Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 51-53
  • Kitabu Cha Biblia Namba 8—Ruthu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Cha Biblia Namba 8—Ruthu
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA RUTHU
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Ndoa Isiyotazamiwa Kati ya Boazi na Ruthu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • “Mwanamke Bora Sana”
    Igeni Imani Yao
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ruthu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Mwanamke Bora Sana”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 51-53

Kitabu Cha Biblia Namba 8—Ruthu

Mwandikaji: Samweli

Mahali Kilipoandikiwa: Israeli

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 1090 K.W.K.

Wakati Uliohusishwa: Miaka 11 ya utawala wa waamuzi

1. (a) Ni kwa nini kitabu cha Ruthu ni zaidi ya kuwa tu hadithi ya mapenzi? (b) Ni mtajo gani wa kipekee unaopewa Ruthu katika Biblia?

KITABU cha Ruthu ni drama (mchezo wa kuigiza) yenye kupendeza ambayo yasitawi na kuwa hadithi nzuri sana ya mapenzi ya Boazi na Ruthu. Hata hivyo, si simulizi la mapenzi tu. Kusudi lacho si kutumbuiza. Kitabu hicho chakazia kusudi la Yehova la kutokeza mrithi wa Ufalme, na chatukuza fadhili zake za upendo. (Ruthu 1:8; 2:20; 3:10) Sifa yenye kupanuka ya upendo wa Yehova yaonekana katika kuchagua Mmoabi wa kike, aliyekuwa hapo awali mwabudu wa mungu mpagani Kemoshi, na ambaye aliongoka kwenye dini ya kweli, awe nyanya wa kale wa Yesu Kristo. Ruthu ni mmoja wa wanawake wanne wanaotajwa kwa jina katika nasaba ya kutoka Abrahamu hadi Yesu. (Mt. 1:3, 5, 16) Ruthu, pamoja na Esta, ni mmoja wa wanawake wawili ambao vitabu vya Biblia vinaitwa kwa majina yao.

2. Matukio ya Ruthu yalitukia lini, kitabu hicho kiliandikwa lini, na nani?

2 “Ikawa zamani za Waamuzi walipoamua . . . ” Kwa maneno hayo ya ufunguzi, kitabu cha Ruthu chaanza simulizi lenye kusisimua. Kutokana na maneno hayo yaeleweka kwamba kitabu chenyewe kiliandikwa baadaye, katika wakati wa wafalme wa Israeli. Hata hivyo, matukio yanayosimuliwa katika kitabu hicho yalihusisha kipindi cha miaka 11 hivi katika wakati wa waamuzi. Ingawa jina la mwandikaji halikutajwa, yaelekea sana alikuwa ni Samweli, ambaye pia yaonekana aliandika Waamuzi na ambaye alikuwa mtu mwaminifu wa kutokeza mwanzoni mwa kipindi cha wafalme. Kwa kuwa mistari ya kumalizia yadokeza kwamba Daudi alikuwa tayari anakuwa maarufu, hilo lingeweka kuandikwa kuwa karibu 1090 K.W.K. Samweli, ambaye aliijua sana ahadi ya Yehova juu ya “simba” kutoka kabila la Yuda, na ambaye alikuwa ametumiwa na Yehova katika kumpaka mafuta Daudi wa kabila hilo awe mfalme katika Israeli, angependezwa sana katika kufanyiza maandishi ya nasaba kufikia Daudi.—Mwa. 49:9, 10; 1 Sam. 16:1, 13; Ruthu 1:1; 2:4; 4:13, 18-22.

3. Ni mambo gani ya uhakika yanayothibitisha Ruthu kuwa chenye kukubalika?

3 Mamlaka ya kukubalika kwa Ruthu haijapata kutiliwa shaka. Uthibitisho wa kutosha wayo ulitolewa wakati Yehova alipopulizia uorodheshaji wa Ruthu katika nasaba ya Yesu kwenye Mathayo 1:5. Sikuzote Ruthu kimetambuliwa na Wayahudi kuwa sehemu ya maandishi ya Kiebrania yaliyokubaliwa. Basi, haishangazi kwamba visehemu-sehemu vya kitabu hicho vimepatikana miongoni mwa vitabu vingine vyenye kukubalika katika Hati-Kunjo za Bahari ya Chumvi ambazo ziligunduliwa kuanzia 1947. Zaidi ya hayo, Ruthu chapatana kabisa na makusudi ya Yehova ya Ufalme na pia matakwa ya Torati ya Musa. Ingawa ndoa pamoja na Wakanaani wenye kuabudu sanamu na Wamoabi ilikatazwa Waisraeli, hilo halikuzuia wageni kama vile Ruthu waliokubali ibada ya Yehova. Katika kitabu cha Ruthu, sheria juu ya kukomboa na ndoa ya ndugu-mkwe yafuatwa kabisa.—Kum. 7:1-4; 23:3, 4; 25:5-10.

YALIYOMO KATIKA RUTHU

4. Ni uamuzi gani unaomkabili Ruthu, na uchaguzi wake wadokeza nini juu ya namna ya ibada yake?

4 Uamuzi wa Ruthu wa kushikamana na Naomi (1:1-22). Hadithi hiyo yaanza wakati wa majira ya njaa kali katika Israeli. Mwanamume fulani wa Bethlehemu, Elimeleki, avuka Yordani pamoja na mke wake, Naomi, na wana wawili, Maloni na Kilioni, walowee (wakalie) kwa muda katika bara la Moabu. Kule wana hao waoa wanawake Wamoabi, Orpa na Ruthu. Msiba wapata familia hiyo, kwanza kwa kifo cha baba, na baadaye kifo cha wana wake wawili. Wanawake watatu waliofiwa na waume, wasio na watoto waachwa, wakiwa hawana mbegu kwa ajili ya Elimeleki. Akisikia tena kwamba Yehova amegeuza tena uangalifu wake kwa Israeli kwa kuwapa watu wake mkate, Naomi aamua kufunga safari ya kurudi Yuda alikozaliwa. Mabinti-wakweze wafunga safari pamoja naye. Naomi awasihi warudi Moabu, akiomba fadhili za upendo za Yehova ziwaandalie waume kutoka kwa watu wao wenyewe. Hatimaye Orpa ‘arejea kwa watu wake, na kwa miungu yake,’ lakini Ruthu, akiwa mwenye moyo mweupe na mwenye nguvu katika uongofu wake kwa ibada ya Yehova, ashikamana na Naomi. Uamuzi wake waonyeshwa vizuri katika maneno yake: “Wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu; na Mungu wako atakuwa Mungu wangu; pale utakapokufa nitakufa nami, na papo hapo nitazikwa; BWANA [Yehova, NW] anitende vivyo na kuzidi, ila kufa tu kutatutenga wewe nami.” (1:15-17) Hata hivyo, Naomi aliyefiwa na mume na asiye na mtoto, ambaye jina lake humaanisha “Uzuri Wangu,” ajipendekezea jina Mara, maana yake “Uchungu.”

5. Ruthu aonyesha sifa gani njema, na Boazi amtiaje moyo?

5 Ruthu aokota masazo ya mavuno katika konde la Boazi (2:1-23). Awasilipo katika Bethlehemu, Ruthu apata ruhusa ya Naomi akaokote masazo ya mavuno ya shayiri. Fikira za Boazi, mwenyeji wa shamba hilo, Myahudi mwenye umri mkubwa na ambaye ni mtu wa ukoo wa karibu wa baba-mkwe wake, Elimeleki, zavutwa kwake. Ingawa sheria ya Mungu yampa Ruthu haki za mwokota masazo ya mavuno, yeye aonyesha upole kwa kuuliza idhini ya kufanya kazi katika shamba hilo. (Law. 19:9, 10) Yatolewa mara moja, na Boazi amwambia aokote katika shamba lake tu pamoja na wanawake wachanga wake. Akisema kwamba amekwisha sikia juu ya mwenendo wake wa ushikamanifu kuelekea Naomi, amtia moyo kwa maneno haya: “BWANA [Yehova, NW] na akujazi kwa kazi yako, nawe upewe thawabu kamili na BWANA [Yehova, NW], Mungu wa Israeli, ambaye umekuja kukimbilia chini ya mabawa yake.” (Ruthu 2:12) Jioni hiyo Ruthu agawana kwa ukarimu matunda ya jasho lake pamoja na Naomi na kumweleza kwamba mafanikio yake katika kuokota masazo ya mavuno ni kwa ajili ya nia njema ya Boazi. Naomi aona katika hilo mkono wa Yehova, akisema: “Na abarikiwe huyo na BWANA [Yehova, NW], ambaye hakuuacha wema wake, wala kwa hao walio hai wala kwao waliokufa. . . . Mtu huyu ni wa mbari yetu, mmojawapo wa jamaa yetu aliye karibu [wakombozi wetu, NW].” (2:20) Ndiyo, Boazi ni mtu wa ukoo wa karibu, anayeweza kutokeza kisheria uzao kwa ajili ya Naomi katika jina la Elimeleki mfu. Ruthu aendelea kuokota masazo ya mavuno katika mashamba ya Boazi mpaka mavuno ya shayiri na mavuno ya ngano yanapofikia mwisho.

6. Ruthu aulizaje ndoa ya kukombolewa, na Boazi ajibu nini?

6 Boazi, akiwa mkombozi, amwoa Ruthu (3:1–4:22). Akiwa yeye ni mzee sana asiweze kuzaa watoto, Naomi amwagiza Ruthu awe badala yake katika ndoa ya ukombozi. Katika majira hayo ya maana, ilikuwa desturi kwa mwenye shamba asimamie binafsi upepetaji wa nafaka, jambo lililofanywa jioni kwa sababu ya pepezi (pepo za uanana) zilizovuma baada ya siku yenye joto. Boazi angekuwa amelala kwenye sakafu ya kupepetea, na hapo ndipo Ruthu ampata. Amjia kimya, afunua miguu yake, na kulala. Boazi aamkapo usiku-kati, Ruthu ajitambulisha na, kwa kupatana na utaratibu wa kidesturi wenye kufuatwa na wanawake wanapodai haki ya ndoa ya ndugu-mkwe, amwuliza atandaze joho lake juu yake.a Boazi ajulisha rasmi hivi, “Mwanangu, ubarikiwe na BWANA [Yehova, NW],” na amsifu kwa ajili ya kutofuatia wanaume vijana kwa sababu ya nyege au pupa. Badala ya kuwa mtu ambaye angefanya utongozi wa uhusiano usio safi, Ruthu afanyiza sifa ya kuwa “mwanamke mwema.” (3:10, 11) Hata hivyo, kama amwambiavyo sasa, kuna mkombozi mwingine aliye wa karibu zaidi yake; atashauriana na huyo asubuhi. Ruthu aendelea kulala penye miguu yake hadi alfajiri. Kisha Boazi ampa zawadi ya nafaka, naye arudi kwa Naomi, ambaye ataka sana kujua tokeo.

7. Boazi ashughulikiaje ndoa hiyo, na ni baraka gani inayotokea?

7 Boazi aenda mapema kwenye lango la jiji ili kumtafuta yule mkombozi. Akichukua kumi kati ya wanaume wazee wa jiji hilo kuwa mashahidi, ampa huyo mtu wa ukoo wa karibu nafasi ya kukomboa yote yaliyokuwa mali ya Elimeleki. Je! atafanya hivyo? Jibu lake la mara hiyo ni ndiyo ionekanapo aweza kuzidisha utajiri wake. Hata hivyo, ajuapo juu ya takwa la kwamba afanye ndoa ya ndugu-mkwe na Ruthu, ahofu kwa ajili ya urithi wake mwenyewe naye aonyesha kisheria katao lake kwa kuvua kiatu chake. Katika maandishi ya Biblia abaki bila jina, akitajwa tu bila heshima kuwa “fulani.” Mbele ya mashahidi ao hao, ndiposa Boazi amkomboa Ruthu kuwa mke wake. Je! anafanya hivyo kwa sababu yoyote ya ubinafsi? La, bali kwamba “jina la mwanamume huyo aliyekufa lisikatiliwe mbali.” (4:1, 10, NW) Watazamaji wote wauliza baraka za Yehova juu ya mpango huo wa upendo, na baraka hizo zawa nzuri ajabu! Ruthu azalia Boazi mwana katika umri wake wa uzee, na Naomi awa mlezi wa mtoto huyo. Aitwa ‘mwana aliyezaliwa Naomi’ na jina lake ni Obedi.—4:17.

8. Ni nini kinachoonyesha zaidi kwamba kutokezwa kwa Mbegu ya ahadi ni kupitia mpango wa Yehova?

8 Mistari ya kumalizia ya Ruthu yatoa nasaba kutoka Perezi, kupitia Boazi, hadi Daudi. Wachambuzi wengine wamebisha kwamba si vizazi vyote vilivyoorodheshwa, kwa kuwa kipindi cha wakati ni kikubwa mno kusiweze kuwapo watu wachache mno hivyo. Je! hiyo ni kweli? Au je! kila mmoja alibarikiwa kwa maisha marefu na mwana katika umri wake wa uzeeni? Mkataa wa mwisho waweza kuwa ndio sahihi, ukikazia kwamba kutokezwa kwa Mbegu aliyeahidiwa ni kwa mpango wa Yehova na kwa fadhili zake zisizostahiliwa, wala si kwa nguvu za asili za kibinadamu. Katika pindi nyingine Yehova alionyesha nguvu zake katika njia kama hiyo, kama katika kuzaliwa kwa Isaka, Samweli, na Yohana Mbatizaji.—Mwa. 21:1-5; 1 Sam. 1:1-20; Luka 1:5-24, 57-66.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

9. Wahusika wakuu katika drama ya Ruthu ni vielelezo vizuri kwetu leo katika njia zipi?

9 Maandishi hayo yenye kupendeza ni yenye mafaa bila shaka, yakisaidia wapendao uadilifu wajenge imani yenye nguvu. Wahusika wote wakuu katika drama hii yenye kusisimua walionyesha imani yenye kutokeza katika Yehova, nao ‘walishuhudiwa kwa sababu ya imani yao.’ (Ebr. 11:39) Walikuwa vielelezo vizuri kwa ajili yetu leo. Naomi alionyesha uhakika wenye kina kirefu katika fadhili za upendo za Yehova. (Ruthu 1:8; 2:20) Kwa nia Ruthu aliacha bara la kwao ili afuatie ibada ya Yehova; alijithibitisha kuwa mshikamanifu na mtiifu, na pia mfanya kazi mwenye nia. Uthamini mkubwa wa Boazi wa sheria ya Yehova na ukubali wake wa unyenyekevu wa kufanya mapenzi ya Yehova, na pia upendo wake kwa ajili ya Naomi mwaminifu, na Ruthu mwenye bidii ya kazi, ndivyo vilimwongoza afanye pendeleo hilo la ndoa ya ukombozi.

10. Ni kwa nini maandishi katika Ruthu yapasa kutia nguvu uhakika wetu katika ahadi za Ufalme?

10 Mpango wa Yehova wa ndoa, na katika pindi hii ndoa ya kukomboa, ulitumiwa kwa heshima yake. Yehova ndiye aliyekuwa Mpangaji wa ndoa ya Boazi na Ruthu, naye aliibariki kulingana na fadhili zake za upendo; aliitumia kuwa njia ya kuhifadhi nasaba isiyokatika ya kifalme ya Yuda ikiongoza kwa Daudi na hatimaye kwa Daudi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo. Uangalifu wa kulinda wa Yehova katika kutokeza Mrithi wa Ufalme kwa kulingana na mpango wake wa kisheria wapasa kutia nguvu uhakikisho wetu na kutufanya tutazamie kwa uhakika utimizo wa ahadi zote za Ufalme. Wapasa kutuchochea tuwe wenye shughuli nyingi katika kazi ya mavuno ya kisasa, tukiwa na uhakika wa malipo kamili kutoka kwa Yehova, Mungu wa Israeli wa kiroho, ambaye ‘tumekimbilia chini ya mabawa yake’ na ambaye makusudi yake ya Ufalme yanasonga mbele kwa utukufu sana yakatimizwe kikamili. (2:12) Kitabu cha Ruthu ni kiungo kingine cha muhimu katika maandishi yanayoongoza kwenye Ufalme huo!

[Maelezo ya Chini]

a Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa 829.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki