Sura ya 38
Upendo wa Nyumba ya Mungu
JE! WEWE unapenda wakati tunapoitwa kwenda kwenye nyumba ya mtu fulani kwa chakula?— Namna gani ikiwa tungeitwa kwenda kwenye nyumba ya Mungu, je! ungetaka kwenda?—
Sasa, labda utasema Mungu haishi katika nyumba. Na ni kweli Mungu haishi katika nyumba kama sisi.
Lakini Mwalimu Mkuu alisema kwamba Mungu alikuwa na “nyumba.” Na Yesu alikuwa akienda kwa nyumba ya Mungu, hata wakati alipokuwa mdogo. Nyumba hiyo ilikuwa hekalu zuri la Yehova katika mji wa Yerusalemu. Hekalu hilo lilikuwa la Mungu. Lilitumiwa kwa ibada yake. Hivyo iliitwa “nyumba ya Yehova.”
Wakati Yesu alipokuwa mtoto, aliishi mbali na “nyumba ya Yehova.” Siku hizo hakuna mtu aliyekuwa na motokaa, na kulikuwa hakuna garimoshi ambalo wangeweza kupanda. Ili kufika kwenye hekalu, ingewapasa watembee kwa miguu. Haikuwa safari ya saa moja tu kutoka mahali ambapo waliishi. ingewapasa kutembea hata kwa siku tatu wafike huko. Na safari ya kurudi nayo ingechukua siku nyingine tatu. Je! ilifaa kujitahidi kufanya safari hiyo? Je! wewe ungalitembea mwendo huo ili utumie wakati katika “nyumba ya Mungu?”
Watu waliopenda “nyumba ya Mungu” hawakufikiri kulikuwa mbali mno. Kila mwaka wazazi wa Yesu walikwenda Yerusalemu kuabudu. Na Yesu alikwenda pamoja nao.
Mwaka mmoja, wakati walipoanza safari kurudi nyumbani, Yesu hakuwa pamoja na jamaa yake. Hakuna mtu aliyejua mpaka walipokuwa wamesafiri mwendo wa mbali. Ndipo wazazi wake wakarudi kwenda kumtafuta. Wewe unadhani alikuwa wapi?—
Walimkuta mle mle katika hekalu. Alikuwa akiwasikiliza waalimu. Alikuwa akiwauliza maulizo. Na wakati walipomwuliza jambo fulani, alijibu. Walistaajabu kwa majibu yake mazuri ambayo alitoa.
Bila shaka, mwishowe wakati wazazi wake walipomkuta, walifurahi sana. Lakini Yesu hakusumbuka. Alijua kwamba hekalu palikuwa mahali pazuri kuwapo. Basi, aliuliza hivi: “Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu?” Alijua kwamba hekalu lilikuwa “nyumba ya Mungu.” Na alipenda aweko huko.—Luka 2:41-49.
Yesu na wazazi wake hawakwenda mara moja tu kwa mwaka kwenye mikutano ili kuabudu. Kila juma kulikuwako mikutano kwa ibada katika mji ambamo waliishi.
Penye mikutano hiyo mtu fulani angesimama na kusoma Biblia. Hawakuwa na Biblia yote katika kitabu kimoja. Iliandikwa penye vitabu vya kukunja. Hivyo wangekunjua mahali ambapo wangetaka kisha kuanza kusoma. Kisha ingeelezwa. Biblia inasema kwamba ilikuwa “desturi” ya Yesu kuhudhuria mikutano hii. Maana yake alikwenda kwa kawaida.—Luka 4:16.
Na sisi imetupasa tufanye hivyo. Lakini leo “nyumba ya Mungu” iko wapi? Imetupasa twende wapi tukamwabudu?—
Hekalu ambako Yesu alikwenda katika Yerusalemu haliko tena huko. Liliharibiwa. Hivyo hatuwezi kwenda huko.
Lakini bado Mungu ana “nyumba.” Si nyumba yenye mawe. Ni nyumba yenye watu. Hiyo ingeweza kuwa namna gani? Nyumba ni mahali pa kuishi. Na Mungu anasema kwamba yuko pamoja na watu wake. Haachi mbingu na kushuka duniani. Bali Mungu yuko karibu na watu wake hata wanaona kana kwamba alikuwa huko pamoja nao.—1 Petro 2:5; Waefeso 2:22; 1 Timotheo 3:15.
Basi, wakati tunapokwenda kwenye “nyumba ya Mungu,” imetupasa twende wapi? Imetupasa twende mahali ambapo watu wa Mungu wamekutana kwa ibada. Ingeweza kuwa katika nyumba kubwa. Ingeweza kuwa katika nyumba ndogo. Au ingeweza kuwa katika nyumba ya mtu fulani. Jambo kubwa ni kwamba wawe watu wa Mungu kweli kweli. Lakini tunaweza kujua namna gani ikiwa wao ni watu wake?—
Basi, wanafanya nini penye mikutano yao? Je! kweli wanafundisha yaliyomo katika Biblia? Je! wanaisoma na kuzungumza juu yake? Hivyo ndivyo tunavyomsikiliza Mungu, sivyo?— Na katika “nyumba ya Mungu” tungetazamia kusikia ambayo Mungu anasema, sivyo?—
Lakini namna gani ikiwa watu wanasema si lazima ufuate ambayo Biblia inasema? Je! ungesema wao ni watu wa Mungu?—
Hapa pana jambo jingine la kufikiria. Biblia inasema kwamba watu wa Mungu wangekuwa “watu wa jina lake.” Jina la Mungu ni jina gani?— Ni Yehova. Basi tunaweza kuuliza watu ikiwa Mungu wao ni Yehova. Wakisema “Hapana,” hapo tutajua kwamba wao si watu wake.—Matendo 15:14, NW.
Lakini haitoshi kusema tu kwamba Yehova ni Mungu wao. Ushuhuda uko wapi? Ingewapasa wawe wakisema juu yake kwa watu wengine. Ingewapasa wawe wakiwaambia watu juu ya ufalme wa Mungu. Ingewapasa wawe na imani katika Mwana wake. Ingewapasa waonyeshe upendo wao kwa Mungu kwa kushika amri zake.—lsaya 43:10.
Je! tunawajua watu wanaofanya mambo hayo yote?— Basi imetupasa tukutane pamoja nao kwa ibada. Na imetupasa tuweko huko kwa kawaida. Imetupasa tusikilize wale wanaofundisha, na kujibu maulizo wakati yanapoulizwa. Ndivyo Yesu alifanya wakati alipokuwa katika “nyumba ya Mungu.” Tukifanya hivyo, tunaonyesha kwamba sisi, vile vile, tunaipenda “nyumba ya Mungu” kweli kweli.
(Imetupasa tupendezwe katika kuhudhuria mikutano kwa kawaida pamoja na watu wa Mungu. Soma yanayosemwa juu ya hili katika Zaburi 122:1; Waebrania 10:23-25.)