Sura ya 8
Maisha ya Jamaa—Namna Unavyoweza Kufanikiwa
WATU wengi sana wanakubali kwamba maisha ya jamaa na furaha ni mambo yanayohusiana. Katika uchunguzi mmoja uliofanywa, asilimia 85 ya wanaume walisema ‘wanaona maisha ya jamaa yanahitajiwa sana ili maisha yafurahishe na kuridhisha.’ Hata hivyo labda unawajua wanaume wengi ambao wamechagua talaka. Pia, wanawake wanaotaka talaka ili kukomesha ndoa zenye kuchosha, zenye magombano au uonevu, wanazidi kuwa wengi.
2 Hatuwezi kubadili matendo ya watu wale wengine. Lakini inatupasa tupendezwe na kufanyia maendeleo maisha ya jamaa zetu wenyewe, hasa uhusiano kati ya mume na mke. Inafaa sote tujiulize hivi: ‘Uhusiano huo ukoje katika jamaa yangu?’
3 Muumba ndiye Mwanzishi wa mpango wa jamaa. (Waefeso 3:14, 15) Yeye anatoa maoni yenye mafaa yaliyosaidia watu wengi sana waliooana wafanikiwe katika maisha ya jamaa. Maoni ayo hayo yanaweza kukufaidi wewe.
MASOMO YENYE MAFAA TUNAYOJIFUNZA KATIKA NDOA ILE YA KWANZA
4 Katika kisehemu cha kwanza cha Biblia, tunapata maandishi yanayoonyesha namna Mungu alivyoanzisha jamaa ya kwanza ya kibinadamu. Muda fulani Yehova Mungu alipokwisha kuumba mtu wa kwanza, Adamu, Yeye alisema:
“‘Si vizuri mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’ Na Yehova Mungu akaanza kuujenga ubavu aliokuwa ameutoa kwa huyo mwanamume kuwa mwanamke, naye akamleta huyo mwanamke kwa yule mwanamume. Ndipo huyo mwanamume aliposema: ‘Huu hatimaye ni mfupa wa mfupa yangu na nyama ya nyama yangu. . . . ‘Hiyo ndiyo sababu mwanamume ataacha baba yoke na mama yake na inampasa ashikamane kabisa na mke wake na inawapasa wawe mwili mmoja.”—Mwanzo 2:18, 22-24, NW.
5 Angalia kwamba hapo hapasemi jamaa ya kwanza ilifanyika kwa sababu ya watu wawili kujiamulia wenyewe waishi pamoja. Mungu ndiye aliyetoa ruhusa kuwe na ndoa hiyo, nao wakaunganishwa katika mwungano wa daima. Adamu alimkubali Hawa awe mkewe mbele za Mkuu mwenye cheo kikubwa zaidi katika ulimwengu mzima.
6 Wakati mwanamume na mwanamke wanapochukua hatua zinazotakwa ili kufanyiza ndoa halali na yenye kukubaliwa, wanajifunganisha katika wajibu mmoja mbele ya watu wote. (Mwanzo 24:4, 34-67; Mathayo 25:1-10) Watu wawili hawajifunganishi katika wajibu huo wakati wanapoanza kuishi pamoja tu bila ya kuoana kisheria. Uhusiano wao unakuwa ule unaoitwa na Biblia “uasherati” au “uzinzi.” (Waebrania 13:4) Hata waseme wanapendana, baadaye uhusiano wao utaelekea kuharibika kwa sababu hauna mfungamano imara unaoonyeshwa na Biblia kuwa wa maana sana katika ndoa. Kwa mfano:
Mwanamke wa miaka 34 anaeleza hivi: “Labda mimi nafuata mambo ya kizamani, lakini mfungamano wa ndoa unanifanya nijisikie zaidi kwamba nina usalama. . . . Ninafarijika sana kwa kujua tulikubaliana sisi wenyewe na pia mbele ya ulimwengu kwamba tunakusudia kushikamana kabisa.”
Mwalimu wa miaka 28 alieleza mambo aliyoona baadaye, akasema: “Miaka kadha iliyopita, nilianza kujisikia kama kwamba maisha yangu yalikuwa ya bure tu. Kuishi pamoja [bila kuoana] hakukutuletea matazamio yo yote ya wakati ujao.”
Wakati Nancy M. Clatworthy, mchunguzi wa hali ya jamii ya watu, alipoliangalia sana jambo hilo alikuta kwamba waume na wake waliojifunga wajibu wa ndoa kwa kuoana, ambao hawakuwa wameishi pamoja kabla ya ndoa, ndio walioonyesha “furaha na uradhi mwingi zaidi.”
7 Masimulizi ya Biblia juu ya ndoa ya kwanza yanaweza pia kutusaidia tuepuke matatizo yanayohusu wazazi na wakwe. Mshauri mmoja wa ndoa alisema matatizo hayo ni kati ya yale yanayotokea sana. Hata hivyo, kabla hakujaweza kuwa na nafasi ya matatizo yo yote yanayohusu wazazi na wakwe, Biblia ilisema hivi juu ya ile ndoa ya kwanza: “Mwanamume ataacha baba yake na mama yake na inampasa ashikamane kabisa na mke wake.”—Mwanzo 2:24, NW.
8 Ni asili ya wengi wetu kuwapenda wazazi wetu. Biblia hata inatutia moyo tuwape msaada wa kimwili katika miaka yao ya uzee, wakiuhitaji. (1 Timotheo 5:8; Kumbukumbu la Torati 27:16; Mithali 20:20) Lakini Maandiko yanakazia kwamba ukiisha kuoa au kuolewa mwenzi wako ndiye anayekuwa mtu wa karibu zaidi wa ukoo wako. Mume au mke wako anakuwa ndiye wa kwanza kupendwa, kutunzwa na kuendewa ili upate mashauri kwake.
9 Maoni hayo yanazuia mtu asiwe ‘akikimbilia nyumbani’ kwa baba na mama wakati matatizo yanapotokea. Tena yanasaidia wazazi wafahamu kwamba watoto wao wakiisha kuoa au kuolewa ‘wanawaacha’ na kujifanyizia jamaa ambazo si lazima ziongozwe tena na wazazi hao, hata ikiwa desturi (mila) au hali ya kifedha inafanya watoto hao waishi karibu au pamoja na wazazi wao kwa muda. Inafaa watoto wathamini hekima na ujuzi wa kuishi kwingi kwa wazazi wao, na labda hata wawaombe mashauri juu ya maisha. (Ayubu 12:12; 32:6, 7) Hata hivyo, maneno ya Mwanzo 2:24 yanaonyesha wazazi wajihadhari wasielekeze au kusimamia-simamia maisha za watoto wao waliofunga ndoa. Ndiyo, kufuata shauri hilo la Biblia kunaweza kusaidia ndoa ifanikiwe.
WANAWAKE WANGAPI?
10 Tunaweza kuona pia kutokana na maandishi ya Mwanzo kwamba Mungu alimpa Adamu mke mmoja tu. Katika utamaduni wa mahali fulani-fulani mwanamume anaruhusiwa kuoa wake wengi. Lakini je! ndoa yenye wake wengi inaleta furaha katika jamaa? Matukio ya kweli yanaonyesha kwamba mara nyingi inatokeza wivu mwingi sana au ushindani mkali, na pia wake wale wa zamani-zamani wanatendwa kikatili. (Mithali 27:4; Mwanzo 30:1) Ndoa za wake wengi na kutaliki wanawake ni mambo yaliyokuwa kati ya Waebrania wa kale. Mungu ajaporuhusu Waisraeli kufanya hivyo, aliwapa sheria za kuzuia matendo mabaya sana. Yesu alizungumza jambo hilo kwa kuonyesha watu mapenzi ya Mungu yaliyo katika kitabu cha Mwanzo. Alipoulizwa habari za talaka inayotegemea sababu mbalimbali, Yesu alisema:
“Je! hamkasoma kwamba yeye aliyewaumba wao tangu mwanzoni aliwafanya wakawa mtu mume na mtu mke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume ataacha baba yake na mama yake na atashikamana kabisa na mke wake . . .’? . . . Basi, vile ambavyo Mungu amefunganisha katika nira moja mwanadamu ye yote asivitenganishe. . . . Musa [katika sheria ya Mungu], kwa sababu ya kufikiria ugumu wa mioyo [ya Waebrania] aliwatolea ninyi idhini ya kutaliki wake wenu, lakini haijawa hivyo tangu mwanzoni. Mimi nawaambia ninyi kwamba mtu ye yote atalikiye mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.”—Mathayo 19:3-9, NW.
11 Yesu alionyesha wazi kwamba, kama Mungu alivyokuwa amepanga hapo mwanzoni, kanuni ambayo ingefuatwa kati ya wafuasi wake ni kuwa na mke mmoja tu, wala si wengi. (1 Timotheo 3:2) Kuikubali hekima ya Mungu na mamlaka yake katika jambo hili ni hatua moja ya kuelekea kwenye furaha.
12 Ndivyo ilivyo pia kuhusu maneno ya Yesu juu ya talaka. Inapowezekana kupata talaka vyepesi, hesabu ya talaka inakuwa kubwa sana. Tunaona hivyo leo. Lakini Mungu anaiona ndoa kuwa jambo la kudumu. Ni kweli kwamba Yesu alisema mwenzi wa mtu akiwa na hatia ya “uasherati” (Kigiriki, porneia, maana yake matumizi machafu sana ya viungo vya uzazi), na hivyo kuwa “mwili mmoja” na mtu mwingine, labda mwenzi asiye na hatia anaweza kutaliki mwenzake na kuoa au kuolewa upya. Lakini katika hali za kawaida, Muumba anawaona watu waliooana kuwa wameungana daima. Basi wale wanaokubali kwamba Mungu ana mamlaka ya kuamua shauri hilo wanapaswa wajitahidi zaidi kuimarisha ndoa yao na kushinda matatizo yo yote waliyo nayo. (Mhubiri 4:11, 12; Warumi 7:2, 3) Kwa hiyo, maoni hayo yanasaidia watu wafanikiwe katika ndoa, wala hayawaletei huzuni. Matukio ya kweli yanathibitisha jambo hilo.
13 Lakini bado huenda watu fulani wakawa na maoni ya kwamba ‘ndoa nyingine zina matatizo makubwa, au watu waliooana wanashindwa kabisa kupatana.’ Halafu? Kuna mafaa mengine tunayoweza kufunzwa na Biblia.
MUME ANAYEPENDA MKE WAKE KWELI KWELI
14 Njia ya kufanikiwa katika jamaa ni namna mume anavyomwona na kumtendea mkewe. Lakini ni nani mwenye mamlaka ya kuamua njia iliyo bora zaidi ya kufanya hivyo? Maneno ya Biblia juu ya ile ndoa ya kwanza yanatusaidia kwa mara nyingine. Maandishi yanayohusu ndoa hiyo yanatueleza kwamba Mungu alitumia sehemu ya mwili wa Adamu kumfanyizia mke. Baadaye Biblia iliongeza maelezo zaidi juu ya jambo hilo:
“Waume wanapaswa WAWE WAKIWAPENDA WAKE ZAO KAMA MIILI YAO WENYEWE. Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu aliyepata kuchukia mwili wake mwenyewe wakati wo wote; bali anaulisha na kuuthamini sana, kama vile Kristo pia anavyolifanyia lile kundi.”
Halafu, baada ya kutumia maneno ya Mwanzo 2:24, Paulo aliendelea kusema: “Acheni kila mtu mmoja mmoja kati yenu apende mke wake kama anavyojipenda mwenyewe.”—Waefeso 5:28-33, NW.
15 Huenda wanaume wengine wakadhani inawapasa wawe wakali sana au wenye kujitenga sana wanaposhughulika na wake zao. Lakini Mwanzishi wa ndoa anasema kwamba mume anapaswa kupenda sana mke wake na kuonyesha kwamba anampenda. Ili mke awe na furaha ya kweli, anahitaji kuhakikishiwa anapendwa kikweli.
16 Wajibu wa mume wa ‘kumlisha na kumthamini sana mke wake kama mwili wake mwenyewe’ unatia ndani kujitahidi kuwa mtoaji mzuri wa riziki. Lakini asiwe na shughuli nyingi mno akitafuta riziki mpaka asahau kutumia wakati akiwa na mkewe na kumchangamkia sana kibinafsi. Tena, hakuna mwanamume mwenye kichwa kizuri anayeuchukia mwili wake mwenyewe wala kuutenda kikatili hata anapoudhika. Kwa hiyo, maneno ya Biblia yanamkataza kabisa mwanamume asimkasirikie mkewe kwa jeuri.—Zaburi 11:5; 37:8.
17 Mwanamke wa kwanza alifanywa awe ‘kikamilisho cha mumewe.’ (Mwanzo 2:18, NW) Mungu alijua kwamba mwanamume na mwanamke huyo walikuwa na maumbile tofauti. Mpaka leo maumbile hayo hayajabadilika. Kama ilivyo kawaida, wanawake wanatofautiana na wanaume katika sifa zao na matendo. Huenda mwanamume akawa mtu wa kukata maneno upesi, hali mwanamke huenda akawa mtu wa kusubiri kwa sababu ya huruma. Huenda mwanamke akapenda kuwa mahali penye watu wengi, lakini mwanamume apende kuwa mahali pa upweke. Huenda mwanamume akakazia sana mambo yafanywe bila kucheleweshwa, lakini huenda mwanamke akawa mwenye ‘kufanya polepole zaidi.’ Maelezo ya Biblia yanayosema Mungu alimwumba Hawa awe “kikamilisho” yanapasa yasaidie waume wazifahamu tofauti hizo.
18 Mtume Petro anasihi waume ‘wakae na wake zao kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu.’ (1 Petro 3:7) “Heshima” hiyo inatia ndani kumruhusu mke aonyeshe mapendezi mbalimbali anayoweza kuwa nayo. Huenda mume akawa anapenda michezo, lakini mkewe huenda akafurahia kwenda kutazama vitu vinavyouzwa madukani, vyenye kuonyeshwa madirishani, au kutazama dansi ya kuigiza jambo fulani. Mume hana cha kumfanya aone mapendezi yake ndiyo bora kuliko ya mkewe. Kuheshimu mkewe kutamwezesha azikubali tofauti zilizo kati yao.
19 Furaha na hasira za mke, zenye kuletwa na vipindi vyake vya hedhi, huenda zikamtatiza sana mume, na labda hata mke mwenyewe. Lakini mume anaweza kufanya wote wawili wafurahiane kwa kujaribu kumwelewa na ‘kukaa naye kwa akili.’ Mara nyingi jambo ambalo mke anahitaji zaidi ni kushikwa karibu-karibu kwa mapenzi wakati mumewe anapoongea naye.
MKE ANAYEHESHIMU MUMEWE
20 Kwa kuwa ni lazima mke pia atimize fungu lake ndipo kuwe na jamaa yenye furaha, Muumba anatolea wake pia mwongozo.
21 Mara tu baada ya kueleza waume wapende wake zao, Biblia inaongeza kusema: “Kwa upande mwingine, huyo mke anapaswa kumheshimu sana mume wake,” (Waefeso 5:33, NW) Katika ndoa ile ya kwanza, kuna mambo fulani ya wazi ambayo yangalipasa kumfanya Hawa ategemee uongozi wa mumewe. Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza. Ndiye aliyekuwa na maarifa na ujuzi mwingi zaidi katika maisha, kwa maana Mungu ndiye aliyempa maelekezo juu ya atakavyotenda.
22 Lakini namna gani juu ya ndoa leo? Mume akijaribu kutumia maoni ya Biblia kwa unyofu wa moyo kama ilivyotangulia kuzungumzwa, inaelekea sana kwamba mkewe atamheshimu. Hata ikiwa mke anampita mumewe kwa njia fulani, au ikiwa mume anapungukiwa na jambo fulani, bado mke huyo ana sababu ya kusitawisha heshima—kwa sababu ya kuuheshimu mpango wa Yehova, na jamaa ni sehemu ya mpango huo. Mtume Paulo aliandika hivi:
“Acheni wake wawe katika kuwatii waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia ni kichwa cha lile kundi.”—Waefeso 5:22, 23, NW.
23 Si kusema kwamba mume anapaswa awe mtawala mkatili anayejifanya ndiye mwenye ujuzi wa mambo yote katika jamaa. Kufanya hivyo kungekuwa kinyume cha mfano wenye upendo, huruma na ufahamu, uliowekwa na Kristo. Mungu anahimiza wake wategemee uongozi wa waume zao. Mume na mke wanaweza kushauriana juu ya mambo makubwa ya kijamaa, wakishirikiana namna viungo mbalimbali vya mwili vinavyotenda kazi kwa umoja. Hata ikiwa hivyo, bado mwanamume ndiye anayepaswa hasa kumpa Mungu sababu ya mambo yanayotendeka katika jamaa.—Wakolosai 3:18, 19.
24 Matukio ya kweli yanaonyesha kwamba maneno ya Biblia kuhusu jambo hili yanafaa sana. Mke anapoendelea kujitahidi astahili kupendwa na kutunzwa na mumewe, kisha ategemee mwongozo wake katika mashauri ya kijamaa, mara nyingi ataona kwamba mumewe anatimiza madaraka yake kwa nia na kwa upendo.—Mithali 31:26-28; Tito 2:4, 5.
KUJITAHIDI PAMOJA ILI JAMAA IFANIKIWE
25 Kupashana habari ni jambo la maana sana linalokosekana katika jamaa nyingi mno. Mtaalamu mmoja wa hali za jamii ya watu alisema: “Watu wengi waliooana hawasikilizi wakati mwenzio anaposema, tena wengi huanza kupigana kwa sababu hiyo.” Bila shaka nyakati fulani tutaudhiwa na mambo fulani, tuvurugike akili na kukatishwa tumaini maishani. Tunaweza kuyazuiaje mambo hayo yasiharibu ndoa yetu? Kupashana habari kwa njia nzuri kunasaidia. Jiangalieni msidhani kupashana habari ni jambo linalojileta lenyewe, kisha mje kujikuta mnasemezana mara chache zaidi na zaidi.
26 Jitahidini mpashane habari. Je! kweli ninyi mna mazoea ya kuelezana mambo mbalimbali mliyofanya na namna mnavyojisikia moyoni? Mara nyingi tunafanya mambo kukuru-kukuru hata tunakosa nafasi ya kuongea na kusikia anayoyasema yule mwingine. (Mithali 10:19, 20; Yakobo 1:19, 26) Badala ya kungojea nafasi ijitokeze yenyewe ndipo uweze kuongea, sikiliza, jaribu kufahamu, labda uwe ukiitikia yanayosemwa kwa kuuliza, ‘Yaani, unataka kusema kwamba . . .?’ au, ‘Unataka kuniambia kwamba . . .?’ (Mithali 15:30, 31; 20:5; 21:28) Mume au mke anayesikiliza mawazo na maoni ya moyoni ya mwenzake hataelekea sana kuwa mchoyo au kung’ang’ania jambo lake tu.
27 Kupashana habari kutathaminika zaidi ikiwa wenzi wa ndoa wataelezana matatizo yao kwa kusaidiwa na mashauri ya Biblia. Kwa mfano, msingi bora kabisa wa kuzungumzia mapato (mshahara) ya jamaa na mipango ya matumizi ya fedha unapatikana kwenye 1 Timotheo 6:6-10, 17-19 na Mathayo 6:24-34. Maoni mengi ya Kimaandiko juu ya mambo yanayotendeka sana katika maisha ya jamaa yanapatikana katika kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.a
28 Kwa kuwa maoni ya Biblia yanatokana na mamlaka inayoyajua vizuri zaidi mambo ya ndoa na maisha ya jamaa, yaani, Yehova Mungu, ni wazi kwamba tukiyafuata kwa subira na bila ugeu-geu, mashauri yaliyomo yataweza kutusaidia tujitahidi kufanikiwa. Maelfu ya waume na wake Wakristo duniani pote wamefanya hivyo na ndoa zao zikawa zenye furaha.
[Maelezo ya chini]
a Kimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society.
[Mambo ya Kuzungumziwa]
Ni kwa njia gani tunavyoweza kujitahidi tufanikiwe zaidi katika maisha ya jamaa? (1-3)
Kujifunganisha katika wajibu wa ndoa kulihusikaje katika ndoa ya kwanza, na kwa sababu gani wajibu huo ni jambo la maana kabisa? (4-6)
Tunaweza kujifunza nini kutokana na ndoa ya kwanza juu ya wazazi na wakwe? (7-9)
Tunaweza kujifunza somo gani lenye mafaa kutokana na kitabu cha Mwanzo juu ya hesabu ya wanawake ambao mwanamume anapaswa kuoa? (10, 11)
Biblia inatia watu moyo wawe na maoni gani juu ya talaka? (12, 13)
Waume wanaweza kutumia mashauri wanayopewa na Biblia kwa njia gani? (14-16)
Mke kuwa “kikamilisho” kunapasa kuwe na maana gani kwa mumewe? (17-19)
Ni maoni gani ambayo Biblia inahimiza mke awe nayo juu ya mumewe? (20-22)
Sababu gani wake wanaweza kuamini kwamba mashauri hayo yatasaidia? (23, 24)
Kupashana habari kunasaidiaje jamaa ifanikiwe? (25-28)
[Sanduku katika ukurasa wa 80]
“Wakati wa maisha yangu ya ndoa,” anaeleza mwanamume mmoja wa magharibi ya United States (Amerika), “nilikuwa nimepata kila kitu cha kimwili nilichotaka —makao mazuri, magari, mashua na farasi wengi. Lakini vitu hivyo havikuniletea furaha. Mke wangu hakupendezwa na vitu nilivyopendezwa navyo. Nyakati zote kazi yetu ilikuwa ni kugombana. Mimi nilikuwa nikivuta bangi ili nipate amani ya akilini.
Nilitumia Jumamosi na Jumapili nyingi nikiwinda mbali na nyumbani. Pia, kazi yangu ilinihitaji niwe safarini mara nyingi. Hiyo ikanifanya niwe nikiishi maisha ya uzinzi. Mimi nilijisikia kwamba mke wangu hakunipenda, kwa hiyo nikahama na kuanza kufanya ngono na wanawake wengi mpaka maisha yangu yakaonekana hayana maana kabisa.
“Wakati huo nikasoma Biblia kwa kadiri fulani. Waefeso sura ya tano ilinisadikisha nijaribu tena kutengeneza mambo yangu na mke wangu. Nikaona kwamba yeye hakuwa amekuwa mtiifu, wala mimi sikuwa nimetoa uongozi unaofaa. Lakini juma iliyofuata nikazini tena nikiwa katika safari ya kazi.
“Rafiki ya mtu huyo alimweleza kwamba kama kweli alipendezwa na mambo ya Mungu, Mashahidi wa Yehova wangeweza kumsaidia. Mwanamume huyo mwenyewe anaendelea kusema hivi: “Kweli Mashahidi walinisaidia. Mmoja wa waangalizi katika kundi alitumia wakati wake akijifunza Biblia nami. Mke wangu alijiunga nasi katika funzo kwa sababu ya badiliko kubwa nililofanya maishani mwangu. Sasa kwa mara ya kwanza maisha ya jamaa yetu yana furaha, na hata binti zetu wawili wanaweza kuliona badiliko. Nashindwa kupata maneno yenye mkazo unaoweza kueleza furaha kubwa ajabu ambayo mke wangu na mimi tumepata kwa kufuata maneno ya Biblia katika maisha zetu.”
[Picha katika ukurasa wa 85]
Kupashana habari kunahitajiwa kabisa ndipo ndoa iwe yenye furaha