Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 14 kur. 131-139
  • Uovu—Sababu Gani Mungu Anauruhusu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uovu—Sababu Gani Mungu Anauruhusu?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MUNGU ANAJIBU KWA KUSEMA: ‘MIMI NAJALI’
  • MASUALA YANAYOHUSU ULIMWENGU MZIMA YANATOKEA
  • KUPATA FAIDA KUTOKANA NA WAKATI ULIORUHUSIWA
  • JE! WEWE UNATAKA KUISHI WAKATI UOVU UTAKAPOKUWA UMEKWISHA?
  • Mtumaini Yehova Uishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Waovu Wataendelea Hata Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Wenye Shangwe Katika Mungu wa Wokovu Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kitabu Cha Biblia Namba 35—Habakuki
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 14 kur. 131-139

Sura ya 14

Uovu​—Sababu Gani Mungu Anauruhusu?

KAMA rafiki yako angenyang’anywa vitu vyake, alalwe kwa nguvu au auawe kisha mhalifu (mkora) mwenye tendo hilo aachiliwe, je! usingevurugika moyoni, uone maumivu moyoni na kukasirika? Uhalifu na udhalimu wa namna hiyo ni mfano mdogo tu wa mambo makubwa ambayo yamepata wanadamu.

2 Historia imejaa sana habari ya vita vyenye ukatili wa kinyama, umaskini wenye kumaliza watu, uhalifu na uonezi. Kwa sababu ya mambo hayo, watu wengine wameanza kutia shaka kama kweli kuna Mungu. Sisi tunajua kuna ushuhuda wenye kusadikisha kwamba Muumba yupo. (Waebrania 3:4; Warumi 1:20) Lakini hata uovu upo. Kwa hiyo, hata watu wengi wanaoamini Mungu yupo wanajiuliza, ‘Kweli yeye anatujali?’ Wanauliza, ‘Ikiwa Mungu anajali, mbona ameruhusu uovu uwepo kwa muda mrefu sana?’

3 Mara nyingi wanafalsafa na viongozi wa kidini wa-mejaribu kujibu maulizo hayo bila kutoa majibu yenye kuridhisha. Lakini Mungu mwenyewe anasema nini?

MUNGU ANAJIBU KWA KUSEMA: ‘MIMI NAJALI’

4 Kwa mambo tunayoona, tunaweza kufahamu kilichompa Habakuki nabii Mwebrania maoni yake juu ya jeuri na udhalimu. Yeye aliishi wakati ambao Wayahudi walikuwa wameangukia mazoea mengi mabaya, nayo yalimwuma Habakuki moyoni na kumfanya amwulize Mungu:

“Mbona wewe wanifanya mimi niutazame udhalimu? Mbona wewe waachilia ubaya? Uharibifu na jeuri vi mbele yangu; kuna ugomvi, na kuhitilafiana kunakuwa kwingi. Basi ile sheria na haki haitendi kazi, haishindi kamwe. Wale waovu wanawazinga wale wenye uadilifu, hivi kwamba haki imepotoshwa.”—Habakuki 1:3, 4, New International Version.

Ingawa Habakuki alisadiki Yehova ni mwadilifu, yeye alisumbuliwa sana na jeuri na udhalimu uliokuwa kati ya watu wake. Pia, wakati huo Wababeli walikuwa wakiendelea na mashambulio yenye fujo nyingi, wakifanya ujeuri na kuteka mataifa mengine na kuwaharibu. Ilielekea kuwa kwamba uovu ulishinda kila mahali ukiwa wenye nguvu. Nabii Habakuki alikosa kujua sababu gani Mungu hakufanya lo lote, ajapoona yaliyokuwa yakitendeka.—Habakuki 1:13.

5 Yehova alimhakikishia Habakuki katika njozi kwamba ule ulioelekea kuwa ufanisi wa waovu ulikuwa wa muda tu. Mungu hakuona tu yaliyokuwa yakitendeka, bali alijali pia. Alikuwa na “wakati uliowekwa” wa kutekeleza hukumu ya kimungu. Hata kama wanadamu walidhani hukumu hiyo ilikuwa inakawia, Habakuki alihakikishiwa kwamba, “Hiyo itatokea pasipo kushindwa. Hiyo haitachelewa.”—Habaku-ki 2:3, NW.

6 Mungu aliendelea kuonyesha anajali kwa kumfungua Habakuki macho aone mwito wa kushindana uliowaelekea wanadamu wakati huo. Yehova alisema: “Lakini kwa habari ya yule mwadilifu, kwa uaminifu wake yeye ataendelea kuishi.” (Habakuki 2:4, NW) Je! Habakuki angeukubali mwito huo wa kushindana, afanye yaliyokuwa mema na ya adili hata kama wale waliokuwa karibu yake wangetenda mambo mengine? Alihitaji aonyeshe imani kwamba Mungu angeshughulika na mambo inavyofaa katika ‘wakati wake uliowekwa.’

7 Historia inatueleza yaliyotukia. Wakati ulipofika, Mungu alichukua hatua ya kukomesha jeuri na udhalimu upande wa Wayahudi. Nchi ilishindwa kisha wengi wa wale watu wakachukuliwa mateka. Baadaye, Mungu alifanya hesabu na Babeli. Kama Yehova alivyokuwa ametabiri kupitia manabii wake, Wamedi na Waajemi wakiongozwa na Koreshi waliishinda Milki ya Babeli iliyoelekea kuwa na uwezo usioshindika.—Yeremia 51:11, 12; Isaya 45:1; Danieli 5:22-31.

8 Mfano mdogo huo unaonyesha Muumba wetu hafungi macho kujifanya haoni uovu. Yeye anajua upo na anajali. (Linganisha Mwanzo 18:20, 21; 19:13) Kama ni hivyo, basi sababu gani Mungu ameruhusu uovu uendelee mpaka sasa? Ili tuyaelewe maelezo yanayofaa ya Biblia, tunahitaji kurudi huko nyuma zilikoanzia taabu za kibinadamu.

MASUALA YANAYOHUSU ULIMWENGU MZIMA YANATOKEA

9 Kama inavyoelezwa katika Mwanzo sura ya tatu, Ibilisi alimwuliza Hawa habari za kutii kwake amri ya Mungu ya kutokula matunda ya mti uliotajwa wazi-wazi. Hawa alijibu kwamba kutokutii kungeleta hukumu ya kifo. Lakini Shetani akarudisha hivi:

“Ninyi hamtakufa hakika. Kwa maana Mungu anajua kwamba katika ile siku yenyewe ya kula kwenu kutokana na huo macho yenu hayana budi kufunguliwa na ninyi hamna budi kuwa kama Mungu, wenye kujua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5, NW.

Hapa Shetani alitokeza madai au masuala yaliyovihusu viumbe vyote vya Mungu, wanadamu na malaika.

10 Kwanza yule Ibilisi alitilia mashaka unyofu wa Mungu. Fikiria alitaka kuonyesha nini. Ikiwa Mungu hakusema kweli katika jambo hilo, je! angeweza kutumainiwa katika jambo, jingine lo lote? Je! viumbe vyake duniani au mbinguni vingelazimika nyakati zote kuyashuku maneno yote ya Mungu baada ya hapo? Tunajua leo namna watu wanavyoshuku wanasiasa wanaowasimamia, wanaotawala kwa kutumia uongo mwingi.—Linganisha Zaburi 5:9.

11 Dai la Shetani la kwamba Mungu ni mdanganyifu na ananyima viumbe vyake vitu vizuri lilitokeza pia suala la kwamba, Je! Mungu anastahili kutawala? Ulizo la kufaa kwa njia ya Mungu ya kutawala lilihusu ulimwengu mzima.

12 Tena, Shetani alipinga akisema kwamba wanadamu wanaweza kujiendesha wenyewe bila kumtegemea Mungu, kwamba wanaweza kujitawala wenyewe na wanapaswa kufanya hivyo. Ulizo likawekwa mbele ya wanadamu na malaika, Je! wanadamu wanaweza kusimamia mambo yao vizuri bila kumtegemea Mungu?

13 Masuala hayo mazito yanayohusu mema na mabaya yalipasa kujibiwa kabisa. Njia ambayo Mungu alichagua afanye hivyo inaonyesha wazi ana hekima na anataka kuona tukiwa na hali njema, sasa na wakati ujao pia. Mungu aliruhusu wakati upite, na wakati huo viumbe wote wenye akili wangeweza kuuona ushuhuda. Ili ulifahamu jambo hilo, fikiria ungefanya nini mtu fulani akidai mbele ya watu wengi kwamba wewe si mwanajamaa mwema, kwamba wewe ni msema-uongo na unatumia mamlaka yako kwa kuogopesha watu. Huenda mtu mwenye wasiwasi akaanza kuteta kwa kupiga makelele au hata kupigana na mshtaki huyo. Lakini ukiwa na uhakika wa kwamba shtaka lenyewe ni la uongo, ungeweza kuondoa mashaka akilini mwa watu kwa kuruhusu wakati upite ili watu wote watazame njia zako na matokeo mema yaliyo katika jamaa yako.—Mathayo 12:33.

14 Wakati umefunua ushuhuda gani juu ya masuala yaliyotokezwa katika Edeni? Kutokutii kwa wanadamu kumeleta magonjwa na uzee halafu kifo, kama Mungu alivyotangulia kuonya. Kwa hiyo Mungu hakuwa mdanganyifu kwa kutoa onyo lake, wala katika jambo hilo hakukuwa na msingi wa kutilia mashaka kufaa kwa utawala wake. Kuna uthibitisho pia wa kwamba mwanadamu hawezi kujiwekea viwango vyake mwenyewe, ajitawale mwenyewe bila kumtegemea Mungu. Hakuna namna yo yote ya serikali ya kibinadamu ambayo imeweza kuzuia vita, mafamba, uonezi, uhalifu na udhalimu. Hayo yanahakikisha maneno haya ya Biblia: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Zaidi ya hilo, wakati umethibitisha kwamba wanadamu hawawezi kukomesha taabu; bali, mara nyingi wao ndio wanaileta taabu yenyewe.

15 Taabu yenyewe inaonwa na watu wenye mioyo minyofu, walio na nia ya kukubali utawala wa Mungu na viwango vyake. Kwa kuwafikiria wao, Mungu atawachukulia hatua wale wanaoendesha uovu, sawa na alivyofanya kwa kiasi kidogo kinachotajwa katika kitabu cha Habakuki. Yehova atawamalizia mbali wote walio katika mbingu na juu ya dunia wanaoleta uovu na taabu. Kuna “wakati uliowekwa” wa jambo hilo, sawa na vile Mungu alivyomwambia Habakuki. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba “hiyo itatokea pasipo kushindwa. Hiyo haitachelewa.”—Habakuki 2:3, NW.

KUPATA FAIDA KUTOKANA NA WAKATI ULIORUHUSIWA

16 Watu wengi wanafikiria taabu za wanadamu tu wanapowaza kwamba Mungu ameruhusu uovu uwepo. Wanakosa kuyathamini masuala ya maana yanayoendelea kujibiwa. Pia, huenda, wakakosa kuziona faida wanazoweza kupokea kwa sababu Mungu ameruhusu wakati wa kuyajibu.—2 Petro 3:9.

17 Wakati ambao Mungu ameuruhusu ili kujibu masuala hayo umekuwa na urefu wa kutosha mpaka sisi tukaweza kuzaliwa. Mambo yo yote ambayo tumefurahia yamewezekana kwa sababu Mungu ameruhusu kuwe na wakati wa kufanya hivyo. Zaidi ya hilo, tumepewa nafasi ya kuthibitisha tunampenda Mungu na sisi ni washikamanifu kwake. Shetani alitokeza dai la kwamba hakuna mwanadamu ambaye angekuwa mwaminifu kwa Mungu, hata kusingekuwa na mmoja ambaye Mungu angeweza kumtaja kwamba, “Hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na uelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.” Tunaona jambo hilo katika kitabu cha Biblia cha Ayubu, sura za 1 na 2. Kumhusu yule Ayubu mwenye unyofu, Ibilisi alisema: “Je! huyo Ayubu yuamcha [Mungu] bure?” Shetani alidai kwamba Ayubu alifanya hivyo kwa sababu za kichoyo, kwa sababu Mungu alimpa ufanisi, lakini kama Ayubu angepata hasara ya ufanisi huo angemlaani Mungu. (Ayubu 1:7-12) Je! Shetani angeweza kugeuza wanadamu wote wamwache Mungu?

18 Mungu alimruhusu Shetani amletee Ayubu taabu nyingi. Ayubu akapoteza utajiri wake. Watoto wake wakauawa. Akapigwa kwa ugonjwa mbaya kiasi cha kutapisha mtu. Ayubu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu ingawa hakujua kwamba Shetani ndiye aliyekuwa akimfanya awe mtu wa kushambuliwa kipekee. (Ayubu 27:5) Ayubu alikuwa na uhakika Yehova asingemsahau na kwamba Muumba hata angemfufua akifa. (Ayubu 14:13-15) Yehova hawaachi washikamanifu wake hata kidogo. Katika wakati unaofaa alichukua hatua akauondoa uharibifu uliofanywa na Shetani. Ayubu alirudishiwa afya nzuri. Akapata watoto wengine 10 wenye sura nzuri, pamoja na ufanisi mkubwa na maisha marefu. Unaweza kusoma habari zote hizo zinazotia moyo katika Ayubu 42:10-17.

19 Pia masimulizi hayo yanatusaidia tufahamu sababu gani Mungu ameruhusu uovu uwepo. Kwa njia hiyo ilithibitishwa kwamba wanadamu fulani wangempenda Mungu yajapokuwapo matatizo ya maisha kisha wawe washikamanifu kwake wakiwa chini ya jaribu lo lote. Inafaa tujiulize, ‘Je! hivyo ndivyo sisi tumetenda tujapotaabika? Je! ndivyo tunavyotaka tuwe, kwa njia hiyo tusaidie kukanusha lile shtaka alilotokeza Shetani?’ (Mithali 27:11) Kitabu cha Ayubu kinatupa pia sababu ya kuhakiki kwamba Mungu anaweza kuondoa taabu zo zote wanazozipata wanadamu wakati huu ambao uovu umeruhusiwa uwepo.—Linganisha 2 Wakorintho 4:16, 17.

20 Sasa Mungu anawakumbuka wanadamu wanaoendelea kuwa washikamanifu kwake wajapopatwa na hali za uovu, kama vile alivyotazama Ayubu na Habakuki kisha akawakubali. Naye hatakosa kuwapa thawabu.—Malaki 3:16-18.

JE! WEWE UNATAKA KUISHI WAKATI UOVU UTAKAPOKUWA UMEKWISHA?

21 Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu anakusudia kuirudisha dunia hii katika hali ya paradiso, kama ile waliyoifurahia Adamu na Hawa kabla hawajauacha ushikamanifu. (Luka 23:43, NW au ZSB; Ufunuo 21:4, 5) Ndipo zitakapotimia kwa ukamili ahadi za Biblia kama hizi:

“Wale waovu watatokomea; huenda wewe ukawatafuta, lakini hutawaona wao; bali wale wanyenyekevu [au, wapole] watapata milki ya ile nchi wafurahie ufanisi na amani.”—Zaburt 37:10, 11, Good News Bible; Mithali 24:1, 20.

22 Watu wengi wanalalamika juu ya uovu na taabu, hata kumlaumu Mungu kwa sababu ya mambo hayo. Lakini kweli watu hao wanataka uovu uondolewe mbali, au kile wanachokitaka tu ni kumalizwa kwa maumizo yanayopata watu wakiisha kutenda uovu? Mwanadamu ndiye anayejiletea nyingi za taabu zake; basi anavuna anachopanda. (Wagalatia 6:7; Mithali 19:3) Uasherati na uzinzi unaleta magonjwa ya kisonono na kaswende (au sekeneko na tego), utoaji mimba na talaka. Uvutaji sigara unaleta kansa (donda baya sana) ya mapafuni. Ulevi na matumizi mabaya ya dawa za kulevya vinaharibu ini na ubongo. Kuvunja sheria zinazoongoza magari kunaleta misiba ya kifo. Je! wale wenye kusema, ‘Mbona Mungu anaruhusu uovu uwepo? Ataukomesha lini?’ wanataka kweli Mungu aukomeshe? Akifanya hivyo sasa hivi, kwa kuzuia mazoea hayo yasiwepo, wengi watalalamika wakisema anawawekea vizuizi.

23 Kwa hiyo, Mungu anaporuhusu uovu, hiyo inatupa nafasi ya kuonyesha tuko upande gani, tuna nini mioyoni. Mungu alimwambia Habakuki hivi: “Kwa habari ya yule mwadilifu, kwa uaminifu wake yeye ataendelea kuishi.” Jambo hilo linataka mtu asitawishe kuchukia mambo ambayo Mungu anaonyesha ni mabaya au maovu. (Habakuki 2:4, NW; 97:10) Huenda kuishi maisha ya namna hiyo kukafanya tusipendwe na jirani na washirika wengine. (1 Petro 4:3-5) Ayubu na Habakuki walikuwa na nia ya kuwa tofauti ili wawe washikamanifu kwa Mungu na kupata kibali yake. Ndivyo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova leo wanavyothibitisha kwamba jambo hilo linawezekana. Basi wao wanafurahia maisha zenye faida nyingi na zenye kuwaridhisha zaidi.

24 Watu wanaoufuata mwendo huu wanaongezea ushuhuda wenye kuonyesha Shetani ni mwongo wa mwisho. Wanathibitisha kwamba wanadamu wanaweza kuwa waaminifu kwa Mungu, huku wakihakiki kwamba njia yake ya kutawala inafaa na ni yenye uadilifu. Naye Mungu anajua kwamba watu wa namna hiyo wanaweza kuaminiwa wapewe kazi ya kutunza paradiso itakayorudishwa duniani. Wakati huo maisha yatapendeza sana mpaka huzuni na maovu ya zamani yasahauliwe kale na kale. Yatasahauliwa kama vile tumekwisha kusahau rnaumivu na huzuni tuliyokuwa nayo miaka mingi iliyopita, wakati ule tulipokwaruzwa na kitu gotini tukiwa watoto.—Isaya 65:17; Yohana 16:21.

25 Hilo ni taraja la kupendeza sana na linatusaidia kufahamu kwamba ruhusa ambayo Mungu ametoa uovu uwepo ni kipindi kifupi tu kinachoelekeza kwenye utimizo wa kusudi lake la milele. Masuala yale ya kisheria na adili yaliyofanya ruhusa hiyo itolewe yatajibiwa yamalizike milele hata milele.

26 Lakini hata tukifahamu sababu ya Mungu kuruhusu uovu, bado tuna haki ya kutaka kujua hivi: Utakwisha wakati gani? “Wakati uliowekwa” na Mungu wa kukomesha uovu duniani pote ni wakati gani? Acheni sasa tuone.

[Mambo ya Kuzungumziwa]

Sababu gani inafaa kuchunguza inavyosema Biblia juu ya uovu? (1-3)

Tunaweza kujifunza nini kutokana na Habakuki kuhusu jambo hill? (4-8)

Ni kwa njia gani masuala ya maana sana katika ulimwengu mzima yalitokea katika Edeni? Yalikuwa masuala gani? (9-12)

Masuala hayo yangejibiwa kabisa kwa njia gani? (13-15)

Sisi tunahusikaje katika suala jingine linalohitaji kujibiwa kabisa? (16-20)

Biblia inatolea watu taraja gani? Na hilo lina maana gani kwetu? (21-23)

Tunaweza kufaidikaje milele na ruhusa ambayo Mungu ametoa uovu uwepo? (24-26)

[Sanduku katika ukurasa wa 131]

Dakt. W. R. Inge, aliyekuwa kasisi wa St. Paul’s Cathedral, London, miaka kadha iliyopita alisema:

“Maisha yangu yote mimi nimeng’ang’ana sana nilijue kusudi la kuishi. Nimejaribu kujibu matatizo matatu yaliyoelekea nyakati zote kuwa ya maana sana: lile tatizo la umilele; lile tatizo la utu wa kibinadamu; na lile tatizo la uovu. Mimi nimeshindwa. Hakuna hata moja ambalo nimeweza kutatua.”

[Picha katika ukurasa wa 137]

Taabu hazikumfanya Ayubu ampinge Mungu; yeye alivumilia akabarikiwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki