Sababu Kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia
Watu fulani wanasema Biblia haitegemeki, na maoni yao yamekubaliwa mahali pengi. Hivyo watu wengi leo wanasukuma kando mambo yanayosemwa na Biblia kwa kuyaona kuwa yasiyostahili kutumainiwa.
Kwa upande ule mwingine, lile ambalo Yesu Kristo alisema katika sala kwa Mungu linasaidia kuleta utumainifu: “Neno lako ndiyo kweli.” Na Biblia yenyewe inadai kuwa na uongozi wa roho ya Mungu.—Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16.
Wewe unafikiri nini juu ya jambo hilo? Je! kuna msingi timamu wa kuitumaini Biblia? Au je! kweli kuna ushahidi kwamba Biblia haitegemeki, kwamba inajipinga yenyewe na haina upatani?
Je! Inajipinga Yenyewe?
Ingawa huenda watu fulani wakadai kwamba Biblia inajipinga yenyewe, je! mtu ye yote amepata kukuonyesha wewe mfano halisi wa kuonyesha hivyo? Sisi hatujaona kamwe mfano ambao ungeweza kubaki na uthabiti baada ya kuchunguzwa sana. Ni kweli kwamba, huenda ikaonekana kama kuna mitofautiano katika masimulizi fulani ya Biblia. Lakini kwa kawaida tatizo ni ukosefu wa maarifa kuhusu mambo mengi madogo-madogo na hali zilizokuwako nyakati zinazohusika.
Kwa mfano, watu fulani wataonyesha jambo moja wanalofikiria kuwa mtofautiano katika Biblia, wakiuliza hivi: ‘Kaini alipata wapi mke wake?’ Dhana waliyo nayo ni kwamba Kaini na Abeli ndio peke yao waliokuwa watoto wa Adamu na Hawa. Lakini dhana hiyo imewekwa juu ya msingi wa ufahamu wenye makosa juu ya linalosemwa na Biblia. Biblia inaeleza kwamba Adamu “akazaa wana, waume na wake.” (Mwanzo 5:4) Hivyo Kaini alioa mmoja wa dada zake au inawezekana kwamba alioa mtoto wa dada yake mmoja.
Mara nyingi wachambuzi wanakuwa wakitafuta tu mambo yanayopingana na kwa hiyo huenda wakatangaza hivi: ‘Mathayo mwandikaji wa Biblia anasema kwamba afisa wa jeshi alimjia Yesu kuomba hisani, huku Luka akisema kwamba wawakilishi ndio waliotumwa wakaiombe. Ni yupi aliye sahihi?’ (Mathayo 8:5, 6; Luka 7:2, 3) Lakini je! huo ni mpingano wa kweli kweli?
Wakati utendaji au kazi ya watu inapohesabiwa kuwa imefanywa na yule aliye hasa na daraka la kuisimamia, mtu mwenye kufikiri vizuri hadai kwamba huo ni mtofautiano. Kwa mfano, je! wewe unafikiria ripoti kuwa yenye kosa ikisema kwamba meya alijenga barabara hata ingawa ujenzi wenyewe hasa wa barabara hiyo ulifanywa na wahandisi na wafanya kazi wake? Hapana, hufikiri hivyo! Vivyo hivyo, si ukosefu wa upatani Mathayo kusema kwamba afisa wa jeshi ndiye aliyemtolea Yesu ombi lakini, kama anavyoandika Luka, ombi hilo lilitolewa kupitia wawakilishi fulani.
Kadiri mambo zaidi madogo-madogo yanavyojulikana ile iliyoonekana kama mitofautiano katika Biblia inakuwa haionekani tena.
Historia na Sayansi
Usahihi wa kihistoria wa Biblia ulikuwa ukitiliwa shaka na watu wa mahali pengi wakati mmoja. Kwa mfano, wachambuzi walitia shaka kama kweli walikuwako watu wanaotajwa na Biblia kama Mfalme Sargoni wa Ashuru, Belshaza wa Babuloni, na gavana Mroma Pontio Pilato. Lakini magunduzi ya hivi majuzi yamethibitisha ukweli wa usimulizi mmoja wa Biblia baada ya mwingine. Hivyo mwanahistoria Moshe Pearlman aliandika hivi: “Kwa ghafula, watia-mashaka waliokuwa wameshuku unyofu hata wa sehemu za kihistoria za Agano la Kale walianza kurudia kusahihisha maoni yao.”
Ikiwa sisi tutaitumaini Biblia, ni lazima iwe sahihi pia katika mambo ya sayansi. Je! ndivyo ilivyo? Muda usio mrefu uliopita, kwa kupinganisha Biblia wanasayansi walishikilia sana kwamba ulimwengu wote mzima haukuwa na mwanzo. Hata hivyo, hivi majuzi mstadi wa kuchunguza nyota Robert Jastrow, alielekeza kwenye habari mpya zaidi zinazokanusha jambo hilo akieleza hivi: “Sasa sisi tumeona jinsi ushahidi wa elimu ya nyota unavyoongoza kwenye maoni ya Kibiblia juu ya asili ya ulimwengu. Yale mambo madogo-madogo yanatofautiana, lakini mawazo-asilia yaliyo katika masimulizi ya uchunguzi wa nyota na yale ya Kibiblia juu ya kitabu cha Mwanzo ni mamoja.”—Mwanzo 1:1.
Wanadamu wamebadili pia maoni yao yanayohusiana na umbo la dunia. Kitabu The World Book Encyclopedia, kinaeleza kwamba, “safari zilizofanywa baharini kugundua mambo zilionyesha kwamba ulimwengu ni wa mviringo, si tambarare kama vile watu walio wengi walivyokuwa wameamini.” Lakini Biblia ilikuwa sahihi muda wote ule! Miaka zaidi ya 2,000 kabla ya safari hizo za baharini, Biblia ilisema kwenye Isaya 40:22: “Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia,” au kama vile tafsiri nyingine zinavyosema, “tufe la dunia.” (tafsiri ya Douay), “muviringo wa dunia.” (Zaire Swahili Bible)
Hivyo kwa kadiri ambavyo wanadamu wanazidi kujua mambo, ndivyo ushahidi unavyokuwa mkubwa zaidi kwamba Biblia inaweza kutumainiwa. Mmoja aliyekuwa mkurugenzi wa Nyumba ya Makumbusho ya Uingereza, Sir Frederic Kenyon, aliandika hivi: “Matokeo ambayo tayari yamepatikana yanathibitisha jambo ambalo imani ingelidokeza, kwamba jambo moja tu linaloweza kutendeka ni kwamba Biblia itaendelea kuungwa mkono kwa kadiri ambavyo maarifa yanaendelea kuongezeka.”
Kuutabiri Wakati Ujao
Lakini je! sisi tunaweza kuyatumaini kweli kweli matabiri ya Biblia kwa wakati ujao, kutia na ahadi zayo za ‘mbingu mpya na dunia mpya zenye uadilifu’? (2 Petro 3:13, NW; Ufunuo 21:3, 4) Basi, katika wakati uliopita Biblia imekuwaje kwa habari ya kutegemeka? Mambo ya unabii yaliyotolewa hata mamia ya miaka mapema yametimia-timia kabisa hata katika mambo yale madogo-madogo!
Kwa mfano, Biblia ilitabiri juu ya kupinduliwa kwa Babuloni yenye nguvu nyingi karibu miaka 200 kabla jambo hilo halijatukia. Kwa kweli, Waamedi, waliojipanga upande mmoja na Waajemi, ndio waliotajwa kuwa washindi. Na ingawa Koreshi, mfalme Mwajemi, hakuwa amezaliwa wakati huo, Biblia ilitabiri kwamba angehusika sana katika ushindi huo. Ilisema kwamba maji ya Babuloni, ule mto Eufrati, “yatakaushwa,” na kwamba “malango [ya Babuloni] hayatafungwa.”—Yeremia 50:38; Isaya 13:17-19; 44:27–45:1.
Mambo hayo madogo-madogo yaliyotajwa waziwazi yalitimizwa, kama vile alivyoripoti mwanahistoria Herodoto. Tena, Biblia ilitabiri kwamba hatimaye Babuloni ungekuwa magofu yasiyokaliwa na watu. Na jambo hilo hasa ndilo lililotukia. Leo Babuloni ni rundo la mabomoko yasiyo na watu. (Isaya 13:20-22; Yeremia 51:37, 41-43) Na Biblia imejawa na mambo mengine ya unabii ambayo yamepata utimizo wa kutazamisha.
Basi Biblia inatabiri nini kuhusu mfumo wa mambo wa sasa wa ulimwengu? Inasema hivi: “Kipindi cha mwisho wa ulimwengu huu kitakuja kuwa wakati wa taabu-taabu. Watu hawatapenda kitu isipokuwa pesa na wao wenyewe; watakuwa wenye ufidhuli, wenye kujisifu, na wenye kutukana; bila heshima kwa wazazi, bila shukrani, bila staha kwa Mungu, bila shauku ya upendo wa kiasili . . . Watakuwa watu wanaoweka raha katika mahali pa Mungu, watu wanaoihifadhi namna ya nje-nje ya dini, lakini wao ni mkano thabiti wa uhakika wa kuwako kwayo.”—2 Timotheo 3:1-5, The New English Bible.
Kwa uhakika, sisi tunauona utimizo wa jambo hilo sasa! Lakini Biblia inatabiri pia kwa ajili ya “kipindi cha mwisho cha ulimwengu huu” mambo haya: “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme, na kutakuwako upungufu wa chakula.” Kwa kuongezea, “kutakuwako matetemeko ya dunia makubwa, na mahali hapa na mahali hapa magonjwa ya kipuku.”—Mathayo 24:7; Luka 21:11, NW.
Kwa kweli, mambo ya unabii wa Biblia yanaendelea kutimizwa leo! Basi, namna gani juu ya ahadi ambazo bado zitatimizwa, kama vile: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele,” na “Watafua panga zao ziwe majembe . . . , hawatajifunza vita tena kamwe”?—Zaburi 37:29; Isaya 2:4.
‘Hayo hayasadikiki,’ huenda watu fulani wakasema. Lakini kwa kweli, hatuna sababu ya kutia shaka juu ya jambo lo lote ambalo Muumba wetu anaahidi. Neno lake linaweza kutumainiwa! (Tito 1:2) Kwa kuuchunguza ushahidi zaidi, wewe utasadikishwa zaidi na zaidi juu ya jambo hilo.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, mitajo yote ya Biblia imetolewa katika Biblia ya Union Version na New World Translation of the Holy Scriptures (NW) ya Kiingereza.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
“Matokeo ambayo tayari yamepatikana yanathibitisha jambo ambalo imani ingelidokeza, kwamba jambo moja tu linaloweza kutendeka ni kwamba Biblia itaendelea kuungwa mkono kwa kadiri ambavyo maarifa yanaendelea kuongezeka.”