Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 106-111
  • Kitabu Cha Biblia Namba 20—Mithali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Cha Biblia Namba 20—Mithali
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA MITHALI
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Uongozi Timamu kwa Vijana wa Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Methali
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Pata Hekima na Ukubali Nidhamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Mwogope Yehova Nawe Utakuwa Mwenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 106-111

Kitabu Cha Biblia Namba 20—Mithali

Wanenaji: Sulemani, Aguri, Lemueli

Mahali Kilipoandikiwa: Yerusalemu

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 717 K.W.K.

1. Ni hekima gani inayopatikana katika kitabu cha Mithali?

WAKATI Sulemani, mwana wa Daudi, alipokuwa mfalme wa Israeli katika 1037 K.W.K., yeye alisali kwa Yehova kwa ajili ya “hekima na maarifa” ili ‘kuhukumu watu hawa wengi.’ Katika kujibu, Yehova alimpa ‘maarifa na hekima na uelewevu wa moyo.’ (2 Nya. 1:10-12; 1 Fal. 3:12; 4:30, 31, NW) Kama tokeo, Sulemani akaja ‘kunena mifano elfu tatu.’ (1 Fal. 4:32) Baadhi ya hekima hiyo iliyonenwa iliandikwa katika kitabu cha Biblia cha Mithali. Kwa kuwa hekima yake ilikuwa kwa kweli ile “Mungu aliyomtia moyoni,” basi kwa kuchunguza Mithali kwa kweli twachunguza hekima ya Yehova Mungu. (1 Fal. 10:23, 24) Mithali hizo zajumlisha kweli za milele. Ni za kisasa sasa kama zilivyokuwa hapo ziliposemwa mara ya kwanza.

2. Ni kwa nini wakati wa Sulemani ulifaa kutoa uongozi wa kimungu katika Mithali?

2 Utawala wa Sulemani ulikuwa wakati wenye kufaa wa kutoa uongozi huo wa kimungu. Sulemani alisemekana ‘anaketi juu ya kiti cha enzi cha Yehova.’ Ufalme wa kitheokrasi wa Israeli ulikuwa katika kilele cha fanaka, na Sulemani alipendelewa na “fahari ya kifalme.” (1 Nya. 29:23, 25) Ulikuwa wakati wa amani na utele, wakati wa usalama. (1 Fal. 4:20-25) Hata hivyo, hata chini ya utawala huo wa kitheokrasi, watu bado walikuwa na matatizo na magumu ya kibinafsi kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu. Kwamba watu hao wangemtumaini Mfalme Sulemani mwenye hekima awasaidie kutatua matatizo yao ni jambo lenye kueleweka. (1 Fal. 3:16-28) Katika kutamka hukumu katika visa vingi hivyo, yeye alisema semi za kimithali zilizofaana na hali nyingi za maisha zenye kutokea siku kwa siku. Semi hizo fupi lakini zenye kuvutia zilionwa kuwa hazina kubwa na wale waliotamani kurekebisha maisha zao kwa kulingana na mapenzi ya Mungu.

3. Mithali kilikujaje kukusanywa?

3 Maandishi hayasemi kwamba Sulemani aliandika Mithali. Hata hivyo, yasema kwamba ‘alinena’ mithali, pia kwamba ‘alitafuta-tafuta, akatunga mithali nyingi,’ hivyo kuonyesha kwamba alipendezwa kuhifadhi mithali kwa ajili ya matumizi ya baadaye. (1 Fal. 4:32; Mhu. 12:9) Katika wakati wa Daudi na Sulemani, kulikuwako waandishi rasmi katika orodha za maofisa wa baraza. (2 Sam. 20:25; 2 Fal. 12:10) Kama waandishi hao katika baraza waliandika na kukusanya mithali zake, sisi hatujui, lakini semi za mtawala yeyote wa jinsi hii zingeheshimiwa sana na kwa kawaida zingeandikwa. Hukubaliwa kwa ujumla kwamba kitabu hicho ni mkusanyo uliojumlishwa kutokana na mikusanyo mingine.

4. (a) Kitabu cha Mithali hugawanywaje kwa ujumla? (b) Ni nani mwanzilishi wa sehemu kubwa ya mithali?

4 Kitabu cha Mithali chaweza kugawanywa katika sehemu tano. Hizo ni: (1) Sura 1-9, zikifungua na maneno, “Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi”; (2) Sura 10-24, zinazoelezwa kuwa “Mithali za Sulemani”; (3) Sura 25-29, sehemu inayoanza hivi: “Hizi nazo ni mithali za Sulemani, ambazo, watu wa Hezekia, mfalme wa Yuda, walizinakili”; (4) Sura 30, inayotangulizwa kuwa “Maneno ya Aguri bin Yake”; na (5) Sura 31, ambayo yajumulisha “Maneno ya mfalme Lemueli; mausia aliyofundishwa na mama yake.” Kwa hiyo Sulemani alikuwa mwanzilishi wa sehemu kubwa ya mithali. Kwa habari ya Aguri na Lemueli, hakuna lolote hususa linalojulikana juu ya kitambulisho chao. Waelezaji wengine wadokeza kwamba Lemueli laweza kuwa lilikuwa jina jingine la Sulemani.

5. Mithali kiliandikwa na kukusanywa lini?

5 Mithali kiliandikwa na kukusanywa lini? Sehemu kubwa bila shaka iliandikwa wakati wa utawala wa Sulemani (1037-998 K.W.K.) kabla ya kukengeuka kwake. Kwa sababu hakuna uhakika wa utambulisho wa Aguri na Lemueli, haiwezekani kuipa habari yao tarehe. Kwa kuwa mojawapo mikusanyo hiyo ulifanywa katika utawala wa Hezekia (745-717 K.W.K.), haingewezekana kuwa kwamba mkusanyo wa mwisho ulifanywa kabla ya utawala wake. Je! ile migawanyo miwili ya mwisho ilikusanywa pia chini ya mamlaka ya Hezekia? Katika kujibu kuna kielezi-chini kinachotoa nuru kuhusu Mithali 31:31 katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References: “[Chapa] fulani za maandishi ya [Kiebrania] zaonyesha traigramatoni, au herufi tatu, Chehth, Za’yin, Qohph (חזק) ambazo zasimama kuwa saini ya Mfalme Hezekia ya kazi ya kunakili iliyofanywa na waandishi wake ili kuonyesha kwamba kazi hiyo ilikuwa imekamilishwa.”

6. Mithali ni nini, na ni kwa nini kichwa cha Kiebrania cha kitabu hicho chafaa?

6 Hapo kwanza katika Biblia za Kiebrania kitabu hicho kiliitwa kwa neno la ufunguzi, mish·lehʹ, maana yake “mithali.” Mish·lehʹ ni namna ya wingi, hali-muundo, ya kiwakilishi cha Kiebrania ma·shalʹ, kiwakilishi ambacho kwa ujumla hudhaniwa chatokana na neno la msingi linalomaanisha “kuwa kama” au “kuwa -enye kulinganika.” Maneno hayo yaeleza vizuri yaliyomo katika kitabu hicho, kwa maana mithali ni semi zenye nguvu ambazo mara nyingi hutumia ufanani au ulingani na ambazo zimekusudiwa kumfanya msikiaji afikiri. Namna fupi ya mithali yazifanya ziwe rahisi kueleweka na zenye kupendeza, na katika namna hiyo yazifanya kuwa rahisi kufundisha, kujuliwa, na kukumbukwa. Wazo hukwamilia.

7. Ni nini kinachopasa kuangaliwa juu ya mtindo wa Mithali?

7 Pia mtindo wa usemi katika kitabu hiki ni wenye kupendeza sana. Ni wa mtindo wa kishairi wa Kiebrania. Muundo wa sehemu kubwa ya kitabu hiki ni ushairi wenye ulingani. Hilo halifanyi miisho ya mistari au beti kuwa yenye vina vilevile, au kutoa sauti ileile. Wahusisha kufanya mistari-wizani ileile itoe mafikira au mawazo yanayofanana. Uzuri na nguvu za kuagiza kwao vimo ndani ya huu wizani-wazo. Huenda mawazo yakawa ashibahi (yenye maana moja) au adhidadi (yenye maana kinyume), lakini nguvu za ulingani zipo ili kupanua wazo, kuzidisha wazo, na kuhakikisha kupokeza maana katika wazo. Vielelezo vya ulingani wa adhidadi vyapatikana kwenye Mithali 11:25; 16:18, na 18:15, navyo vielelezo vya ulingani wa adhidadi ambavyo ni vingi zaidi kwenye Mithali 10:7, 30; 12:25; 13:25; na 15:8. Aina nyingine ya muundo yapatikana mwishoni kabisa mwa kitabu hicho. (Mit. 31:10-31) Ile mistari 22 iliyopo imepangwa ili kwamba katika Kiebrania kila mmoja waanza na herufi yenye kuandama ya alfabeti ya Kiebrania, hiyo ikiwa ni mtindo wa kiherufi unaotumiwa pia katika hesabu fulani ya zaburi. Kwa habari ya uzuri, mtindo huu hauna kifani katika maandishi ya kale.

8. Matumizi ya Mithali na Wakristo wa kwanza yashuhudiaje uasilia wacho?

8 Uasilia wa Mithali waonyeshwa pia na matumizi mapana ya kitabu hiki na Wakristo wa mapema katika kueleza viwango vya mwenendo. Yaonekana Yakobo alizoeleana na Mithali na alitumia kanuni zayo za msingi katika shauri zuri alilotoa la mwenendo wa Kikristo. (Linganisha Mithali 14:29; 17:27 na Yakobo 1:19, 20; Mithali 3:34 na Yakobo 4:6; Mithali 27:1 na Yakobo 4:13, 14.) Manukuu ya moja kwa moja kutoka Mithali yapatikana pia katika vifungu vifuatavyo: Warumi 12:20—Mithali 25:21, 22; Waebrania 12:5, 6—Mithali 3:11, 12; 2 Petro 2:22—Mithali 26:11.

9. Mithali chapatanaje na sehemu inayobaki ya Biblia?

9 Kuongezea hayo, Mithali chajionyesha kuwa chapatana na sehemu nyinginezo za Biblia, hivyo kuthibitisha hicho ni sehemu ya “Andiko lote.” Kinatoa umoja wa wazo wenye kutokeza kinapolinganishwa na Sheria ya Mungu, kufundisha kwa Yesu, na maandishi ya wanafunzi na mitume wa Yesu. (Ona Mithali 10:16—1 Wakorintho 15:58 na Wagalatia 6:8, 9; Mithali 12:25—Mathayo 6:25; Mithali 20:20—Kutoka 20:12 na Mathayo 15:4.) Hata wakati wa kugusia mambo kama vile kutayarisha dunia kwa ajili ya kukaliwa na binadamu, kuna umoja wa kufikiri pamoja na waandikaji wengine wa Biblia.—Mit. 3:19, 20; Mwa. 1:6, 7; Ayu. 38:4-11; Zab. 104:5-9.

10, 11. Ni nini kinachoshuhudia zaidi upulizio wa kimungu wa kitabu hicho?

10 Pia lenye kushuhudia upulizio wa kimungu wa kitabu hicho ni usahihi wacho wa kisayansi, iwe mithali inahusisha kanuni za kikemia, kitiba au kiafya. Mithali 25:20 yaelekea yatuambia juu ya michemko ya asidi-alikali. Mithali 31:4, 5 hukubaliana na utafiti wa sayansi ya kisasa kwamba kileo hudhoofisha taratibu za kufikiri. Madaktari wengi na wataalamu wa ulaji unaofaa hukubali kwamba asali ni chakula chenye afya, ikikumbusha mithali hii: “Mwanangu, ule asali, kwa maana ni njema.” (Mit. 24:13) Uchunguzi mbalimbali wa kisasa juu ya uhusiano baina ya mwili na hisia za ndani si jambo jipya kwa Mithali. “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri.”—17:22; 15:17.

11 Kweli kweli, kitabu cha Mithali kinahusisha kikamili kila uhitaji na hali ya kibinadamu hata kwamba mjuzi mmoja alieleza hivi: “Hakuna ukamatano wowote maishani usio na agizo lao linalofaa, hakuna elekeo jema au lenye uovu lisilo na kichocheo au sahihisho linalofaa. Kila mahali fahamu ya kibinadamu yakamatanishwa kikaribu na Mungu, . . . na binadamu hutembea katika kuwapo kwa Mfanyizaji na Hakimu wake . . . Kila aina ya binadamu yapatikana katika kitabu hiki cha kale; na ingawa kilichorwa miaka elfu tatu iliyopita, kingali cha kweli kuhusu asili kama kwamba sasa ndipo chatolewa kutoka mwakilishi wacho aliye hai.”—Dictionary of the Bible cha Smith, 1890, Buku 3, ukurasa 2616.

YALIYOMO KATIKA MITHALI

12. (a) Ni shairi gani lenye kukamatana linalofanyiza sehemu ya kwanza ya Mithali? (b) Kinafundisha nini kuhusu hekima na mwenendo wa kibinadamu? (c) Mithali 1:7 pawekaje kigezo cha kitabu chote?

12 Sehemu ya Kwanza (1:1–9:18). Hili ni shairi lenye kukamatana lililofanyizwa kwa hotuba fupi-fupi kama kwamba kutoka kwa baba kuelekea kwa mwana, lashughulika na uhitaji wa hekima ili iongoze moyo, au mtu mzima wa ndani, na kuelekeza tamanio. Chafundisha thamani ya hekima na baraka zayo: furaha, upendezi, amani, na uhai. (1:33; 3:13-18; 8:32-35) Chatofautisha hilo na ukosefu wa hekima na matokeo ya hilo: kutaabika na hatimaye kifo. (1:28-32; 7:24-27; 8:36) Kikizungumza juu ya hali na nafasi za maisha zisizo na mwisho, chatolea mtu uchunguzi wa msingi katika mwenendo wa kibinadamu na matokeo ya wakati huu na wakati ujao ya mwenendo huo. Maneno kwenye Mithali 1:7, NW, yanaweka kigezo cha kitabu chote: “Hofu kwa Yehova ndiyo mwanzo wa maarifa.” Vitendo vyote lazima vionyeshe kwamba Yehova anafikiriwa. Kuna kukariri daima uhitaji wa kutosahau sheria za Mungu, kukaribia amri zake na kutoziacha.

