Mambo Ambayo Baadhi Ya Watu Huamini
Wahindu
wanaamini kwamba nafsi huzaliwa upya katika mwili mwingine mara kadhaa. Pia, wanaamini kuteseka ni matokeo ya matendo ambayo mtu anafanya sasa au aliyofanya zamani. Mtu anaweza kufikia moksha, yaani, hali ya kukombolewa kutoka katika mzunguko wa kuzaliwa upya, ikiwa atashikamana na mambo ya kidini.
Waislamu
wanaamini kuteseka ni adhabu ya dhambi na pia ni jaribu la imani. Dakt. Sayyid Syeed, kiongozi wa shirika la Islamic Society of North America alisema kwamba majanga hutukumbusha umuhimu wa “kuendelea kumshukuru Mungu kwa baraka zote ambazo ametupatia na pia yanatukumbusha kuwasaidia wenye uhitaji.”
Imani ya Kiyahudi
ni kwamba kuteseka ni matokeo ya matendo ya mtu mwenyewe. Baadhi ya Wayahudi wanasema kutakuwa na ufufuo, na wakati huo watu wasio na hatia ambao waliteseka watapata thawabu. Kabbalah (mafumbo ya dini ya Kiyahudi) inafundisha kwamba nafsi inapozaliwa upya katika mwili mwingine inapewa nafasi ya kutubu makosa.
Wabudha
wanaamini kwamba nafsi huzaliwa upya mara kadhaa. Wanasema kwamba mtu ataendelea kuteseka hadi atakapoacha matendo mabaya, hisia mbaya na mielekeo isiyofaa. Mtu anaweza kufikia Nirvana, yaani, hali ambayo mtu huacha kuteseka, ikiwa atafanya mambo mazuri, atakuwa na hekima, na kudumisha mawazo safi.
Wakonfyushasi
wanaamini kwamba kuteseka hutokana na “makosa ya wanadamu.” Wakonfyushasi wanafundisha kwamba wanadamu wanaweza kuteseka kwa kiwango kidogo wakiishi maisha mazuri, hata hivyo, mara nyingi kuteseka kunasababishwa na “viumbe wa roho walio na uwezo mkubwa kuliko wanadamu. Kwa sababu hiyo, wanadamu hawana uwezo wa kupinga kile ambacho viumbe hao wa roho wameamua.”—A Dictionary of Comparative Religion
Baadhi ya dini za kimila
zinafundisha kwamba kuteseka kunasababishwa na uchawi. Kulingana na imani hizi, wachawi wanaweza kuleta bahati nzuri au majanga. Matatizo wanayosababisha yanaweza kupungua kwa kufuata desturi fulani. Mtu anapokuwa mgonjwa anaweza kupata nafuu kwa kufuata mambo ya kimila na dawa anazopewa na waganga wa kienyeji.
Wakristo
wanaamini kwamba kuteseka kunasababishwa na dhambi ambayo wanadamu wa kwanza walifanya kama inavyoelezwa kwenye Biblia katika kitabu cha Mwanzo. Hata hivyo, dini nyingi zimepotosha fundisho hilo. Kwa mfano, baadhi ya Wakatoliki wanasema kwamba Mungu anaweza kutumia matatizo ambayo mtu anakabili ili kunufaisha kanisa au kumkomboa mtu mwingine.
JIFUNZE MENGI ZAIDI
Tazama video Je, Mungu Anakubali Aina Zote za Ibada? kwenye jw.org/sw.