Sura 7
Tenda kwa Hekima Unapokabili Msiba
1. Kwa nini watu waliangamia bure (a) wakati meli Titaniki ilipozama? (b) wakati Mlima Pelée ulipolipuka?
WATU wenye hekima wanachukua hatua ili walinde maisha zao, wanapoonywa na chanzo chenye kutegemeka kwamba msiba unakaribia sana. (Mithali 22:3) Lakini maelfu yasiyo na hesabu wameangamia bure kwa sababu uhakika wao haukuwekwa mahali pazuri. Ijapokuwa maonyo mengi yalitolewa ili kuingia katika mashua za kuokokea, mamia ya wasafiri walizama kilindini pamoja na meli Titaniki mwaka wa 1912 kwa sababu waliamini lile dai la kwamba ilikuwa isiyozamika. Wakati Mlima Pelée katika Martinike ulipoanza kutupa majivu na mawe yenye moto wa volkano mwaka wa 1902, wakazi wa mji jirani wa Saint-Pierre waliogopa sana, lakini kwa kuwa masilahi ya kichoyo ya watu wakubwa-wakubwa wa jumuiya hiyo yangepotea kama wangekimbia, wanasiasa wa huko na mhariri wa gazeti la huko walitaka kutuliza woga wa watu, wakiwaomba sana wasiondoke. Ghafula mlima huo ulilipuka, na watu 30,000 wakaangamia.
2. (a) Ni onyo gani la haraka linalotolewa siku zetu? (b) Kwa nini hali hiyo ni yenye hatari sana?
2 Wakati wetu huu onyo ambalo ni la haraka hata zaidi linatolewa—si juu ya msiba wa mahali fulani tu, bali juu ya kukaribia kwa vita ya Mungu ya ulimwengu mzima, yaani, Har–Magedoni. (Isaya 34:1, 2; Yeremia 25:32, 33) Mashahidi wa Yehova wametembelea nyumba za watu ulimwenguni pote kwa kurudia-rudia, wakiwaomba sana watende kwa hekima, ili waje wahifadhi maisha zao. Je! wewe unapenda uhai vya kutosha kuchukua hatua inayohitajika, na kufanya hivyo kwa haraka sana, bila kukawia?
“ULIMWENGU UNAPITA”
3. Kwa nini mwelekeo wetu juu ya ulimwengu utageuza tazamio letu la kuokoka?
3 Jambo la maana sana katika kutazamia kwako wokovu ni mwelekeo wako juu ya ulimwengu. Umo katika ulimwengu, maadamu uko hai kama binadamu. Lakini si lazima ushiriki tamaa zake mbaya na kufuata mfano wa vitendo vyake visivyo vya kumwogopa Mungu. Si lazima ujishirikishe nao kwa kuweka tumaini lako katika wanadamu na katika mipango yao badala ya kumtumaini Mungu na kusudi lake. Lakini ni lazima uchague. Huwezi kuwa pande zote mbili. “Ye yote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” Kwa nini? Kwa sababu, kama Neno la Mungu linavyotuambia, “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.”—Yakobo 4:4; 1 Yohana 5:19, New World Translation; Zaburi 146:3-5.
4. (a) Kwa kutumia Biblia yako, eleza mazoea na mielekeo itakayozuia watu wasiishi chini ya Ufalme wa Mungu. (b) Kwa nini wo wote ambao wameshiriki mambo hayo wamepaswa wayaache haraka?
4 Kwa wazi, Yehova hatahifadhi waingie katika Utaratibu Mpya wenye uadilifu watu ambao njia ya maisha yao inaonyesha kwamba wanang’ang’ania mambo ambayo Mungu analaani. Ni nini baadhi ya mambo hayo? Ulimwengu unaona shughuli nyingi na mielekeo mingi kuwa mambo ya kawaida tu. Lakini tukitaka kuokoka mwisho wa ulimwengu huu mbovu, basi, bila kujali mambo ambayo watu wengine wanafanya na kufikiri, tutafuata onyo la Biblia linalosema waasherati, wazinzi, watu wenye kulalana wao kwa wao na wale wanaoshiriki uchafu usio wa adili na mwenendo mpotovu hawatakuwa kati ya waokokaji. Hata wengine watumie uwongo na wivi mara nyingi, sisi tutakataa njia hiyo ya maisha. Ijapokuwa mazoea ya mambo ya siri ya uchawi yapendwe na watu wengi, sisi tutayaepuka. Ijapo wengine wawe wenye wivu, wachochee fitina, wawe wenye kukasirika upesi, au wajaribu kuepuka vipingamizi kwa kutumia dawa za kulevya au kunywa pombe kupita kiasi, sisi hatutafuata mfano wao. Na ikiwa tumeshiriki mambo hayo, itatubidi tubadilike. Hata kama baadhi ya mambo hayo yalionekana kuwa “ya kawaida” kwetu zamani, tutayaacha. Kwa nini? Kwa sababu sisi twampenda Mungu kweli kweli, twapenda uzima, na Neno la Mungu linaonya kwamba “watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21; Waefeso 5:3-7; 1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1; Ufunuo 22:15.
5. (a) Ikiwa uhai ni wenye thamani kwetu, imetupasa tujifunze kufanya nini? (b) Ni sifa gani njema zinazotajwa katika maandiko yaliyo mwishoni mwa fungu hili? Ni za maana kadiri gani? Tunaweza kuzisitawishaje?
5 Ikiwa nafasi ya kuishi milele kwa furaha ni ya maana kwetu, tunahitaji kujifunza jinsi ya kumpendeza Mpaji-uzima, Yehova Mungu. (Matendo 17:24-28; Ufunuo 4:11) Ni lazima hatua kwa hatua tulitumie Neno lake lihusu kila sehemu ya maisha zetu. Tunapofanya hivyo, upesi tutachunguza kwa uzito mwelekeo wetu ulivyo kwetu wenyewe na kwa watu wengine, kwa mali za kibinafsi na mambo tunayopata, na kufikiria jinsi unavyohusu msimamo wetu mbele za Mungu. Huenda watu walio karibu yetu wakawa wenye kujivunia ubinafsi, wenye kujivunia kabila au taifa lao wenyewe, lakini sisi tutalifikiria kwa uzito andiko linalosema: “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”—Yakobo 4:6; Sefania 2:2, 3; Zaburi 149:4.
6, 7. Kwa nini imetupasa tuchunguze maisha zetu wenyewe kwa msaada wa 1 Yohana 2:15-17?
6 Hata ijapo wengine wanajiruhusu wafanywe watumwa wa tamaa zinazochochewa na jamii ya watu yenye kupenda mali au wanasukumwa na tamaa ya ukubwa wa kibinafsi, sisi tutachunguza maisha yetu wenyewe kwa msaada wa 1 Yohana 2:15-17, New World Translation: “Msiwe mkipenda wala ulimwengu wala vitu vilivyomo katika ulimwengu. Mtu ye yote akipenda ulimwengu, upendo wa Baba haumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilichomo katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake—hakitokani na Baba, bali chatokana na ulimwengu. Tena, ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” Ikiwa tunataka kufanya mabadiliko, huu ndio wakati wa kufanya hivyo.
7 Ulimwengu huu na njia yake ya maisha hautaendelea milele. Si ‘usiozamika.’ Huenda watu wa ulimwengu wakajaribu kuwategemea wafuasi wao, wawafanye wahisi kwamba jitihada zao zaweza kuufanya ulimwengu kuwa bora. Lakini njia moja tu ya kuja kuokolewa katika msiba unaokaribia sana ni kusikiliza ujumbe wa Mungu wenye kuonya. Watu wa Ninewi katika siku za nabii Yona wanaweka mfano wa jambo hilo, mfano unaofaa tuuzingatie moyoni.
“WALITUBU KWA SABABU YA MAHUBIRI YA YONA”
8. Waninewi walionyeshaje hekima wakati Yona alipowatolea onyo la Mungu, kukawa matokeo gani?
8 Katika karne ya tisa K.W.K., Yehova alimwagiza Yona aende kwa watu wa Ninewi, mji mkuu wa Ashuru, akawatangazie kwamba, kwa sababu ya ubaya wao, Ninewi ungepinduliwa. Yona alipowaonya kwamba kwa muda wa siku 40 tu wangeangamia, walitenda namna gani? Badala ya kupuuza, “wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia.” Mfalme mwenyewe alijiunga nao, akawaomba sana watu wote wamwombe Mungu kwa bidii na kugeuka waache njia yao mbaya na ujeuri wao. Aliwaza hivi: “Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka . . . na kuiacha hasira yake kali, ili tusiangamizwe?” Kwa sababu waliacha njia yao mbaya, Yehova aliwaonyesha rehema. Maisha zao ziliokolewa.—Yona 3:2-10.
9, 10. (a) Ni katika jambo gani Yesu alisema Waninewi walikuwa mfano wa kufuatwa? (b) Ni nani leo walio kama Waninewi hao?
9 Ili uwe uthibitisho kwa Wayahudi wasioamini katika karne ya kwanza, Yesu alielekeza fikira kwenye kituko hicho cha kihistoria, akasema: “Watu wa Ninewi watatokea siku ya hukumu, nao watakihukumu kizazi hiki kwamba kina hatia. Maana, Waninewi walitubu kwa sababu ya mahubiri ya Yona, na kumbe hapa yupo mkuu zaidi kuliko Yona!”—Mathayo 12:41, Habari Njema kwa Watu Wote.
10 Vipi siku zetu? Je! kuna ye yote anayeonyesha toba kama hiyo? Ndiyo; kuna maelfu mengi ulimwenguni pote ambao, kama Waninewi hao, yaelekea hapo mbele hawakupata kujidai kumwabudu Mungu wa Biblia lakini wanasikiliza sasa ujumbe wa Yehova wa kuonya. Wanapojifunza na kujua sababu itakayofanya uharibifu uje juu ya ulimwengu huu, wanaomba Mungu awaonyeshe rehema. Wana badiliko la kweli la akili na moyo juu ya njia yao ya zamani ya maisha na sasa wanajitahidi watende “matendo yanayopatana na kutubu kwao.” (Matendo 26:20; ona pia Warumi 2:4.) Je! unatamani kuwa mmoja wao? Ikiwa ndivyo, usikawie.
FANYA MAPATANO YA AMANI HARAKA
11. (a) Wagibeoni walikuwa ni wa asili gani? (b) Kwa nini walifanya mapatano ya amani pamoja na Israeli?
11 Wagibeoni pia siku za Yoshua walitenda kwa hekima ili maisha zao zipate kuokolewa. Hao walikuwa Wakanaani ambao njia yao ya maisha haikuwa ya adili na ilikuwa ile ya kupenda mno mali, kuabudu sanamu na ya kishetani. Yehova alikuwa ametoa amri waharibiwe. Walijua jinsi Yehova alivyokuwa ameokoa Waisraeli kutoka Misri miaka 40 iliyotangulia na ya kwamba wafalme wenye nguvu wa Kiamori upande wa mashariki wa Mto Yordani walikuwa wameshindwa kusimama mbele yao. Kila mtu alikuwa anajua kwamba, bila kutumiwa kwa mitambo ya kubomolea maboma, kuta nene za Yeriko zilikuwa zimeanguka mpaka chini mbele yao na ya kwamba mji wa Ai ulikuwa umefanywa kuwa rundo lenye magofu. (Yoshua 9:3, 9, 10) Wakazi wa mji wa Gibeoni walitaka waishi, lakini walijua kwamba hawangeweza kamwe kushinda vita ya kupigana na Mungu wa Israeli. Kuna jambo lililokuwa linahitajika kufanywa haraka. Jambo gani? Hawangeweza kusisitizia kufanya mapatano ya amani pamoja na Waisraeli, lakini wakafikiri ingewapasa angalau wajaribu kufanya kuwe na mapatano. Jinsi gani?
12. (a) Ijapokuwa mbinu waliyotumia, kwa nini Wagibeoni waliokolewa? (b) Iliwabidi wafanye mabadiliko gani, na walipewa kufanya kazi gani?
12 Basi, wakatumia akili, wakamtumia Yoshua wanaume ambao sura zao zilionyesha kama wametoka mbali sana. Walipomfikia Yoshua, wakasema wametoka nchi ya mbali, kwamba wamesikia habari za mambo makuu ambayo Yehova alikuwa amefanya na, kwa kuwakilisha watu wao, wamekuja ili wajitoe wenyewe wawe watumishi na kuomba agano lifanywe pamoja nao. Yoshua na wakuu wa Israeli wakakubali. Baadaye, udanganyifu huo ulipofunuka, Wagibeoni hao wakaungama kwa unyenyekevu wakisema walikuwa wamehofia maisha zao, wakaonyesha utayari wa kufanya lo lote ambalo wangetakwa wafanye. (Yoshua 9:4-25) Yehova alikuwa ametazama shauri lote hilo. Yeye hakudanganywa. Angeweza kuona kwamba hawakujaribu kuchafua watu wake, kama Wamoabi walivyokuwa wametangulia kufanya, naye alithamini tamaa yao yenye bidii ya kuishi. Basi akawaruhusu wagawiwe kazi ya kufanya chini ya Walawi katika hema takatifu, kazi ya kukusanya kuni na kuteka maji, waunge mkono ibada ya Yehova kwa njia hiyo. Bila shaka, ili wakubalike kwa utumishi huo, iliwapasa waache mazoea yao machafu ya zamani.—Yoshua 9:27; Mambo ya Walawi 18:26-30.
13. (a) Sisi tunaweza kufaidikaje na mfano huo wa kiunabii kuhusu Wagibeoni? (b) Ili waje waokolewe na Yoshua Mkubwa Zaidi, watu wa leo wanatakwa wafanye nini?
13 Kwa kuwa sisi tunaishi karibu sana na ukomo wa “siku za mwisho,” ni lazima watu wote wanaotaka kuokolewa wachukue hatua bila kukawia, wafanye hivyo kwa unyofu wote wa moyo. Yesu Kristo, aliye mtekelezaji wa hukumu wa Yehova leo, hawezi kudanganywa kama Yoshua. Njia moja tu ambayo watu kama hao wanaweza kuingia katika mpango pamoja naye ili waje waokoke kuuawa ni kutangaza peupe imani yao katika Yehova kuwa Mungu wa kweli. (Linganisha Matendo 2:17-21.) Ni lazima pia wamkubali Yesu Kristo katika vyeo alivyogawiwa na Mungu na baada ya hapo waishi wakiwa watu wasiopenda njia ya maisha ya ulimwengu huu uliolaaniwa. Kisha inawapasa wawe watumishi wa Mungu walio wanyenyekevu, wamtolee utumishi mtakatifu kwa kushirikiana na kundi la watu wake.—Yohana 17:16; Ufunuo 7:14, 15.
14. Kwa nini tendo la Yehova la kuokoa Wagibeoni katika majeshi ya adui ni lenye maana kwetu?
14 Mara Wagibeoni walipokwisha kuchukua msimamo wao pamoja na watu wa Yehova, walipatwa na mkazo mkubwa. Wafalme watano wa Waamori walivamia mji wa Gibeoni ili wanaokaa humo walazimike kurudia upande wao, kinyume cha Waisraeli. Wagibeoni wakapeleka mbio ombi la haraka kwa Yoshua ili awasaidie. Na wokovu waliopata ulikuwa mmojapo uokovu wenye kutazamisha zaidi katika historia yote. Yehova aliwavuruga adui, akawavurumishia mawe ya mvua kutoka mbinguni, kisha akafanya mchana urefushwe kimuujiza mpaka Waisraeli walipokuwa wamewashinda adui kabisa. (Yoshua 10:1-14) Kuokolewa huko kwa Wagibeoni kulikuwa mfano wa unabii wa kuokolewa kimuujiza hata zaidi kwa umati mkubwa wa waabudu wa yule Mungu wa kweli katika vita ya ulimwengu mzima ya Har–Magedoni. Nafasi ya kuja kufaidika na wokovu huo inapatikana kwa watu wa kila taifa ikiwa wanatenda kwa hekima sasa. Je! unaitumia nafasi hiyo kwa faida yako?—Ufunuo 7:9, 10.