Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • na kur. 3-5
  • “Jina Lako Litukuzwe”—Jina Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Jina Lako Litukuzwe”—Jina Gani?
  • Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Majina Katika Nyakati za Biblia
  • Jina la Mungu Ni Jina Gani?
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Majina Yana Maana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Mungu Anaitwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu Wote)—2019
  • Jinsi ya Kujua Jina la Mungu
    Amkeni!—2004
Pata Habari Zaidi
Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
na kur. 3-5

“Jina Lako Litukuzwe”—Jina Gani?

JE! WEWE ni mtu wa dini? Basi, bila shaka wewe, kama wengine wengi, unamwamini Mtu Mkuu Kuliko Wote. Na inaelekea unaiheshimu sana ile sala inayojulikana sana inayotolewa kwa Mtu huyo. Sala ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake inayojulikana kuwa Sala ya Bwana, au Baba Yetu. Sala hiyo inaanza hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.”—Mathayo 6:9.

Je! umetaka kujua ni kwa nini Yesu alitanguliza ‘kutukuzwa,’ au kutakaswa kwa jina la Mungu katika sala hiyo? Kisha, alitaja mambo mengine kama Ufalme wa Mungu uje, mapenzi yafanywe duniani na dhambi zetu zisamehewe. Hatimaye kutimizwa kwa mambo mengine hayo yanayoombwa kutakuwa na maana ya amani isiyo na mwisho duniani na uzima wa milele kwa wanadamu. Unaweza kufikiria jambo lo lote lenye maana kuliko hilo? Hata hivyo, Yesu alitufundisha tuombe katika sala kwanza jina la Mungu litakaswe.

Yesu hakufundisha bila kukusudia tu kwamba wafuasi wake watangulize jina la Mungu katika sala zao. Kwa kuwa alilitaja mara nyingi katika sala zake mwenyewe, kwa wazi jina hilo lilikuwa lenye maana kubwa sana kwake. Pindi moja alipokuwa akisali peupe kwa Mungu, alisikiwa akisema: “Baba, litukuze jina lako!” Mungu mwenyewe akajibu: “Nimelitukuza, na nitalitukuza tena.”—Yohana 12:28, The Jerusalem Bible.

Jioni ile kabla Yesu hajafa, alikuwa akisali na wanafunzi wake wakisikia, tena akasikiwa akikazia umaana wa jina la Mungu. Alisema: “Mimi nimejulisha jina lako kwa watu uliochukua kutoka ulimwengu ili unipe mimi.” Baadaye, akarudia kusema: “Nimejulisha jina lako kwao na nitaendelea kulifanya lijulikane.”—Yohana 17:6, 26, JB.

Kwa nini jina la Mungu lilikuwa la maana sana kwa Yesu? Kwa nini alionyesha kwamba ni la maana kwetu sisi, pia, kwa kutuambia tusali ili litakaswe? Ili tufahamu hilo, tunahitaji kujua jinsi majina yalivyoonwa katika nyakati za Biblia.

Majina Katika Nyakati za Biblia

Ni wazi kwamba Yehova Mungu aliweka katika mwanadamu tamaa ya kuviita vitu majina. Mtu wa kwanza alikuwa na jina, Adamu. Katika habari ya uumbaji, mojapo la mambo ya kwanza ambayo Adamu ameripotiwa kuwa akifanya ni kuwaita wanyama majina. Mungu alipompa Adamu mke, mara hiyo Adamu akamwita “Mwanamke” (’Ish·shahʹ, katika Kiebrania). Baadaye, akampa jina Hawa, maana yake “Aliye Hai,” kwa sababu “yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai.” (Mwanzo 2:19, 23; 3:20) Hata leo tunafuata desturi ya kuwapa watu majina. Ndiyo, ni vigumu kuwazia namna tungeweza kuishi bila kuwa na majina.

