Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g17 Na. 1 kur. 3-7
  • Ni Nini Kinachoweza Kuwasaidia Vijana Walioshuka Moyo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Kinachoweza Kuwasaidia Vijana Walioshuka Moyo?
  • Amkeni!—2017
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAMBO YANAYOWEZA KUSABABISHA KIJANA ASHUKE MOYO
  • TUNZA AKILI NA MWILI WAKO
  • Kutambua Vyanzo
    Amkeni!—2001
  • Jinsi ya Kutibu Ugonjwa wa Kushuka Moyo
    Amkeni!—2009
  • Namna Uwezavyo Kusaidia
    Amkeni!—2001
  • Kutambua Dalili
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2017
g17 Na. 1 kur. 3-7
Kijana ameketi kitandani akiwa ameshuka moyo

HABARI KUU

Ni Nini Kinachoweza Kuwasaidia Vijana Walioshuka Moyo?

BINTI anayeitwa Anna,a anasema hivi: “Ninaposhuka moyo ninakosa hamu ya kufanya chochote, hata mambo ambayo kwa kawaida huwa napenda kufanya. Kitu pekee ninachotaka ni kulala. Mara nyingi ninahisi kwamba watu hawanipendi, sina thamani, na mimi ni mzigo kwa wengine.”

Julia anakumbuka hivi: “Nilifikiria kujiua. Kusema kweli sikutaka kufa. Nilitaka tu kuepuka hisia mbaya nilizokuwa nazo. Kwa kawaida mimi ni mwenye kujali sana, lakini ninaposhuka moyo, sijali yeyote wala kitu chochote.”

Anna na Julia walikuwa na umri wa miaka 13 na 14 hivi waliposhuka moyo kwa mara ya kwanza. Ni kawaida kwa vijana kuhisi vibaya nyakati fulani, lakini tofauti na hilo, Anna na Julia walishuka moyo kwa majuma au hata miezi kadhaa. Anna anasema kwamba, kushuka moyo “ni kama kufungiwa kwenye shimo kubwa lenye giza na lisilokuwa na mlango wa kutokea.” Anaongeza hivi: “Unahisi kama unarukwa na akili, na kwamba umebadilika kabisa tofauti na ulivyokuwa zamani.”

Watu wengi wamepatwa na hali kama ya Anna na Julia. Idadi ya vijana wanaoshuka moyo inaongezeka kwa kasi sana. Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) linasema kwamba, kushuka moyo ni “chanzo kikuu cha magonjwa na ulemavu kwa wavulana na wasichana wenye umri kati ya miaka 10 na 19.”

Dalili za kushuka moyo zinaweza kuonekana wakati wa kubalehe na zinahusisha mabadiliko katika mazoea ya kulala, hamu ya kula, na kuongezeka au kupungua uzito. Pia, mtu anaweza kuanza kuhisi hana tumaini lolote, huzuni, na kwamba hafai kitu. Ishara zingine ni kama kujitenga na wengine, kushindwa kukazia fikira au kupoteza kumbukumbu, kutaka kujiua, na kuonyesha dalili ambazo hazihusiani na ugonjwa wowote. Wataalamu wa afya wanapohisi kwamba mtu ameshuka moyo, wao huchunguza ikiwa mtu huyo ameonyesha dalili zaidi ya moja zinazodumu kwa majuma kadhaa na ambazo zinaathiri maisha yake ya kila siku.

MAMBO YANAYOWEZA KUSABABISHA KIJANA ASHUKE MOYO

Kulingana na WHO, “kushuka moyo husababishwa na muunganiko tata wa hali za kijamii, kisaikolojia, na kibiolojia.” Hali hizo zinatia ndani mambo yafuatayo.

Matatizo ya kibiolojia na matumizi ya dawa. Kama ilivyokuwa katika kisa cha Julia, mara nyingi tatizo la kushuka moyo huwapata watu kadhaa katika familia moja, jambo linalodokeza kwamba chembe za urithi zinahusika, labda kwa kuathiri utendaji wa kemikali kwenye ubongo. Visababishi vingine ni; ugonjwa wa moyo, mabadiliko ya viwango vya homoni, na matumizi ya dawa za kulevya. Dawa za kulevya zikitumiwa kwa muda mrefu zinaweza kuongeza uwezekano wa mtu kushuka moyo.b

Mkazo. Ingawa mkazo kidogo unaweza kuwa na manufaa, kuwa na mkazo kwa muda mrefu kunaweza kumdhuru mtu kimwili na kisaikolojia, na nyakati nyingine hata kusababisha kijana mwenye matatizo ya kibiolojia ashuke moyo. Pamoja na yote hayo, bado sababu hususa zinazofanya watu washuke moyo hazifahamiki vizuri na zinaweza kuhusisha mambo mbalimbali kama ilivyotajwa awali.

Huenda mkazo unaoweza kusababisha kijana ashuke moyo ukatokana na wazazi kutalikiana au kutengana, kifo cha mpendwa, kutendewa vibaya kimwili au kingono, aksidenti mbaya, ugonjwa, au mtoto kuwa mzito kujifunza, hasa ikiwa anahisi kwamba anabaguliwa. Pia, mkazo unaweza kusababishwa na matarajio ya juu sana kutoka kwa wazazi, labda inapohusu masuala ya elimu. Uonevu shuleni, wasiwasi kuhusu wakati ujao, uhusiano mbaya na mzazi aliyeshuka moyo, na watoto kushindwa kuelewa hisia na matendo ya wazazi wao ni baadhi ya mambo yanayoweza kuwasababishia mkazo pia. Kijana anaweza kufanya nini ili akabiliane na kushuka moyo?

TUNZA AKILI NA MWILI WAKO

Kwa kawaida, mtu aliyeshuka moyo kupita kiasi anahitaji matibabu na ushauri kutoka kwa wataalamu wa afya ya akili.c Yesu Kristo alisema hivi: “Wale walio na nguvu hawahitaji tabibu, bali wale walio wagonjwa wanamhitaji.” (Marko 2:17) Ugonjwa unaweza kuathiri sehemu yoyote ile ya mwili wetu kutia ndani ubongo! Ni vizuri pia kubadili mtindo wa maisha kwa sababu kuna uhusiano mkubwa kati ya ubongo na mwili wetu.

Ikiwa umeshuka moyo, chukua hatua madhubuti zitakazokusaidia kutunza afya ya mwili na akili yako. Kwa mfano, kula vyakula vyenye lishe, lala vya kutosha, na uwe na kawaida ya kufanya mazoezi. Mazoezi huchochea uzalishaji wa kemikali zinazoweza kukufanya ujihisi vizuri, kukuchangamsha, na kuboresha usingizi wako. Ikiwezekana, jaribu kutambua dalili za mapema za kushuka moyo kisha upange jinsi utakavyoshughulikia hali hiyo. Zungumza na mtu unayemwamini. Kuwa na marafiki na washiriki wa karibu wa familia wanaokuunga mkono kutakusaidia unaposhuka moyo au hata kupunguza madhara ya tatizo hilo. Andika mawazo na hisia zako kwenye daftari. Zoea hilo lilimsaidia sana Julia, aliyetajwa awali. Zaidi ya yote, hakikisha unatosheleza uhitaji wako wa kiroho. Hilo linaweza kuboresha mtazamo wako wa maisha kwa kiwango kikubwa sana. Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Binti akiwa anakula pamoja na wazazi wake, akifanya mazoezi, na akiwa amelala

Kula vizuri, fanya mazoezi, na ulale vya kutosha

Binti akisoma Biblia

Utafarijika ikiwa utatosheleza uhitaji wako wa kiroho

Anna na Julia wamefaidika kwa kufuata ushauri wa Yesu. Anna anasema: “Utendaji wa kiroho huniwezesha kukazia fikira watu wengine badala ya matatizo yangu. Hilo si rahisi siku zote, lakini kufanya hivyo huongeza furaha yangu.” Julia anapata faraja kwa kusali na kusoma Biblia. Anasema hivi: “Kummiminia Mungu moyo wangu hufanya nitulie. Na Biblia hunisaidia kuona kwamba nina thamani machoni pa Mungu, naye ananijali kikweli. Pia, kusoma Biblia hunifanya niwe na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao.”

Akiwa Muumba wetu, Yehova Mungu anaelewa kikamili jinsi malezi yetu, mambo tuliyopitia maishani, na chembe zetu za urithi zinavyoathiri mtazamo na hisia zetu. Hivyo, anaweza kutoa faraja na msaada unaohitajika, labda kwa kumtumia mwanadamu mwenzetu mwenye huruma na anayeweza kuelewa vizuri hali zetu. Isitoshe, wakati ujao, Mungu ataponya magonjwa yote, ya kimwili na ya akili. Andiko la Isaya 33:24 linasema: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”

Naam, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Ahadi hii inafariji na kutia moyo sana! Ikiwa ungependa kujifunza zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia na wanadamu, tafadhali tembelea tovuti yetu ya jw.org/sw. Katika tovuti hiyo unaweza kusoma tafsiri nzuri ya Biblia na pia kupata makala zenye habari mbalimbali kutia ndani zinazohusu kushuka moyo.

a Majina yamebadilishwa.

b Ni muhimu kuchunguzwa kwa makini na wataalamu, kwa kuwa kuna vitu vingi vinavyoweza kuathiri hisia za mtu, kama vile magonjwa, matibabu, na dawa za kulevya.

c Gazeti la Amkeni! halipendekezi mazoezi au matibabu fulani hususa.

Mambo Ambayo Wazazi Wanaweza Kufanya

  • Tambua kwamba huenda ikawa vigumu kwa vijana walioshuka moyo kueleza hisia zao au hata kuielewa hali yao. Labda hata hawajui dalili za kushuka moyo.

  • Mara nyingi dalili za kushuka moyo kwa vijana hutofautiana na zile za watu wazima, kwa hiyo chunguza mabadiliko yoyote katika tabia za mtoto wako, mazoea yake ya kula na kulala, hisia, au jinsi anavyoshughulika na wengine, hasa ikiwa hali hiyo inaendelea kwa majuma kadhaa.

  • Usipuuze ishara zozote za kutaka kujiua.

  • Ukihisi kijana wako ameshuka moyo (na si mabadiliko ya kawaida ya kihisia tu), mpeleke akachunguzwe na wataalamu wa afya.

  • Msaidie kijana wako atumie matibabu, na ukigundua kwamba hakuna maendeleo yoyote au matibabu hayo yanamletea madhara, wasiliana na daktari mara moja.

  • Andaa ratiba ya kudumu ya kula, kufanya mazoezi, na kulala kwa ajili ya familia yako.

  • Wasiliana na kijana wako mara kwa mara na umsaidie kukabiliana na maoni mabaya yaliyoenea kuhusu ugonjwa wa kushuka moyo.

  • Kwa kuwa kushuka moyo kunaweza kumfanya kijana ahisi upweke, hana thamani, na kuaibikia hali yake, mhakikishie kwamba unampenda.

Tengeneza “Sanduku la Huduma ya Kwanza” Kwa Ajili ya Hisia Zako

Sanduku la huduma ya kwanza kwa ajili ya hisia, linalotia ndani mambo yenye kujenga na kutia moyo kama vile, maandiko, nyimbo, makala, na matukio muhimu maishani

Ikiwa umeshuka moyo, pendekezo moja linaloweza kukusaidia kudhibiti mawazo na hisia zako ni kujitengenezea sanduku la huduma ya kwanza. Sanduku hilo, ambalo unaweza kuliboresha kadiri unavyoona kuwa inafaa, linaweza kuhusisha mambo mbalimbali kama vile:

  • Namba za simu au anwani za watu unaoweza kuzungumza nao unaposhuka moyo

  • Nyimbo zenye kujenga unazopenda zaidi

  • Misemo yenye kuchochea na makala zinazotia moyo

  • Orodha ya Maandiko yenye kufariji na kujenga kama vile Zaburi 34:18; 51:17; 94:19; Wafilipi 4:6, 7

  • Vitu vinavyokukumbusha kuhusu watu wanaokupenda

  • Daftari ambalo umeandika mawazo na mambo mazuri uliyowahi kufurahia

Ugonjwa wa Kushuka Moyo kwa Wasichana

Inaonekana kwamba idadi ya wasichana wanaoshuka moyo ni kubwa kuliko ile ya wavulana. Huenda sababu moja ni kwamba wasichana wanakabiliana na mkazo unaotokana na kusumbuliwa au kutendewa vibaya kingono, kihisia, au kimwili. Sharon Hersh, mshauri wa afya, aliandika hivi: “Mtu mwenye hisia zilizovurugika anapokumbana na matukio mabaya, mara nyingi analemewa na kuchanganyikiwa.” Pia, wasichana wanaweza kuathiriwa na maoni ya vyombo vya habari kuhusu umbo “linalofaa.” Msichana anayehisi kwamba havutii au anayekazia fikira kupita kiasi jinsi marika wake wanavyomwona ana uwezekano mkubwa wa kushuka moyo.d

d Soma makala “Maoni Ya Biblia—Urembo,” kwenye gazeti la Amkeni! Na. 4 2016.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki