Sura ya 15
Je! Dawa za Kulevya Zinaleta Maisha Bora?
1, 2. (a) Dawa za kulevya zinatumiwa kwa kadiri gani na watu unaowajua? (b) Kwa nini vijana wanatumia dawa za kulevya?
BILA shaka, nyumbani kwenu mnazo dawa za aina fulani kama zile zenye kumpa mtu nguvu na nyingine zinazotuliza akili na kuleta usingizi, maana wengi wetu leo twaishi kati ya watu wenye kuzoea sana kutumia dawa za kulevya. Kwa mfano, uuzaji wa dawa za kulevya umeongezeka zaidi katika United States mara 30 tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili. Dakt. (mganga) Mitchell S. Rosenthal alisema kwamba katika mwaka wa karibuni dawa nyingi za kugeuza tabia zilipendekezwa na madaktari “ili kumchangamsha ama kumtuliza ama kumfanya mwanamume, mwanamke na mtoto katika [United States] apoteze fahamu kwa mwezi mzima.”
2 Dawa nyingi za kulevya zinapendekezwa na madaktari ili watu wazima wapate kutumia. Lakini katika nchi nyingine vijana wanazitumia sana ‘ili wajifurahishe.’ Wanatumia vilevile dawa za kulevya ambazo kwa kawaida hazifanyizwi zitumiwe kwa kusudi la kutibu, kutia na heroin, LSD na kasumba. Labda vijana wengine wanaelekea kuwaza hivi: “Ikiwa watu wazima wanatumia vibonge, wanavuta tumbako na kulewa, kwa nini mimi nisijifurahishe kwa kuvuta kasumba au kutumia dawa za kulevya?” Wewe waonaje? Je! waona kwamba dawa za kulevya zinaleta maisha yenye furaha zaidi sana?
DAWA ZA KULEVYA AMBAZO WENGI WANATUMIA
3-9. (a) Ni dawa gani za kulevya zinazotumiwa kwa kusudi la kupata raha? Zinawaletea wanaozitumia matokeo gani? (b) Unajua mambo yo yote yanayoonyesha ukweli wa matokeo hayo yaliyowapata watu wenye kutumia dawa za kulevya?
3 Kuna dawa mbalimbali za kulevya ambazo watu wanatumia ili wapate raha. Labda umekwisha kusikia habari nyingi juu ya dawa hizo. Lakini ebu chukua dakika chache uangalie tena namna dawa hizo zilivyo.
4 Kuna dawa zinazoitwa barbiturates, na mara nyingine zinaitwa “downers.” Dawa hizi ni za kutuliza wasiwasi au maumivu, ambazo madaktari wanaweza kuagiza zitumiwe ili kuleta usingizi. Kuna aina ya dawa hizo zaidi ya 24, na zaidi ya tani 525 (tani 476 za vipimo vya mita) zinafanyizwa kila mwaka katika United States peke yake. Sehemu kubwa ya dawa hizo inatumiwa kwa njia haramu.
5 Vilevile kuna dawa nyingi za kuchangamsha zinazotumiwa, zinajulikana na watu wengi kama “pep pills” au “uppers.” Dawa zinazotumiwa sana kati ya hizo ni zile zinazoitwa amphetamines. Madaktari wengine wanapendekeza dawa hizo zitumiwe na wagonjwa ili kuzuia hamu ya kula, kupunguza uchovu au kuondoa hali ya uzito wa roho. Walakini, inakadiriwa kwamba nusu ya dawa hizo zinazofanyizwa kwa njia halali zinatumiwa kwa njia haramu.
6 LSDa ndiyo dawa yenye nguvu kupita dawa nyingi za kulevya zinazomfanya mtu aone mambo yasiyo ya kweli. Miaka ya karibuni viwanda vingi vya haramu vimeanza kufanyiza dawa hiyo. Inafanyiza matokeo yasiyo ya kawaida katika wale wanaoitumia. Sana sana uwezo wa kuona unabadilika. Mazigazi na kupotewa akili kwaweza kutukia hata ikiwa kumepita miezi mingi baada ya kutumia kiasi cha mwisho cha dawa hiyo. Mambo ambayo mtu anaona katika njozi wakati anapopotewa akili, yaweza kuwa yenye kuogofya sana.
7 Marijuana, ambayo ni namna fulani ya bangi, ni mojawapo ya dawa za kulevya zinazotumiwa zaidi mahali pote. Je! unawajua watu ambao wameivuta? Si kali sana kama LSD, lakini nayo vilevile inapotoa fahamu. Mtu anapovuta marijuana, huenda dakika tano zikaonekana kama saa nzima. Huenda sauti na rangi za vitu zikaonekana kubwa sana.
8 Heroin ni dawa inayofanyizwa kwa morphine, inayotokana na afyuni. Ni dawa hatari sana. Baada ya kutungwa sindano yake kwa mara chache tu, watu wanaweza kuizoea sana, na kupata taabu sana ya kuiacha nao wanazidi kuitumia. Watu wakizoea kutumia heroin, inaweza kuharibu nia na uwezo wao wa kujifunza. Wanaongozwa na mazoea yanayowaharibu polepole. Mwanachama wa baraza kuu ya New York aliandika hivi: “Heroin imeharibu masomo yetu ya shule.”
9 Bila shaka, kuna dawa nyingine za kulevya ambazo watu wengi wanadhani zitawaletea maisha yenye furaha zaidi. Kati ya hizo kuna dawa inayoitwa cocaine. Halafu kuna ile sumu iliyomo katika tumbako. Je! utumie dawa hizo za kulevya? Kama tulivyokwisha kuona katika sura iliyotangulia, Biblia hailaumu vileo vinavyoweza kumburudisha mtu na kufurahisha moyo wake vikitumiwa kwa kiasi. Basi, je! ni jambo linalofaa au la hekima kutumia yo yote ya dawa nyingi hizo za kulevya zilizo mbalimbali kwa kutaka kufanya maisha yawe yenye kufurahisha zaidi?
ZINAWEZA KUTUMIWA KWA NJIA FULANI?
10-12. (a) Daktari awezaje kutumia dawa ya kulevya amsaidie mtu? (b) Lakini kutumia vibaya dawa za kulevya kunaumiza watu sana namna gani?
10 Kwa wazi dawa za kulevya zina matumizi yake, na mara nyingine huenda daktari akapendekeza utumie dawa moja ya hizo kwa sababu ya ugonjwa wako. Ikiwa unaumwa sana, pengine daktari atakupiga sindano ya morphine ili maumivu yatulie. Bila shaka dawa za aina ya barbiturates na amphetamines zimesaidia wagonjwa wengine. Vilevile, heroin inatumiwa mahali pengine kutuliza maumivu ya mara kwa mara ya watu wenye ugonjwa wa donda baya.
11 Lakini, kwa upande mwingine, dawa za kulevya zinaumiza sana mamilioni ya watu. Yapata watu milioni moja katika United States wanasemekana kuwa wenye kuzoea dawa za aina ya barbiturate, na zaidi ya watu 3,000 wanakufa kila mwaka kwa sababu ya kuzitumia kupita kiasi. Kuzoelea heroin na kuitumia kupita kiasi kunaleta vifo vingi kila siku, na pia kufanya makumi ya maelfu ya watu wawe wahalifu (wavunjaji wa sheria) wabaya sana. Ili waendeleze mazoea yao yenye kupoteza fedha nyingi sana, wenye kuzoea dawa hizo za kulevya wanaiba mali yenye bei zaidi ya shilingi 104,000,000 (au zaire 2,600,000) mjini New York, kila siku kwa wastani!
12 Jambo hilo linamaanisha nini? Je! dawa za kulevya ziondolewe kabisa? Si lazima, kwa kuwa dawa nyingi za kulevya zinaweza kutumiwa kwa kusudi jema. Lakini tatizo ni kwa vile zinavyotumiwa vibaya mahali pote. Mamilioni ya watu wanazitumia hata bila sababu ya kutaka kuponya ugonjwa, tena kupita kiasi kinachokusudiwa kutumiwa katika utabibu. Mara nyingi mtumiaji wa dawa za kulevya anatamani tu kujisikia yuko katika hali yenye raha sana. Je! matumizi hayo ni yenye sababu nzuri?
MATOKEO MWILINI
13-17. (a) Kama inavyoonyeshwa katika vitabu vya dawa, dawa zote za kulevya ni nini? (b) Kwa hiyo, hata ikiwa zinatumiwa kuponya magonjwa, kwa nini ni kujiletea hatari? (c) Eleza namna kila mojawapo la maandiko yafuatayo linavyoonyesha maoni ya Mungu juu ya matumizi yo yote ya dawa za kulevya kwa kusudi la kupata raha zaidi: 2 Wakorintho 7:1; Warumi 13:13; 12:1.
13 Labda unajua kwamba dawa nyingi za kulevya zinapatikana kwa kupendekezwa na daktari tu, na kwamba hata nyingine ni haramu katika nchi nyingi. Jiulize mwenyewe: Kwa nini? Ni kwa kutulinda sisi sote. Ndiyo, dawa za kulevya zaweza kuwa hatari, hata zinaweza kuua. Kwa kweli, dawa za kulevya ni upanga wenye makali mawili, zaweza mara nyingine kuponya, lakini zaweza kuumiza au hata kuua mara nyingine. Kitabu, Drugs kilichotungwa na mtaalamu wa elimu ya dawa pamoja na mtungaji mwingine, chaeleza hivi:
14 “Dawa zote za kulevya ni sumu, na sumu zote ni dawa za kulevya. Maneno haya ‘poison’ na ‘potion’ yatokana na asili moja, wala neno hili la Kigiriki pharmakon, tunaloona kuwa asili ya maneno yetu haya ‘pharmacy’’ na ‘pharmacology,’ halikutokea bila kusudi kwa sababu hapo kwanza lilikuwa na maana ya dawa ya kuponya na ya kuua vilevile.”
15 Kwa hiyo, hata unapokuwa mgonjwa, kutumia dawa ya kulevya ni hatari ya kujitakia mwenyewe. Lakini kwa sababu unathamini uhai wako labda utaikubali hatari hiyo na kutumia dawa ya kulevya ili utulize maumivu au upate kupona. Lakini je! ingekufaa kumeza au kutia ndani ya mwili au, kuvuta puani dawa ya kulevya ili upate raha zaidi, usahau matatizo na kuanza kuona njozi ya mambo yasiyokuwako? Je! kuutumia mwili wa ajabu uliopewa na Mungu katika njia hiyo kunapatana na namna Muumba alivyokusudia?
16 Fikiria hili. Kama ungeweza kumpa mtu zawadi bora, tuseme motokaa mpya, ungeonaje kama angeitumia ovyoovyo tu? Tuseme kama angejaribu kuiendesha bila kuweka mafuta ndani yake au bila kugeuza mafuta ya zamani na kuweka mapya, na kuitumia kuchukulia samadi (mbolea)? Labda ungeudhika na kumwona ni mtu ovyo sana kwa kutokujali zawadi yako, sivyo? Basi, unadhani Yehova Mungu anaonaje ikiwa tunautumia mwili wetu ovyoovyo tu, tukiujaza sumu kwa kutafuta raha tu? Neno lake latujulisha kwa kututia moyo hivi: “Na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kwa hiyo, ikiwa tunachafua miili yetu kwa kuitia dawa za kulevya ili tutafute raha tu, hatuishi kupatana na mapenzi ya Mungu.
17 Fikiria jambo hili pia. Tumetangulia kuzungumza shauri la Muumba juu ya ulevi. Ameonyesha waziwazi katika Neno lake kwamba mtu anayekosa kujiweza kwa sababu ya kunywa kupita kiasi anajivunjia heshima mwenyewe, akiwa mchafu na mpumbavu na mtu wa kuaibisha wengine walio karibu naye. Hakika Muumba wetu ameona yafaa alaumu ulevi. Basi, je! maoni ya Mungu yangekuwa tofauti ikiwa mtu angelewa heroin, bangi au dawa nyingine ya kulevya? Hata matokeo ya dawa za kulevya yajapokuwa si sawa na yale ya vileo, huenda mtu akakosa kujiweza hata kuliko wale wanaolewa vileo (pombe). Kwa hiyo, kulingana na shauri la hekima na busara linalopatikana katika Biblia, twaweza kuona ubora wa kutokutumia dawa za kulevya kwa kusudi la kupata furaha za ulevi.
NAMNA GANI KUTUMIA TUMBAKO?
18-21. (a) Ni kwa sababu gani watu wengi sana wanavuta tumbako hata ijapokuwa inajulikana sana kwamba kufanya hivyo ni hatari kwa afya ya mtu? (b) Toa angaa sababu mbili za kuonyesha kwamba lingekuwa kosa Mkristo kuvuta tumbako.
18 Labda utauliza hivi: “Basi, namna gani kutumia tumbako, iliyo na sumu ndani yake? Makumi ya mamilioni ya watu wazima wanavuta tumbako ‘kwa kusudi la kupata raha,’ kama wasemavyo. Je! hii inafaa? Sivyo, haifai, kama inavyoonyeshwa na onyo linaloonekana penye vifurushi vya tumbako inayouzwa katika United States vyenye kusema: KUVUTA TUMBAKO NI HATARI KWA AFYA YAKO. Hivyo ndivyo ilivyo hata ikiwa unaishi nchi gani. Basi, ni kwa sababu gani wengi ambao ni watu wazima wanawekea vijana mfano mbaya kwa makusudi na kuharibu afya yao wenyewe pia kwa kuvuta tumbako? Sana sana ni kwa sababu wamezoea hivyo. Taarifa katika Science World yaeleza hivi:
19 “Dawa ya kulevya . . . inayofanya mtu azoee sana kuitumia ni ile sumu iliyo ndani ya tumbako . . . Wakati hakuna sumu hiyo, mwili waitamani sana. Unaitamani sana hata ikikosekana mara nyingi mwili unakuwa mnyonge. Zinaanza dalili za kuacha—kujiona mnyonge. . . . Baadhi ya dalili hizo ni hali ya kusinzia, maumivu ya kichwa, machafuko ya tumboni, kutokwa jasho, na moyo kupiga isivyo kawaida.”
20 Ni wazi kwamba, kuvuta tumbako kunaharibu mwili wa mtu tena ni ‘uchafu wa mwili’ mmojawapo ambao Muumba wetu anahimiza Wakristo wajitakase nao. Kwa hiyo labda utaona kwamba watu wazima wanaovuta tumbako hawastahili kulaumu vijana wanaojiharibu kwa kutumia dawa za kulevya. Na hilo ni kweli. Kama wazazi wanaendelea kujiharibu wenyewe kwa kuvuta sumu ya tumbako, wanawezaje kutazamia watoto wao wathamini wanayosema juu ya ubora wa kuepuka dawa za kulevya? Hata hivyo, kila mmoja wetu atahukumiwa na Mungu kwa kadiri ya matendo yake hata watu wengine watende au kusema namna gani. Neno la Mungu Biblia linasema jambo jingine linaloonyesha kwamba ni vibaya Mkristo kuvuta tumbako.
21 Biblia yaamuru hivi: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:39) Lakini unawezaje kuvuta tumbako mbele ya wengine na bado useme wampenda jirani yako? Tunauliza hivi kwa sababu ya maelezo haya ya Medical Tribune: “Kuvuta tumbako kunaharibu si afya ya mvutaji tu—kwaweza kuharibu pia mtu aliye karibu, asiye na hatia.” Jarida (gazeti) lenye kujulikana sana la habari za dawa lilisema hivi pia: “Mahali pasipo na hewa safi, afya ya mtu asiyevuta tumbako inahatirishwa na mvuta tumbako.” Kwa kuwa kuvuta tumbako kunaharibu vilevile wale walio karibu na mvutaji, je! si wazi kwamba huwezi kuvuta tumbako na wakati uo huo useme wampenda jirani yako?
JE! BANGI NI TOFAUTI?
22-25. (a) Matokeo ya kutumia bangi hata kwa kiasi kidogo yako tofauti namna gani na yale ya vileo? (b) Mungu anatusaidiaje kweli tupate faida zote za maisha kwa kutuonya juu ya mazoea yenye kuharibu? (Isaya 48:17; Zaburi 16:11; Mithali 3:1-7)
22 Vijana wengine wanataka kulinganisha kuvuta bangi na kunywa vileo (pombe). Huenda wakawaona wazazi wao au watu wazima wengine wakipata raha nyingi kwa kunywa vileo wakakata shauri kwamba kuvuta bangi kwa kusudi la kupata matokeo yale yale si tofauti. Je! ndivyo?
23 Kumbuka kwamba, ijapokuwa Biblia yakubali kunywa vileo kwa kiasi, inalaumu sana kuvitumia kupita kiasi, ikisema kwamba ‘walevi hawataurithi ufalme wa Mungu.’ (1 Wakorintho 6:9, 10) Walakini, huenda vijana wengi wakasema kwamba wanavuta bangi kwa kiasi, si kwa kadiri ya kufanyiza matokeo yanayofanana na ulevi. Lakini bangi ni tofauti na kileo. Mwili wako waweza kugeuza kileo iwe nguvu unayoweza kutumia katika mishipa yako. Ni chakula. Lakini mwili hauwezi kutumia bangi. Zaidi ya hayo, kileo hakikai muda mrefu mwilini wala katika visehemu vya ubongo. Baada ya saa chache kinaondolewa mwilini. Walakini, sumu ya bangi haiondolewi upesi, inafanyiza matokeo yenye kuharibu mwili. Madaktari sita wa kutoka Chuo Kikuu cha Masomo ya Waganga wa Dawa na Waganga wa Kupasua walieleza katika barua waliyomwandikia mhariri (mwandikaji) wa New York Times hivi:
“Bangi ina sumu . . . zinazoyeyushwa katika mafuta tu na kuwekwa akiba kama DDT kwa juma nyingi na miezi mingi katika chembe za mwili na katika ubongo. Chembe za mwili zina nafasi kubwa sana ya kuwekwa sumu hizo—na hiyo inaonyesha matokeo yenye kuharibu polepole wale wanaozoea kuvuta tumbako. Ye yote anayetumia sumu hizo zaidi ya mara moja kila juma hawezi kuepuka matokeo ya dawa za kulevya.”
24 Hivyo Dakt. Robert Heath wa Chuo Kikuu cha Tulane anadharau kulinganisha vileo na bangi akisema ni “upuzi mtupu.” Anasema kwamba vileo vina “matokeo ya muda. Bangi ina matokeo yenye kuendelea.” Kwa wazi hata kutumia bangi kwa kiasi kidogo sikuzote kwaweza kuwa na matokeo mabaya, kama gazeti Detroit Free Press linavyoeleza: “Wachunguzi wa dawa wanaarifu juu ya mavumbuzi mapya yanayoonyesha kwamba bangi—na [hashish]—zinaharibu sana afya ya mwili na ya akili zinapotumiwa kwa kawaida, hata mara moja au mara mbili kila juma.”
25 Kwa kweli, twaweza kumshukuru Muumba wetu kwa kutupa kanuni za kutuongoza. Anatupenda, na kwa sababu hiyo anatusihi tuepuke kitu kitakachochafua miili yetu na kutuumiza, mahali pa kutuletea furaha na hali njema ya milele. Huenda dawa fulani za kulevya zikamsaidia mtu aliye mgonjwa, lakini zaweza kuumiza wale wanaozitumia kwa kutaka raha tu. Si njia ya maisha bora.
[Maelezo ya Chini]
a Lysergic acid diethylamide.
[Picha katika ukurasa wa 108]
[Picha katika ukurasa wa 113]
Je! inafaa uvute tumbako kwa sababu tu mamilioni ya watu wazima wanaivuta?