Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • sj kur. 17-21
  • Shughuli za Baada ya Masomo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shughuli za Baada ya Masomo
  • Shule na Mashahidi wa Yehova
  • Habari Zinazolingana
  • Ugumu wa Utofautiano wa Kidini
    Mashahidi wa Yehova na Elimu
  • Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Sikukuu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Krismasi Ni ya Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
Pata Habari Zaidi
Shule na Mashahidi wa Yehova
sj kur. 17-21

Shughuli za Baada ya Masomo

Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba maisha si kujifunza na kufanya kazi tu. Mazoezi na tafrija fulani wakati wa saa za shule zinatoa pumziko na burudisho linalohitajiwa. Hata hivyo labda umepata kuona kwamba vijana-Mashahidi wengi hawashiriki. Maelezo mafupi yanaweza kukusaidia ufahamu maoni yetu juu ya jambo hili.

Tayari wazazi-Mashahidi wana mpango wa shughuli zinazotegemea ibada yao. Na wazazi wanatiwa moyo watie tafrija katika mpango huo wa jamaa. Kwa kuwa wazazi ndio wanaopanga na kuangalia tafrija na vitumbuizo vya watoto wao, wakishiriki nao mara nyingi, usimamizi unaohitajiwa unatolewa.

Huenda nyakati nyingine jamaa chache za Mashahidi zikakutana pamoja ili zifurahie namna mbalimbali za vitumbuizo. Pia jamaa hizo zinasafiri mara kadha kila mwaka zikahudhurie mikusanyiko mikubwa zaidi inayoitwa makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya. Mara nyingine safari hizo zinatoa nafasi za kutembelea nyumba za vitu vya ukumbusho, sehemu za kihistoria na mahali pengine penye mambo ya kupendeza ya utamaduni. Kwenye mikusanyiko hiyo vijana-Mashahidi wanakutana na kufurahia ushirika wa vijana wengine kutoka sehemu nyingine za nchi walio na mradi mmoja nao wa kumtumikia Mungu wao, Yehova.

Sisi tunaliona kuwa jambo la maana sana vijana wetu wafurahie ushirika huo ulio mzuri, hasa kwa sababu viwango vya adili vya jamii ya kibinadamu leo vinazidi kuharibika. Mashahidi wa Yehova wanafuata kwa uzito onyo hili la Biblia: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” Na, kama tulivyotangulia kusema, sisi tunajaribu kufuata maneno haya ambayo Kristo aliwaambia wafuasi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 15:33; Yohana 15:19, New World Translation) Kanuni hizo zinaongoza maoni ya jamaa za Mashahidi juu ya shughuli za shule za baada ya masomo, pamoja na zifuatazo:

Michezo: Mazoezi ya mwili, kama yale tunayopata katika michezo ni mazuri kwetu. Lakini ili jambo hilo lionwe kwa maoni yanayofaa, Biblia inasema: “Uwe ukijizoeza utawa kuwa shabaha yako. Kwa maana kujizoeza kimwili ni kwenye faida kidogo; lakini utawa ni wenye faida kwa mambo yote.” (1 Timotheo 4:7, 8, New World Translation) Kupatana na shauri hilo, Mashahidi wa Yehova wanathamini ubora wa mitaala ya elimu ya kimwili inayotolewa wakati wa saa za shule.

Lakini, pia wazazi-Mashahidi wanaona kwamba mara nyingi shule zinakazia mno michezo. Kwa hiyo wanapozoeza watoto wao, wanajaribu kuweka mkazo wa kiasi juu ya faida ya michezo. Wanatumaini watoto wao watataka wafuatie kazi yao ya maisha ya kuwa wahudumu wa Mungu, wala si kuwa wanamichezo. Hivyo wazazi-Mashahidi wanawatia moyo watoto wao watumie saa za baada ya shule sana-sana wakifuatia mapendezi ya kiroho, badala ya kuwa bingwa katika mchezo fulani.

Tunaamini kwamba kushiriki michezo iliyopangwa na vyama vya michezo, kungefanya vijana-Mashahidi wawe na mashirika mabaya. Pia tunaona kwamba ile roho ya kushindana katika michezo ya kisasa, yaani, wazo la kusema ‘hakuna jambo jingine ISIPOKUWA kushinda tu,’ ni lenye matokeo hatari. Hivyo ikiwa vijana-Mashahidi wanahitaji tafrija ya ziada, wazazi wao wanawatia moyo watafute tafrija hizo wakiwa pamoja na waamini wenzao, ndiyo, “pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi.”—2 Timotheo 2:22.

Dansi za Shule: Kama michezo, kucheza dansi kunaweza pia kuwa shughuli nzuri, yenye afya. Ni wazi kwamba Yesu Kristo hakupinga kucheza dansi, kwani alitaja kucheza dansi kuwa sehemu ya mwadhimisho unaofaa katika mfano wake juu ya mwana mpotevu. (Luka 15:25) Hata hivyo, labda umeona kwamba kwa kawaida vijana-Mashahidi hawahudhurii dansi zinazodhaminiwa na shule. Kwa nini?

Sababu hasa ni mazingira yasiyofaa ambayo mara nyingi yanahusiana na dansi za shule. Kwa ujumla kunakuwa na kuvuta tumbaku, kunywa pombe kupita kiasi, matumizi ya dawa za kulevya, na pia mwenendo wenye sifa mbaya unaohusu ngono. Hivyo mtu anayehudhuria dansi hizo, bila kuepukika anawekwa pamoja na washiriki wasio safi. Hivyo, kupatana na shauri la kufuatia shughuli “pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi,” ni desturi ya Mashahidi wa Yehova kujiepusha na dansi za shule.

Matembezi ya Wavulana Pamoja na Wasichana: Nyakati za hivi majuzi matembezi ya wavulana pamoja na wasichana yamekuwa namna ya tafrija inayopendwa sana mahali pengi. Hata vijana wenye miaka kama 13, 14 na 15 kufika 17 hivi wote wanafanya matembezi ya wavulana pamoja na wasichana. Wanaweza kuonwa shuleni wakishikana mikono, wakibusiana, au hata kufanya vituko kuzidi hivyo. Wazazi-Mashahidi hawaamini inafaa watoto wao ambao bado ni wachanga mno kuoana wajitenge wakiwa peke yao, mvulana na msichana, na kujitia katika mwenendo ambao kwa jumla unahusiana na matembezi ya wavulana pamoja na wasichana.

Vyama vya Shule: Wanafunzi wenye mapendezi yanayofanana huenda wakataka kushiriki mapendezi hayo wakiwa wanachama wa chama cha shule. Lakini, mara nyingi kusudi kubwa la vyama hivyo ni kutimiza shughuli za starehe. Na imeonwa kwamba kushiriki shughuli hizo pamoja na vikundi fulani vya wanafunzi mara nyingi kunaongoza kwenye mwenendo usio wa adili nzuri. Kwa sababu ya kwamba jambo baya laweza kutokea, sisi tunaona kwamba inafaa kufikiria hilo kwa uangalifu kabla ya kujiunga na chama cha shule.

Maswali ya maana ambayo vijana-Mashahidi na wazazi wao wangefikiria ni haya: Je! shughuli za chama zinafanywa wakati wa saa za shule tu? Je! zinasimamiwa sana na shule? Je! kuwa mwanachama kutataka kutumia wakati baada ya shule ambao ungetumiwa vya kufaa katika shughuli za jamaa au za kundi? Hatimaye, ni daraka la wazazi-Mashahidi kuamua ni vyama au matengenezo gani ya shule, yakiwapo, ambayo wataruhusu watoto wao wajiunge nayo.

Michezo ya Kuigiza ya Shule: Mashahidi wa Yehova hawakatazi michezo yenyewe ya kuigiza. Michezo ya kuigiza ya Biblia ni sehemu ya maana ya programu zetu za mikusanyiko ya wilaya. Hata hivyo wazazi-Mashahidi watafikiria mambo kadha kabla ya kuamua kama wataruhusu au hawataruhusu watoto wao washiriki michezo ya kuigiza ya shule. Kwa mfano, Je! kinachofananishwa katika mchezo kinapatana na kanuni za Biblia? Vijana-Mashahidi hawangeshiriki mchezo wa kuigiza ambao ungekubali viwango vya adili ambavyo Biblia inalaumu. Tena, wakati mwingi unahitajiwa ili kujizoeza mchezo, na kuna uwezekano wa kuwa na mashirika yasiyofaa. Hivyo katika kuamua kama vijana-Mashahidi watashiriki au hawatashiriki mchezo wa kuigiza, wazazi wao watafikiria kwa uangalifu mambo hayo.

Michango ya Damu na Michango Mingine: Mara kwa mara wanafunzi katika shule nyingi wanaombwa watoe michango ya kusaidia kusudi moja au jingine. Mara nyingine ombi linalotolewa ni la kuchanga damu itakayotumiwa katika utibabu wa kuitia mishipani mwa mtu mwingine. Lakini, ufahamu wetu wa amri ya Biblia ‘kujiepusha na damu’ ni kwamba haipasi kuliwa wala kutumiwa kwa njia yo yote. Kwa hiyo, kwa sababu ya dhamiri, sisi hatutoi wala kupokea damu.—Mwanzo 9:4-6; Mambo ya Walawi 17:10-14; Matendo 15:19, 20, 28, 29.

Kwa sababu zilizotangulia kuzungumzwa katika broshua hii, kama kuna ombi la kuchanga fedha za kuendeleza kusudi fulani la kisiasa au kuhusiana na sikukuu fulani au mwadhimisho fulani wa kidini, Mashahidi wa Yehova hawangetoa mchango wa kusudi hilo. Wala sisi hatungeshiriki michezo ya bahati nasibu wala shughuli zo zote kama hizo za kucheza kamari. Lakini, kuna sehemu nyingine ambazo mtu binafsi angetoa uamuzi wa kama atachanga au hatachanga kulingana na hali zenyewe. Kwa mfano, kama kuna mwanashule mwenzao ambaye ameumia au ni mgonjwa na kuna uhitaji wa kuchanga fedha ili kununua maua au zawadi nyingine, wanafurahi kushiriki upaji wa namna hiyo wakiwa na uwezo wa kufanya hivyo.—Matendo 20:35.

[Blabu katika ukurasa wa 16]

‘‘Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.’’—1 Wakorintho 15:33, New World Translation

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki