Sura ya 34
Ibada ni Ya Mungu
MIMI nitakuuliza ulizo la maana. Ni la maana sana hata njia ambayo unajibu inageuza maisha yako ya wakati ujao. Mungu wako ni nani?—
Mungu wako ni yeye ambaye unaabudu. Katika dunia yote watu wanaabudu namna nyingi za miungu. Mingine ya miungu hiyo inachorwa tu au inafanyizwa kwa mti au jiwe. Mingine ni watu ambao wanajulikana sana katika michezo au muziki. Wanasemekana kama “mabingwa” na “watukufu.” Lakini je! ni vizuri kuipa miungu hii mingine utukufu?—
Mwalimu Mkuu alisema: “Msujudie [Yehova] Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”—Mathayo 4:10.
Basi Yesu alionyesha wazi. Ibada yetu ni ya Yehova Mungu peke yake. Hatuwezi kumpa mungu mwingine ye yote hata sehemu ndogo ya ibada yetu. Kuna hadithi ya kufurahisha katika Biblia juu ya vijana wanaume wengine waliojua hili.
Majina yao walikuwa Shadraka, Meshaki na Abednego. Walikuwa Waebrania, lakini waliishi katika nchi ya Babeli. Mfalme wa Babeli alijenga sanamu kubwa mno ya dhahabu. Aliamuru kwamba wakati muziki unapopigwa, kila mtu imempasa asujudie sanamu yake. ‘Mtu ye yote asiyeanguka na kuabudu atatupwa saa iyo hiyo katika tanuru inayowaka moto,’ alionya. Wewe ungalifanya nini?—
Shadraka, Meshaki na Abednego walifanya kwa kawaida kila jambo ambalo mfalme aliamuru. Lakini walikataa kufanya hivi. Unajua kwa sababu gani?— Ni kwa sababu sheria ya Mungu ilisema: ‘Haikupasi uwe na miungu mingine yo yote zaidi ya mimi. Haikupasi ujifanyie sanamu ya kuchonga na kuisujudia.’ Basi Shadraka, Meshaki na Abednego walitii amri ya Yehova kuliko amri ya mfalme.—Kutoka 20:3, 4.
Mfalme alikasirika wakati aliposikia juu ya hili. Mara hiyo aliamuru Shadraka, Meshaki na Abednego waletwe mbele yake. Alisema hivi: ‘Je! ni kweli ninyi hamwitumikii miungu yangu? Nitawapa nafasi nyingine. Sasa, wakati mtakaposikia muziki, mwanguke na kuabudu sanamu ambayo nimefanya. Ikiwa sivyo, mtatupwa katika tanuru inayowaka moto. Naye ni mungu gani anayeweza kuokoa ninyi katika mikono yangu?’
Sasa Shadraka, Meshaki na Abednego wangefanya nini? Wewe ungalifanya nini?— Walimtumaini Yehova. Walisema kwa nguvu na wakamwambia mfalme: ‘Mungu wetu ambaye tunatumikia anaweza kutuokoa sisi. Lakini hata ikiwa yeye hatuokoi, sisi hatutaitumikia miungu yako. Sisi hatutasujudia sanamu yako ya dhahabu.’
Mfalme alikasirika sana. Akaamuru: ‘Ipasheni tanuru moto mara saba zaidi kuliko kawaida!’ Aliamuru wanaume wake hodari wafunge Shadraka, Meshaki na Abednego. Ndipo akasema: Watupieni katika tanuru!’
Watumishi wa mfalme waliwatupia ndani. Lakini tanuru ilikuwa na moto mwingi sana hata wanaume wa mfalme mwenyewe waliuawa kwa miali ya moto! Namna gani Waebrania watatu?
Shadraka, Meshaki na Abednego waliangukia katikati ya moto. Lakini ndipo waliposimama! Hawakuumia. Na hawakuwa wamefungwa tena. Jambo hili lingewezekana namna gani?
Mfalme alichungulia katika tanuru, na aliyoona yalimwogopesha. ‘Je! hatukutupia wanaume watatu katika moto?’ akauliza.
Watumishi wake walimjibu: ‘Ndiyo, Ee mfalme.’ Lakini mfalme alisema: ‘Tazama! mimi naona wanaume wanne wakitembea ndani, na moto haumwumizi ye yote kati yao.’
Je! unajua mtu yule wa nne alikuwa nani?— Alikuwa malaika wa Yehova. Naye alikuwako alinde watumishi hao watatu waaminifu wa Kiebrania wa Mungu wa kweli.
Alipoona haya, mfalme alikwenda kwenye mlango wa tanuru na alisema kwa sauti kuu: “Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku!” Walipotoka nje, kila mtu aliweza kuona kwamba hawakuchomwa na moto. Kulikuwa hakuna hata harufu ya moto juu yao.
Ndipo mfalme alisema: ‘Abarikiwe Mungu wa Shadraka, Meshaki na Abednego aliyewaokoa watumishi wake, kwa sababu wasingemwabudu mungu ye yote ila Mungu wao wenyewe.’—Danieli sura ya tatu.
Je! hiyo haikuwa vizuri sana?— Yehova alipendezwa na jambo ambayo vijana hao wanaume watatu walifanya. Na sisi twaweza kuchukua mfano wa hilo.
Hata leo wanadamu wanasimamisha sanamu kwa kuabudu. Nyingine zinafanyizwa kwa miti au mawe au maaini. Je! wewe ungesujudia sanamu hizi?—
Sanamu nyingine zinafanyizwa kwa nguo. Umepata kuona sanamu ya namna hiyo?— Je! unafikiri inafanya tofauti kwa Mungu ikiwa inafanyizwa kwa nguo au kwa miti au mawe?— Je! ingekuwa vizuri kwa mtumishi wa Yehova kufanya tendo la kuabudu mbele ya sanamu niyo?
Shadraka, Meshaki na Abednego walimwabudu Yehova peke yake. Mungu alipendezwa na wao. Je! utafuata mfano wao?
(Tena wale wanaomtumikia Yehova hawawezi kuabudu sanamu. Soma yanayosemwa juu ya hili katika Isaya 42:8 na Yoshua 24:14, 15, 19-22.)