Sura ya 44
“Utakuwa Pamoja na Mimi katika Paradiso”
UNAPENDA wanyama?— Ungependa kuweza kucheza pamoja na simba? Au ungependa kuwa na dubu kama rafiki?—
Unakuja wakati utakapoweza kufanya hivyo. Chukua Biblia yako tusome juu yake pamoja.
Andiko liko katika kitabu cha Isaya, sura ya 11, mstari wa 6. Linasema hivi: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.”
Kungetukia nini leo ikiwa mbwa-mwitu angemkaribia mwana-kondoo?— Angemtafuna kabisa kabisa, sivyo? Na kungetukia nini ikiwa chui angekuwa pamoja na mwana-mbuzi?— Mwana-mbuzi huyo angekuwa chakula cha chui.
Lakini Biblia inasema kwamba kutakuwa na mageuzi ya hilo. Mungu atawafanya wanyama hao wale majani, pahali pa kulana. Wakati wanyama wote watakapokuwa na urafiki, itakuwa furaha kuwa na simba kama rafiki, sivyo?— Hiyo itatukia katika Paradiso.
Unajua Paradiso ni nini?— Paradiso ni bustani au shamba zuri la kutembelea. Ni mahali pa amani na furaha.
Mungu alimpa mtu wa kwanza, Adamu, na mke wake Paradiso mwa kuishi. Iliitwa Bustani ya Edeni. Walikuwako wanyama katika bustani hiyo. Lakini hakuna mmoja wao aliyeumiza wengine. Ilikuwako miti vile vile yenye matunda mengi matamu sana. Na kulikuwako mto. Palikuwa mahali pazuri pa kuishi.
Lakini Adamu na Hawa walipoteza Paradiso hiyo. Hawakumtii Mungu, hivyo hawakuweza kuishi tena katika Paradiso. Sasa hakuna Bustani ya Edeni. Basi, inawezekana kwetu namna gani kuishi katika Paradiso?—
Basi, mbele ya kufa kwake penye mti wa mateso, Mwalimu Mkuu alisema juu ya Paradiso mpya. Mtu mmoja alikuwa amemwambia hivi: “Yesu, unikumbuke mimi wakati unaingia katika ufalme wako.” Yesu alijibu: “Kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43, NW.
Yesu hakusema kwamba wangekuwa katika Paradiso siku ile ile. Wote wawili walikufa na wakazikwa siku ile. Lakini Yesu alikuwa akisema juu ya jambo ambalo lingetukia akiisha ‘kuingia katika ufalme wake.’ Ndipo kutakuwako Paradiso tena. Paradiso mpya itaendelea milele.
Paradiso hiyo itakuwa wapi?— Paradiso ya kwanza ilikuwa apa hapa duniani, sivyo? Basi Paradiso mpya itakuwa apa hapa duniani tena. Ndiyo sababu Yesu alitufundisha sisi kuombea mapenzi ya Mungu yafanyike duniani. Utakapofika wakati huo, dunia nzima itakuwa Paradiso.
Katika Paradiso kutafanyika mageuzi makubwa. Hewa itakuwa safi na yenye kuburudisha na nzuri kuvuta. Maji katika mito yatakuwa safi na mazuri. Ardhi itaotesha wingi wa chakula hata hakuna mtu atakayeona njaa. Dunia nzima itakuwa kama shamba la kutembelea. ltajaa na ndege na wanyama, miti na maua ya kila namna.
Lakini mageuzi makubwa zaidi yatakuwa katika watu. Ni watu ndio wanachafua dunia, sivyo?— Wengine kati yao wanaishi katika nyumba chafu-chafu. Na wanatupa takataka kila mahali wanapokwenda. Lakini Paradiso haitakuwa hivyo. Itakuwa mahali safi na pazuri kuishi. Basi, ikiwa tunataka kuishi katika Paradiso, je! usingesema kwamba sasa ndio wakati wa kujifunza kuweka vitu katika utaratibu mzuri na safi?— Hiyo ndiyo njia moja kuonyesha kwamba sisi kweli tunataka dunia iwe Paradiso, sivyo?
Watu watageuka tena katika njia nyingine. Paradiso itakuwa mahali pa amani. Lakini si kila mtu leo ni mwenye kutaka amani. Watu wengine wanapigia wengine kelele nyingi. Wanapiga na kuumiza watu wengine. Wanatenda kama wanyama wa mwitu. Lazima wajifunze kuishi katika amani. Katika Paradiso, “hawatadhuru wala hawataharibu.”—Isaya 11:9.
Je! sikuzote wewe ni mwenye amani kwa wengine?— Ikiwa tutaishi katika Paradiso, ni lazima tujifunze kuwa wenye amani, sivyo?—
ltakuwa vizuri sana kuishi katika Paradiso. Mungu anaahidi kwamba wakati huo atatufanyia mambo ya ajabu. Fungua Biblia yako katika Ufunuo sura ya 21, mistari 3 na 4, na tusome ambayo linasema: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”
Ebu fikiria hilo! Mungu atatuangalia sisi. Haitakuwa lazima tulie hata kidogo kwa sababu tunahuzunika. Hakuna mtu atakayeona maumivu kwa sababu yeye ni mgonjwa. Na haitakuwa lazima mtu afe. Hivyo ndivyo itakuwa katika Paradiso.
Je! kweli wewe unataka kuishi katika Paradiso?— Mimi nataka. Mambo tunayofanya kila siku sasa ndiyo yatakayosaidia kuamua kama tutakuwako huko au sivyo. Ikiwa tunataka kuishi katika Paradiso, sasa ndio wakati wa kujitayarisha kwa Paradiso hiyo.
(Dunia hii itaendelea milele na Mungu ataifanya iwe mahali pazuri sana pa kuishi. Soma zaidi juu ya hili katika Zaburi 104:5; 37:10, 11; Mithali 2:21, 22; Isaya 35:5; Mika 4:3, 4.)