Sura ya 40
Yesu Alitoa Uhai Wake kwa Ajili Yetu
UNAO rafiki fulani wazuri, sivyo?— Lakini ikiwa wangekuwa katika hatari kubwa je! Namna gani ikiwa wangekuwa katika chombo ambacho kingekuwa kinazama? Je! ungetaka kuwaokoa ikiwa ungeweza?— Je! ungefanya hivyo hata ikiwa lazima wewe mwenyewe ufe wakati unawasaidia? Mtu ambaye angetoa uhai wake ili kuokoa watu wengine anaonyesha kwamba yeye anawapenda sana sana.
Yesu alionyesha kwamba alikuwa na upendo wa namna hiyo kwetu. Yeye alikuwa na nia ya kuacha mbingu na kutumwa duniani ili atufie sisi. Je! unajua kwamba alikufa kwa ajili yetu?—
Ungependa kusikia namna alivyofanya hili?— Na tujifanye kana kwamba tuko huko na tunaweza kuona kinachotukia.
Ni usiku sana siku moja ya Machi au Aprili katika Yerusalemu. Mwezi unatoa mwanga mwingi sana. Wakati tunapotazama mji tunamwona Yesu na mitume wake wakipita katika lango kubwa na kutoka mjini. Wanakuja kwenye kilima kinachoitwa Mlima wa Mizeituni na kuingia katika bustani. Je! tuwafuate?—
Wakati tunapotazama, tunamwona Yesu anatoka katika wanafunzi wake na kupiga magoti ili aombe kwa Baba yake. Anafanya hivi mara tatu. Na kila anaporudi anawaambia wanafunzi wake kwamba imewapasa nao wawe wakiomba. Sababu gani? Kutatukia nini?—
Tazama! Unawaona watu wale wanaokuja kwenye bustani? Wengine kati yao wana taa. Wengine wana marungu. Kuna askari wenye panga. Wanaonekana wakali sana. Bila shaka Yesu amewaona wakija. Je! asijaribu kukimbia?—
Yesu anawaona, lakini hakimbii. Sasa askari wanafika na kumkamata Yesu. Je! atawaacha wamkamate? Anaweza kumwomba Baba yake. Mungu anaweza kumpelekea maelfu ya malaika. Wanaweza kuwaharibu watu wale kwa dakika chache. Ikiwa wewe ungalikuwa Yesu, je! ungaliomba malaika?—
Lakini Yesu anawaacha watu wamkamate Sababu gani?— Kwa sababu anataka kufa kwa ajili yetu. Kuna sababu iliyo kubwa hata zaidi. Anamwambia mwanafunzi Petro: ‘Lazima Neno la Mungu litimie.’ Unaona, ilikwisha kuandikwa katika Biblia kwamba Yesu angetoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu.
Sasa wanafunzi wa Yesu wanaogopa na wanakimbia. Askari wanamrudisha Yesu mjini. Acha tuwafuate tuone kitakachotukia.
Wanampeleka Yesu mbele ya makuhani wakuu. Makuhani hawa wanamchukia Yesu kwa sababu amekuwa akionyesha watu kwamba makuhani hawafundishi Biblia.
Makuhani wanafanya hukumu. Wanaleta watu wanaosema uongo juu ya Yesu. Wanamwuliza Yesu maulizo kujaribu kuonyesha kwamba amefanya kosa. Lakini hawawezi kuonyesha kosa juu yake. Kisha makuhani wanamwambia Yesu: ‘Je! wewe ni Mwana wa Mungu?’ Yesu anasema: ‘Ndiyo.’ Makuhani wanakasirika na kusema: ‘Ana hatia! Imempasa auawe!’ Wengine wote wanakubali. Basi wengine kati ya watu wanaanza kumcheka Yesu. Wanamtemea mate na kumpiga kwa ngumi zao. Je! Yesu anaanza kusikitika kwa vile amefundisha kweli kutoka katika Biblia? Wewe ungalionaje?—
Basi, Yesu hasikitiki na hata hanung’uniki au kurudisha pigo.
Sasa kumekucha asubuhi. Yesu amekaa bila kulala usiku wote. Sasa makuhani wanaagiza Yesu afungwe, na wanampeleka kwa Pilato, gavana.
Wanamwambia Pilato hivi: ‘Yesu anapinga serikali. Imempasa auawe.’ Lakini Pilato anaweza kuona kwamba makuhani wanasema uongo. Basi Pilato anawaambia hivi: ‘Mimi sioni kosa katika mtu huyu. Nitamwacha aende.’ Lakini makuhani na wengine wanapaza sauti hivi: ‘Hapana! Mwue!’
Mwisho, Pilato anajaribu tena kuwaambia watu kwamba atamfungua Yesu. Lakini makuhani wanachochea makutano ya watu kupaza sauti hivi: ‘Ikiwa wewe unamfungua na wewe vile vile unapinga serikali! Mwue!’ Sasa kunakuwa kelele sana. Pilato atafanya nini?
Anashindwa. Kwanza anaagiza Yesu apigwe viboko. Ndipo amtoa kwa askari ili auawe.
Wanampa Yesu nguzo au mti mkubwa achukue. Mwisho wanafika mahali panapoitwa Fuvu la Kichwa nje ya mji. Huko wanapigilia mikono na miguu ya Yesu misumari kwa mti. Ndipo wanausimamisha ili Yesu aninginie juu yake. Anatoka damu. Maumivu ni makubwa sana.
Yesu hafi mara hiyo. Ananing’inia tu pale penye mti. Makuhani wakuu wanamcheka. Wanasema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwa mti wa mateso!” (NW) Lakini Yesu anajua jambo ambalo Baba yake amemtuma afanye. Anajua kwamba yampasa atoe uhai wake mkamilifu ili tuweze kuwa na nafasi ya kupata uzima wa milele. Mwisho, kama saa tisa za alasiri hiyo, Yesu analia kwa sauti kuu kwa Baba yake na anakufa.—Mathayo 26:36-27: 50; Luka 22:39-23:46; Yohana 18:1-19:30.
Lo! namna Yesu alivyokuwa tofauti na Adamu! Adamu hakuonyesha upendo kwa Mungu. Hakumtii Mungu. Wala Adamu hakuonyesha upendo kwetu. Kwa sababu alifanya dhambi, sisi sote tumezaliwa tukiwa na dhambi ndani yetu. Lakini Yesu alionyesha upendo kwa Mungu na kwetu sisi. Alimtii Mungu sikuzote. Alitoa uhai wake ili aondoe dhara ambalo Adamu alitutenda sisi.
Je! wewe unaheshimu jambo zuri sana ambalo Yesu alifanya? Wakati unaposali kwa Mungu, je! unamshukuru kwa jambo ambalo Mwana wake alifanya?—
(Ili kuongeza heshima kwa jambo ambalo Yesu alitufanyia, soma Yohana 3:16; Warumi 5:8, 19; 1 Timotheo 2:5, 6; Mathayo 20:28.)