13. Onyesha ulingani mashuhuri uliomo katika sehemu yote ya kwanza ya Mithali.

13 Ulingani mashuhuri unaopatikana katika kiini cha sehemu hii ya kwanza ni hekima inayotumika, maarifa, hofu kwa Yehova, nidhamu, na busara. Maonyo yatolewa juu ya wenzi wabaya, kukataa nidhamu ya Yehova, na uhusiano usiofaa pamoja na wanawake wageni. (1:10-19; 3:11, 12; 5:3-14; 7:1-27) Mara mbili, hekima yaelezwa kuwa imo katika sehemu za umma, hivyo yaweza kupatikana, ipo. (1:20, 21; 8:1-11) Inaonyeshwa kuwa yenye utu na hunena kwa kuvutia na asiye na ujuzi, hata kuangaza kadiri fulani juu ya uumbaji wa dunia. (1:22-33; 8:4-36) Hiki ni kitabu cha kustaajabisha kama nini! Sehemu hii yafunga kwa kichwa kikuu cha habari cha ufunguzi, kwamba “hofu kwa Yehova ndiyo mwanzo wa hekima.” (9:10, NW) Kotekote, chatoa hoja kwamba kutambua Yehova katika njia zetu zote, pamoja na ushikamano wetu na uadilifu wake, ndiyo njia ya uhai na kwaweza kutulinda na mengi yasiyotamanika.

14. Ni ulingani gani wenye kutofautiana unaofanyiza mafundisho yenye kutumika ya Mithali yatokeze?

14 Sehemu ya Pili (10:1–24:34). Hapa twapata kanuni nyingi bora, zisizokamatana ambazo zinatumikisha hekima kwa hali zenye kutatanika za maisha. Kwa kutufunza matumizi yanayofaa, kinalenga kuhimiza furaha kubwa zaidi na maisha yenye kupendeza. Tofauti katika ulingani zafanya mafundisho hayo yatokeze katika akili zetu. Hapa pana kisehemu cha orodha ya habari ambazo zimezungumzwa katika sura 10, 11, na 12:

upendo kinyume cha chuki

hekima kinyume cha upumbavu

unyoofu kinyume cha kulaghai

uaminifu kinyume cha uchongezi

ukweli kinyume cha ubandia

ukarimu kinyume cha unyimivu

bidii kinyume cha ulegevu

kutembea katika ukamilifu kinyume cha njia zilizo kombo

shauri jema kinyume cha ukosefu wa mwelekezo wa ustadi

mke mwenye kuweza mambo kinyume cha mke mwenye kuaibisha

uadilifu kinyume cha uovu

kiasi kinyume cha kimbelembele

Kufikiria orodha hii kwa kukamatana na maisha ya kila siku lazima kutusadikishe kwamba Mithali ni kitabu kinachotumika kweli kweli!

15. Toa vielelezo kadhaa vya hali mbalimbali za kibinadamu zinazoshughulikiwa katika Mithali.

15 Salio la sehemu hii (13:1–24:34) laendelea na vikumbusho vyayo vya viwango vya Yehova ili tuwe na muono-ndani na busara. Orodha ya hali nyingi mbalimbali za kibinadamu zilizoshughulikiwa itaonyesha jinsi kitabu hiki kinavyohusisha mambo mengi. Kuna mafaa sana kuwa na shauri hili la Biblia juu ya kujifanya, kimbelembele, kutimiza ahadi, werevu, mashirika, usahihisho na mazoezi ya mtoto, maoni ya binadamu juu ya yaliyo haki, kutokasirika upesi, hisani kwa wenye taabu, upunjaji, sala, dhihaka, uradhi na vitu vya lazima maishani, kiburi, faida isiyo ya haki, rushwa, mashindano, kujiweza, kujitenga, kimya, kuegemea upande mmoja, kugombana, unyenyekevu, anasa, kutunza baba na mama, vileo, kulaghai, sifa za mke, zawadi, kuazima, kukopesha, fadhili, siri, mambo ya mali, kujenga watu wa nyumbani, husuda, kulipa kisasi, ubatili, jibu pole, kutafakari, na uenzi wa kweli. Huo ni utajiri kweli kweli wa shauri la kutumiwa ili kupata uongozi timamu wa mambo ya kila siku! Kwa wengine, baadhi ya mambo hayo huenda yakaonekana si ya maana, lakini hapa twaona kwamba Biblia haipuuzi mahitaji yetu hata katika mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa madogo. Katika hilo, Mithali ni chenye thamani isiyokadirika.

16. Ni shauri gani lenye kujenga linalotolewa katika sehemu ya tatu ya Mithali?

16 Sehemu ya Tatu (25:1–29:27). Shauri lenye kujenga latolewa juu ya mambo kama staha, saburi, maadui, kushughulika na wapumbavu, kujifurahisha, kurai-rai, wivu, umizo linalosababishwa na rafiki, njaa, uchongezi, kuangalia daraka, riba, ungamo, matokeo ya utawala mwovu, kichwa kigumu, baraka za utawala wa uadilifu, kutokutii sheria kwa watoto, jinsi ya kutendea watumishi, muono-ndani, na njozi.

17. (a) Ni “mausia” gani anayotoa Aguri? (b) Anaeleza juu ya mafungu gani tofauti ya vitu vinne?

17 Sehemu ya Nne (30:1-33). Haya ni “mausia” anayohesabiwa Aguri. Baada ya kukubali kwa unyenyekevu juu ya yeye kutokuwa wa maana, mwandikaji huyo arejezea kwa binadamu ambaye hawezi kuumba dunia na vitu vilivyomo. Aita Neno la Mungu kuwa lililosafishwa na ngao. Auliza kwamba neno la kusema uwongo liondolewe kwake na kwamba asipewe ama utajiri wala umaskini. Aeleza juu ya kizazi kisichotakata, chenye kiburi, na chenye pupa kinacholaani wazazi. Vitu vinne ambavyo havijasema ‘vimeshiba’ vyatambulishwa, pamoja na vitu vinne ambavyo ni vigumu sana kuvielewa. (30:15, 16) Kujitetea kwa ukaidi kwa mwanamke mzinzi kwaelezwa. Kisha vyaelezwa vitu vinne ambavyo chini yavyo dunia haiwezi kuvumilia, vitu vinne vidogo vyenye hekima ya kisilika, na vitu vinne vinavyotia fora sana katika kwenda kwavyo. Kwa ulinganishi mbalimbali unaofaa, mwandikaji huyo aonya kwamba “kuchochea hasira hutokeza ugomvi.”—30:33.

18. Mfalme Lemueli asema nini juu ya (a) mwanamke mbaya na (b) mke anayeweza mambo?

18 Sehemu ya Tano (31:1-31). Hapa pana “mausia” mengine, yale ya Lemueli mfalme. Yako katika mitindo miwili ya uandishi. Kisehemu cha kwanza chazungumza juu ya uharibifu ambao mtu aweza kupatwa nao kupitia mwanamke mbaya, chaonya jinsi kileo kinavyoweza kupotosha hukumu, na chatoa wito kwa ajili ya hukumu ya uadilifu. Mpangilio wa kiherufi katika kisehemu cha baadaye unahusu maelezo mazuri sana ya mke mwenye kuweza mambo. Kwa undani chazungumza juu ya thamani yake, kikitaja kwamba yeye atumainiwa na amthawabisha mwenyewe. Sifa zake ni kutia na kuwa na bidii ya kazi, mwenye kuamka mapema, mnunuzi mwangalifu, mfadhili kwa maskini, na pia mwenye kuona mambo kimbele na kunena kwa hekima. Pia yuko chonjo, astahiwa na watoto wake, na kusifiwa na mume wake. Zaidi ya yote, anahofu Yehova.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

19. Mithali chenyewe chajulishaje kusudi lacho lenye mafaa?

19 Kusudi lenye mafaa la Mithali laelezwa katika mistari ya ufunguzi: “Kujua hekima na adabu; kutambua maneno ya ufahamu; kufundishwa matendo ya busara, katika haki na hukumu na adili. Kuwapa wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari.” (1:2-4) Kwa kupatana na kusudi hilo lililoelezwa, kitabu hicho chakazia maarifa, hekima, na uelewevu, kila moja likiwa ni lenye mafaa katika njia yalo.

20. Mithali chasema nini juu ya maarifa?

20 (1) Maarifa ni uhitaji mkubwa wa binadamu, kwa maana si vizuri binadamu kuwa asiye na maarifa. Mtu hawezi kupata maarifa sahihi bila kuhofu Yehova, kwa maana maarifa huanzia na kuhofu huko. Maarifa yapendelewa zaidi ya dhahabu yenye bei. Kwa nini? Kupitia maarifa waadilifu huokolewa; hutuzuia tusifanye haraka kuingia kwenye dhambi. Jinsi tunavyohitaji kuyatafuta, kuyatwaa! Ni yenye thamani sana. Kwa hiyo “tega sikio lako uyasikie maneno ya wenye hekima, na kuuelekeza moyo wako kwa maarifa yangu.”—22:17; 1:7; 8:10; 11:9; 18:15; 19:2; 20:15.

21. Fundisho la kimungu juu ya hekima ni nini?

21 (2) Hekima, kuweza kutumia maarifa sawasawa iwe kwa sifa ya Yehova, ndilo jambo “bora.” Jipatie hiyo. Chanzo chayo ni Yehova. Hekima yenye kutoa uhai mwanzo wake ni kujua na kuhofu Yehova Mungu—hiyo ndiyo siri kuu ya hekima. Kwa hiyo hofu Mungu, si binadamu. Hekima ikipewa utu yapiga mbiu, ikisihi wote warekebishe njia zao. Hekima yalia kwa sauti kuu katika barabara zenyewe. Yehova atoa wito kwa wale wote wasio na ujuzi na wale wenye moyo unaopungukiwa wageuke na kujilisha kwa mkate wa hekima. Kisha, pamoja na kuhofu Yehova, watakuwa wenye furaha hata ikiwa wana kidogo. Baraka za hekima ni nyingi; matokeo yayo ni yenye thamani kubwa. Hekima na maarifa—hivyo ndivyo misingi ya kwanza ya kuweza kufikiri, kwa aina ile ambayo itatulinda. Kama vile asali ilivyo yenye mafaa na yenye kupendeza, ndivyo na hekima. Ni ya thamani zaidi ya dhahabu; ni mti wa uhai. Watu huangamia bila hekima, kwa maana hekima huhifadhi uhai; yamaanisha uhai.—4:7; 1:7, 20-23; 2:6, 7, 10, 11; 3:13-18, 21-26; 8:1-36; 9:1-6, 10; 10:8; 13:14; 15:16, 24; 16:16, 20-24; 24:13, 14.

22. Ni ulinzi gani unaopatikana katika uelewevu?

22 (3) Zaidi ya maarifa na hekima, uelewevu ni muhimu; kwa hiyo, “pamoja na yote ambayo wewe wajipatia, jipatie uelewevu.” (NW) Uelewevu ni uweza wa kuona jambo katika sehemu zalo zenye kulikamatanisha; humaanisha busara, sikuzote kwa kufikiria Mungu, kwa maana binadamu hawezi kuegemea uelewevu wake mwenyewe. Jinsi isivyowezekana kabisa kuwa na uelewevu au busara ikiwa mtu anapingana na Yehova! Ili kuifanya iwe yetu, ni lazima tutafute uelewevu kwa bidii kama hazina iliyofichika. Ili kuelewa, ni lazima tuwe na maarifa. Kutafuta ambako mwenye uelewevu hufanya kwa ajili ya maarifa huthawabishwa, na hekima iko mbele yake. Yeye hulindwa na mitego mingi ya ulimwengu huu, kama vile watu wabaya wengi wanaoweza kujaribu kumnasa mtu atembee pamoja nao katika njia ya giza. Shukrani zimwendee Yehova Mungu—Chanzo cha maarifa, hekima, na uelewevu wenye kutoa uhai!—4:7; 2:3, 4; 3:5; 15:14; 17:24; 19:8; 21:30.

23. Kisha ni aina gani ya shauri la hekima itakayozungumzwa?

23 Kwa kupatana na kusudi lenye mafaa la Mithali, kitabu hiki chatoa kwa wingi shauri lenye hekima lililopuliziwa na Mungu ili kutusaidia tupate uelewevu na kulinda moyo, “maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” (4:23) Yanayofuata ni chaguo la shauri la hekima linalokaziwa katika kitabu chote.

24. Ni nini kinachoelezwa kuhusu waovu na waadilifu?

24 Waovu na waadilifu watofautishwa: Mwovu atakamatwa katika njia zake kombo, na hazina zake hazitamwokoa katika siku ya hasira kali. Mwadilifu yuko kwenye njia ya uhai na atathawabishwa na Yehova.—2:21, 22; 10:6, 7, 9, 24, 25, 27-32; 11:3-7, 18-21, 23, 30, 31; 12:2, 3, 7, 28; 13:6, 9; 14:2, 11; 15:3, 8, 29; 29:16.

25. Mithali chaonyaje juu ya ukosefu wa adili?

25 Uhitaji wa maadili safi: Sulemani aonya kwa uendelevu juu ya ukosefu wa adili. Watu wazinzi watapokea pigo na pia kuvunjiwa staha, na suto lao halitafutwa. “Maji yaliyoibwa” huenda yakaonekana kuwa matamu kwa kijana, lakini malaya hushuka kwenye kifo na huandamana huko na watu alionasa wasio na ujuzi. Wale wanaoanguka ndani ya shimo refu la ukosefu wa adili wanalaaniwa vikali na Yehova.—2:16-19; 5:1-23; 6:20-35; 7:4-27; 9:13-18; 22:14; 23:27, 28.

26. Ni nini kinachosemwa kuhusu kujiweza?

26 Uhitaji wa kujiweza: Ulevi na ulafi vyalaaniwa vikali. Wote watakaopata kibali cha Mungu lazima wazoee kiasi katika kula na kunywa. (20:1; 21:17; 23:21, 29-35; 25:16; 31:4, 5) Wale wasiokasirika upesi wamejawa na busara na ni wakubwa zaidi ya mtu hodari anayeteka mji. (14:17, 29; 15:1, 18; 16:32; 19:11; 25:15, 28; 29:11, 22) Kujiweza pia kwahitajiwa ili kuepuka husuda na wivu, ambavyo ni kuoza katika mifupa ya mtu.—14:30; 24:1; 27:4; 28:22.

27. (a) Ni nini matumizi yasiyo ya hekima ya uneni? (b) Ni kwa nini matumizi ya midomo na ulimi wetu kwa hekima ni muhimu sana?

27 Matumizi ya uneni wa hekima na usio wa hekima: Uneni ulio kombo, mchongezi, shahidi bandia, na msema yasiyo ya kweli watafunuliwa, kwa maana ni chukizo kubwa kwa Yehova. (4:24; 6:16-19; 11:13; 12:17, 22; 14:5, 25; 17:4; 19:5, 9; 20:17; 24:28; 25:18) Ikiwa kinywa cha mtu chanena mambo mema, ni chanzo cha uhai; lakini kinywa cha mpumbavu huharakisha uharibifu wake. “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; na wao waupendao watakula matunda yake.” (18:21) Uchongezi, uneni wa kudanganya, kurai-rai, na maneno ya mbiombio yalaaniwa vikali. Ni mwendo wa hekima kunena kweli, kustahi Mungu.—10:11, 13, 14; 12:13, 14, 18, 19; 13:3; 14:3; 16:27-30; 17:27, 28; 18:6-8, 20; 26:28; 29:20; 31:26.

28. Ni dhara gani linaloletwa na kiburi, lakini ni mafaa gani yanayotokana na unyenyekevu?

28 Hasara ya kiburi na uhitaji wa unyenyekevu: Mtu mwenye kiburi hujikweza kwenye kimo asichokuwa nacho kwa kweli, hivyo anaporomoka chini. Wenye kiburi cha moyo ni wenye kuchukiza sana Yehova, lakini yeye huwapa wanyenyekevu hekima, utukufu, utajiri, na uhai.—3:7; 11:2; 12:9; 13:10; 15:33; 16:5, 18, 19; 18:12; 21:4; 22:4; 26:12; 28:25, 26; 29:23.

29. Uvivu wapasa kuonwaje, na juhudi ina thamani gani?

29 Juhudi, si ugoigoi: Kuna maelezo mengi juu ya mtu mvivu. Apaswa kwenda kwa sisimizi akapate somo na kuwa na hekima. Bali mwenye juhudi—atafanikiwa!—1:32; 6:6-11; 10:4, 5, 26; 12:24; 13:4; 15:19; 18:9; 19:15, 24; 20:4, 13; 21:25, 26; 22:13; 24:30-34; 26:13-16; 31:24, 25.

30. Mithali chakaziaje ushirika unaofaa?

30 Ushirika unaofaa: Si jambo la akili kushirikiana na wale wasiomhofu Yehova, na waovu au wapumbavu, na watu wenye kuhamaki, na wenye kilimilimi, au walafi. Badala yake, shirikiana na wenye hekima, nawe utakuwa mwenye hekima hata zaidi.—1:10-19; 4:14-19; 13:20; 14:7; 20:19; 22:24, 25; 28:7.

31. Ni nini shauri la hekima kuhusu karipio?

31 Uhitaji wa karipio na sahihisho: “Yule ambaye Yehova hupenda yeye hukaripia,” (NW) na wale wanaosikiliza nidhamu hiyo wako kwenye njia ya utukufu na uhai. Yeye achukiaye karipio atavunjiwa heshima.—3:11, 12; 10:17; 12:1; 13:18; 15:5, 31-33; 17:10; 19:25; 29:1.

32. Ni onyo gani zuri linalotolewa kuhusu kuwa mke mwema?

32 Shauri juu ya kuwa mke mwema: Kwa kurudia-rudia Mithali chaonya mke asiwe mshindani na asitende kwa kuaibisha. Mke mwenye busara, mwenye kuweza mambo anayehofu Mungu ana sheria ya fadhili za upendo kwenye ulimi wake; yeyote apataye mke kama huyo apata nia njema kutoka kwa Yehova.—12:4; 18:22; 19:13, 14; 21:9, 19; 27:15, 16; 31:10-31.

33. Ni ushauri gani wenye mafaa unaotolewa juu ya kuzoeza mtoto?

33 Kulea watoto: Wafundishe amri za Mungu kwa ukawaida ili kwamba ‘wasisahau.’ Walee tangu utotoni katika maagizo ya Yehova. Usiache kutumia fimbo inapohitajiwa; vikiwa wonyesho wa upendo, fimbo na karipio humpa mvulana hekima. Wale wanaolea watoto katika njia ya Mungu watakuwa na watoto wenye hekima watakaoleta shangwe na upendezi mwingi kwa baba na mama.—4:1-9; 13:24; 17:21; 22:6, 15; 23:13, 14, 22, 24, 25; 29:15, 17.

34. Kuna faida gani kuchukua daraka la kusaidia wengine?

34 Daraka la kusaidia wengine: Hilo hukaziwa mara nyingi katika Mithali. Ni lazima mwenye hekima aeneze maarifa huku na huku kwa ajili ya mafaa ya wengine. Ni lazima pia mtu awe mkarimu katika kuonyesha kibali kwa wale wanyonge, na katika kufanya hivyo, kwa kweli anamwazima Yehova, ambaye anatoa uhakikisho wa kulipa.—11:24-26; 15:7; 19:17; 24:11, 12; 28:27.

35. Kikitoboa kiini chenyewe cha matatizo yetu, Mithali chatoa shauri gani?

35 Kutegemea Yehova: Mithali chatoboa kiini cha matatizo yetu katika kushauri kwamba tutumaini Mungu kwa ukamili. Ni lazima tumfikirie Yehova katika njia zetu zote. Binadamu aweza kupanga mwendo wake, lakini Yehova lazima aelekeze hatua zake. Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu, ambamo waadilifu hukimbilia na kupata ulinzi. Tumaini katika Yehova na uliendee Neno lake kwa ajili ya uongozi.—3:1, 5, 6; 16:1-9; 18:10; 20:22; 28:25, 26; 30:5, 6.

36. Mithali chaweza kuelezwa kuwa cha kisasa, chenye kutumika, na chenye mafaa kwa maoni gani mbalimbali?

36 Jinsi kitabu cha Mithali kilivyo chenye mafaa kwa kufundisha na kutia nidhamu kwetu na kwa wengine! Hakuna sehemu yoyote ya uhusiano wa kibinadamu ambayo yaelekea kusahauliwa. Je! kuna mtu anayejitenga na waabudu wenzake wa Mungu? (18:1) Je! mtu aliye kwenye cheo cha juu anakata kauli kabla ya kusikia pande mbili za jambo? (18:17) Je! mtu ni mfanya mizaha yenye vitendo hatari? (26:18, 19) Je! mtu anaelekea kubagua? (28:21) Mfanya biashara katika duka lake, mkulima katika shamba lake, mume na mke na mtoto—wote wanapokea maagizo timamu. Wazazi wanasaidiwa ili wafunue mitego mingi inayootea-otea katika njia ya vijana. Wenye hekima waweza kufundisha wasio na ujuzi. Mithali ni zenye kutumika popote tuishipo; maagizo na shauri la kitabu hicho havichakai: “Kitabu cha Mithali,” pindi moja alisema mwelimishaji Mwamerika William Lyon Phelps, “ni cha kisasa zaidi ya gazeti la asubuhi hii.”a Kwa sababu kimepuliziwa na Mungu kitabu cha Mithali ni cha kisasa, chenye kutumika, na chenye mafaa kwa ajili ya kufundisha.

37. Mithali chapatanaje na mafundisho ya Sulemani Mkubwa Zaidi?

37 Kikiwa chenye mafaa ya kunyoosha mambo, kitabu cha Mithali, ambacho kwa sehemu kubwa kimenenwa na Sulemani, chageuza watu kwa Mungu Mweza Yote. Ndivyo alivyofanya Yesu Kristo pia, ambaye alirejezewa kwenye Mathayo 12:42 kuwa “aliye mkuu kuliko Sulemani.”

38. Mithali chaongezeaje uthamini wetu wa Ufalme wa Mungu na kanuni zao za uadilifu?

38 Jinsi tunavyoweza kuwa wenye shukrani kwamba Huyu mwenye hekima nyingi zaidi ni chaguo la Yehova kuwa Mbegu ya Ufalme! kiti chake cha enzi ndicho ‘kitakachothibitishwa katika haki,’ kwa ajili ya utawala wenye amani ulio mtukufu zaidi ya hata ule wa Mfalme Sulemani. Kuhusu utawala huo wa Ufalme, itasemwa hivi, “Fadhili na uaminifu humhifadhi mfalme, na kiti chake cha enzi huthibitishwa kwa fadhili.” Hiyo itafungua umilele wa serikali ya uadilifu kwa ajili ya ainabinadamu, jambo ambalo kulihusu Mithali yasema hivi: “Mfalme awahukumuye maskini kwa uaminifu; kiti chake cha enzi kitathibitika milele.” Kwa hiyo, twaja kuthamini kwa shangwe kwamba Mithali hazimuliki njia yetu tu ya maarifa, hekima, na ufahamu, na pia uhai wa milele, lakini, la maana zaidi, zinaadhimisha Yehova kuwa Chanzo cha hekima ya kweli, ambayo yeye hutoa kupitia Kristo Yesu, Mrithi wa Ufalme. Mithali huongezea sana uthamini wetu wa Ufalme wa Mungu na kanuni za uadilifu ambazo kwazo sasa unaongoza.—Mit. 25:5; 16:12; 20:28; 29:14.

[Maelezo ya Chini]

a Treasury of the Christian Faith. 1949, edited by Stuber and Clark, page 48.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki