Sura 14
Namna “Mbingu Mpya na Dunia Mpya” Zitakavyoanza
1. (a) Ni nini kinachotajwa mara nyingi katika Biblia kuwa “mbingu”? (b) Maana ya “dunia” ni nini katika vifungu fulani?
KUTAJWA kwa mbingu kunafanya watu wengi wafikirie anga la juu zaidi, mwezi na nyota. Biblia inahusianisha pia “mbingu” na utawala. (Matendo 7:49) Mara nyingine inatumia usemi “mbingu” kumaanisha Mungu mwenyewe akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima. (Danieli 4:26; Mathayo 4:17) Hata serikali za wanadamu zinatajwa kuwa “mbingu,” kwa sababu hizo zina cheo kilicho juu ya raia zao. (2 Petro 3:7) Hali kadhalika, mara nyingi “dunia” inamaanisha tufe, lakini inaweza pia kumaanisha jamii ya kibinadamu. (Mwanzo 11:1; Zaburi 96:1) Kujua hilo kunaweza kukusaidia ufahamu maana ya ahadi zenye kuvutia kuhusu “mbingu mpya na dunia mpya.” Baadhi ya ahadi hizo zilipata utimizo wa kwanza siku za Israeli wa kale.
‘FURAHINI KWA AJILI YA HIVI NINAVYOUMBA’
2. Kwa nini Yehova aliruhusu Israeli wapelekwe katika uhamisho, lakini alitabiri nini?
2 Taifa la Israeli lilikuwa katika agano na Mungu, likiwa limekubali rasmi kumtii yeye. Lakini wakaja kuwa wasio washikamanifu. Kwa sababu hiyo, Yehova akajulisha kwamba angeondoa ulinzi wake, aruhusu Yerusalemu uharibiwe na watu wapelekwe uhamishoni katika Babuloni. (Isaya 1:2-4; 39:5-7) Lakini pia kwa rehema alitabiri kurudishwa kwa mabaki wenye kutubu.—Isaya 43:14, 15; 48:20.
3. Ahadi katika Isaya 65:17 ilikuwa na maana gani?
3 Kwa sababu hilo lilikuwa jambo la hakika, Yehova alisema juu ya kurudishwa ambako kungetokea wakati ujao kana kwamba tayari kunatokea, akisema: “Tazama, mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya, na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini mufurahi, na mushangilie daima, kwa ajili ya hivi ninavyoumba; maana, tazama, ninaumba Yerusalema uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.” (Isaya 65:17, 18, Zaïre Swahili Bible) Hiyo ingekuwa na maana ya kukombolewa kwa Waisraeli hao wenye kutubu.
4. (a) Ukombozi uliotabiriwa ulikuja wakati gani? (b) Wakati huo, ni nini zilizokuwa “mbingu mpya” na “dunia mpya”?
4 Ijapokuwa kwa maoni ya kibinadamu jambo hilo lilikuwa limeonekana kuwa lisilowezekana, Babuloni wenye nguvu uliangushwa na Wamedi na Waajemi mwaka wa 539 K.W.K. Wayahudi wakaja kuwa chini ya serikali mpya, “mbingu mpya.” Sairasi (Koreshi) Mkuu alijazia cheo mashuhuri katika “mbingu mpya” hizo. Ijapo Sairasi hakugeuka awe mwongofu wa Kiyahudi, yeye alikiri kwamba Yehova alimruhusu awe na mamlaka hiyo aliyoitumia na kwamba Yehova alikuwa amemwagiza ajengeshe upya hekalu katika Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 36:23; ona Isaya 44:28.) Huko nyuma Yerusalemu katika mwaka wa 537 K.W.K., Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua walitumikia pia wakiwa na cheo katika “mbingu mpya” hizo za kiserikali, na mabaki ya Wayahudi waliorudishwa wakawa “dunia mpya,” jamii safi iliyoanzisha tena ibada safi katika nchi hiyo.—Ezra 5:1, 2.
5, 6. (a) Ni nini ambacho kingetoa ushuhuda kwamba walikuwa watu waliobadilika kweli kweli? (b) Yehova alipowakaripia, itikio lao lilitofautianaje na lile la kabla ya uhamisho?
5 Ili uwe ushahidi wa kwamba walikuwa watu waliobadilika katika akili na katika moyo, walihitajiwa watangulize katika maisha zao faida za ibada safi, waheshimu kweli kweli enzi kuu ya Yehova na kuwasikiliza manabii wake. Kupatana na hilo, kati ya mambo ya kwanza waliyofanya walipofika Yuda ni ‘ujenzi wa madhabahu ya Mungu wa Israeli’ na kutoa dhabihu.—Ezra 3:1-6.
6 Wakati maelekeo ya kupenda mali na kuogopa wanadamu yalipozuia kumalizwa kwa ujenzi wa hekalu, Yehova alikaripia watu kupitia manabii wake, nao wakasikiliza. (Hagai 1:2, 7, 8, 12; 2:4, 5) Baadaye, walipotajiwa kosa kubwa la kutofuata matakwa ya Torati juu ya ndoa, watu walisahihisha njia zao. (Ezra 10:10-12) Badala ya kuwa na macho ambayo, kwa njia ya mfano, hayakuwa yanaona na masikio yaliyokuwa hayasikii neno la Mungu, waliponeshwa kiroho, wakatumia akili zao kupatana na mapenzi ya Yehova. (Linganisha Isaya 6:9, 10 na 35:5, 6.) Matokeo yakawa ni kufanikishwa na Mungu kupatana na ahadi zinazopatikana katika Isaya 65:20-25.
7. Twajuaje kungekuwa na utimizo zaidi wa unabii wa Isaya?
7 Je! huo ulikuwa ndio utimizo pekee wa unabii kuhusu “mbingu mpya na dunia mpya”? Bila shaka sivyo. Petro mtume Mkristo alisema kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa wakitazamia kwa shauku utimizo zaidi. (2 Petro 3:13, New World Translation) Walichokuwa wakingojea sasa kinafunuliwa mbele ya macho yetu. Kwa njia gani? Kukamatana na matukio yanayohusu kutawazwa kwa Sairasi Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo aliyetukuzwa.
8. (a) Ni wakati gani Yehova alipotokeza hizo “mbingu mpya,” na hilo linalinganishwaje na utimizo wa kwanza wa unabii huo? (b) Idadi ya washiriki wa “mbingu mpya” imekuzwaje hatua kwa hatua?
8 Kama tulivyokwisha kuona, Yehova Mungu alimpa Mwanaye mamlaka katika mwaka wa 1914 aanze kutawala katikati ya adui zake. Zile “mbingu mpya” zilizongojewa muda mrefu zikatokea. Kilichotokea kilikuwa chenye utukufu mkubwa kuliko yale matukio yaliyohusiana na kukombolewa kwa Israeli wa kale. (Zaburi 110:2; Danieli 7:13, 14) Serikali iliyozaliwa mwaka wa 1914 inatawala hasa kutoka mbinguni, na Mungu ameipa mamlaka juu ya dunia yote. Kukuzwa kwa serikali hiyo kulitokea baadaye wakati walipofufuliwa wafuasi wa Kristo wapakwa-mafuta kwa roho (waliokuwa wamekwisha kufa), wawe wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Bwana wao. Kwa kuwa washiriki wengine wa jamii hiyo ya Ufalme wamemaliza maisha yao ya kidunia, nao pia wameongezwa kwenye idadi yenye kuongezeka ya washiriki wa “mbingu mpya.” (1 Wathesalonike 4:14-17; Ufunuo 14:13) Kufikia hapa walio wengi wa warithi washirika wa Kristo wanatawala sasa katika Ufalme huo wa kimbingu. Wakristo hao waliozaliwa kwa roho wenye kuungana hivyo pamoja na Kristo wanakuwa Yerusalemu Mpya, ambao juu yake Yehova alisema: “Tazama, naumba Yerusalema uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.”—Isaya 65:18, Zaïre Swahili Bible.
9. Ni “furaha” gani ambayo Yehova alifanyiza apa hapa duniani mwaka wa 1919?
9 Yehova hakufanyiza “furaha” katika mbingu tu, bali pia duniani. Mabaki wachache wa warithi wa Ufalme wangali hapa duniani. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mapadri wa Jumuiya ya Wakristo walitumia kichaa cha wakati wa vita ili wawashtaki hao Wanafunzi wa Biblia na kufanya washiriki wa Baraza Linaloongoza wahukumiwe vifungo vya muda mrefu. Lakini mwaka wa 1919 wakakombolewa, kwa hakika wakifunguliwa katika utumwa uliochochewa na Babeli (Babuloni) Mkuu. Kwa kutegemezwa na roho ya Yehova, walijipanga upya kuwa tengenezo la watu wenye kujitoa kwa kusudi tu la kuendeleza ibada safi na faida za Ufalme wa Mungu.
10. (a) Matazamio ya Waisraeli hao wa kiroho yalitofautianaje na yale ya Wayahudi waliorudishwa kwao mwaka wa 537 K.W.K.? (b) Ni kazi gani ambayo Yehova aliwapa wafanye? (c) Amewabarikije kwa wingi wakiwa bado duniani, na maandiko yaliyotumiwa katika fungu hili yanasimuliaje hali wanazofurahia?
10 Ingawa hivyo, matumaini na matazamio yao yalikuwa tofauti na yale ya Wayahudi waliorudia nchi yao mwaka wa 537 K.W.K. Washiriki wa Israeli wa kiroho walikuwa wakitazamia urithi “uliotunzwa mbinguni” kwa ajili yao. (1 Petro 1:3-5) Lakini kabla hawajapokea hasa zawadi hiyo, Yehova alikuwa na kazi aliyotaka wafanye. Kuhusu kazi hiyo, alisema hivi kiunabii: “Nitaweka maneno yangu katika kinywa chako, na kwa kivuli cha mkono wangu hakika nitakufunika wewe, ili kuzipanda mbingu na kuuweka msingi wa dunia na kusema kwa Sayuni, ‘Ninyi ni watu wangu.’” (Isaya 51:16, New World Translation) Aliweka “maneno” yake, ujumbe wake, katika kinywa cha watumishi wake ili watangaze duniani pote. Wakiwa na uhakika walianza kujulisha kwamba Mungu amezipanda “mbingu mpya” kwa dhati sana hivi kwamba wala wanadamu wala mashetani hawawezi kuzing’oa. Njia ambayo kwa hiyo Yehova ameshughulika na wawakilishi wa Sayuni wa kimbingu imewatambulisha waziwazi kuwa ni watu wake. Tofauti na hali yenye ukiwa wa kiroho na kiadili ya ulimwengu, ile “nchi” inayokaliwa na Israeli wa kiroho, shamba lao la utendaji, imekuwa mahali ambapo kanuni bora na shughuli za kiroho zinasitawi. Ni paradiso ya kiroho! (Isaya 32:1-4; 35:1-7; 65:13, 14; Zaburi 85:1, 8-13) Lakini namna gani “dunia mpya” iliyotabiriwa katika Isaya 65:17?
MATAYARISHO KWA AJILI YA “DUNIA MPYA”
11. (a) Hasa ni tangu lini Yehova amekuwa akitayarisha wanaotazamiwa kuwa washiriki wa “dunia mpya”? (b) Walifananishwa na watu gani walioondoka Babuloni wa kale?
11 Kuanzia hasa mwaka wa 1935, Yehova alifanya washiriki wa Israeli wa kiroho waone kwamba wakati ulikuwa umefika wa kukusanywa kwa umati mkubwa wa watu wenye matazamio ya uzima wa milele juu ya dunia-Paradiso. Wakilinganishwa na “kundi dogo” la warithi wa Ufalme, wamekuwa umati mkubwa kweli kweli. (Ufunuo 7:9, 10) Hao, pia, wameingizwa katika paradiso ya kiroho. Walifananishwa na watu wasio Waisraeli walioondoka Babuloni pamoja na Wayahudi mwaka wa 537 K.W.K. na pia wale walioondoka baadaye. (Ezra 2:58, 64, 65; 8:17, 20) Umati mkubwa wote huo wa mashahidi wa kisasa wa Yehova wenye matumaini ya kidunia ni watu wanaotazamiwa kuwa washiriki wa “dunia mpya.”
12. Watu wanatayarishwaje sasa ili waweze kuwa msingi unaofaa wa “dunia mpya”?
12 Wale watakaookoka dhiki kubwa na walio na taraja la uzima mkamilifu wa kibinadamu mbele yao kwa hakika watakuwa ndio msingi wa hiyo “dunia mpya,” watakuwa ndio washiriki wayo wa kwanza. Ni jambo la maana kwamba msingi huo uwe timamu. Hivyo, kwa sasa wanafundishwa kikamilifu katika njia za Yehova. Wanasaidiwa wapate kuthamini kwa moyo lile suala la enzi kuu ya ulimwengu mzima. Wanajifunza wajue jinsi inavyofaa sana ‘kumtumaini Yehova kwa moyo wao wote na si kutegemea akili zao wenyewe.’ (Mithali 3:5, 6) Wana nafasi ya kujithibitisha kuwa wenye bidii na waungaji-mkono washikamanifu wa Ufalme wa Mungu kwa kushiriki sana kutangaza “habari njema ya ufalme” sasa. (Mathayo 24:14) Wanaona kinachomaanisha kuwa sehemu ya jamii ya dunia yote ambayo katika hiyo watu kutoka mataifa yote na lugha na jamii za watu wanafanya kazi pamoja kwa udugu wenye upendo. (Yohana 13:35; Matendo 10:34, 35) Je! wewe binafsi unajitahidi ili ujifaidi kwa ukamili na programu hiyo ya elimu? Mbele kuna matazamio mazuri ajabu kwa wote wanaofanya hivyo.
“DUNIA MPYA” INATOKEA
13. “Dunia mpya” inayokuja itakuwaje utimizo wa ahadi ya Yehova ulio mkubwa zaidi ya ule uliotukia mwaka wa 537 K.W.K.?
13 Utimizo wa mwisho, ulio kamili wa ahadi ya Yehova ya kutokeza “dunia mpya” utakuwa mkubwa zaidi ya ule uliotukia mwaka wa 537 K.W.K. Wale walio sehemu ya “dunia mpya” hawatakuwa watu waliokombolewa kutoka Babeli Mkuu tu, bali pia hiyo milki nzima ya ulimwengu ya dini ya uwongo itakuwa imeangamizwa milele. (Ufunuo 18:21) Jamii hiyo ya kibinadamu yenye uadilifu—“dunia mpya”—haitazungukwa na mataifa yanayomsuta Yehova na kutesa watumishi wake, kama ilivyokuwa katika utimizo wa kwanza wa unabii wa Isaya. Kwa sababu zinakataa kutii enzi kuu ya Yehova, serikali zote za kibinadamu zitakuwa zimeondolewa kwa kuvunjwa-vunjwa, na jamii mbovu ya kibinadamu ya sasa itakuwa imekatiliwa mbali itoke duniani. (Danieli 2:44; Mithali 2:21, 22) Utaratibu Mpya wa Mungu wenye uadilifu utakapoanza, watu watakaokaa katika Dunia-sayari watakuwa wale tu wanaomheshimu Yehova, wanaofurahia kikamilifu njia zake.—Zaburi 37:4, 9.
14. (a) Maneno ya 2 Petro 3:13 na Ufunuo 21:1 yatatimizwa lini? (b) Tofauti itakuwa nini juu ya hali ambazo katika hizo “mbingu mpya” zitafanya kazi wakati huo? (c) Ni nani watakaotiwa katika “dunia mpya”?
14 Ni kwenye wakati huo wenye utukufu alikoelekezea fikira mtume Petro katika barua yake ya pili iliyoongozwa kwa roho ya Mungu. (2 Petro 3:13) Akielekeza kwenye tazamio ilo hilo lenye kusisimua, mtume Yohana aliripoti mambo mbalimbali ya ufunuo aliopewa, akisema: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu za kwanza na dunia ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena.” (Ufunuo 21:1, Zaïre Swahili Bible) Dhiki kubwa itakapokuwa imepita na Shetani na mashetani wake watakapokuwa wamefungwa katika shimo refu, muhula mpya utaanza. Ule uvutano mbaya sana wa Shetani na mashetani wake utakuwa umepita. Mfumo mzima wa mambo yake utakuwa umeharibiwa. Ndipo zile “mbingu mpya” zitakapotimiza kusudi la upendo la Yehova kwa viumbe wake bila kizuizi cho chote kutoka serikali zinazopuuza enzi kuu ya Yehova. Chini ya hizo “mbingu mpya” kutakuwa “dunia mpya” kweli kweli, yenye “mkutano mkubwa” ambao Mungu anatolea tazamio bora la uzima usio na mwisho katika Paradiso ya dunia yote yenye uzuri, shibe, furaha na amani. Utakapofika wakati wa Mungu uliowekwa ili wafu wafufuliwe, hao pia watakuwa na nafasi ya kuwa sehemu ya hiyo “dunia mpya” ambayo ndani yake uadilifu utakaa.—Ufunuo 20:12, 13.
15. Kwa nini ahadi iliyo katika Ufunuo 21:3, 4 ni ya maana kwako?
15 Kuhusu yale ambayo Mungu ameweka akiba kwa ajili ya wanadamu wakati huo, mtume Yohana alisikia tangazo hili kutoka mbinguni: “Tazama, hema ya Mungu ni pamoja na watu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake, na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao, atakuwa Mungu wao. Naye atapangusa kila chozi katika macho yao; wala mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa maana maneno ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufunuo 21:3, 4, Zaïre Swahili Bible) Uzima utakuwa wenye kusisimua kama nini!
16. Ni matazamio gani juu ya wakati ujao yanayoamshwa mioyoni mwetu na ahadi zilizo katika (a) Isaya 11:6-9? (b) Isaya 35:1-7? (c) Isaya 65:20-25? (d) Ni nani anayefanya matazamio hayo yenye kupendeza yawezekane kwetu?
16 Hali zilizokuwamo Edeni na ile miujiza iliyofanywa na Yesu inatoa mionjo ya jinsi maisha yatakavyokuwa katika hiyo “dunia mpya.” Tena, sehemu za mambo ya unabii wa Isaya 11:6-9 na Isaya 35:1-7 na 65:20-25 zitapata utimizo halisi wakati huo, iwe baraka kubwa kwa wanadamu watiifu. Itaburudisha kama nini wakati hali zinazohitajika sana za afya na ufanisi wa kiroho zitakapoweza kufurahiwa pamoja na ukamilifu wa mwili na wa akili katika dunia ambayo kwa kila jambo imefanywa kuwa Paradiso! Tukiwa na tazamio hilo la ajabu mbele yetu, tufanyeje vingine kuliko kuinua sauti zetu katika kumshukuru Yehova, yule Muumba Mkuu wa yote!