Ingawa hivyo, katika nyakati za Waisraeli, majina hayakuwa vibandiko tu vya kutambulisha vitu. Yalikuwa na maana ya kitu fulani. Kwa mfano, jina la Isaka, “Kicheko,” lilikumbusha kile kicheko cha wazazi wake wazee waliposikia mara ya kwanza kwamba wangekuwa na mtoto. (Mwanzo 17:17, 19; 18:12) Jina la Esau lilikuwa na maana ya “Mwenye Malaika” (mavuzi ya mwili) likieleza tabia ya mwili. Jina lake jingine, Edomu, “Mwekundu,” lilikuwa kikumbusho cha kwamba aliuza haki yake ya mzaliwa wa kwanza ili apate mlo wa mchuzi mwekundu. (Mwanzo 25:25, 30-34; 27:11; 36:1) Ijapokuwa alipitwa umri kidogo tu na ndugu-yake-pacha, Esau, Yakobo alinunua haki ya mzaliwa wa kwanza kutoka kwa Esau, akapokea baraka ya mzaliwa wa kwanza kutoka kwa baba yake. Tangu kuzaliwa, maana ya jina la Yakobo ilikuwa “Kushika Kisigino” au “Mwenye Kuchukua Mahali pa Mwingine.” (Mwanzo 27:36) Hali moja na hiyo jina Sulemani, ambaye katika utawala wake Waisraeli walifurahia amani na ufanisi, lilikuwa na maana ya “Mwenye Kuamanika.”—1 Mambo ya Nyakati (Siku) 22:9.

Hivyo, kamusi The Illustrated Bible Dictionary (Buku la 1, ukurasa wa 572) inaeleza hivi: “Uchunguzi wa neno ‘jina’ katika Agano la Kale unafunua jinsi lilivyo na maana sana katika Kiebrania. Jina si kibandiko tu cha kutambulisha kitu, bali linatoa maana ya utu halisi wa mwenye jina.”

Uhakika wa kwamba Mungu anaona majina kuwa ya maana unaonekana, kwa sababu kupitia malaika, aliwaagiza wale ambao wakati ujao wangekuwa wazazi wa Yohana Mbatizaji na Yesu ambavyo majina ya wanao yangepasa kuwa. (Luka 1:13, 31) Na nyakati fulani yeye alibadili majina, au akawapa watu majina ya ziada, ili aonyeshe mahali ambapo pangekuwa pao katika kusudi lake. Kwa mfano, Mungu alipotabiri kwamba Abramu (“Baba ya Utukuzo”) mtumishi wake angekuwa baba ya mataifa mengi Yeye alibadili jina lake akawa Abrahamu (“Baba ya Umati wa Watu”). Tena akabadili jina la Sarai (“Mgomvi”) mke wake likawa Sara (“Binti-Mfalme”), kwa kuwa angekuwa mama ya mbegu (uzao) ya Abrahamu.—Mwanzo 17:5, 15, 16; linganisha Mwanzo 32:28; 2 Samweli 12:24, 25.

Yesu, pia, alifahamu umaana wa majina hata akataja jina la Petro alipokuwa akimpa pendeleo la utumishi. (Mathayo 16:16-19) Hata viumbe wa kiroho wana majina. Wawili wanaotajwa katika Biblia ni Gabrieli na Mikaeli. (Luka 1:26; Yuda 9) Mwanadamu anapovipa majina vitu visivyo na uhai kama nyota, sayari, miji, milima na mito, anafuata tu mfano wa Muumba wake. Kwa mfano, Biblia inatuambia kwamba Mungu anaita kila nyota kwa jina.—Isaya 40:26.

Ndiyo, majina ni ya maana machoni pa Mungu, naye aliweka ndani ya mwanadamu tamaa ya kutambulisha watu na vitu kwa majina. Hivyo malaika, watu, wanyama, pia nyota na vitu vingine visivyo na uhai, vina majina. Je! lingekuwa jambo linalopatana Muumba wa vitu vyote hivyo ajiache mwenyewe bila jina? Hasha, hangejiacha bila jina, kwa sababu maneno ya mtunga zaburi yanasema: “Wote wenye mwili na walihimidi jina [la Mungu] takatifu milele na milele.”—Zaburi 145:21.

Kamusi The New International Dictionary of New Testament Theology (Buku la 2, ukurasa wa 649) inasema: “Moja ya sehemu zilizo za msingi na za maana sana za ufunuo wa kibiblia ni uhakika wa kwamba Mungu si mtu asiye na jina: ana jina la kibinafsi, ambalo kwa hilo anaweza, na anapaswa kuabudiwa.” Kwa hakika Yesu alikuwa akifikiria jina hilo alipofundisha wafuasi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.”—Mathayo 6:9.

Kwa sababu ya yote hayo, ni wazi kwamba ni jambo la maana sisi tujue jina la Mungu ni jina gani. Je! wewe unajua jina la Mungu binafsi?

Jina la Mungu Ni Jina Gani?

Ni jambo la kushangaza kwamba walio wengi wa yale mamia ya mamilioni ya washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wangeelekea kuona ni vigumu kujibu ulizo hilo. Baadhi yao wangesema kwamba jina la Mungu ni Yesu Kristo. Lakini katika sala Yesu alikuwa akiomba mtu fulani mwingine aliposema: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale [wewe] ulionipa katika ulimwengu.” (Yohana 17:6) Alikuwa akisali kwa Mungu aliye mbinguni, kama mwana anayesema na baba yake. (Yohana 17:1) Jina la Baba yake wa kimbingu ndilo lilipasa “litukuzwe,” au litakaswe.

Hata hivyo Biblia nyingi za siku hizi hazina jina hilo, na halitumiwi mara nyingi katika makanisa. Kwa sababu hiyo, kuliko ‘kutukuzwa,’ jina hilo limepotea lisionwe na mamilioni ya wasomaji wa Biblia. Kama mfano wa jinsi watafsiri wa Biblia wamelitendea jina la Mungu, angalia mstari mmoja tu kati ya mahali linapoonekana: Zaburi 83:18. Hivi ndivyo andiko hilo limetafsiriwa katika Biblia nne tofauti-tofauti:

“Waache wajue kwamba wewe peke yako, ambaye jina lake ni BWANA, ndiwe Aliye Juu Zaidi Sana ya dunia yote.” (Revised Standard Version ya mwaka wa 1952)

“Wajue kwamba wewe pekee ndiwe Mwenyezi-Mungu; Mungu Mkuu juu ya dunia yote.” (Habari Njema kwa Watu Wote, Agano Jipya na Zaburi, ya mwaka wa 1984)

“Waache wajue hili: wewe pekee mwenye lile jina Yahweh, Aliye Juu Zaidi Sana ya ulimwengu mzima.” (Jerusalem Bible ya Katoliki, ya mwaka wa 1966)

“Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Union Version ya Kiswahili, ya mwaka wa 1978)

Kwa nini jina la Mungu linaonekana tofauti sana katika tafsiri hizo? Je! jina lake ni BWANA, Mwenyezi-Mungu, Yahweh au Yehova? Au majina yote hayo yanakubalika?

Ili tujibu ulizo hili, yatupasa tukumbuke kwamba hapo awali Biblia haikuandikwa katika Kiswahili wala Kiingereza. Waandikaji wa Biblia walikuwa Waebrania, na sana sana waliandika katika lugha za wakati wao za Kiebrania na Kigiriki. Wengi wetu hatusemi lugha hizo za kale. Lakini Biblia imetafsiriwa katika lugha nyingi za kisasa, na tunaweza kutumia tafsiri hizo tunapotaka kulisoma Neno la Mungu.

Wakristo wanaiheshimu sana Biblia na wanaamini kwa usahihi kwamba “kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16, Zaïre Swahili Bible) Kwa sababu hiyo, kutafsiri Biblia ni daraka kubwa. Mtu akibadili au akiacha kwa makusudi sehemu ya mambo yaliyo katika Biblia, anaharibu Neno lililotolewa kwa uongozi wa Mungu. Onyo hili la Kimaandiko lingemhusu mtu kama huyo: “Mtu ye yote akiyaongeza [mambo hayo], Mungu atamwongezea hayo mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki. Na mtu ye yote akiondoa lo lote katika maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mungu atamwondolea sehemu yake katika ule mti wa uzima.”—Ufunuo 22:18, 19; ona pia Kumbukumbu la Torati 4:2.

Bila shaka watafsiri wengi wa Biblia wanaiheshimu Biblia na wanataka kwa unyofu wa moyo ieleweke katika kizazi hiki cha kisasa. Lakini watafsiri hawakuongozwa na roho ya Mungu. Pia, wengi wao ni wenye kushikilia kauli yao juu ya mambo ya kidini, na huenda wakaongozwa na mawazo ya kibinafsi na yale wanayopendelea wao. Wanaweza pia kufanya makosa ya kibinadamu katika kuamua.

Kwa sababu hiyo, tunayo haki ya kuuliza maulizo fulani ya maana: Jina halisi la Mungu ni jina gani? Na kwa nini tafsiri mbalimbali za Biblia zinampa Mungu majina tofauti-tofauti? Tukiisha pata jibu la maulizo hayo, ndipo tunaweza kurudi kwenye ulizo letu la kwanza: Kwa nini kutakaswa kwa jina la Mungu ni kwa maana sana?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Malaika, watu, wanyama, pia nyota na vitu vingine visivyo na uhai, vina majina. Je! lingekuwa jambo linalopatana Muumba wa vitu vyote hivyo awe bila jina?

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Kwa kuwa alilitaja mara nyingi katika sala zake mwenyewe, kwa wazi jina la Mungu lilikuwa lenye maana kubwa sana kwa Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki