Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 12/13 kur. 12-13
  • Jinsi ya Kumsikiliza Mwenzi Wako kwa Makini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kumsikiliza Mwenzi Wako kwa Makini
  • Amkeni!—2013
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIKWAZO
  • Mtendee Mwenzi Wako wa Ndoa kwa Heshima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Mume na Mke Wasipoelewana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Jinsi ya Kutatua Matatizo
    Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha
  • Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2013
g 12/13 kur. 12-13

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kumsikiliza Mwenzi Wako kwa Makini

KIKWAZO

“Hunisikilizi!” mwenzi wako anasema. ‘Lakini nilikuwa nikimsikiliza,’ unajiambia. Hata hivyo, ni wazi kwamba kile ulichosikia ni tofauti na kile ambacho mwenzi wako alisema. Kwa sababu hiyo, mnaanza kubishana tena.

Unaweza kuepuka hali hiyo ya kutoelewana. Hata hivyo, kwanza unahitaji kujua ni nini kinachokufanya usisikie habari muhimu ambazo mwenzi wako anasema—hata ingawa unadhani kuwa unasikiliza.

KWA NINI JAMBO HILI HUTUKIA

Umekengeushwa fikira au umechoka. Watoto wanapiga kelele, televisheni imefunguliwa kwa sauti ya juu, na unafikiria tatizo ulilokuwa nalo kazini. Sasa mwenzi wako anaanza kuongea nawe, akikueleza kwamba jioni mtakuwa na wageni. Unaitikia “sawa,” lakini kweli ulisikia kile ambacho mwenzi wako alisema? Yaelekea hukusikia.

Unakisia mambo. Unahisi kwamba kuna ujumbe fulani uliofichwa katika maneno ya mwenzi wako, na huenda isiwe hivyo. Kwa mfano, wazia mwenzi wako anasema hivi: “Umetumia wakati mwingi sana kufanya kazi ya ziada juma hili.” Nawe ukihisi unachambuliwa, unasema: “Hilo si kosa langu! Ninalazimika kufanya kazi saa za ziada kwa sababu unatumia pesa nyingi sana.” Mwenzi wako anajibu kwa hasira, “Sikuwa ninakulaumu!” Kumbe alitaka tu muwe pamoja mwisho-juma.

Unakimbilia kutafuta suluhisho. “Nyakati nyingine ninataka tu kueleza jinsi ninavyohisi” asema Marcie,a “lakini Mike hutaka kuniambia jinsi ya kutatua tatizo langu. Nia yangu si kulitatua. Nataka tu ajue jinsi ninavyohisi.” Tatizo ni nini? Akili ya Mike inakazia fikira kutafuta suluhisho. Tokeo ni kwamba, huenda asisikie baadhi au maneno yote ambayo Marcie anasema.

Hata tatizo liwe nini, unawezaje kumsikiliza mwenzi wako kwa makini?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mkazie mwenzi wako fikira. Mwenzi wako ana jambo muhimu la kusema, je, uko tayari kusikiliza? Huenda sivyo. Huenda kwa wakati huu akili yako inafikiria mambo mengine. Ikiwa ndivyo, usijifanye unasikiliza. Ikiwezekana, acha jambo unalofanya na umkazie fikira mwenzi wako, au unaweza kumwomba mwenzi wako asubiri mpaka wakati utakapoweza kumsikiliza kwa makini.—Kanuni ya Biblia: Yakobo 1:19.

Mwenzi wako anapoongea, nyamaza na umsikilize. Ikiwa ni zamu yako kusikiliza, epuka kukimbilia kumkatiza au kumpinga. Utakuwa na zamu ya kuongea. Kwa wakati huu, wewe sikiliza tu.—Kanuni ya Biblia: Methali 18:13.

Uliza maswali. Hilo litakufanya uelewe vizuri anayosema mwenzi wako. Marcie, aliyenukuliwa mwanzoni anasema hivi: “Napenda Mike anapouliza maswali. Hilo hunionyesha kuwa anapendezwa na jambo ninalosema.”

Sikiliza ujumbe, si maneno tu. Angalia hisia zinazoonyeshwa na ishara za mwili, macho, na sauti. Neno “sawa” huenda likamaanisha “si sawa”—ikitegemea jinsi linavyosemwa. Maneno “Hakuna wakati ambapo wewe unanisaidia” huenda yakamaanisha “Nahisi mimi si muhimu kwako.” Jaribu kupata maana ya ujumbe, hata kama ujumbe wenyewe hausemwi. Usipofanya hivyo, huenda ukaanza kukisia maneno yaliyosemwa yalikuwa na maana gani.

Endelea kusikiliza. Usiache kusikiliza au usiondoke hata kama hupendezwi na mambo unayosikia. Kwa mfano, vipi ikiwa mwenzi wako anakuchambua? “Endelea kusikiliza,” anashauri Gregory, ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka 60. “Fikiria kwa uzito maneno ambayo mwenzi wako anasema. Hilo linahitaji ukomavu, lakini utafaidika sana.”—Kanuni ya Biblia: Methali 18:15.

Pendezwa kikweli na mwenzi wako. Kusikiliza kwa makini si mbinu tu, bali ni tendo la upendo. Ikiwa unapendezwa kikweli na yale ambayo mwenzi wako anasema, itakuwa rahisi kwako kusikiliza na utafanya hivyo bila kulazimishwa. Kwa njia hiyo utakuwa ukifuata himizo hili la Biblia: “Pasiwe na mtu anayetafuta faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake.”—Wafilipi 2:4, Biblia Habari Njema.

a Majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAANDIKO MUHIMU

  • ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’—Yakobo 1:19.

  • “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.”—Methali 18:13.

  • “Sikio la wenye hekima hutafuta kupata ujuzi.”—Methali 18:15.

UNAPOONGEA

Ukijaribu kuzungumza na mwenzi wako huku akiwa katika chumba kingine au anakazia fikira jambo lingine, je, atasikia unayosema? Ingekuwa bora kwanza kuhakikisha kwamba mwenzi wako anakusikiliza au usubiri mpaka wakati unaofaa.—1 Petro 3:8.

Fikiria mfano huu wa Biblia: Yesu alipotaka kusema jambo fulani muhimu kuhusu unyenyekevu, hakuropoka. Alisubiri hadi mitume wake walipokuwa katika hali zinazofaa kusikiliza. Kisha akawaita na kuwaambia jambo hilo.—Marko 9:33-35; 12:41-44.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki