho wao kwamba Biblia ni neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.”

Faida za Kufuata Mafundisho ya Biblia

Aliyekuwa waziri mkuu wa Ubelgiji alipopewa na jirani yake kitabu chenye kichwa Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi kinachozungumza kuhusu maisha ya Yesu, alipendezwa sana na mambo aliyosoma. Alimwandikia jirani huyo hivi, “Ni wazi kwamba ikiwa watu wangependezwa zaidi na ujumbe wa Injili na wafuate kanuni za Yesu Kristo, ulimwengu leo ungekuwa tofauti kabisa.”

Aliongezea hivi, “Hatungehitaji Baraza la Usalama, wala hakungekuwa na mashambulizi ya kigaidi, [na] jeuri ingepigwa marufuku.” Lakini alifikia mkataa huu: “Yote hayo ni ndoto tu.” Lakini, je, hilo ni kweli? Hata sasa, katika ulimwengu huu uliojaa jeuri, Biblia imewasaidia watu wengi kutoka katika tamaduni zote wakatae jeuri na washinde chuki kali inayotokea wakati watu wanapoishi kwa makumi ya miaka katika maeneo yaliyojaa umwagaji wa damu.

Kama ilivyotajwa katika habari ya kwanza, karibu Andre afe katika bomu lililowaua baadhi ya rafiki zake. Lilikuwa limetegwa hapo na kikundi fulani cha wanamgambo. Baada ya hapo alijifunza na kufuata mashauri ya Biblia kwamba mtu anapaswa ‘kusamehe kwa hiari.’ (Wakolosai 3:13) Baadaye, Hafeni, ambaye baada ya miaka mingi alikuja kuwa mshiriki wa kikundi hichohicho, alijifunza kufuata kanuni za Biblia na akaacha matendo ya jeuri. (Zaburi 11:5) Sasa, wote wawili ni Mashahidi wa Yehova na wanafanya kazi pamoja katika ofisi ya tafsiri ya Mashahidi katika nchi moja ya Afrika.

Kutakuwa na Wakati Ujao Wenye Usalama

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanaona kwamba kujifunza Biblia kunawapa uhakika kwamba kutakuwa na wakati ujao wenye usalama. Kwa mfano, siku moja Andre alikuwa akimwonyesha jirani yake ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya wenye uadilifu utakaokuja. (Isaya 2:4; 11:6-9; 65:17, 21-25; 2 Petro 3:13) Ghafula, askari-jeshi walizingira nyumba hiyo wakiwa na bunduki na kumwamuru Andre atoke akahojiwe. Baada ya kugundua kwamba Andre alikuwa mwalimu wa Biblia ambaye jirani yake alimthamini sana, askari hao waliondoka.

Andre alikuwa tu ameeleza kwamba Mungu ataingilia mambo ya wanadamu, kama alivyokuwa amefanya katika siku za Noa wakati ambapo ‘dunia ilikuwa imejaa jeuri.’ (Mwanzo 6:11) Mungu aliharibu ulimwengu wa wakati huo kupitia gharika ya ulimwenguni pote na akawahifadhi hai Noa pamoja na familia yake kwa sababu walikuwa wapenda-amani. “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa,” Yesu alisema, “ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37-39.

Yesu, yule “Mwana wa binadamu,” ndiye Mtawala aliyechaguliwa na Mungu wa serikali ya kimbingu inayoitwa Ufalme wa Mungu, naye atayaongoza majeshi ya kimbingu ya Mungu hivi karibuni yaondoe jeuri kutoka duniani. (Luka 4:43) Akiwa Mfalme wa kimbingu, Yesu ‘atamtendea kila mtu kwa haki, na kutakuwa na amani.’ Atawalinda raia zake “kutokana na vifo vya ukatili na jeuri.”—Zaburi 72:7, 14, Contemporary English Version.

Baadaye, wale wote wanaopenda mema na wanaokuwa raia wa Mfalme huyo wa kimbingu wataona dunia ikigeuzwa kuwa paradiso yenye amani. (Luka 23:42, 43) Biblia inaahidi hivi: “Milima itawazalia watu amani, na vilima . . . haki.”—Zaburi 72:1-3, Union Version.

Je, hungependa kuishi katika ulimwengu unaotawaliwa na mfalme kama huyo? Bila shaka, ulimwengu huo hautakuwa na ugaidi.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Hafeni na Joseba walijionea kwamba mafundisho ya Biblia yanaweza kubadili maisha ya mtu

[Blabu katika ukurasa wa 9]

‘Ikiwa watu wangefuata kanuni za Yesu Kristo, ulimwengu leo ungekuwa tofauti kabisa. Hatungehitaji Baraza la Usalama, wala hakungekuwa na mashambulizi ya kigaidi, na jeuri ingepigwa marufuku.’—Aliyekuwa waziri mkuu wa Ubelgiji

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kufuata kanuni za Biblia kuliwasaidia Hafeni na Andre kupendana kikweli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki