Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 166-168
  • Kitabu Cha Biblia Namba 37—Hagai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Cha Biblia Namba 37—Hagai
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA HAGAI
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • “Mimi Nipo Pamoja Nanyi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Acheni Wote Wamtukuze Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • “Nitayatikisa Mataifa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Mikono Yenu na Iwe na Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 166-168

Kitabu Cha Biblia Namba 37—Hagai

Mwandikaji: Hagai

Mahali Kilipoandikiwa: Yerusalemu

Uandikaji Ulikamilishwa: 520 K.W.K.

Wakati Uliohusishwa: Siku 112 (520 K.W.K.)

1, 2. Ni habari gani zinazotolewa juu ya nabii Hagai, na ujumbe wake wenye sehemu mbili ulikuwa nini?

HAGAI lilikuwa ndilo jina lake; nabii na “mjumbe wa BWANA [Yehova, NW]” kilikuwa ndicho cheo chake, lakini asili yake ilikuwa nini? (Hag. 1:13) Yeye alikuwa nani? Hagai ndiye wa kumi kati ya wale waitwao manabii wenye umaana mdogo, naye alikuwa ndiye wa kwanza wa watatu waliotumikia baada ya Wayahudi kurudia bara la kwao katika 537 K.W.K., wale wengine wawili wakiwa ni Zekaria na Malaki. Jina la Hagai (Kiebrania, Chag·gaiʹ) lamaanisha “[Aliyezaliwa wakati wa] Sherehe.” Huenda hiyo ikawa yaonyesha alizaliwa siku ya karamu.

2 Kulingana na vile habari imewasilishwa na mapokeo ya Kiyahudi, ni jambo la kiakili kukata shauri kwamba Hagai alizaliwa katika Babuloni na kurudi Yerusalemu pamoja na Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua. Hagai alitumikia pamoja na nabii Zekaria, na kwenye Ezra 5:1 na 6:14, hao wawili waonyeshwa wakiwatia moyo wana wa uhamisho warudie ujenzi wa hekalu. Yeye alikuwa nabii wa Yehova kwa sehemu mbili, katika maana ya kwamba alihimiza Wayahudi watimize wajibu wao mbalimbali kuelekea Mungu na pia alitabiri, miongoni mwa mambo mengine, kutikiswa kwa mataifa yote.—Hag. 2:6, 7.

3. Wayahudi walikuwa wamekosa kujua nini kwa habari ya kusudi la kurudi kwao kutoka uhamishoni?

3 Kwa nini Yehova alimpa Hagai utume? Kwa sababu hii: Katika 537 K.W.K., Koreshi alikuwa ametoa amri iliyoruhusu Wayahudi warudie bara la kwao kujenga upya nyumba ya Yehova. Lakini sasa ilikuwa 520 K.W.K., na hekalu lilikuwa mbali na kukamilishwa. Muda wa miaka yote hiyo Wayahudi walikuwa wameacha vipingamizi vya adui pamoja na ubaridi wao wenyewe na ufuatiaji vitu vya kimwili uwazuie kutimiza kusudi lenyewe la kurudi kwao.—Ezra 1:1-4; 3:10-13; 4:1-24; Hag. 1:4.

4. Ni nini kilichokuwa kimezuia ujenzi wa hekalu, lakini ni mambo gani yaliyotukia wakati Hagai alipoanza kutoa unabii?

4 Kama vile maandishi yanavyoonyesha, mara tu msingi wa hekalu ulipowekwa (katika 536 K.W.K.) “watu wa nchi wakaidhoofisha mikono ya watu wa Yuda, wakawasumbua [wakiwavunja moyo, NW], walipokuwa wakijenga. Wakawaajiri washauri juu yao, ili kuwapinga kusudi lao.” (Ezra 4:4, 5) Hatimaye, katika 522 K.W.K., wapinzani hao wasio Wayahudi walifaulu kufanya kuwepo marufuku rasmi juu ya kazi. Ilikuwa katika mwaka wa pili wa utawala wa mfalme Mwajemi Dario Haistaspo, yaani, katika 520 K.W.K., kwamba Hagai akaanza kutoa unabii, na hiyo iliwatia moyo Wayahudi warudie ujenzi wa hekalu. Ndiposa, Dario akapelekewa barua na maliwali jirani wakiomba kwamba shauri likatwe kuhusu jambo hilo; Dario alihuisha ile amri ya Koreshi na kuwaunga mkono Wayahudi juu ya adui zao.

5. Ni nini uthibitisho wa kwamba kitabu cha Hagai chafaa kuwa katika vitabu vinavyokubaliwa vya Biblia?

5 Hakukuwa na shaka kamwe miongoni mwa Wayahudi juu ya kama unabii wa Hagai ulikuwa sehemu ya vitabu vya Kiebrania vilivyokubaliwa, na jambo hilo laungwa mkono pia na kurejezewa kwake katika Ezra 5:1 kuwa akitoa unabii “kwa jina la Mungu wa Israeli,” na pia katika Ezra 6:14. Kwamba unabii wake ni sehemu ya “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu” yathibitishwa na kunukuliwa kwao na Paulo kwenye Waebrania 12:26: “Sasa ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia.”—Hag. 2:6.

6. Unabii wa Hagai wajumlisha nini, na ni mkazo gani unaotiwa juu ya jina la Yehova?

6 Unabii wa Hagai una jumbe nne zilizotolewa kwa kipindi cha siku 112. Mtindo wake ni mwepesi kueleweka na wa moja kwa moja, na mkazo wake juu ya jina la Yehova una ustahiki kamili wa kuangaliwa. Katika mistari yake 38, ataja jina la Yehova mara 35, mara 14 katika usemi “BWANA [Yehova, NW] wa majeshi.” Yeye haachi shaka lolote kwamba ujumbe wake umetoka kwa Yehova: “Hagai mjumbe wa BWANA [Yehova, NW], katika ujumbe wa BWANA [Yehova, NW], akawaambia watu, akisema, Mimi nipo pamoja nanyi, asema BWANA [Yehova, NW].”—1:13.

7. Hagai alitia Wayahudi moyo wafanye nini, na kiini cha ujumbe wake kilikuwa nini?

7 Huu ulikuwa wakati wa maana sana katika historia ya watu wa Mungu, na kazi ya Hagai ilithibitika kuwa yenye mafaa sana. Yeye hakusita-sita kutimiza fungu lake akiwa nabii wala hakupunguza uzito wa maneno aliyoambia Wayahudi. Alisema moja kwa moja katika kuwaambia kwamba ulikuwa wakati wa kuacha kuahirisha-ahirisha mambo na wa kuanza kazi bila mchezo. Ulikuwa wakati wa kujenga upya nyumba ya Yehova na kurejesha ibada yenye kutakata ikiwa walitaka kuona shangwe ya ufanisi wowote kutoka mkono wa Yehova. Kiini kizima cha ujumbe wa Hagai ni kwamba ikiwa mtu atakuja kufurahia mibaraka kutoka kwa Yehova, ni lazima atumikie Mungu wa kweli na kufanya kazi ambayo Yehova aamuru ifanywe.

YALIYOMO KATIKA HAGAI

8. Kwa nini Wayahudi hawabarikiwi na Yehova kwa vitu vya kimwili?

8 Ujumbe wa kwanza (1:1-15). Huu waelekezwa kwa Liwali Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua, lakini masikioni mwa watu hao. Watu hao wamekuwa wakisema, “Huu sio wakati utupasao kuja, huu sio wakati wa kujengwa nyumba ya BWANA [Yehova, NW].” Kupitia Hagai Yehova auliza swali la kupekua-pekua maoni: “Je! huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika?” (1:2, 4) Wao wamepanda mbegu nyingi kwa kufuatia vitu vya kimwili, lakini hawakunufaika sana kwa njia ya chakula, kinywaji, na nguo. “Zitafakarini njia zenu,” Yehova aonya kwa upole. (1:7) Wakati umefika wa kuleta mbao na kujenga nyumba ile, ili Yehova apate kutukuzwa. Wayahudi watunza vizuri nyumba zao wenyewe, lakini nyumba ya Yehova imelala hali ya ukiwa. Kwa hiyo, Yehova amekuwa mnyimivu ili umande wa mbinguni na ongezeko la shambani na baraka yake visiwe juu ya mwanadamu na jasho lake.

9. Yehova achocheaje Wayahudi wafanye kazi?

9 Kumbe, wameelewa! Hagai hakutoa unabii bure. Watawala na watu waanza ‘kutii sauti ya Yehova, Mungu wao.’ Hofu kwa Yehova yawa badala ya hofu kwa mwanadamu. Uhakikishio wa Yehova kupitia Hagai mjumbe wake ni kwamba: “Mimi nipo pamoja nanyi.” (1:12, 13) Yehova mwenyewe ndiye anayeamsha roho ya liwali, roho ya kuhani mkuu, na roho ya baki la watu Wake. Waanza kazi, siku 23 tu baada ya Hagai kuanza kutoa unabii na kujapokuwa na marufuku rasmi ya serikali ya Uajemi.

10. Wayahudi fulani wahisi nini juu ya hekalu wanalojenga, lakini Yehova aahidi nini?

10 Ujumbe wa pili (2:1-9). Muda unaopungua mwezi mmoja wapita baada ya kuanzishwa tena kwa utendaji wa kujenga, na Hagai atoa ujumbe wake wa pili wenye pumzi ya Mungu. Huo umeelekezwa kwa Zerubabeli, Yoshua, na waliobaki wa watu hao. Kwa wazi baadhi ya Wayahudi waliorudi kutoka uhamishoni na waliokuwa wameona hekalu la kwanza la Sulemani walihisi kwamba hekalu hili halingekuwa kitu likilinganishwa na hilo jingine. Lakini ni nini tangazo la Yehova wa majeshi? ‘Mwe hodari, mkafanye kazi, kwa kuwa mimi ni pamoja nanyi.’ (2:4) Yehova awakumbusha agano lake pamoja nao, na kuwaambia wasiogope. Awaimarisha kwa ahadi ya kwamba atatikisa mataifa yote na kusababisha vitu vyayo vyenye kutamanika vije ndani na kwamba atajaza nyumba yake utukufu. Utukufu wa nyumba hii ya baadaye utakuwa mkubwa hata kuliko ule wa ile ya kwanza, na yeye atatia amani katika mahali hapa.

11. (a) Ni kwa kutumia ufananishi gani Hagai aonyesha wazi kutojali kwa makuhani? (b) Ni nini kimetokana na jambo hilo?

11 Ujumbe wa tatu (2:10-19, NW). Miezi miwili na siku tatu baadaye, Hagai asema kwa makuhani. Atumia ufananishi ili kuelewesha wazi wazo lake. Je! kuchukua kwa kuhani mnofu mtakatifu kutafanya chakula kingine chote anachogusa kiwe kitakatifu? Jibu ni la. Je! kugusa kitu kisicho safi, kama vile maiti, kwafanya mwenye kuigusa awe si safi? Jibu ni ndiyo. Ndipo Hagai anapotumia ufananishi huo. Watu wa bara lile si safi kwa sababu ya kutojali kwao ibada yenye kutakata. Chochote wanachotoa chaonekana si safi kwa Yehova Mungu. Kwa sababu hiyo, Yehova hakubariki kazi zao za jasho, na kuongezea hilo amewapelekea joto lenye kuchoma sana, kuvu, na mawe ya mvua. Acha wao wabadili njia zao. Kisha Yehova atawabariki.

12. Ni ujumbe gani wa mwisho ambao Hagai aelekezea Zerubabeli?

12 Ujumbe wa nne (2:20-23). Hagai atoa ujumbe huu siku ile ile aliyotoa ujumbe wa tatu, lakini waelekezwa kwa Zerubabeli. Kwa mara nyingine tena Yehova anena juu ya ‘kutikisa mbingu na dunia,’ lakini wakati huu arefusha kichwa hicho cha habari kihusishe kufutiliwa mbali kabisa kwa falme za mataifa. Wengi wataangushwa, “kila mtu kwa upanga wa ndugu yake.” (2:21, 22) Hagai amalizia unabii wake kwa uhakikisho wa kuonyeshwa kwa Zerubabeli upendeleo wa Yehova.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

13. Utoaji-unabii wa Hagai ulikuwa na mafaa gani ya mara moja?

13 Jumbe nne za Yehova zilizowasilishwa kupitia Hagai zilikuwa zenye mafaa kwa Wayahudi wa siku hiyo. Wao walitiwa moyo wajihusishe na kazi, na katika miaka minne na nusu, hekalu lilikamilishwa ili kusogeza mbele ibada ya kweli katika Israeli. (Ezra 6:14, 15) Yehova alibariki utendaji wao wa bidii. Ilikuwa katika wakati huo wa ujenzi wa hekalu kwamba Dario mfalme wa Uajemi alichunguza kumbukumbu za maandishi ya taifa na kukariri amri ya Koreshi. Hivyo kazi ya hekalu ilikamilishwa kwa tegemezo lake rasmi.—Ezra 6:1-13.

14. Hagai atoa shauri gani lenye hekima kwa ajili ya siku yetu?

14 Pia unabii huo una shauri la hekima kwa ajili ya siku yetu. Vipi? Jambo moja ni kwamba wakazia uhitaji wa kiumbe kutanguliza faida za ibada ya Mungu mbele ya faida za kibinafsi zacho chenyewe. (Hag. 1:2-8; Mt. 6:33) Pia wakazia jambo la kwamba ubinafsi waleta hasara, kwamba ni ubatili kufuatia mali; amani na baraka ya Yehova ndizo hutajirisha. (Hag. 1:9-11; 2:9; Mit. 10:22) Pia wakazia kwamba utumishi wa Mungu wenyewe haumfanyi mtu kuwa safi isipokuwa uwe watakata na wa nafsi yote, na kwamba haupaswi kunajisiwa kwa mwenendo mchafu. (Hag. 2:10-14; Kol. 3:23; Rum. 6:19) Waonyesha kwamba watumishi wa Mungu hawapaswi kuwa na maoni yasiyofaa, wakitazama nyuma “siku njema zilizopita,” bali wawe wenye kutazama mbele, ‘wakitafakari njia zao’ na kutafuta kuletea Yehova utukufu. Kisha Yehova atakuwa pamoja nao.—Hag. 2:3, 4; 1:7, 8, 13; Flp. 3:13, 14; Rum. 8:31.

15. Kitabu cha Hagai chaonyesha nini kuwa matokeo ya utii wenye bidii?

15 Mara walipojishughulisha na kazi ya hekalu, Wayahudi walipendelewa na Yehova, nao wakasitawi. Vipingamizi vikatokomea. Kazi hiyo ilitimizwa kwa wakati unaofaa. Utendaji usio na hofu, wenye bidii kwa ajili ya Yehova sikuzote utathawabishwa. Magumu, halisi au ya kuwaziwa, yaweza kushindwa kwa kuzoea imani ya moyo mkuu. Utii kwa ‘neno la Yehova’ huleta matokeo.—Hag. 1:1.

16. Unabii wa Hagai una uhusiano gani na tumaini la Ufalme, nao wapasa kutuchochea kwenye utumishi gani leo?

16 Vipi juu ya unabii wa kwamba Yehova ‘atatikisa mbingu na nchi’? Mtume Paulo atoa matumizi ya Hagai 2:6 katika maneno haya: “Lakini sasa [Mungu] ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia. Lakini neno lile, Mara moja tena, ladhihirisha kuhamishwa vile viwezavyo kutetemeshwa, kama vitu vilivyoumbwa, ili vitu visivyoweza kutetemeshwa vikae. Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; maana Mungu wetu ni moto ulao.” (Ebr. 12:26-29) Hagai aonyesha kwamba kutikiswa huko ni kwa kusudi la ‘kupindua kiti cha enzi cha falme, na kuharibu nguvu za falme za mataifa.’ (Hag. 2:21, 22) Katika kunukuu unabii huo, Paulo anena kwa kutofautisha, juu ya Ufalme wa Mungu “usioweza kutetemeshwa.” Basi kwa kufikiria tumaini hili la Ufalme, acheni tuwe ‘hodari tukafanye kazi,’ tukitolea Mungu utumishi mtakatifu. Pia, na tufikirie kwamba kabla Yehova hajapindua mataifa ya dunia, kitu fulani chenye thamani lazima kikorogwe kitoke kwayo, kwa ajili ya kuhifadhiwa: “Nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema BWANA [Yehova, NW] wa majeshi.”—2:4, 7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki