Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 124-uku. 131
  • Kuteseka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuteseka
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtu Akisema—
  • Faraja kwa Wanaoteseka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kwa Nini Wanadamu Wanateseka na Kupatwa na Mambo Mabaya?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 124-uku. 131

Kuteseka

Maana: Jambo linalompata mtu anapokuwa na maumivu au taabu. Huenda kuteseka kukawa kwa kimwili, kiakili, au kihisia-moyo. Mambo mengi yanaweza kusababisha kuteseka; kwa mfano, madhara yanayotokana na vita na pupa ya kibiashara, udhaifu unaorithiwa, ugonjwa, misiba, “misiba ya asili,” mambo mabaya ambayo wengine husema au kufanya, kusumbuliwa na pepo, kujua msiba unaokaribia, au upumbavu wa mtu mwenyewe. Kuteseka kunakotokana na sababu hizo mbalimbali kutazungumziwa hapa. Hata hivyo, huenda pia mtu akateseka kwa sababu anawahurumia watu wengine walio katika hali mbaya au akateseka kwa sababu ya kuwaona watu wakitenda mambo yanayomvunjia Mungu heshima.

Kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka?

Ni nani hasa anayepaswa kulaumiwa?

Wanadamu wanastahili kulaumiwa kwa sababu ya kuteseka kwingi. Wao hupigana vita, hutenda uhalifu, huchafua mazingira, mara nyingi hufanya biashara kwa njia inayochochewa na pupa kuliko kuwahangaikia wanadamu wenzao, na nyakati nyingine hutenda mambo wanayojua yanaweza kudhuru afya yao. Waotenda mambo hayo, wao hujiumiza wenyewe na kuwaumiza wengine. Je, tutazamie kwamba wanadamu wanaweza kuepuka matokeo ya matendo yao? (Gal. 6:7; Met. 1:30-33) Je, ni jambo la busara kumlaumu Mungu kwa mambo hayo ambayo wanadamu wenyewe hufanya?

Shetani na roho wake waovu pia wana lawama. Biblia inafunua kwamba kuteseka kwingi hutokana na uvutano wa roho waovu. Kuteseka ambako watu wengi wanamlaumu Mungu hakutoki kwake hata kidogo.—Ufu. 12:12; Mdo. 10:38; ona pia ukurasa wa 272, 273, chini ya kichwa, “Shetani Ibilisi.”

Kuteseka kulianzaje? Kuchunguza sababu kunaelekeza fikira kwa wanadamu wa kwanza, ambao ni wazazi wetu, Adamu na Hawa. Yehova Mungu aliwaumba wakiwa wakamilifu, akawaweka katika mazingira ya paradiso. Kama wangemtii Mungu, hawangekuwa kamwe wagonjwa wala kufa. Wangefurahia milele uzima mkamilifu wa kibinadamu. Kuteseka hakukuwa sehemu ya kusudi la Yehova kwa wanadamu. Lakini Yehova alimwambia Adamu waziwazi kwamba alipaswa kutii ili aendelee kufurahia yale ambayo Yeye alikuwa amewapa. Kwa wazi, ilikuwa lazima wapumue, wale, wanywe, na kulala usingizi ili waendelee kuishi. Na ilikuwa lazima washike matakwa ya kiadili ya Mungu ili wafurahie uzima kikamili na wapewe pendeleo la kuendelea kuishi milele. Lakini walichagua kufuata njia yao wenyewe, kujiwekea viwango vyao wenyewe vya mema na mabaya, na hivyo wakamwacha Mungu, ambaye ni Mpaji-Uzima. (Mwa. 2:16, 17; 3:1-6) Dhambi ilileta kifo. Adamu na Hawa walizaa watoto wakiwa watenda-dhambi, nao hawangeweza kuwapa watoto wao kile ambacho hawakuwa nacho tena. Wote walizaliwa katika dhambi, wakiwa na maelekeo ya kutenda mabaya, udhaifu ambao ungeweza kuleta ugonjwa, urithi wenye dhambi ambao mwishowe ungetokeza kifo. Kwa sababu kila mtu duniani leo alizaliwa katika dhambi, sote tunateseka katika njia mbalimbali.—Mwa. 8:21; Rom. 5:12.

Andiko la Mhubiri 9:11 linasema kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” pia huathiri maisha yetu. Huenda tukaumia, si kwa sababu Ibilisi amesababisha jambo hilo moja kwa moja au kwa sababu mwanadamu yeyote amefanya hivyo, bali kwa sababu jambo fulani baya limetukia tukiwa mahali fulani wakati usiofaa.

Kwa nini Mungu hafanyi lolote ili kuwaletea wanadamu kitulizo? Kwa nini sisi sote tunateseka kwa sababu ya jambo ambalo Adamu alifanya?

Katika Biblia, Mungu anatuambia jinsi tunavyoweza kuepuka kuteseka kwingi. Ameandaa shauri bora zaidi kuhusu maisha. Shauri hilo linapofuatwa, hufanya maisha yetu yawe na kusudi, hutokeza maisha ya familia yenye furaha, hutuleta katika ushirika wa karibu pamoja na watu wanaopendana kikweli, na hutulinda tusitende mambo yanayoweza kusababisha tuteseke bure kimwili. Tukipuuza msaada huo, je, ni haki kumlaumu Mungu kwa taabu tunayojiletea sisi wenyewe na kuwaletea wengine?—2 Tim. 3:16, 17; Zab. 119:97-105.

Yehova amefanya uandalizi wa kumaliza kuteseka kote. Aliwaumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu, naye kwa upendo akawaandalia kila kitu ili maisha yawe mazuri kwao. Walipomwacha Mungu kimakusudi, je, Mungu alikuwa na wajibu wa kuingilia kati ili awalinde watoto wao wasipatwe na matokeo ya mambo ambayo wazazi wao walikuwa wamefanya? (Kum. 32:4, 5; Ayu. 14:4) Kama tunavyojua, mume na mke wanaweza kupata furaha inayotokana na kupata watoto, lakini pia wana madaraka. Mitazamo na matendo ya wazazi huwa na matokeo juu ya watoto wao. Hata hivyo, Yehova alionyesha fadhili za ajabu zisizostahiliwa kwa kumtuma duniani Mwana wake mpendwa ili autoe uhai wake uwe fidia, na kuandaa kitulizo kwa wazao wa Adamu ambao kwa kuthamini wangekuwa na imani katika uandalizi huo. (Yoh. 3:16) Matokeo ni kwamba, nafasi hiyo iko wazi kwa watu wanaoishi leo wapate kile ambacho Adamu alipoteza—uzima mkamilifu wa kibinadamu, bila kuteseka, katika dunia paradiso. Lo! Huo ni uandalizi mzuri kama nini!

Ona pia ukurasa wa 78-80, chini ya kichwa, “Fidia.”

Lakini kwa nini Mungu mwenye upendo aruhusu kuteseka kuendelee muda mrefu hivyo?

Je, sisi tumepata faida kwa sababu ameruhusu kuteseka mpaka sasa? “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyoona kukawia, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Ikiwa Mungu angewaua mara moja Adamu na Hawa, baada ya dhambi yao, hakuna mmoja kati yetu ambaye angekuwepo leo. Bila shaka sisi hatungependa mambo yawe hivyo. Zaidi ya hayo, kama Mungu angewaharibu watenda-dhambi wote wakati fulani baadaye, hatungezaliwa. Kwa kuwa Mungu ameruhusu ulimwengu huu wenye dhambi uwepo mpaka sasa, tumepata nafasi ya kuishi na kujifunza njia zake, tufanye mabadiliko yanayohitajiwa katika maisha yetu, na kujifaidi wenyewe na maandalizi yake ya upendo ya kupata uzima wa milele. Yehova ameonyesha kwamba ana upendo mkubwa kwa kutupatia nafasi hiyo ya kuishi. Biblia inaonyesha kwamba Mungu ameweka wakati wa kuuharibu ulimwengu huu mbovu, naye atauharibu hivi karibuni.—Hab. 2:3; Sef. 1:14.

Mungu anaweza, naye atayaondoa madhara yote ambayo huenda yakawapata watumishi wake katika ulimwengu huu. Mungu siye anayesababisha kuteseka. Lakini kupitia Yesu Kristo, Mungu atawafufua wafu, atawaponya watiifu magonjwa yao yote, ataondoa kabisa dhambi zote, naye hata ataondoa huzuni ya zamani kutoka katika akili zetu.—Yoh. 5:28, 29; Ufu. 21:4; Isa. 65:17.

Wakati ambao umepita umehitajiwa ili kumaliza masuala yaliyotokezwa katika Edeni. Ili kupata habari zaidi, ona ukurasa wa 272, 273, pia 352-354.

Sisi binafsi tunatamani sana kupata kitulizo. Lakini Mungu atakapochukua hatua, ni lazima iwe kwa faida ya wote wanaopenda mema, wala si wachache tu. Mungu hana ubaguzi.—Mdo. 10:34.

Mifano: Je, si kweli kwamba mzazi mwenye upendo anaweza kumruhusu mtoto afanyiwe upasuaji wenye maumivu kwa sababu ya faida ambazo mtoto anaweza kupata? Pia, je, si kweli kwamba tiba ya haraka-haraka tu kwa magonjwa mabaya mara nyingi inakuwa ya kijuujuu tu? Mara nyingi wakati mwingi huhitajiwa ili kuondoa kisababishi cha tatizo.

Kwa nini Mungu hakumsamehe Adamu na hivyo kuzuia kuteseka kubaya sana ambako wanadamu wanapata?

Je, kwa kweli kufanya hivyo kungezuia kuteseka au, kungemfanya Mungu alaumike? Ni jambo gani ambalo hutokea wakati baba anapoachilia tu kosa ambalo mtoto wake anafanya kimakusudi badala ya kuchukua hatua za kumtia nidhamu? Mara nyingi watoto hutenda kosa moja baada ya lingine, na baba hasa ndiye hulaumiwa.

Vivyo hivyo, ikiwa Yehova angesamehe dhambi ambayo Adamu alifanya kimakusudi, hilo kwa kweli lingemshirikisha Mungu katika kosa hilo. Jambo hilo halingeboresha hali duniani hata kidogo. (Linganisha na Mhubiri 8:11.) Zaidi ya hayo, lingewafanya malaika, ambao ni wana wa Mungu, wakose kumheshimu, nalo lingemaanisha kwamba hakuna msingi wa kweli wa kuwa na tumaini la jambo lolote lililo bora. Lakini hali kama hiyo haingetokea kamwe, kwa sababu uadilifu ni msingi usiobadilika wa utawala wa Yehova.—Zab. 89:14.

Kwa nini Mungu anaruhusu watoto wazaliwe wakiwa na kasoro kubwa za kimwili na akili?

Mungu hasababishi kasoro hizo. Aliwaumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu, wakiwa na uwezo wa kuzaa watoto wakamilifu wanaofanana nao.—Mwa. 1:27, 28.

Tumerithi dhambi kutoka kwa Adamu. Urithi huo unaweza kusababisha kasoro za kimwili na akili. (Rom. 5:12; kwa maelezo zaidi ona ukurasa wa 125, 126.) Sisi tuna urithi huo wa dhambi tangu wakati wa kutungwa mimba katika tumbo la uzazi. Hiyo ndiyo sababu Mfalme Daudi aliandika hivi: “Mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zab. 51:5) Ikiwa Adamu hangefanya dhambi, kungekuwako tabia nzuri tu za kurithi. (Ili kupata maelezo kuhusu Yohana 9:1, 2, ona ukurasa wa 151.)

Wazazi wanaweza kuwadhuru watoto wao ambao hawajazaliwa—kwa mfano, kwa kutumia dawa za kulevya au kwa kuvuta sigara wakati wa mimba. Hata hivyo, si kweli kwamba katika kila kisa mama au baba analaumika kwa kasoro za mtoto au afya mbaya ya mtoto wao.

Kwa sababu ya upendo wa Yehova, watoto pia wanaweza kufaidika kutokana na dhabihu ya fidia ya Kristo. Kwa sababu anawajali wazazi wanaomtumikia kwa uaminifu, yeye huwaona watoto wao wachanga kuwa watakatifu. (1 Kor. 7:14) Jambo hilo huwachochea wazazi wanaomwogopa Mungu wawe waangalifu kuhusu msimamo wao mbele za Mungu, kwa sababu wanawahangaikia watoto wao kwa upendo. Nao watoto walio na umri wa kutosha kuwa na imani na kuzitii amri za Mungu, wana pendeleo kutoka kwa Yehova la kuwa na msimamo unaokubalika wakiwa watumishi wake. (Zab. 119:9; 148:12, 13; Mdo. 16:1-3) Inafaa kukumbuka kwamba Yesu, aliyekuwa mrudisho mkamilifu wa utukufu wa Baba yake, alipendezwa kwa njia ya pekee na watoto, hata alimfufua mtoto fulani. Bila shaka ataendelea kufanya hivyo akiwa Mfalme wa Kimasihi.—Mt. 19:13-15; Luka 8:41, 42, 49-56.

Kwa nini Mungu anaruhusu “misiba ya asili,” inayosababisha hasara kubwa na kuwaua watu wengi?

Mungu hasababishi matetemeko ya nchi, tufani, mafuriko, ukame, na milipuko ya volkano ambazo hutajwa mara nyingi katika habari za leo. Yeye hatumii matukio hayo ili kuwaadhibu watu fulani. Kwa kadiri kubwa, mambo hayo husababishwa na nguvu za asili ambazo zimekuwako tangu kuumbwa kwa dunia. Biblia ilitabiri matetemeko makubwa ya nchi na upungufu wa chakula, mambo ambayo yangetukia katika wakati wetu, lakini hilo halimaanishi kwamba Mungu au Yesu ndio wanaoyasababisha, kama vile mtabiri wa hali ya hewa siye anayesababisha hali ya hewa anayotabiri. Mambo hayo hutukia pamoja na mambo mengine yote yaliyotabiriwa kuwa ishara yenye mambo mengi ya umalizio wa ulimwengu huu, kwa hiyo, hayo ni baadhi ya mambo yanayoonyesha kwamba baraka za Ufalme wa Mungu ziko karibu.—Luka 21:11, 31.

Mara nyingi wanadamu ndio hasa wanaopaswa kulaumiwa kwa sababu ya madhara yanayotokea. Kwa njia gani? Hata wanapopewa onyo la kutosha, watu wengi hukataa kutoka katika eneo la hatari au hukosa kuchukua tahadhari zinazohitajiwa.—Met. 22:3; linganisha na Mathayo 24:37-39.

Mungu anaweza kuzuia nguvu hizo za asili. Alimwezesha Yesu Kristo kutuliza upepo mkubwa juu ya Bahari ya Galilaya, ili kuonyesha yale ambayo Yeye atawafanyia wanadamu chini ya Ufalme Wake wa Kimasihi. (Marko 4:37-41) Kwa kumkataa Mungu, Adamu alikataa msaada kutoka kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe na wazao wake. Wale watakaopewa uzima wakati wa Utawala wa Kristo wa Kimasihi watauona utunzaji huo wenye upendo ambao serikali iliyowekwa na Mungu peke yake ndiyo inayoweza kuutoa.—Isa. 11:9.

Je, watu wanaopatwa na taabu wanaadhibiwa na Mungu kwa sababu ya kutenda maovu?

Wale wanaovunja viwango vya Mungu vya maisha hupata matokeo mabaya. (Gal. 6:7) Nyakati nyingine wao huvuna upesi mavuno machungu. Katika visa vingine, huenda wakaonekana wanafanikiwa kwa muda mrefu. Tofauti na hilo, Yesu Kristo, ambaye hakufanya kosa kamwe, alitendewa kikatili na kuuawa. Kwa hiyo, katika ulimwengu huu, ufanisi haupasi kuonwa kuwa uthibitisho wa kwamba mtu ana baraka ya Mungu, wala taabu isifikiriwe kuwa uthibitisho wa kwamba mtu amekataliwa na Mungu.

Ayubu alipopoteza mali zake naye akasumbuliwa na ugonjwa mbaya, hilo halikuwa kwa sababu ya kukataliwa na Mungu. Biblia inasema waziwazi kwamba Shetani ndiye aliyesababisha hayo. (Ayu. 2:3, 7, 8) Lakini rafiki waliokuja kumtembelea Ayubu walidai kuwa hali mbaya ya Ayubu ilithibitisha kwamba amefanya jambo ovu. (Ayu. 4:7-9; 15:6, 20-24) Yehova aliwakaripia, akisema: “Hasira yangu imewaka juu yako . . . kwa maana ninyi hamkusema mambo ya kweli kunihusu mimi kama mtumishi wangu Ayubu.”—Ayu. 42:7.

Huenda waovu wakafanikiwa kwa muda fulani. Asafu aliandika hivi: “Niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu. Wala hawamo katika taabu ya mwanadamu anayeweza kufa, wala hawapati mapigo kama wanadamu wengine. Wao hudhihaki na kuzungumza juu ya yaliyo mabaya; wanazungumza juu ya upunjaji kwa majivuno. Tazama! Hao ndio waovu waliostarehe mpaka wakati usio na kipimo. Wameongeza mali yao.”—Zab. 73:3, 5, 8, 12.

Siku ya Mungu ya kutoza hesabu itafika. Wakati huo atawaadhibu waovu, na kuwaharibu milele. Andiko la Methali 2:21, 22 linasema hivi: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” Hapo ndipo wanyoofu, ambao wengi wao wameteseka, watakapopata afya kamilifu na kufurahia mazao mengi ya dunia.

Mtu Akisema—

‘Kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka?’

Unaweza kujibu hivi: ‘Hilo ni jambo linalotuhangaisha sana sisi sote. Hebu nikuulize, Kwa nini umeuliza swali hilo leo?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘(Tumia habari katika ukurasa wa 124-128.)’ (2) ‘(Tumia maandiko mengine yanayoonyesha kwamba hali fulani hususa ambayo imemfanya mtu huyo binafsi ateseke itaondolewa.)’

Au unaweza kusema: (ikiwa wanahangaishwa na ukosefu wa haki ulimwenguni): ‘Biblia inaonyesha kwa nini hali hizi zipo leo. (Mhu. 4:1; 8:9) Je, unajua kwamba inaonyesha pia mambo ambayo Mungu atafanya ili atuletee kitulizo? (Zab. 72:12, 14; Dan. 2:44)’

Pia unaweza kusema: ‘Inaonekana wewe unamwamini Mungu. Je, unaamini kwamba Mungu ni upendo? . . . Je, unaamini kwamba yeye ni mwenye hekima na kwamba yeye ni mweza-yote? . . . Basi ni lazima awe ana sababu fulani nzuri za kuruhusu kuteseka. Biblia inaonyesha sababu hizo. (Ona ukurasa wa 124-128.)’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki