3. Kwa Nini Watu Wanaotenda Mema Wanateseka?
Kwa Nini ni Muhimu Kupata Jibu la Swali Hilo?
Ni jambo lisilo la haki kwa mtu anayetenda mema kuteseka. Baadhi ya watu wanafikiri kwamba hakuna sababu ya kutenda mema kwa kuwa hata watu wema wanateseka.
Jambo la Kufikiria
Baadhi ya watu wanaamini wanadamu wanakufa na kuzaliwa upya mara kadhaa. Wanasema kwamba watu waliofanya mambo mema wanazaliwa upya na kuishi maisha mazuri, lakini wale waliotenda mambo mabaya wanazaliwa upya na kuishi maisha magumu. Kulingana na imani hiyo, hata mtu mwema anaweza kuteseka ikiwa alifanya mambo mabaya “zamani.” Hata hivyo . . .
Kuteseka kutakuwa na kusudi gani ikiwa mtu anayedaiwa kuzaliwa upya hata hakumbuki maisha yake ya zamani?
Ikiwa tunakuwa wagonjwa au kupatwa na aksidenti kwa sababu ya matendo mabaya tuliyofanya zamani, kwa nini tujitahidi kutunza afya zetu na kuepuka aksidenti?
JIFUNZE MENGI ZAIDI
Tazama video Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka? kwenye jw.org/sw.
Mambo Ambayo Biblia Inafundisha
Kuteseka si adhabu kutoka kwa Mungu.
Badala yake, matukio mengi mabaya yanatokea bila kutarajiwa na mara nyingi mtu anaweza kupatwa na mambo mabaya akiwa mahali pasipofaa na wakati usiofaa.
“Sikuzote si wenye mbio wanaoshinda mbio, wala wenye nguvu hawashindi vita, wala wenye hekima hawapati chakula sikuzote, wala werevu hawawi na utajiri sikuzote, wala wenye ujuzi hawafanikiwi sikuzote, kwa sababu wakati na matukio yasiyotarajiwa huwapata wote.”—MHUBIRI 9:11.
Dhambi tuliyorithi husababisha kuteseka.
Mara nyingi watu hutumia neno “dhambi” kurejelea matendo mabaya ambayo mtu anafanya. Hata hivyo, Biblia inatumia neno hilo pia kurejelea hali ambayo wanadamu wote wamerithi, iwe wanatenda mema au mabaya.
“Nilizaliwa nikiwa na hatia ya kosa, na nilikuwa na dhambi tangu mama yangu aliponichukua mimba.”—ZABURI 51:5, Maelezo ya chini.
Dhambi imekuwa na matokeo mabaya kwa wanadamu.
Imeharibu uhusiano wetu na Muumba na pia imesababisha tusiwe na ushirikiano mzuri na viumbe wengine. Jambo hilo limesababisha matatizo makubwa kwa mtu mmoja-mmoja na kwa wanadamu wote.
“Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—WAROMA 7:21.
“Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.”—WAROMA 8:22.