Babiloni Mkubwa
Maana: Milki ya ulimwengu ya dini za uwongo, inayotia ndani dini zote ambazo mafundisho na matendo yake hayapatani na ibada ya kweli ya Yehova, Mungu wa pekee wa kweli. Baada ya Gharika ya siku za Noa, dini ya uwongo ilianzia Babeli (ambapo baadaye paliitwa Babiloni). (Mwa. 10:8-10; 11:4-9) Kisha, imani za kidini za Kibabiloni na matendo yalienea kwenye nchi nyingi. Kwa hiyo, Babiloni Mkubwa likawa jina linalofaa dini za uwongo kwa ujumla.
Ni mambo gani yanayomtambulisha Babiloni Mkubwa, anayetajwa katika kitabu cha Ufunuo?
Hawezi kuwa lile jiji la kale la Babiloni. Kitabu cha Ufunuo kiliandikwa mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. na kinaeleza mambo ambayo yangetukia hata wakati wetu. The Encyclopedia Americana yasema hivi: “Lile jiji [Babiloni] lilitwaliwa na Waajemi walioongozwa na Koreshi Mkuu mwaka wa 539 K.W.K. Baadaye Aleksanda Mkuu alipanga kufanya Babiloni liwe jiji kuu la milki yake ya mashariki, lakini baada ya kifo chake, Babiloni lilipoteza umaarufu wake hatua kwa hatua.” (1956, Buku la 3, uku. 7) Leo jiji hilo ni magofu yasiyokaliwa na watu.
Katika lugha ya mfano ya kitabu cha Ufunuo, Babiloni Mkubwa linatajwa kuwa “jiji kubwa,” “ufalme” unaotawala wafalme wengine. (Ufu. 17:18) Kama jiji, lingekuwa na mashirika mengi ndani yake; na kama ufalme unaotia ndani wafalme wengine katika milki yake, lingekuwa la kimataifa. Linasimuliwa kuwa lina uhusiano na watawala wa kisiasa na linachangia kwa wingi utajiri wa wanabiashara, huku likiwa sehemu ya tatu ‘ambayo imekuwa makao ya roho waovu’ na mtesaji wa ‘manabii na watakatifu.’—Ufu. 18:2, 9-17, 24.
Babiloni la kale lilijulikana sana kwa dini zake na ukaidi wake kwa Yehova
Mwa. 10:8-10: “Nimrodi . . . akajionyesha kuwa mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova. . . . Nao mwanzo wa ufalme wake ukawa Babeli [baadaye ukaitwa Babiloni].”
Dan. 5:22, 23: “Na wewe, [Belshaza mfalme wa Babiloni] . . . ulijiinua juu ya Bwana wa mbingu, . . . nawe umeisifu miungu minyonge ya fedha na ya dhahabu, shaba, chuma, miti na mawe, ambayo haioni chochote, wala kusikia chochote, wala kujua chochote; lakini hukumtukuza Mungu ambaye pumzi yako imo mkononi mwake na ambaye njia zako zote ni zake.”
Maandishi fulani ya kale yanasema hivi: “Kwa ujumla katika Babiloni kuna mahekalu 53 ya miungu mikuu, mahekalu madogo 55 ya Marduku, mahekalu madogo 300 kwa ajili ya miungu ya kidunia, mahekalu madogo 600 kwa ajili ya miungu ya kimbingu, madhabahu 180 kwa ajili ya mungu wa kike Ishtar, 180 kwa ajili ya miungu Nergali na Adadi na madhabahu mengine 12 kwa ajili ya miungu mbalimbali.”—Yamenukuliwa katika The Bible as History (New York, 1964), W. Keller, uku. 301.
The Encyclopedia Americana inaeleza hivi: “Ustaarabu wa Kisumeri [uliokuwa sehemu ya Babilonia] ulitawaliwa na makuhani; na mkuu wa serikali alikuwa lugal (kihalisi ‘mtu mkuu’), mwakilishi wa miungu.”—(1977), Buku la 3, uku. 9.
Kwa hiyo, Babiloni Mkubwa kama linavyotajwa katika Ufunuo ni la kidini. Kwa kuwa liko kama jiji na milki, si kikundi kimoja tu cha kidini bali hutia ndani dini zote zinazompinga Yehova, Mungu wa kweli.
Mafundisho na matendo ya kale ya kidini ya Babiloni yanapatikana katika dini ulimwenguni pote
“Misri, Uajemi, na Ugiriki ziliathiriwa na dini ya Kibabiloni . . . Mchanganyiko mkubwa wa mambo ya Kisemiti katika hadithi za kwanza za Kigiriki na pia katika madhehebu ya kwanza ya Kigiriki sasa unakubaliwa kwa ujumla na wasomi hivi kwamba hauhitaji maelezo zaidi. Mambo hayo ya Kisemiti kwa kadiri kubwa ni ya Kibabiloni hasa.”—The Religion of Babylonia and Assyria (Boston, 1898), M. Jastrow, Jr., uku. 699 na 700.
Miungu yao: Kulikuwako miungu mitatu-mitatu, na kati ya miungu yao kulikuwako miungu iliyowakilisha nguvu mbalimbali za asili na miungu iliyotumia uvutano wa pekee katika utendaji fulani wa wanadamu. (Babylonian and Assyrian Religion, Norman, Okla.; 1963, S. H. Hooke, uku. 14-40) “Utatu wa Plato, ukiwa tu mpangilio mpya wa miungu mitatu-mitatu ya watu wa kale, waonekana kuwa ndio utatu wenye kupatana na akili na falsafa wa sifa tatu-tatu, uliotokeza sehemu tatu za maana sana za utatu au miungu mitatu inayofundishwa na makanisa ya Kikristo. . . . Fundisho hilo la mwanafalsafa Mgiriki [Plato] la miungu mitatu . . . linapatikana katika dini zote za kale [za kipagani].”—Nouveau Dictionnaire Universel (Paris, 1865-1870), kilichohaririwa na M. Lachâtre, Buku la 2, uku. 1467.
Matumizi ya sanamu: “[Katika dini ya Mesopotamia] sanamu zilitimiza sehemu kubwa katika madhehebu na pia katika ibada ya watu binafsi, kama vile kuenea kwa mifano ya sanamu hizo kunavyoonyesha. Kwa msingi, iliaminiwa kwamba mungu alikuwa katika sanamu yake ikiwa sanamu hiyo ilikuwa na maumbo fulani pamoja na vifaa hususa, nayo ilitunzwa inavyofaa.”—Ancient Mesopotamia—Portrait of a Dead Civilization (Chicago, 1964), A. L. Oppenheim, uku. 184.
Imani kuhusu kifo: “Watu wala viongozi wa imani za kidini [katika Babiloni] hawakukubali kamwe uwezekano wa kuangamizwa kabisa kwa kiumbe kilichoumbwa. Kifo kilikuwa njia ya kuingia kwenye maisha ya aina nyingine.”—The Religion of Babylonia and Assyria, uku. 556.
Cheo cha makasisi: “Dini [ya Kibabiloni] huwatenganisha makasisi na watu wa kawaida.”—Encyclopædia Britannica (1948), Buku la 2, uku. 861.
Mazoea ya unajimu, uaguzi, uchawi, na ulozi: Mwanahistoria A. H. Sayce anaandika hivi: “[Katika] dini ya Babilonia ya kale . . . kila kitu na kila nguvu ya asili ilidhaniwa kuwa ina zi au roho, ambayo ingeweza kudhibitiwa na uchawi wa Shaman, au kasisi wa ulozi.” (The History of Nations, New York, 1928, Buku la 1, uku. 96) “Wakaldayo [Wababiloni] walifanya maendeleo makubwa katika uchunguzi wa nyota wakijitahidi kuvumbua wakati ujao kupitia nyota. Ufundi huo tunauita ‘unajimu.’”—The Dawn of Civilization and Life in the Ancient East (Chicago, 1938), R. M. Engberg, uku. 230.
Babiloni Mkubwa ni kama kahaba asiye na maadili, anayeishi maisha ya anasa bila aibu
Andiko la Ufunuo 17:1-5 lasema hivi: “‘Njoo, nitakuonyesha hukumu juu ya yule kahaba mkubwa anayekaa juu ya maji [watu] mengi, ambaye wafalme wa dunia walifanya uasherati naye, na wale ambao hukaa katika dunia walileweshwa kwa divai ya uasherati wake.’ . . . Na juu ya paji la uso wake jina, fumbo, lilikuwa limeandikwa: ‘Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa machukizo ya dunia.’” Andiko la Ufunuo 18:7, laongeza kwamba ‘alijitukuza mwenyewe na kuishi katika anasa isiyo na aibu.’
Je, si kweli kwamba mashirika makuu ya kidini yamekuwa na zoea la kushirikiana na watawala wa kisiasa ili wapate mamlaka na mali, ijapokuwa hilo limewafanya watu wa kawaida wateseke? Pia, je, si kweli kwamba makasisi wao wenye vyeo vya juu wanaishi kwa anasa, hata ijapokuwa wengi wa watu ambao wanapaswa kuwahudumia huenda wakawa ni maskini?
Kwa nini si kosa kuziona dini zinazodai kuwa za Kikristo, pamoja na wale wasiojua lolote kumhusu Mungu wa Biblia, kuwa sehemu ya Babiloni Mkubwa?
Yak. 4:4: “Enyi wazinzi, je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Kwa hiyo, ingawa wanajua yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu, wanajifanya kuwa adui zake ikiwa wanachagua urafiki pamoja na ulimwengu kwa kufuata njia za ulimwengu.)
2 Kor. 4:4; 11:14, 15: “Mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini, ili nuru ya habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, isipenyeze mwangaza.” “Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa kama wahudumu wake wakiendelea pia kujigeuza wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu. Lakini mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.” (Kwa hiyo, adui mkuu wa Yehova, Shetani Ibilisi mwenyewe, ndiye kwa kweli anayeheshimiwa na wote wasiomwabudu Mungu wa kweli kwa njia ambayo Yeye ameweka, ingawa huenda wakadai kwamba wao ni Wakristo. Ona pia 1 Wakorintho 10:20.)
Mt. 7:21-23: “[Yesu Kristo alisema:] Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia. Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”
Kwa nini ni muhimu kutoka Babiloni Mkubwa bila kukawia?
Ufu. 18:4: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.”
Ufu. 18:21: “Na malaika mwenye nguvu akainua jiwe kama jiwe kubwa la kusagia na kulitupa ndani ya bahari, akisema: ‘Hivi ndivyo Babiloni lile jiji kubwa litakavyotupwa chini kwa mtupo wa kasi sana, naye hatapatikana tena.’”
Luka 21:36: “Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”
Ni nini kitakachowapata watu ambao hawakujua ukweli wa Biblia bali waliishi na wakafa zamani wakiwa katika Babiloni Mkubwa?
Mdo. 17:30: “Ni kweli, Mungu ameachilia mbali nyakati hizo za kutojua, lakini sasa anawaambia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.”
Mdo. 24:15: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mungu ndiye atakayeamua ni akina nani kati ya “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa.)
Ayu. 34:12: “Kwa kweli, Mungu hatendi kwa uovu, na Mweza-Yote hapotoshi hukumu.”