Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • na kur. 23-27
  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
  • Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jina Hilo Lilikuwa Humo
  • Kuondolewa kwa Jina Hilo
  • Kuhitajiwa kwa Jina Hilo
  • Je! Jina Hilo Lirudishwe?
  • Upinzani kwa Jina Hilo
  • Magumu ya Kujua Maana ya Jina la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Yehova
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
Pata Habari Zaidi
Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
na kur. 23-27

Jina la Mungu na “Agano Jipya”

CHEO cha jina la Mungu katika Maandiko ya Kiebrania, “Agano la Kale,” ni kile kisichotikisika. Ijapokuwa hatimaye Wayahudi waliacha kulitamka, imani zao za kidini ziliwazuia wasiliondoe jina hilo walipokuwa wakiandika nakala za hati za kale za Biblia. Kwa sababu hiyo, Maandiko ya Kiebrania yana jina la Mungu mara nyingi zaidi ya jina jinginelo lote.

Hali hiyo ni tofauti kwa habari ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, “Agano Jipya.” Hati za kitabu cha Ufunuo (kile kitabu cha mwisho cha Biblia) zina jina la Mungu kwa namna ya kifupi hiki, “Yah,” (katika neno hili “Haleluya”). Lakini zaidi ya hiyo, hakuna hati ya Kigiriki ya kale-kale tuliyo nayo leo tangu Mathayo mpaka Ufunuo iliyo na jina la Mungu kwa ukamili. Je! maana yake ni kwamba jina hilo halipasi kuwa humo? Hilo lingekuwa jambo la kustaajabisha kwa sababu wafuasi wa Yesu waliukubali umaana wa jina la Mungu, na Yesu alitufundisha tusali jina la Mungu litakaswe. Basi ilikuwaje?

Ili ufahamu hilo, kumbuka kwamba zile hati za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tulizo nazo leo si nakala zenyewe zile za awali. Vitabu vyenyewe vilivyoandikwa na Mathayo, Luka na waandikaji wengine wa Biblia vilitumiwa sana navyo vilichakaa upesi. Kwa sababu hiyo, nakala nyingine ziliandikwa, nazo zilipochakaa, nakala zaidi zikaandikwa kutokana na nakala hizo. Hivyo ndivyo tungetazamia, kwani kwa kawaida nakala hizo ziliandikwa zitumiwe, si zitunzwe.

Kuna maelfu ya nakala za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zinazopatikana leo, lakini nyingi zazo ziliandikwa wakati wa karne ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu au baada ya hapo. Hiyo inaonyesha kwamba yawezekana kuwe kulitokea jambo hili: Je! kuna kitu kilichoyapata maandishi ya awali ya Maandiko ya Kigiriki kabla ya karne ya nne kilichofanya jina la Mungu liachwe kutumiwa? Mambo ya hakika yanathibitisha kwamba kitu fulani kilifanya hivyo.

Jina Hilo Lilikuwa Humo

Tunaweza kuwa na hakika kwamba mtume Mathayo alitia jina la Mungu katika Injili yake. Kwa nini? Kwa sababu hapo awali aliandika katika Kiebrania. Katika karne ya nne, Jerome, aliyetafsiri Biblia ya Kilatini iitwayo Vulgate, alitoa ripoti hivi: “Mathayo, aliye pia Lawi, na ambaye kwenye kazi ya kutoza kodi akawa mtume, alitunga kwanza Injili ya Kristo katika Yudea katika lugha ya Kiebrania . . . Hakuna uhakika wa kutosha juu ya aliyeitafsiri katika Kigiriki baada ya hapo. Isitoshe, Kiebrania chenyewe hicho kimetunzwa mpaka leo hii katika maktaba katika Kaisaria.”

Kwa kuwa Mathayo aliandika katika Kiebrania, haiwaziki kwamba yeye hakulitumia jina la Mungu, hasa alipokuwa akinakili maneno kutoka sehemu za “Agano la Kale” zilizokuwa na jina hilo. Ingawa hivyo, waandikaji wengine wa sehemu ya pili ya Biblia waliandikia wasikilizaji ulimwenguni pote katika lugha ya mataifa yote iliyokuwa ya wakati huo, yaani, Kigiriki. Kwa sababu hiyo, hawakunakili maneno kutoka maandishi ya awali ya Kiebrania bali kutoka tafsiri ya Kigiriki iitwayo Septuagint. Na hata Injili ya Mathayo ilitafsiriwa hatimaye katika Kigiriki. Je! jina la Mungu lingalionekana katika maandishi hayo ya Kigiriki?

Visehemu fulani vya kale sana vya Septuagint Version vilivyokuwako hasa katika siku za Yesu vimesalimika mpaka wakati wetu, na ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba jina la kibinafsi la Mungu lilionekana humo. The New International Dictionary of New Testament Theology (Buku la 2, ukurasa wa 512) inasema hivi: “Mavumbuzi ya maandishi ya awali ya hivi majuzi yanatilia shaka wazo la kwamba watungaji wa LXX [Septuagint] waliitafsiri tetragramatoni YHWH kwa kutumia kyrios. [Hati] LXX MSS (visehemu) zilizo za kale sana zinazopatikana kwetu sasa zina tetragramatoni ikiwa imeandikwa kwa herufi za Kiebrania na kwa maandishi ya Kigiriki. Desturi hiyo ilitunzwa na watafsiri wa Kiyahudi waliokuja baadaye wa Agano la Kale katika karne zile za kwanza A.D.” Kwa hiyo, kwamba Yesu na wanafunzi wake waliyasoma Maandiko hayo katika Kiebrania ama katika Kigiriki, wangeliona jina la Mungu.

Hivyo, Profesa George Howard, wa Chuo Kikuu cha Georgia, U.S.A., alieleza hivi: “Wakati Septuagint ambayo kanisa la Agano Jipya lilitumia na kunakili maneno yake ilipokuwa na namna ya Kiebrania ya jina la kimungu, bila shaka waandikaji wa Agano Jipya waliitia Tetragramatoni katika maneno yao waliyonakili.” (Biblical Archaeology Review, Machi 1978, ukurasa wa 14) Ni mamlaka gani ambayo wangalikuwa nayo wafanye tofauti na hivyo?

Jina la Mungu liliendelea kuwa katika tafsiri ya Kigiriki ya “Agano la Kale” kwa muda zaidi kidogo. Katika sehemu ya kwanza ya karne ya pili W.K., Akila, mwongofu wa Kiyahudi alifanya tafsiri mpya ya Maandiko ya Kiebrania akiyaleta katika Kigiriki, na humo aliwakilisha jina la Mungu kwa Tetragramatoni katika herufi za kale za Kiebrania. Katika karne ya tatu, Origeni aliandika hivi: “Na katika hati zilizo sahihi zaidi sana LILE JINA linaonekana kwa herufi za Kiebrania, lakini si kwa [herufi za] Kiebrania cha leo, bali kwa zile zilizo za kale zaidi sana.”

Hata katika karne ya nne, Jerome anaandika hivi katika utangulizi wa vitabu vya Samweli na Wafalme: “Na tunaliona jina la Mungu, ile Tetragramatoni [יהוה] katika mabuku fulani ya Kigiriki likionyeshwa hata leo hii katika herufi za kale.”

Kuondolewa kwa Jina Hilo

Ingawa hivyo, kufikia wakati huo uasi-imani uliotabiriwa na Yesu ulikuwa umetokea, na jina hilo, lijapoonekana katika hati, liliendelea kutumiwa mara chache sana. (Mathayo 13:24-30; Matendo 20:29, 30) Mwishowe, wasomaji wengi hata hawakulitambua na Jerome anaripoti kwamba katika wakati wake “kwa sababu ya kufanana kwa herufi, watu fulani wasiojua kitu walipokuta [ile Tetragramatoni] katika vitabu vya Kigiriki, walizoea kusoma ΠΙΠΙ.”

Katika nakala zilizofuata za Septuagint, jina la Mungu liliondolewa na maneno kama “Mungu” (The·osʹ) na “Bwana” (Kyʹri·os) yakatumiwa badala yalo. Tunajua kwamba jambo hilo lilitukia kwa sababu tuna visehemu vya mapema vya Septuagint ambamo jina la Mungu lilitiwa ndani na nakala zilizofuata za sehemu izo hizo za Septuagint ambamo jina la Mungu limeondolewa.

Jambo lile lile lilitukia katika “Agano Jipya,” au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Profesa George Howard anaendelea kusema: “Wakati namna ya Kiebrania ya jina la kimungu ilipoondolewa na maneno ya Kigiriki yakatumiwa badala yalo katika Septuagint, liliondolewa pia katika maneno yaliyonakiliwa ya Septuagint yakatiwa katika Agano Jipya. . . . Muda si muda lile jina la kimungu likapotea lisionekane kwa kanisa la Mataifa isipokuwa kama vile kufikia hapa lilivyoonyeshwa kwa vifupi vilivyotumiwa badala yalo au lilivyokumbukwa na wasomi.”

Kwa sababu hiyo, ijapokuwa Wayahudi walikataa kutamka jina la Mungu, kanisa la Kikristo lenye kuasi imani lilifaulu kuliondoa kabisa katika hati za lugha ya Kigiriki za sehemu za Biblia, na pia katika tafsiri za lugha nyingine.

Kuhitajiwa kwa Jina Hilo

Mwishowe, kama tulivyotangulia kuona, lile jina lilirudishwa kwenye tafsiri nyingi za Maandiko ya Kiebrania. Lakini namna gani Maandiko ya Kigiriki? Basi, watafsiri na wanafunzi wa Biblia wakajua baadaye kwamba pasipo jina la Mungu, ni vigumu sana kufahamu sawasawa sehemu fulani za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kulirudisha jina hilo ni msaada mkubwa wa kuongeza kueleweka na kufahamika kwa sehemu hiyo ya Biblia iliyotolewa kwa uongozi wa Mungu.

Kwa mfano, yaangalie maneno haya ya Paulo kwa Warumi: “Kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka.” (Warumi 10:13) Ili tuokoke, inatupasa tuliitie jina la nani? Kwa kuwa mara nyingi Yesu anasemwa kuwa “Bwana,” na hata andiko moja linasema: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka,” je! tukate shauri kwamba hapa Paulo alikuwa akisema juu ya Yesu?—Matendo 16:31.

Hapana, haitupasi kufanya hivyo. Habari ya pembeni inayoelekezwa kwenye Warumi 10:13 inatupeleka kwenye Yoeli 2:32 katika Maandiko ya Kiebrania. Ukiangalia andiko hilo, utaona kwamba Paulo alikuwa akinakili hakika maneno ya Yoeli akiyatia katika barua yake kwa Warumi; na yale ambayo Yoeli alisema katika Kiebrania cha awali yalikuwa: “Awae yote atakaelilingana jina la Jehova ataponywa.” (OTSWMSA) Ndiyo, hapa Paulo alimaanisha kwamba imetupasa tuite juu ya jina la Yehova. Kwa sababu hiyo, ijapo inatupasa tumwamini Yesu, wokovu wetu unakamatana sana na kuthamini kunakofaa kwa jina la Mungu.

Mfano huo unaonyesha jinsi kuondolewa kwa jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki kulivyoongeza kutatiza akili za watu wengi wasipate kutofautisha kati ya Yesu na Yehova. Bila shaka, kuliongezea sana kusitawishwa kwa lile fundisho la Utatu!

Je! Jina Hilo Lirudishwe?

Kwa kuwa hati zilizopo leo hazina jina hilo, je! mtafsiri angekuwa na haki yo yote kulirudisha? Ndiyo, angekuwa na haki hiyo. Kamusi nyingi za Kigiriki zinakubali kwamba mara nyingi neno hili “Bwana” katika Biblia linaelekeza kwa Yehova. Kwa mfano, katika sehemu yayo chini ya neno hili la Kigiriki Kyʹri·os (“Bwana”), kamusi ya Robinson inayoitwa A Greek and English Lexicon of the New Testament (iliyochapishwa mwaka wa 1859) inasema kwamba linamaanisha “Mungu akiwa ndiye Bwana Mkuu Kuliko Wote na mwenye enzi ya ulimwengu mzima, kwa kawaida katika Septuagint badala ya Kiebrania יְהוָֹה Yehova.” Kwa sababu hiyo, katika mahali ambapo waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wananakili maneno kutoka Maandiko ya Kiebrania yaliyotangulia, mtafsiri ana haki ya kutafsiri neno Ky΄ri·os kuwa “Yehova” kila linapoonekana jina la Mungu katika Kiebrania cha awali.

Watafsiri wengi wamefanya hivyo. Kuanzia angalau na karne ya 14, tafsiri nyingi za Kiebrania zilifanywa kutokana na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Watafsiri hao walifanya nini walipokuta maneno yaliyonakiliwa kutoka “Agano la Kale” ambamo jina la Mungu lilionekana? Mara nyingi, waliona wamelazimika kurudisha jina la Mungu mahali lilipokuwa katika maandishi ya awali. Sehemu nyingi au Maandiko ya Kigiriki yote yaliyotafsiriwa katika Kiebrania yana jina la Mungu.

Tafsiri nyingi katika lugha za kisasa, hasa zile zinazotumiwa na wamisionari, zimefuata mfano huo. Hivyo tafsiri nyingi za Maandiko ya Kigiriki katika lugha za Kiafrika, Kiesia, Kimarekani na za visiwa vya Pasifiki, zinatumia sana jina Yehova, hata wasomaji wanaweza kuona waziwazi tofauti kati ya Mungu wa kweli na miungu ya uwongo. Vilevile, jina hilo limeonekana katika tafsiri nyingi za lugha za Ulaya.

Tafsiri moja inayorudisha kwa ujasiri jina la Mungu ikiwa na mamlaka nzuri ni ile ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures. Tafsiri hiyo, ambayo kwa sasa inapatikana katika lugha 11, ikiwa ni pamoja na Kiingereza, imerudisha jina la Mungu kila mara ambayo sehemu fulani ya Maandiko ya Kiebrania iliyo nalo inanakiliwa katika Maandiko ya Kigiriki. Kwa jumla, jina hilo linaonekana likiwa na msingi timamu mara 237 katika tafsiri hiyo ya Maandiko ya Kigiriki.

Upinzani kwa Jina Hilo

Ijapokuwa jitihada za watafsiri wengi za kurudisha jina la Mungu katika Biblia, nyakati zote kumekuwako mkazo wa kidini wa kuliondoa kabisa. Wayahudi, wajapoliacha liwe katika Biblia zao, walikataa kulitamka, Wakristo waasi-imani wa karne za pili na za tatu waliliondoa walipoandika nakala za hati za Biblia ya Kigiriki na waliliondoa walipofanya tafsiri za Biblia. Watafsiri katika nyakati za kisasa wameliondoa, hata walipotegemeza tafsiri zao juu ya Kiebrania cha awali, ambamo linaonekana karibu mara 7,000. (Linaonekana mara 6,973 katika maandishi ya awali ya Kiebrania ya New World Translation of the Holy Scriptures, ya Kiingereza, chapa ya 1984.)

Yehova anawaonaje wale wanaoliondoa jina lake katika Biblia? Kama wewe ungekuwa mtungaji wa kitabu, ungeonaje juu ya mtu ambaye angefanya kila awezalo hata kuliondoa jina lako katika kitabu ulichotunga? Watafsiri wanaolikataa jina hilo, kwa sababu ya matatizo ya kutamka au kwa sababu ya mapokeo ya Kiyahudi, wanaweza kufananishwa na wale ambao Yesu aliambia kuwa “mnatoa nzi katika kinywaji, lakini mnammeza ngamia!” (Mathayo 23:24, Habari Njema kwa Watu Wote) Wanajikwaa juu ya matatizo hayo yaliyo madogo zaidi lakini mwishowe wanafanyiza tatizo kubwa—kwa kuliondoa jina la mtu aliye mashuhuri zaidi kuliko wote katika ulimwengu mzima, lisiwemo katika kitabu kilichoandikwa kwa uongozi wake.

Mtunga zaburi aliandika: “Mpaka lini, O Mungu, mpinzani ataendelea kukusuta? Je! adui ataendelea kulitendea jina lako bila heshima milele?”—Zaburi 74:10, NW.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

Je! “BWANA” ni Sawa na Kusema “Yehova”?

Kuondoa jina binafsi la Mungu na lililo mashuhuri katika Biblia na badala yake kuweka mtajo kama vile “Bwana” au “Mungu” kunapunguza nguvu za maandishi na kuyafanya yawe yasiyofaa kwa njia nyingi. Kwa mfano, kunaweza kuongoza kwenye miungano ya maneno yasiyo na maana. Katika dibaji yake, The Jerusalem Bible inasema: “Kusema, ‘Bwana ni Mungu,’ kwa uhakika ni kurudia-rudia jambo moja tu bure, bila maana, lakini kusema ‘Yahweh ni Mungu’ si kurudia-rudia jambo lile lile.”

Maneno hayo yenye kutumiwa badala ya jina yanaweza kuongoza pia kwenye vifungu visivyoeleweka vizuri. Hivyo katika Zaıre Swahili Bible, Zaburi 8:9 inasomwa hivi: “Ee BWANA, Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu duniani mwote!” Inaeleweka vizuri zaidi kama nini wakati jina Yehova linaporudishwa katika maandishi hayo! Hivyo, The Old Testament in Swahili (Mombasa) chapa ya 1949 inasomwa hapo hivi: “Ewe Jehova, Bwana wetu, jina lako jinsi lilivyo na maana duniani mwote!”

Kuondoa jina hilo kunaweza pia kuongoza kwenye machafuko. Zaburi 110:1 inasema hivi: “Neno la BWANA kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako.” (Union Version na Zaıre Swahili Bible) Ni nani anayesema, na anasema na nani? Tafsiri hii ni bora kama nini: “Jehova amwambia Bwana wangu, Keti upande wa mkono wangu wa kuume, hata nishe waweka adui zako kuwa nta-za-nyayo ya maguu yako.”—The Old Testament in Swahili (Mombasa).

The Imperial Bible-Dictionary (Buku la 1, ukurasa wa 856) inaeleza tofauti kati ya “Mungu” (Elohim) na “Yehova,” ikisema: “Kila mahali [Yehova] ni jina la kipekee, lenye kuonyesha aliye Mungu wa kibinafsi na yeye pekee; lakini Elohim linahusu cheo cha ujumla, likionyesha kwa kawaida yeye Aliye Mkuu, lakini si kwa lazima wala kwa upatani hivyo.”

J. A. Motyer, mkuu wa Trinity College, Uingereza, anaongeza kusema: “Mambo mengi yanapotea katika kusoma Biblia ikiwa tunafikiria tu neno [Bwana au Mungu] linalotumiwa badala ya lile jina la Mungu mwenyewe la kibinafsi na la usiri. Kwa kuwaambia watu wake jina lake, Mungu alikusudia kuwafunulia sifa yake ya ndani-ndani.”—Eerdmans’ Handbook to the Bible, ukurasa wa 157.

La, hakuna awezaye kutafsiri jina mashuhuri la kipekee kwa kutumia mtajo tu. Mtajo hauwezi kamwe kutoa maana yote, yenye mambo mengi ya jina la Mungu la awali.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Kisehemu hiki cha Septuagint (kulia) cha tarehe ya mpaka karne ya kwanza W.K. na chenye Zekaria 8:19-21 na 8:23–9:4 kiko katika Nyumba ya Vitu vya Ukumbusho ya Israeli katika Yerusalemu. Kina jina la Mungu mara nne, tatu za mara hizo zimeonyeshwa hapa. Katika Hati ya Aleksandria (kushoto), nakala ya Septuagint iliyoandikwa baadaye miaka 400, jina la Mungu limebadilishwa katika mistari ile ile kwa kutumia KY na KC, vifupi vya neno la Kigiriki Ky΄ri·os (“Bwana”)

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Wakati wa karne ya 19, John W. Davis, misionari katika China alieleza sababu gani alisadiki jina la Mungu limepasa liwe katika Biblia: “Ikiwa Roho Mtakatifu anasema Yehova katika mahali po pote kwa Kiebrania, kwa nini mtafsiri asiseme Yehova katika Kiingereza au Kichina? Ana haki gani kusema, mimi nitatumia Yehova mahali hapa, na hapa nitatumia neno jingine badala yalo? . . . Ikiwa kuna mtu ye yote anayesema kwamba kuna visa ambavyo katika hivyo ingekuwa kosa kutumia jina la Yehova, na aonyeshe ni sababu gani; onus probandi [jukumu la kuthibitisha] linamkalia. Ataona kazi hiyo kuwa ngumu, kwa maana ni lazima ajibu ulizo hili lililo rahisi—Ikiwa katika kisa cho chote ni kosa kutumia Yehova katika tafsiri basi ni kwa nini mwandikaji aliyeongozwa na Mungu alilitumia katika nakala ya awali?”—The Chinese Recorder and Missionary Journal, Buku la 7, Shanghai, 1876.

[Picha katika ukurasa wa 23]

New World Translation of the Christian Greek Scriptures inatumia kwa kufaa jina la Mungu mara 237

[Picha katika ukurasa wa 24]

Jina la Mungu juu ya kanisa katika Minorca, Hispania;

juu ya sanamu karibu na Paris, Ufaransa;

na juu ya Chiesa di San Lorrenzo, Parma, Italia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki