Sura ya 11
Je! Jina Lako Limo Katika Kitabu cha Uhai?
SARDISI
1. Ni nini iliyo hali ya kiroho ya kundi katika Sardisi, naye Yesu anaanzaje ujumbe wake?
KILOMETA zapata 48 kusini mwa Akhisari (Thiatira) wa ki-siku-hizi, ndipo mahali pa kundi linalofuata kupokea ujumbe kutoka kwa Yesu aliyetukuzwa: Sardisi. Katika karne ya sita kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, jiji hili lilikuwa ndilo jiji kuu lenye kiburi la ufalme wa kale wa Lidia na kao la Mfalme Kroeso mwenye utajiri mwingi sana. Kufikia siku ya Yohana, limeingia katika nyakati ngumu, na ile fahari yalo chini ya Kroeso ni historia tu. Hali moja na hiyo, kundi la Kikristo la huko limekuwa maskini kiroho. Kwa mara ya kwanza, Yesu haanzi ujumbe wake kwa neno la pongezi. Badala ya hiyo, yeye anasema: “Na kwa malaika wa kundi katika Sardisi andika: Hivi ndivyo vitu ambavyo husema yeye ambaye ana roho saba za Mungu na nyota saba, ‘Mimi najua matendo yako, ya kwamba wewe una jina la kwamba wewe u hai, lakini wewe u mfu.’”—Ufunuo 3:1, NW.
2. (a) Kuna umaana gani kwa Wakristo katika Sardisi kwamba Yesu ana “roho saba”? (b) Kundi la Sardisi lilikuwa na sifa gani, lakini mambo ya hakika yalikuwa nini?
2 Ni kwa nini Yesu ajitambulisha kuwa yeye “ambaye ana roho saba”? Kwa sababu roho hizi huwakilisha roho takatifu ya Yehova ikitiririka kwa ujazi wayo. Baadaye, Yohana anazieleza pia kuwa “macho saba,” kuonyesha mwono wenye kupenya ambao roho takatifu inampa Yesu. (Ufunuo 5:6, NW) Hivyo, yeye anaweza kugubua na kushughulikia hali yoyote ambayo huenda ikawako. (Mathayo 10:26; 1 Wakorintho 4:5) Lile kundi katika Sardisi lina sifa ya kuwa hai, lenye kutenda. Lakini Yesu anaweza kuona kwamba limekufa kiroho. Kwa wazi, walio wengi wa washiriki walo wamerudia utepetevu unaofanana na hali waliyokuwa nayo kabla ya kuwa Wakristo.—Linga Waefeso 2:1-3; Waebrania 5:11-14.
3. (a) Ni kwa nini imempasa “malaika wa kundi katika Sardisi” aangalie kwa njia maalumu uhakika wa kwamba Yesu ana “nyota saba”? (b) Ni shauri gani kali ambalo Yesu analipa kundi katika Sardisi?
3 Yesu anamkumbusha pia “malaika wa kundi katika Sardisi,” kwamba Yeye ndiye ambaye ana “nyota saba.” Yeye anashika hao wazee wa kundi katika mkono wake wa kulia, akiwa na mamlaka kuwaelekeza katika kazi yao ya kuchunga. Inawapasa wao kuweka mioyo yao katika ‘kujua hakika mwonekano wa kundi.’ (Mithali 27:23, NW) Kwa sababu hiyo, afadhali wasikilize kwa makini maneno ya Yesu yanayofuata: “Uwe mwenye kulinda, na kuimarisha vitu vinavyobaki vilivyokuwa tayari kufa, kwa kuwa mimi sikupata kuona matendo yako yakiwa yamefanywa kwa ukamili mbele za Mungu wangu. Kwa hiyo, endelea kukumbuka jinsi wewe umepokea na jinsi wewe ulisikia, na kuzidi kukishika, na kutubu. Kwa hakika usipoamka, mimi nitakuja kama mwivi, na wewe hutajua hata kidogo ni kwenye saa gani mimi nitakuja juu yako wewe.”—Ufunuo 3:2, 3, NW.
4. Maneno ya Petro yangesaidiaje kundi katika Sardisi “kuimarisha vitu vinavyobaki”?
4 Wazee katika Sardisi wanahitaji kukumbuka ile furaha waliyokuwa nayo kwanza wakati walipojifunza ule ukweli na zile baraka walizopokea wakati huo. Lakini sasa wao ni wafu kwa habari ya utendaji wa kiroho. Taa yao ya kikundi ilikuwa ikiwaka na kuzimika kwa kukosa kazi za imani. Miaka mingi huko nyuma, mtume Petro aliandikia makundi katika Esia (yaelekea kutia na Sardisi) wajenge uthamini kwa ajili ya zile habari njema tukufu ambazo Wakristo walikuwa wamekubali na zilizokuwa zimetangazwa “kwa roho takatifu iliyotumwa kutoka mbinguni”—kama inavyowakilishwa na zile roho saba za njozi ya Yohana. Petro alikumbusha pia Wakristo hao wa Esia kwamba wao walikuwa ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya mali ya pekee, ili wapate kutangaza kotekote sifa bora za mmoja ambaye aliwaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Petro 1:12, 25; 2 Petro 2:9, NW) Kutafakari juu ya kweli hizo za kiroho kutasaidia kundi katika Sardisi litubu na ‘kuimarisha vitu vinavyobaki.’—Linga 2 Petro 3:9, NW.
5. (a) Ni jambo gani lililoupata uthamini wa Wakristo katika Sardisi? (b) Ni jambo gani litakalotukia ikiwa Wakristo wa Sardisi hawaitikii shauri la Yesu?
5 Kwa wakati uliopo, uthamini na upendo wao kwa ajili ya ukweli ni kama moto ambao karibu umepoa. Ni makaa machache tu yanayoendelea kuwaka. Yesu anawatia moyo wapulize, wachochee moto huo, watubu dhambi ambazo katika hizo uzembe wao umewaongoza, na kuwa kundi hai kiroho tena. (Linga 2 Timotheo 1:6, 7.) La sivyo, wakati Yesu ajapo bila kutazamiwa—“kama mwivi”—kutekeleza hukumu, kundi katika Sardisi litakuwa haliko tayari.—Mathayo 24:43, 44.
Kuja “Kama Mwivi”
6. Yesu alikujaje “kama mwivi” katika 1918, na alikuta hali gani miongoni mwa waliodai kuwa wafuasi wake?
6 Onyo la Yesu kwamba yeye angekuja “kama mwivi” linafika mpaka ndani ya nyakati za ki-siku-hizi. Lilikuwa na tumizi la pekee kwa Wakristo walioishi mpaka kuingia katika siku ya Bwana. Upesi baada ya 1914, kulikuwako utimizo wa unabii wa Malaki: “‘Kwa ghafula Bwana wa kweli atakuja kwenye hekalu Lake, ambaye nyinyi watu mnatafuta, na mjumbe wa agano ambaye katika yeye nyinyi mnapendezwa. Tazama! Yeye atakuja kwa hakika,’ Yehova wa majeshi amesema.” (Malaki 3:1, NW; Ufunuo 1:10) Akiwa “mjumbe wa agano,” Yesu alikuja kukagua na kuhukumu wale waliodai kuwa wafuasi wake. (1 Petro 4:17) Wakati huo, katika 1918, Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imejitia katika umwagaji-damu katika Vita ya Ulimwengu 1, na ilikuwa mfu kabisa, kiroho. Hata Wakristo wa kweli, ambao kabla ya vita walikuwa wamehubiri kwa bidii, walipitia wakati wa lepe la usingizi wa kiroho. Baadhi ya wazee wao mashuhuri walitiwa gerezani, na utendaji wa kuhubiri ukakaribia kukoma. Wakati roho ya Yehova ilipoamsha Wakristo hawa mwaka uliofuata, si wote waliokuwa tayari. Baadhi yao, kama wale wanawali wapumbavu wa mfano wa Yesu, hawakutayarishwa kwa vifaa kiroho kwa ajili ya pendeleo la kumtumikia Yehova. Hata hivyo, kwa furaha, walikuwako wengi ambao, kama wale wanawali waangalifu, walikuwa wametii onyo la Yesu: “Fulizeni kulinda, basi, kwa sababu nyinyi hamjui wala siku yenyewe wala saa yenyewe.”—Mathayo 25:1-13, NW.
7. Ni kwa nini Wakristo leo wanahitaji kukaa hali wameamka?
7 Uhitaji wa Mkristo kuendelea kuwa chonjo haukumalizika mapema katika siku ya Bwana. Katika unabii wake mkubwa kuhusu “ile ishara wakati mambo yote haya yamekusudiwa kuja kwenye umalizio,” Yesu alitoa onyo lenye mkazo: “Kuhusu siku hiyo au saa hakuna mtu anayejua . . . Fulizeni kutazama, fulizeni kuamka, kwa maana nyinyi hamjui wakati uliowekwa ni lini. Lakini kitu ninachoambia nyinyi ninaambia wote, fulizeni kulinda.” (Marko 13:4, 32, 33, 37, NW) Ndiyo, mpaka saa ii hii, kila mmoja wetu, awe ni wa wapakwa-mafuta au wa ule umati mkubwa, anahitaji kukaa chonjo na kupiga vita dhidi ya kupeperushwa kuingia ndani ya usingizi wa kiroho. Siku ya Yehova ijapo ‘kama mwivi usiku,’ sisi na tupatikane tukiwa tumeamka kabisa ili tupokee hukumu yenye upendeleo.—1 Wathesalonike 5:2, 3; Luka 21:34-36, NW; Ufunuo 7:9.
8. Jamii ya Yohana imechocheaje watu wa Mungu leo wafulize kuwa hai kiroho?
8 Ile jamii ya Yohana leo yenyewe imeamka kuona uhitaji wa kuchochea watu wa Mungu waendelee kuwa hai kiroho. Kwa kusudi hilo, makusanyiko ya pekee hupangwa kotekote duniani mara kadhaa kila mwaka. Katika mwaka mmoja wa majuzi, hadhirina kwenye mikusanyiko ya wilaya 2,981 ilijumlika kuwa 10,953,744, na waumini wapya 122,701 wakabatizwa. Kwa zaidi ya miaka mia moja, ile jamii ya Yohana imetumia gazeti Mnara wa Mlinzi katika kutangaza jina na kusudi la Yehova. Katika kuitikia minyanyaso mikali wakati wa vile vita viwili vya ulimwengu, Mnara wa Mlinzi uliwaamsha Mashahidi wa Yehova kwenye bidii mpya kwa kutangaza makala kama vile “Wabarikiwa ni Wasioogopa” (1919), “Mwito Kwenye Tendo” (1925), na “Kushindwa kwa Mnyanyaso” (1942).
9. (a) Imewapasa Wakristo wote wawe wakijiuliza wenyewe nini? (b) Ni kitia-moyo gani kimetolewa na Mnara wa Mlinzi?
9 Kama vile katika Sardisi, ndivyo ilivyo katika makundi leo, uchunguzi mwendelevu wa kibinafsi ni wa muhimu kwa Wakristo wote. Sisi sote inatupasa tuendelee kujiuliza wenyewe: Je! ‘matendo yetu yamefanywa kikamili’ mbele za Mungu wetu? Bila ya kuhukumu wengine, je! sisi kibinafsi tunasitawisha ile roho ya kujidhabihu na kujitahidi kutoa utumishi wa nafsi yote kwa Mungu? Kuhusiana na hili gazeti Mnara wa Mlinzi limetoa kitia-moyo kwa kuzungumzia habari kama vile “Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo” na “Kuishi Si kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena.”a Tukiwa na misaada kama hiyo ya Kimaandiko, acheni sisi tuchungue utu wetu wa ndani-ndani zaidi tunapojaribu kutembea kwa unyenyekevu na kwa sala katika ukamilifu mbele za Yehova.—Zaburi 26:1-3; 139:23, 24.
“Majina Machache”
10. Ni jambo gani lenye kutia-moyo aliloona Yesu katika kundi katika Sardisi, na hilo limepasa lituathirije sisi?
10 Maneno ya Yesu yanayofuata kwa kundi la Sardisi yanatia moyo zaidi sana. Yeye anasema: “Hata hivyo, wewe una majina machache katika Sardisi ambayo hayakuchafua mavazi yao ya nje, nao watatembea pamoja na mimi katika meupe, kwa sababu wao wanastahiki. Yeye ambaye hushinda atapambwa hivyo mavazi ya nje meupe; na mimi kwa njia yoyote sitafuta jina lake kutoka kitabu cha uhai, bali mimi nitakiri jina lake mbele za Baba yangu na mbele ya malaika zake.” (Ufunuo 3:4, 5, NW) Je! maneno haya hayatuamshi na kuimarisha azimio letu la kuwa waaminifu? Kwa sababu ya uzembe upande wa baraza la wazee, kundi kwa ujumla huenda likaingia ndani ya usingizi wa kiroho. Hata hivyo, baadhi ya watu mmoja mmoja humo huenda wakajitahidi kishujaa kutunza utambulisho wao wa Kikristo ukiwa safi na bila kutiwa madoa na hivyo waendelee kuwa na jina zuri pamoja na Yehova.—Mithali 22:1.
11, 12. (a) Hata katika pindi ya ule uasi-imani mkubwa, ni lazima wengine wawe walikuwaje kama yale “majina machache” yenye uaminifu katika Sardisi? (b) Ni kitulizo gani kilichowajia Wakristo wa mfano wa ngano wakati wa siku ya Bwana?
11 Ndiyo, hayo “mavazi ya nje” yanarejeza kwenye utambulisho wa uadilifu wa mtu akiwa Mkristo. (Linga Ufunuo 16:15; 19:8.) Ni lazima Yesu achangamke moyo kuona kwamba, kujapokuwa utepetevu wa idadi iliyo kubwa, “majina machache,” Wakristo wapakwa-mafuta wachache katika Sardisi, bado wanafaulu kuendeleza utambulisho huu. Vivyo hivyo, wakati waliodai kuwa Wakristo walipovama katika Babuloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini bandia, wakati wa zile karne ndefu za ule uasi-imani mkubwa, ni lazima kuwe sikuzote kulikuwako watu wachache mmoja mmoja waliojaribu kufanya mapenzi ya Mungu, ijapokuwa vipingamizi vikubwa. Hawa walikuwa waadilifu kama ngano iliyofichwa kati ya mvuvumuko wa magugu ya kifarakano.—Ufunuo 17:3-6; Mathayo 13:24-29.
12 Yesu aliahidi kwamba yeye angekuwa pamoja na Wakristo hao mfano wa ngano “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Yeye anajua wao ni akina nani na ni jina gani zuri walilojifanyia wenyewe. (Mathayo 28:20, NW; Mhubiri 7:1) Ebu wazia shangilio la hao waaminifu ‘wachache’ ambao walikuwa wangali hai mwanzoni mwa siku ya Bwana! Mwishowe walitenganishwa na Jumuiya ya Wakristo iliyokufa kiroho nao walikusanywa wakaingizwa ndani ya kundi lenye uadilifu linalofanana zaidi na lile kundi katika Smirna.—Mathayo 13:40-43.
13. Ni baraka gani zilizo akibani kwa Wakristo wapakwa-mafuta ambao ‘hawachafui mavazi yao ya nje’?
13 Wale katika Sardisi ambao ni waaminifu mpaka mwisho na hawachafui utambulisho wao wa Kikristo wanafikia utimizo wa tumaini zuri ajabu. Baada ya kusimamishwa kwa Ufalme wa Kimesiya katika 1914, wanafufuliwa kwenye uhai wa kiroho na wakiwa washindi hupambwa mavazi meupe ya nje yakiwa ufananisho wa uadilifu wao usio na kasoro, wala waa. Wakiwa wamekwisha tembea katika ile njia yenye kusonga iongozayo kwenye uhai, watafurahia thawabu ya milele.—Mathayo 7:14; Ona pia Ufunuo 6:9-11.
Milele Katika Kitabu cha Uhai!
14. Kitabu cha uhai ni nini, na ni majina ya akina nani yaliyorekodiwa humo?
14 “Kitabu cha uhai,” ni nini na ni majina ya akina nani yatakayotunzwa humo? Kitabu, au hati-kunjo, cha uhai hurejezea rekodi ya watumishi wa Yehova wanaokuja katika mstari wa kupokea tuzo la uhai wa milele. (Malaki 3:16) Humu katika Ufunuo rejezo mahususi limefanywa kwenye majina ya Wakristo wapakwa-mafuta. Lakini majina ya wale walio katika mstari wa uhai wa milele duniani yamerekodiwa pia humo. Zaidi ya hilo, majina yanaweza ‘kufutwa’ katika kitabu hicho. (Kutoka 32:32, 33) Hata hivyo, wale wa jamii ya Yohana ambao majina yao yanabaki katika kile kitabu cha uhai mpaka kifo chao wanapokea uhai usioweza kufa katika mbingu. (Ufunuo 2:10) Haya ndiyo majina ambayo Yesu anakiri hasa mbele za Baba yake na mbele ya malaika Zake. Lo! ni kubwa mno jinsi gani thawabu hiyo!
15. Washiriki wa ule umati mkubwa wataandikishaje majina yao bila kufutika katika kitabu cha uhai?
15 Ule umati mkubwa, ambao majina yao yameandikwa pia katika kitabu cha uhai, watatoka katika dhiki kubwa wakiwa hai. Kwa kuzoea imani muda wote wa Utawala wa Mileani wa Yesu na wakati wa mtihani wenye kukata maneno unaofuata, hawa watathawabishwa na uhai wa milele katika Paradiso duniani. (Danieli 12:1; Ufunuo 7:9, 14; 20:15; 21:4) Ndipo majina yao yatakapobaki yameandikwa bila kufutika katika kitabu cha uhai. Kwa kujua kinachotolewa hapa kwa njia ya roho takatifu, je! wewe huitikii kwa idili waadhi hii ya Yesu yenye kurudiwarudiwa: “Acheni yeye ambaye ana sikio asikie ambacho roho husema kwa makundi”?—Ufunuo 3:6, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi Julai 15, 2005, na Machi 15, 2005.
[Picha katika ukurasa wa 57]
Jina lako na libaki katika kitabu cha uhai