Jinsi Nilivyopata Suluhisho la Ukosefu wa Haki
Limesimuliwa na Ursula Menne
Tangu nilipokuwa mtoto, nimekuwa na tamaa kubwa ya kuona kila mtu akitendewa kwa haki. Tamaa hiyo ilikuwa kubwa sana hivi kwamba ilifanya nifungwe jela katika Ujerumani Mashariki ya Kikomunisti. Jambo la ajabu ni kwamba nilipata suluhisho la ukosefu wa haki nikiwa jela. Acha nieleze.
NILIZALIWA mnamo 1922 katika mji wa Halle, nchini Ujerumani, mji ambao una historia iliyorekodiwa ya zaidi ya miaka 1,200. Mji wa Halle ulio kilomita 200 kusini-magharibi ya Berlin, ulikuwa ngome ya kwanza kabisa ya dini ya Kiprotestanti. Dada yangu Käthe, alizaliwa katika mwaka wa 1923. Baba alikuwa mwanajeshi. Mama alikuwa mwimbaji kwenye jumba la maonyesho.
Baba ndiye aliyenichochea sana kuwa na tamaa ya kukomesha ukosefu wa haki. Alipoacha kufanya kazi jeshini, Baba alifungua duka. Kwa kuwa wateja wake wengi walikuwa maskini, aliwahurumia na hivyo akawakopesha vitu. Hata hivyo, tendo hilo la upendo lilimfanya afilisike. Nilipaswa kujifunza kutokana na kisa hicho cha baba kwamba tofauti na nilivyofikiri, ni vigumu sana kukabiliana na ukosefu wa usawa na ukosefu wa haki. Hata hivyo, ni vigumu sana kuondoa tamaa ya ujana ya kutaka kubadilisha mambo.
Nilirithi kipawa cha usanii kutoka kwa Mama, naye alitufundisha mimi na dada yangu Käthe kuimba na kucheza dansi. Nilikuwa mtoto mchangamfu na mimi na Käthe tulifurahia sana maisha. Lakini mambo yalibadilika katika mwaka wa 1939.
Mambo Yenye Kutisha Yaanza Kutukia
Baada ya kumaliza masomo yangu ya msingi, nilihudhuria shule ya kujifunza dansi ya ballet, ambako pia nilijifunza Ausdruckstanz (dansi ambayo mtu huonyesha hisia zake), na mwalimu wetu alikuwa Mary Wigman. Alikuwa mmoja wa wale walioanzisha dansi hiyo ambapo mcheza dansi anapaswa kuonyesha hisia zake waziwazi kwa kucheza dansi. Pia nilianza kuchora. Hivyo, mwanzoni, miaka yangu ya ujana ilikuwa imejaa msisimuko na nilijifunza mambo mapya. Lakini, mwaka wa 1939 ulipofika Vita vya Pili vya Ulimwengu vikalipuka. Tulipata pigo lingine katika mwaka wa 1941, Baba alipokufa kutokana na ugonjwa wa kifua kikuu.
Kwa kweli, vita ni jinamizi. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka 17 tu vita vilipoanza, nilifikiri kuwa ulimwengu ulikuwa umeshikwa na kichaa. Niliwaona raia ambao walikuwa na akili timamu wakishikwa na kichaa fulani cha kuunga mkono kwa ushupavu utawala wa Wanazi. Kisha kukawa na umaskini mkubwa, vifo, na uharibifu. Nyumba yetu iliharibiwa sana baada ya kushambuliwa kwa bomu, na watu kadhaa katika familia yetu wakauawa wakati wa vita hivyo.
Vita vilipokwisha katika mwaka wa 1945, mimi, Mama, na Käthe, bado tulikuwa tunaishi Halle. Kufikia wakati huo, tayari nilikuwa na mume na binti mdogo, lakini ndoa yangu ilikuwa na matatizo chungu nzima. Tulitengana, na kwa kuwa nilihitaji kujiruzuku na kumtunza binti yangu, nilianza kufanya kazi ya uchoraji na kucheza dansi.
Baada ya vita, Ujerumani iligawanyika katika sehemu nne, na mji wetu ulikuwa chini ya sehemu iliyotawaliwa na Muungano wa Sovieti. Hivyo, ilibidi sote tuzoee kuwa chini ya utawala wa Kikomunisti. Mnamo 1949, sehemu tuliyokuwa tukiishi nchini Ujerumani, ambayo ilijulikana kama Ujerumani Mashariki, ikaja kuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani (GDR).
Kutawaliwa na Wakomunisti
Katika kipindi hicho, Mama alikuwa mgonjwa, na ilibidi nimtunze. Niliajiriwa kufanya kazi katika ofisi ya serikali. Muda mfupi baadaye, nilikutana na wanafunzi waasi ambao walikuwa wakijaribu kufichua ukosefu wa haki uliokuwa ukitekelezwa. Kwa mfano, kijana mmoja alinyimwa nafasi katika chuo kikuu kwa sababu baba yake alikuwa ameshirikiana na chama cha Nazi. Nilimfahamu kijana huyo kwa sababu mara nyingi tulicheza muziki pamoja. Nilijiuliza hivi, ‘Kwa nini kijana huyu ateseke kwa sababu ya mambo ambayo baba yake alifanya?’ Nilishirikiana zaidi na vijana hao waasi, na nikaamua kushiriki katika maandamano. Pindi moja nilibandika vikaratasi vyenye ujumbe wa uasi nje ya jengo la mahakama.
Nilikasirishwa zaidi na ukosefu wa haki nilioshuhudia katika barua ambazo nilipaswa kuandika nikiwa karani katika ofisi ya Halmashauri ya Mkoa ya Kudumisha Amani. Katika kisa kingine, kwa sababu za kisiasa, Halmashauri hiyo ilipanga kumtumia mwanamume mmoja mzee aliyeishi Ujerumani Magharibi propaganda za Kikomunisti ili watu waanze kumshuku. Nilikasirishwa sana na tendo hilo la ukosefu wa haki dhidi ya mwanamume huyo, hivi kwamba niliamua kuficha barua hizo. Hivyo, barua hizo hazikutumwa.
“Mtu Mbaya Zaidi Katika Chumba” Alinipa Tumaini
Katika mwezi wa Juni 1951, wanaume wawili waliingia ofisini mwangu na kuniambia kwamba walikuwa wamepewa amri ya kunikamata. Walinipeleka katika gereza lililoitwa Roter Ochse, au Fahali Mwekundu. Mwaka mmoja baadaye nilishtakiwa kwa kosa la kujaribu kuipindua serikali. Mwanafunzi mmoja alinisaliti kwa Stasi, ambao walikuwa polisi wa siri, na kuwaeleza jinsi nilivyohusika katika kusambaza vikaratasi vya uasi wakati wa maandamano. Ni kana kwamba kesi hiyo ilikuwa ya mzaha tu kwani yale yote niliyosema ili kujitetea hayakutiliwa maanani. Nilihukumiwa kifungo cha miaka sita gerezani. Nilipokuwa huko, nikawa mgonjwa na nikalazwa katika chumba cha wagonjwa cha gereza hilo pamoja na wanawake wengine 40 hivi. Nilishikwa na wasiwasi mkubwa baada ya kuona watu hao wote ambao hawakuwa na furaha. Nilikimbia na kuanza kupiga ngumi mlango wa chumba hicho.
“Unataka nini?” askari aliniuliza.
“Lazima nitoke hapa,” nilimjibu kwa hasira. “Hata ikiwa itabidi mnitie katika kifungo cha upweke, ni sawa tu lakini mniondoe hapa!” Hata hivyo, alinipuuza. Muda mfupi baadaye, nilimwona mwanamke mmoja ambaye alikuwa tofauti na wale wengine. Macho yake yalionyesha kwamba alikuwa na utulivu fulani moyoni. Hivyo, niliketi kando yake.
“Ikiwa unataka kuketi kando yangu, lazima uwe mwangalifu sana,” alinieleza, nami nikashangaa sana. Kisha akaongeza, “Wengine wanafikiri kwamba mimi ndiye mtu mbaya zaidi katika chumba hiki kwa sababu mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”
Wakati huo, sikujua kwamba Mashahidi wa Yehova walionwa kuwa maadui wa Serikali ya Kikomunisti. Lakini kile nilichojua kuwahusu ni kwamba Wanafunzi wawili wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) walimtembelea Baba kwa ukawaida nilipokuwa mtoto. Hata nilimkumbuka Baba akisema, “Wanafunzi wa Biblia wanasema kweli!”
Nilitokwa na machozi ya furaha baada ya kukutana na mwanamke huyo mpendwa, aliyeitwa Berta Brüggemeier. “Tafadhali, nieleze kuhusu Yehova,” nilimwambia. Kuanzia wakati huo na kuendelea, tulitumia wakati mwingi pamoja na mara nyingi tulizungumza kuhusu Biblia. Nilijifunza mambo kadhaa kama vile, Mungu wa kweli, Yehova, ni Mungu mwenye upendo, haki, na amani. Pia nilijifunza kwamba ataondoa madhara yote ambayo yamesababishwa na utawala mkatili wa wanadamu waovu. “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani,” inasema Zaburi 37:10, 11.
Kuwekwa Huru na Kutorokea Magharibi
Niliwekwa huru katika mwaka wa 1956, baada ya kuwa gerezani kwa zaidi ya miaka mitano. Siku tano baada ya kuachiliwa, nilitoroka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani na kuhamia Ujerumani Magharibi. Kufikia wakati huo nilikuwa na binti wawili, Hannelore na Sabine, ambao nilihama nao. Nikiwa huko, tulitalikiana na mume wangu na nikakutana na Mashahidi tena. Kadiri nilivyojifunza Biblia, ndivyo nilivyotambua kwamba nilipaswa kufanya mabadiliko kadhaa ili niweze kuishi kupatana na viwango vya Yehova. Nilifanya mabadiliko hayo na nikabatizwa katika mwaka wa 1958.
Baadaye, nilifunga ndoa tena, na mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyeitwa Klaus Menne. Mimi na Klaus tulikuwa na ndoa yenye furaha sana na pia tulipata watoto wawili, Benjamin na Tabia. Hata hivyo, kwa kusikitisha, Klaus alikufa kwenye aksidenti miaka 20 hivi iliyopita, na hivyo nimekuwa mjane tangu wakati huo. Lakini tumaini la ufufuo hunipa faraja kubwa kwa sababu ninajua kwamba wafu watafufuliwa katika Paradiso duniani. (Luka 23:43; Matendo 24:15) Pia ninafarijiwa sana kujua kwamba watoto wangu wote wanne wanamtumikia Yehova.
Ninafurahi sana kwamba nilijifunza Biblia, kwa sababu sasa ninajua kwamba ni Yehova tu anayeweza kuwaletea wanadamu haki ya kweli. Tofauti na wanadamu, yeye anajua mambo yote yanayohusika, kutia ndani malezi yetu—mambo ambayo watu wengine hawayajui. Kujua hilo kumenisaidia sana kwani sasa nina amani, hasa ninapoona ukosefu wa haki ukiendelea au ninapotendewa isivyo haki. Andiko la Mhubiri 5:8 linasema hivi: “Ikiwa katika jimbo fulani unaona maskini akikandamizwa na akinyimwa haki, usishangazwe na kinachotendeka, kwa kuwa kila ofisa ana mkuu juu yake, na aliye juu zaidi huwaangalia wote hao.” (The Revised English Bible) “Aliye juu zaidi,” ni Muumba wetu. “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake,” inasema Waebrania 4:13.
Kutafakari Kuhusu Miaka 90 Hivi Iliyopita
Wakati mwingine watu huniuliza jinsi hali ilivyokuwa chini ya utawala wa Wanazi na Wakomunisti. Maisha hayakuwa rahisi chini ya serikali zote hizo. Na aina zote mbili za serikali, kama vile tu serikali nyingine ambazo wanadamu wamebuni, zimeonyesha kwamba wanadamu hawawezi kujitawala wenyewe. Biblia inasema hivi kwa njia ya wazi na ya kweli: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.
Nilipokuwa mchanga na bila uzoefu wowote, nilitazamia kwamba utawala wa wanadamu utaleta haki. Sasa ninaelewa mambo vizuri. Ni Muumba wetu tu anayeweza kutawala ulimwengu kwa haki, na atafanya hivyo kwa kuangamiza utawala wote mwovu uliopo, na kumkabidhi Mwana wake, Yesu Kristo, utawala wa dunia yote kwani sikuzote Yesu hutanguliza faida za wengine badala ya zake mwenyewe. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria.” (Waebrania 1:9) Ninashukuru sana kwamba Mungu alinivuta kwa Mfalme huyu mzuri ajabu na mwenye haki, ambaye ninatumaini kuishi milele chini ya utawala wake!
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nikiwa na binti zangu Hannelore na Sabine baada ya kufika Ujerumani Magharibi
[Picha katika ukurasa wa 23]
Leo, nikiwa na mwana wangu, Benjamin, na mke wake, Sandra