Sura ya 1
“Ufalme Wako Uje”!
1. Ikiwa Ufalme wa Mungu ungezileta upesi hali zinazoonyeshwa na picha hapa, ungekuwa na maana gani kwako?
MANENO machache ya sala yamesemwa mara nyingi zaidi ya hayo juu. Labda wewe msomaji umeisema sala hiyo. Na bila shaka tunahitaji ufalme wa Mungu! Ingekuwa vizuri ajabu kuishi chini ya hali zile zinazoonyeshwa kwa picha katika kurasa hizi! Hilo ndilo tumaini ambalo ufalme wa Mungu unatutolea: Amani na upatani katika dunia yote. Jamii za wanadamu zimeungana katika vifungo vya upendo wa kweli. Kila mtu anapenda kufanya kazi yenye matokeo na kuyafurahia matunda ya jasho lake. Hewa inajawa na muziki wa viumbe na nyimbo na vicheko vya binadamu wenye furaha. Kuna jamii ya wanadamu yenye afya duniani pote ambayo hakuna anayezeeka wala kuwa mgonjwa. Watu wanafurahia amani pamoja na wanyama, wanafurahia harufu nzuri ya maua, uzuri wa mapambo ya nchi na misimu yenye kuendelea kubadilika. Ndiyo, kama tutakavyoona, yote hayo na mengi zaidi yameahidiwa kuwa katika dunia yetu baada ya kuja kwa ufalme wa Mungu.
2, 3. Ni mabadiliko gani katika miaka ya karibuni yanakazia uhitaji wa ufalme wa Mungu?
2 Walakini, sasa mambo yako tofauti kabisa. Maana tunazipitia nyakati ambazo Biblia inasimulia kuwa “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Unajua namna nyakati hizi zenye hatari zimehusu uhai wako mwenyewe. Wengi watakaosoma kurasa hizi wamefiwa na wapendwa wao katika vita na jeuri nyingine za karne hii. Hata hivyo mataifa yamo katika mashindano yenye kivumbi ya kuunda silaha nyingi kuliko zamani zote zilizotangulia. Na sasa tayari yana silaha nyingi za kiasi kinachozidi zile za kuangamiza wanadamu wote.
3 Matatizo mengine, yanayohusiana sana na nyumbani, yanatuhangaisha pia. Kwa sababu ya ongezeko la masharnbulizi ya kijambazi, mauaji na wanawake kulalwa kinguvu, wengi wetu tunaona ni hatari hata kutembea katika barabara za mjini. Na je! hatupati habari za talaka zaidi, jamaa zenye kuvunjika na kutokutii? Katika kizazi hiki chenye kuendekeza (kuruhusu mno) watu wafanye ngono na kuzoea dawa za kulevya, watu wengi wanaogopa kupeleka watoto wao kwenye shule za watu wote. Iwapo unaishi katika ujirani au nchi fulani ambako matatizo hayo hayajatokea bado, imekupasa ushukuru sana!
4, 5. (a) Ni matatizo gani mengine yanayohusu maisha zetu? (b) maelekeo gani ya ulimwengu yanayoonyesha kwamba inahitajiw haraka ‘ufalme wa Mungu uje’?
4 Inakugharimu fedha ngapi siku hizi kununua chakula? Inakugharimu fedha ngapi kudumisha gari lako? Bei za chakula na mafuta zinapopanda sana, hali dhaifu ya ulimwengu inatoa tumaini baya la wakati ujao. Ulimwengu wetu unaelekea wapi? Kipande cha habari katika gazeti U.S. News & World Report la Agosti 4, 1980, kilikazia uzito wa hatari hiyo. Kilisema: “Hatua kubwa zilizo mpya zisipochukuliwa, miaka 20 tokea sasa ulimwengu utakuwa sayari chafu-chafu isiyo imara, yenye mabilioni ya watu maskini wenye kushindania kupata mali chache za bei za juu. Onyo hilo lilitolewa Julai 24 kutoka tume ya rais iliyo kamilisha uchunguzi wa miaka mitatu.” Kati ya mambo mengine, uchunguzi huo ulifunua kwamba kufikia mwaka wa 2000 idadi ya watu ulimwenguni itafikia bilioni 6.3, kwamba—zaidi ya infuleshoni—bei za chakula zitaongezeka mara mbili, kwamba majangwa yatapanuka na misitu itatoweka, na kwamba angalau nusu ya mafuta ulimwenguni yatatindika. Maana yake, ikiwa mfumo uliopo utaendelea kuwapo muda huo.
5 Mataifa moja moja, au hata ule Umoja wa Mataifa yameweza kufanya nini kuzuia hatari hiyo? Bado hayajafanya mengi. Mambo hayo yote yanaonyesha jinsi tunavyouhitaji ufalme wa Mungu haraka sana!
UFALME HUO NI NINI?
6. Sababu gani tungekaribia kukata tamaa ikiwa ufalme wa Mungu ungekuwa katika mioyo ya watu tu?
6 Je! ni hali tu iliyo ndani ya mioyo ya waamini? Yaani, watu wa kutosha watakapoongoka wawe Wakristo, je! ufalme wa Mungu utakuwa umekuja? Watu fulani wamewaza hivyo, wakielekeza kwenye Luka 17:21 panaposema: “Ufalme wa Mungu umo ndani yenu.” Lakini ikiwa kauli yao ni sahihi, ule ufalme unazidi kuwa mbali sana. Sababu gani? Sababu kile kiasi cha wanaodai kuwa Wakristo ni kidogo sana kuliko asilimia 25, kikilinganishwa na wengine katika ulimwengu leo. Na kinaendelea kupungua. Pia, kuna mamia ya mamilioni ya washiriki wa makanisa wanaoenda kanisani mara chache sana.
7, 8. Kuyachunguza Maandiko kunatusaidiaje kuifikia maana ya kweli ya Luka 17:21?
7 Fikiria hili pia: Yesu alikuwa akiambia nani aliposema, “Ufalme wa Mungu umo ndani yenu”? Ni Mafarisayo wanafiki ambao kuhusu wao Yesu alitumia maneno ya Mungu kupitia nabii Isaya: “Mioyo yao iko mbali nami.” (Mathayo 15:1, 8; Isaya 29:13) Ule Ufalme ungeweza kuingiaje mioyo hiyo migumu? Basi, maneno hayo ya Yesu yana maana gani? Kuna kidokezi katika tafsiri ya Habari Njema kwa Watu Wote. Humo tunasoma hivi: “Utawala wa Mungu uko kati yenu.” Na hivyo ndivyo tafsiri nyingine nyingi za Biblia zinasema pia, kama Jerusalem Bible ya Kikatoliki na The New English Bible.
8 Basi, hapa Yesu alikuwa akijisema kwamba yuko kati yao akiwa ndiye Mfalme-mkusudiwa. Hakika yeye alikuwa miongoni mwao, akiwa mtu halisi. Na sisi pia tunapaswa kufahamu vizuri kwamba ule Ufalme ni ufalme halisi, serikali halisi, kama vile Mfalme wao alivyo mtu halisi.
ULE UHALISI LEO
9, 10. Ufalme halisi ni nini, na unaweza kufaidije raia zao?
9 Leo, falme chache zimesalia katika dunia hii. Hizo ni serikali halisi, kutia ile ya Norway, Uingereza, Yordani na Nepali, kutaja chache. Katika hizo kuna mfalme (au malkia), pamoja na watawala washirika wanaotumika kuwa bunge, baraza au jamii nyingine ya kiserikali. Halaiki za watu wanafanya shughuli zao za kila siku wakiwa chini ya kikundi hicho kinachotawala kilicho kidogo kwa kulinganishwa nao. Halaiki hizo za watu ndio raia za ufalme.
10 Mfalme na watawala wenzake wanapohangaikia sana masilahi ya watu, ufalme unaweza kuwapa faida nyingi. Ndivyo ilivyokuwa katika ufalme wa kale wa Sulemani, watu walipokuwa “wengi kama mchanga wa pwani kwa wingi, wakila, na kunywa, na kufurahi.”—1 Wafalme 4:20; 10:1-9.
11. Ni kwa njia gani ufalme wa Mungu unafanana na falme zilizo hapa duniani?
11 Je! ule uhakika wa kwamba ufalme wa Mungu unatawala ukiwa mbinguni unaufanya usiwe halisi? Sivyo! Kwanza, una mfalme aliye hai na mwenye kutenda sana sana. Huyo ni Bwana Yesu Kristo mwekwa wa Mungu mwenyewe, ambaye Biblia inasema habari zake hivi: “Juu yake mataifa yataweka tumaini lao.” (Warumi 15:12, NW) Kama vile serikali zilizo duniani, ufalme wa kimbingu una jamii inayotawala. Biblia inaonyesha kwamba jamii hiyo ni wafalme washirika wachache, ambao wameonyesha ukamilifu wao kwa Mungu wakiwa wanaume na wanawake hapa duniani. Yesu aliwaambia hao hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32; Ufunuo 5:9, 10; 20:4) Ufalme huo una mamlaka ya kimbingu. Ikiwa mahali panapofaa katika mbingu, serikali hiyo ya Ufalme inaweza kutoa amri zipelekwe kwenye sehemu yo yote duniani, kwa njia yenye nguvu zaidi kushinda radio au chombo cha kukuza nuru ya anga za juu.
12, 13. Ufalme wa Mungu una (a) sheria za aina gani. (b) mpango wa kielimu wa aina gani. (c) mpango wa kiafya wa aina gani?
12 Namna gani sheria? Ndiyo, ufalme wa Mungu unatenda kazi kwa kufuata sheria—sheria zilizo bora zaidi sana, zilizotungwa na Mungu kwa faida ya watu. Unaweza kuzisoma katika Biblia. (Kumbukumbu la Torati 6:4-9; Marko 12:28-31) Je! Ufalme huo una mfumo (mpango) wa kielimu? Bila shaka! Sasa hivi mpango wa kielimu unapanuka ili kusaidia watu wenye mioyo minyofu wa mataifa yote na vikundi vya watu na lugha, kuwatayarisha waje kupata uzima wa milele chini ya usimamizi wenye uadilifu wa Ufalme. Hata uishi katika nchi gani ya dunia, wewe binafsi unaweza kujifaidi na mtaala huo.—Mathayo 24:14; Ufunuo 7:9, 10; Isaya 54:13.
13 Je! Ufalme huo una mpango wa kiafya? Una mpango wa kiafya unaofaa kushinda yote—mpango unaotegemea ile dhabihu ya ukombozi wa Bwana Yesu Kristo. Mpango huo utaondolea wanadamu maumivu yote na udhaifu wa mwili, ili wafikie uzima wa milele kwa ujazi wa afya nzuri. (Isaya 25:8; Yohana 10:10) Alipokuwa hapa duniani, Yesu alifanya miujiza mingi, akaonyesha angekuwa na mamlaka na uwezo wa kuponesha wagonjwa, wa kurudishia vipofu macho, kuponya viwete, na hata kurudisha wafu kwenye uzima. (Luka 7:20-23) Ingawa mpango huo wa Ufalme ungali uko usoni, wale wanaojifunza habari za huo leo wanajifunza pia kuishi kwa usafi na adili, na sasa hivi wanarudishwa kwenye afya bora ya kiroho. Tumaini lao ni halisi.—Isaya 65:14; Warumi 10:11.
14. Alipokuwa hapa duniani, Yesu alikazia nini katika kufundisha kwake?
14 Yesu alipokuwa binadamu hapa duniani, alifundisha mambo mengi juu ya ufalme wa Mungu na, kwa kweli, alitoa mwonjo wa maisha yatakayokuwa chini ya utawala wa ufalme huo. (Luka 4:43; Mathayo 12:22-28) Ili wanafunzi wake waweze kumkaribia Mungu sana katika ule uhusiano wa wana na baba mwenye upendo, aliwafundisha juu ya Mungu. Aliwapa mwongozo mzuri wa kupambana vya kufaa na hali zile tunazokabili maishani.—Yohana 1:18; 14:6.
KILE CHANZO CHA FURAHA YA KWELI
15. Sababu gani watu wa siku za Yesu walihitaji faraja kama sisi leo?
15 Ile sala ya ‘ufalme wa Mungu uje’ ni sehemu ya yale Mahubiri ya Mlimani, ambayo Yesu alitoa upande wa kilima chenye kuelekea Bahari ya Galilaya. Wasikilizaji walikuwa wanafunzi wake wateule, pamoja na halaiki ya watu wengine. Hao walikuwa ‘wamechoka na kutawanywa’ na watu wenye choyo. (Mathayo 9:36) Maneno ya Yesu yalifariji wasikiaji wake, nayo yanaweza kutufariji sisi leo pia.
16. Ni akina nani wanaopata furaha ya kweli, na jinsi gani?
16 Yesu alianza mahubiri yake kwa kuelekeza kwenye chanzo cha furaha ya kweli. Je! kingetazamiwa kupatikana katika utajiri wa kimwili, tafrija, kutafuta raha na msisimuko? Hapana, maana Yesu aliweka mkazo juu ya mambo ya kiroho. Alionyesha kwamba watu “wanaoona uhitaji wao wa kiroho” na “wanaoona njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu” wangepata furaha yenye kuendelea kuhusiana na ufalme wa Mungu. (Mathayo 5:3, 6, NW; Luka 8:1, 4-15) Je! wewe unasitawisha mapendezi hayo ya kiroho?
17, 18. (a) Ni lazima tufanye nini ili tukubaliwe na Mungu? (b) Uhakikisho wa Yesu katika Mathayo 6:26-33 unakuvutiaje?
17 Alipokuwa akiendelea na mahubiri yake, Yesu alionyesha kwamba, ili tukubaliwe na Mungu, ni lazima tujifunze kuwa waigaji wa Baba yetu wa kimbingu. Imetupasa tuonyeshe sifa zake na mwenendo wetu upatane na viwango vyake. (Mathayo 5:43-48; Waefeso 5:1, 2) Ili tumpendeze ibada yetu haiwezi kuwa desturi tu tunayofuata mara moja au mbili kila juma. Ni lazima iwe ibada hai, yenye utendaji, inayoonyeshwa na maisha yetu ya kila siku na namna tunavyohangaikia wanadamu wenzetu kwa upendo.
18 Walakini, je! tukitanguliza mambo ya kiroho maishani mwetu, haitatufanya tukose vitu katika jamii ya leo yenye pupa, yenye kujitafutia faida? Hata kidogo! ‘Tukitafuta kwanza ufalme wa Mungu na haki yake,’ ndipo tutakapoongezewa vitu vingine vyote vilivyo vya lazima maishani. Yesu anaeleza hilo vizuri katika Mathayo 6:26-33, andiko ambalo imekupasa usome.
19, 20. (a) Sababu gani ni jambo la maana kujua maoni ya Mungu juu ya ibada yetu? (b) Tunaweza kusaidiwaje kutanguliza ufalme wa Mungu maishani mwetu? (c) Sababu gani tutafaidika kwa kuifikiria tena “Sala ya Bwana”?
19 Basi, ‘tutatafutaje ufalme kwanza’? Je! maana yake ni kwamba ‘tukienda kwenye kanisa tunalojichagulia’ tutapokea baraka ya Mungu bila shaka? Au tunahitaji kutafuta namna ya ibada ambayo Mungu anatuchagulia? Angalia aliyosema Yesu juu ya hilo: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.” Alionyesha wazi kwamba watu fulani waliodai ati ‘walitoa unabii kwa jina lake na kwa jina lake wakafanya miujiza mingi’ hakika wangekuwa ‘watendao maovu’ kulingana na maoni ya Mungu. (Mathayo 7:21-23; ona pia 7:13, 14.) Tunaweza kujuaje hakika maoni ya Mungu juu ya ibada yetu? Ni kwa kufahamu vizuri tu yale yaliyo katika Neno lake, Biblia.
20 Kuichunguza Biblia kutatusaidia tuuweke ufalme wa Mungu mbele maishani mwetu kama unavyostahili, na kwa jinsi itakavyopatana na hali zetu mmoja mmoja. Kutatusaidia tuwe na maoni mapya juu ya maisha, na kuthamini mambo yaliyo ya maana zaidi ya yote. Hivyo na tuichunguze ile sehemu ya Mahubiri ya Mlimani ya Yesu inayojulikana kuwa “Sala ya Bwana.” (Mathayo 6:9-13) Kuifikiria tena hiyo Sala ya Kielelezo kutatusaidia tupate maoni ya kweli juu ya anayotutaka Mungu tufanye iwapo twataka kuona furaha ya kweli. Kutatuonyesha kwamba kichwa chenye kusisimua cha Biblia ni kutakaswa kwa jina la Mungu kupitia ufalme wake ulio mikononi mwa Yesu Kristo.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
JE! WANADAMU WANAHITAJI UFALME WA MUNGU?
“Ikiwa kifaa cha kinyukilia chenye megatoni moja kingelipuliwa juu ya Jiji la New York, inaelekea kingeua watu milioni 2.25 mara hiyo, kiumize vibaya wengine milioni 3.6, . . . kikundi cha matabibu na wanafizikia wa nyukilia walikubaliana jana. . . . Wanaamini kwamba ulimwengu huu utaangukiwa na vita hiyo kabla ya kumalizika karne hii na kwamba itafanya isiwezekane wanadamu kuendelea kuishi.” —New York “Times,” Septemba 27, 1980.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
UHALISI WA UFALME WA MUNGU
MFALME: Yesu, akiwa na mamlaka ya kutawala muda wa miaka 1,000.
WATAWALA WENZI WA KIMBINGU: Walichaguliwa na Mungu kutoka wanadamu waaminifu.
ENEO LA UTAWALA: Dunia yetu itakayorudishiwa hali za paradiso kote kote.
RAIA WASHIKAMANIFU: Mabilioni, kutia wafu watakaofufuliwa.
SHERIA: Zinategemea uadilifu wa Mungu, sheria ya kifalme ya upendo.
MPANGO WA KIELIMU: Kusaidia watu wa makabila yote wafurahie maisha ya furaha sasa, na kuwatayarisha kuja kupata uzima wa milele katika paradiso ya kidunia.
[Ukurasa mzima wa picha katika ukurasa wa 4]