Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 248-251
  • Kitabu cha Biblia Namba 59—Yakobo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 59—Yakobo
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA YAKOBO
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Jifunze Kutoka kwa Ndugu Mdogo wa Yesu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Yakobo Anahimiza Ibada Safi na Yenye Matendo Ifuatwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • “Watendaji wa Neno” Wenye Shangwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Sababu Tunahitaji Imani na Hekima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 248-251

Kitabu cha Biblia Namba 59—Yakobo

Mwandikaji: Yakobo

Mahali Kilipoandikiwa: Yerusalemu

Uandikaji Ulikamilishwa: Kabla ya 62 W.K.

1. Ni nini chatokeza shaka juu ya kama Yakobo ndiye mwandikaji wa kitabu chenye jina Yakobo?

“AMERUKWA na akili.” Hivyo ndivyo watu wa ukoo wa Yesu walivyomfikiria yeye. Wakati wa huduma yake ya kidunia, “hata nduguze hawakumwamini,” na Yakobo, pamoja na Yusufu, Simoni, na Yuda, hakuhesabiwa kuwa mmoja wa wanafunzi wa mapema wa Yesu. (Mk. 3:21; Yn. 7:5; Mt. 13:55) Basi, ni kwa msingi gani yaweza kusemwa kwamba Yakobo ndugu-nusu wa Yesu aliandika kitabu cha Biblia kilicho na jina Yakobo?

2. Ni nini chatoa hoja ya kwamba ndugu-nusu wa Yesu ndiye aliyekuwa mwandikaji wa Yakobo?

2 Maandishi yaonyesha kwamba Yesu aliyefufuliwa alimtokea Yakobo, na bila shaka jambo hilo lilimsadikisha pasipo shaka kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya. (1 Kor. 15:7) Matendo 1:12-14 husema kwamba hata kabla ya Pentekoste, Mariamu na ndugu za Yesu walikuwa wakikusanyika kwa ajili ya sala pamoja na mitume katika chumba cha juu katika Yerusalemu. Lakini je! si mmoja wa mitume aitwaye Yakobo aliyeandika barua hii? Sivyo, kwa maana tangu mwanzo mwandikaji ajitambulisha akiwa, si mtume, bali kuwa ‘mtumwa wa Bwana Yesu Kristo.’ Zaidi ya hilo, maneno ya utangulizi wa Yuda, ambayo yafanana na yale ya Yakobo, humtaja Yuda (au Yudasi) pia kuwa “mtumwa wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo.” (Yak. 1:1; Yuda 1) Kutokana na hilo twaweza kukata shauri kwa kufaa kwamba Yakobo na Yuda, walio ndugu-nusu za Yesu, ndio walioandika vitabu vya Biblia vilivyo na majina yao.

3. Ni sifa gani zilizostahilisha Yakobo kuandika?

3 Yakobo alikuwa mashuhuri kwa ustahili wa kuandika barua ya shauri kwa kundi la Kikristo. Alistahiwa sana akiwa mwangalizi katika kundi la Yerusalemu. Paulo amtaja “Yakobo, ndugu yake Bwana” kuwa mmoja wa “nguzo” katika kundi pamoja na Kefa na Yohana. (Gal. 1:19; 2:9) Umashuhuri wa Yakobo waonyeshwa na kupeleka kwa Petro neno la mara ile ile kwa “Yakobo na wale ndugu” baada ya kuachiliwa kwake gerezani. Na je! siye Yakobo aliyetenda akiwa msemaji kwa ajili ya “mitume na wazee” wakati Paulo na Barnaba waliposafiri kwenda Yerusalemu kuomba uamuzi kuhusu tohara? Kwa tukio jema, uamuzi huo na barua ya Yakobo zaanza zote mbili kwa salamu inayolingana, “Salamu!”—kionyeshi kingine cha kwamba mwandikaji wa zote alikuwa mmoja.—Mdo. 12:17; 15:13, 22, 23; Yak. 1:1.

4. Ni nini huonyesha kwamba barua ya Yakobo iliandikwa muda mfupi kabla ya 62 W.K.?

4 Mwanahistoria Yosefo hutuambia kwamba Kuhani Mkuu Ananus (Anania), Sadukayo, ndiye aliyesababisha kuuawa kwa Yakobo kwa kupigwa mawe. Hiyo ilikuwa baada ya kifo cha liwali Mrumi Festo, karibu na 62 W.K., na kabla mwandamizi wake, Albino, hajachukua cheo.a Lakini ni lini Yakobo alipoandika barua yake? Yakobo aliandika barua yake kutoka Yerusalemu kwa “kabila kumi na mbili waliotawanyika,” kwa uhalisi, “wale (walio) katika utawanyiko.” (Yak. 1:1, NW, kielezi-chini) Ingalihitaji wakati ili Ukristo uenee baada ya kumiminwa kwa roho takatifu katika 33 W.K., na ingalihitaji wakati, pia, ili hali za kushtua zitajwazo katika barua hiyo zisitawi. Zaidi ya hilo, barua hiyo huonyesha kwamba Wakristo hawakuwa tena vikundi vidogo bali walipangwa kitengenezo katika makundi yenye “wazee” wakomavu ambao wangeweza kusali kwa ajili ya walio dhaifu na kuwategemeza. Kwa kuongezea, wakati wa kutosha ulikuwa umepita ili kadiri fulani ya kukinai na kufuatia desturi ipenye ndani. (2:1-4; 4:1-3; 5:14; 1:26, 27) Kwa hiyo, yawezekana sana kwamba Yakobo aliandika barua yake kwenye tarehe ya baadaye sana, labda muda mfupi kabla ya 62 W.K., ikiwa simulizi la Yosefo juu ya matukio yenye kuzungukia kifo cha Festo na ikiwa vyanzo vinavyokiweka kifo cha Festo karibu 62 W.K. ni sahihi.

5. Ni nini huthibitisha kwamba Yakobo kimedumisha uasilia wa kutungwa kwacho?

5 Kwa habari ya kudumishwa kwa uasilia wa Yakobo, kitabu hicho kimo katika Vatican No. 1209, hati-mkono za Sinaitic na Alexandrine. Kimetiwa katika angalau orodha kumi za kale kabla ya Baraza la Carthage 397 W.K.b Kilinukuliwa sana na waandikaji makasisi wa mapema. Upatani wa kindani na kwa kina kirefu pamoja na sehemu nyingine yote ya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu waonekana wazi sana katika miandiko ya Yakobo.

6. (a) Ni hali gani zilizomhitaji Yakobo aandike barua yake? (b) Badala ya kupinga, Yakobo aongezeaje hoja za Paulo juu ya imani?

6 Kwa nini Yakobo aliandika barua hii? Ufikirio wa uangalifu wa barua hii wafunua kwamba hali za kindani zilikuwa zikisababisha magumu miongoni mwa akina ndugu. Viwango vya Kikristo vilikuwa vikishushwa, ndiyo, hata kupuuzwa, hivi kwamba watu fulani walikuwa wamekuwa wazinzi wa kiroho kuhusu kufanya urafiki na ulimwengu. Watu fulani wakiwa na hamu nyingi ya kutunga kwamba ati kuna mambo yenye kupingana, wamedai kwamba barua ya Yakobo inayotia moyo kuwa na imani kwa matendo hubatilisha miandiko ya Paulo kuhusu wokovu kwa imani wala si kwa matendo. Hata hivyo, habari zenye kuzunguka hufunua kwamba Yakobo hurejezea imani yenye kutegemezwa na matendo, wala si maneno tu, hali kwa wazi Paulo humaanisha matendo ya Sheria. Kwa kweli, Yakobo huongezea maelezo ya ziada kwenye hoja za Paulo, akisonga mbele hatua moja zaidi kwa kufafanua jinsi imani hudhihirishwa. Shauri la Yakobo lina matokeo sana katika kuzungumzia matatizo ya Mkristo ya siku baada ya siku.

7. Yakobo anakilije njia za Yesu za kufundisha, na tokeo likiwa nini?

7 Vielezi kutokana na maisha ya kila siku, kutia na wanyama, mashua, wakulima, na majani-majani, huzitegemeza kwa uvutio mwingi hoja za Yakobo juu ya imani, saburi, na uvumilivu. Kunakili huku kwa njia za Yesu za kufundisha kwa mafanikio hufanya shauri lake liwe na nguvu nyingi kabisa. Barua hii yakazia mtu kwamba Yakobo alikuwa na ufahamu wa wazi sana juu ya makusudio yenye kusukuma watu mmoja mmoja.

YALIYOMO KATIKA YAKOBO

8. Ni nini kitakachotokeza uvumilivu wenye saburi, lakini kutokee nini kutokana na tamaa mbaya?

8 Uvumilivu wenye saburi kwa kuwa “watendaji wa neno” (1:1-27). Yakobo afungua kwa maneno ya kitia-moyo: “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali.” Wao watakamilishwa kupitia uvumilivu wenye saburi. Ikiwa mtu hana hekima, apaswa kuendelea kumwomba Mungu, si kwa shaka, kama wimbi lenye kutupwa-tupwa na upepo wa bahari, bali kwa imani. Walio dhalili (wanyenyekevu) watakwezwa, lakini matajiri watafifilia mbali kama ua ambalo huangamia. Mwenye furaha ni mtu ambaye huvumilia jaribu, kwa maana “ataipokea taji ya uzima, Bwana [Yehova, NW] aliyowaahidia wampendao.” Mungu hajaribu mtu yeyote kwa maovu ili kusababisha anguko lake. Tamaa mbaya ya mtu mwenyewe ndiyo hupata rutuba na kuzaa dhambi, ambayo nayo huzaa kifo.—1:2, 12, 22.

9. Ni nini chahusika katika kuwa “watendaji wa neno,” na ni namna ya ibada gani ambayo yakubaliwa na Mungu?

9 Zawadi zote nzuri hutoka wapi? Hutoka kwa ‘Baba wa mianga’ ya mbinguni asiye na ugeugeu kamwe. Yakobo asema, “Kwa kupenda kwake mwenyewe alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.” Basi, Wakristo wapaswa kuwa wepesi wa kusikia, watu wa polepole kusema, wa polepole kuwa na hasira, na wapaswa kuondolea mbali uchafu wote na ubaya wa kiadili na kukubali kupandwa ndani kwa neno la wokovu. “Iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu.” Kwa maana yeye achunguliaye ndani ya sheria ya uhuru iliyo kama kioo na kudumu humo “atakuwa heri katika kutenda kwake.” Ibada rasmi ya mtu asiyezuia ulimi wake ni bure, lakini “dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.”—1:17, 18, 22, 25, 27.

10. (a) Ni mabaguano gani yapasa kuepukwa kabisa? (b) Ni nini uhusiano wa matendo na imani?

10 Imani yakamilishwa na matendo yafaayo (2:1-26). Akina ndugu wanafanya ubaguzi, wakipendelea matajiri zaidi ya maskini. Lakini kwa kweli “je! Mungu hakuwachagua maskini wa dunia wawe matajiri wa imani na warithi wa ufalme”? Je! matajiri si waonevu? Akina ndugu wapaswa kuizoea sheria ya kifalme, “Mpende jirani yako kama nafsi yako,” na wapaswa kuepuka kabisa upendeleo. Acheni wao wazoee rehema pia, kwa maana kuhusu Sheria, yeyote akoseaye katika jambo moja hukosea katika yote. Imani bila matendo haina maana, kama vile ilivyo kuhusu kuambia ndugu au dada mwenye uhitaji ‘akaote moto na kushiba’ bila kutoa msaada wenye mafaa. Je! imani yaweza kuonyeshwa bila matendo? Je! imani ya Abrahamu haikukamilishwa na matendo yake katika kumtoa Isaka juu ya madhabahu? Vilevile, Rahabu yule kahaba ‘alihesabiwa kuwa ana haki kwa matendo.’ Kwa hiyo imani bila matendo imekufa.—2:5, 8, 16, 19, 25.

11. (a) Ni kwa njia ya vielezi gani Yakobo aonya kuhusu ulimi? (b) Hekima na uelewevu vyapasa kuonyeshwaje?

11 Kuongoza ulimi ili kufundisha hekima (3:1-18). Akina ndugu wapaswa kujihadhari juu ya kuwa walimu, wasije wakapokea hukumu nzito zaidi. Kila mtu hujikwaa mara nyingi. Kama vile lijamu hudhibiti mwili wa farasi na usukani mdogo meli kubwa, ndivyo kiungo kidogo hicho, ulimi, kilivyo na nguvu nyingi. Ni kama moto uwezao kuwasha msitu mkubwa! Wanyama-mwitu waweza kufugwa kwa urahisi kuliko ulimi. Kwa huo wanadamu humbariki Yehova, hata hivyo hulaani binadamu mwenzao. Hiyo haifai. Je! chemchemi hutokeza maji machungu na pia matamu? Je! mtini waweza kutokeza zeituni? mzabibu ukatokeza tini? maji ya chumvi yakatokeza maji matamu? Yakobo auliza hivi: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu?” Acheni yeye aonyeshe matendo yenye usikivu na aepuke ushindani, kujigamba kinyama juu ya ukweli. Kwa maana “hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.”—3:13, 17.

12. (a) Ni hali gani mbaya zilizo katika kundi, na chanzo chazo ni nini? (b) Ni maoni gani yapasa kuepukwa na sifa gani kusitawishwa ili kupata kibali cha Yehova?

12 Epuka kabisa anasa ya kuamsha nyege, urafiki pamoja na ulimwengu (4:1-17). “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi?” Yakobo ajibu swali lake mwenyewe: “Katika tamaa zenu!” Makusudio ya watu fulani ni mabaya. Wale ambao wangependa kuwa marafiki wa ulimwengu ni “wazinzi,” nao huwa maadui wa Mungu. Kwa hiyo, yeye awasihi hivi: “Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” Yehova atawakweza wanyenyekevu. Kwa hiyo akina ndugu wapaswa kuacha kuhukumiana. Na kwa kuwa hakuna mtu awezaye kuwa na uhakika juu ya uhai wake wa kutoka siku moja mpaka nyingine, wao wapaswa kusema: “Bwana [Yehova, NW] akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.” Kiburi ni kiovu, na ni dhambi kujua kufanya lililo sawa na usilifanye.—4:1, 4, 7, 8, 15.

13. (a) Kwa nini kuna ole kwa matajiri? (b) Yakobo aonyeshaje uhitaji wa saburi na uvumilivu, na kwa matokeo gani?

13 Wenye furaha ni wale wavumiliao katika uadilifu! (5:1-20). ‘Enyi matajiri, lieni mkapige yowe!’ Yakobo ajulisha. ‘Kuoza kwa utajiri wenu kutawashuhudia. Bwana [Yehova, NW] wa majeshi ameingiwa masikioni na vilio vya wavunaji ambao nyinyi mlizuia ujira wao. Mmefanya anasa na kujifurahisha kwa tamaa, mmehukumu mwenye haki mkamwua.’ Hata hivyo, kwa sababu ya ukaribio wa kuwapo kwa Bwana, akina ndugu wapaswa kujizoeza saburi, kama mkulima anayengojea mavuno yake, na kufikiria kigezo cha manabii, “walionena kwa jina la Bwana [Yehova, NW].” Wenye furaha ni wale ambao wamevumilia! Akina ndugu wapaswa kukumbuka uvumilivu wa Ayubu na tokeo ambalo Yehova alitoa, “ya kwamba Bwana [Yehova, NW] ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”—5:1-6, 10, 11.

14. Ni shauri gani la kumalizia latolewa kuhusu kuungama dhambi na kuhusu sala?

14 Wao na waache kuapa. Bali, acheni ‘ndiyo yao iwe ndiyo’ na ‘siyo yao, siyo.’ Yawapasa kuungamamiana wazi dhambi zao na kusali kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Kama ionyeshwavyo na sala za Eliya, “kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana.” Ikiwa mtu yeyote apotoshwa kutoka kwenye ile kweli, yule amgeuzaye kurudi ‘ataokoa roho [nafsi, NW] yake na mauti, na kufunika wingi wa dhambi.’—5:12, 16, 20.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

15. Yakobo afanyaje utumizi wa Maandiko ya Kiebrania? Toa kielezi.

15 Ingawa Yakobo ataja jina Yesu mara mbili tu (1:1; 2:1), yeye afanya utumizi mwingi wenye kutumika juu ya mafundisho ya Bwana-Mkubwa, kama vile ulinganishi wa uangalifu wa barua ya Yakobo na Mahubiri ya Mlimani wafunua. Wakati ule ule, jina la Yehova laonekana mara 13 (NW), na ahadi zake zakaziwa kuwa thawabu za Wakristo washika-imani. (4:10; 5:11) Yakobo atumia tena na tena vielezi katika Maandiko ya Kiebrania na manukuu yafaayo hali ili kusitawisha shauri lake lenye kutumika vizuri. Atambulisha chanzo chayo kwa semi zake: “kama ilivyoandikwa,” “maandiko yale yakatimizwa,” na “maandiko yasema”; na aendelea kutumia maandiko hayo kuhusu maisha ya Kikristo. (2:8, 23; 4:5) Katika kujulisha wazi mashauri na kujenga imani katika Neno la Mungu kuwa fungu zima lenye upatani, Yakobo afanya marejezo yafaayo kwenye matendo ya Abrahamu ya imani, kwenye wonyesho wa Rahabu wa imani kupitia matendo, kwenye uvumilivu mwaminifu wa Ayubu, na kwenye tegemeo la Eliya juu ya sala.—Yak. 2:21-25; 5:11, 17, 18; Mwa. 22:9-12; Yos. 2:1-21; Ayu. 1:20-22; 42:10; 1 Fal. 17:1; 18:41-45.

16. Yakobo atoa mashauri na maonyo gani, na hekima hiyo yenye kutumika vizuri ni ya kutoka chanzo gani?

16 La thamani kubwa ni shauri la Yakobo kuwa watendaji wa lile neno wala si wasikiaji tu, kuendelea kuthibitisha imani kwa matendo ya uadilifu, kupata shangwe katika kuvumilia majaribu mbalimbali, kuendelea kuomba Mungu hekima, sikuzote kumkaribia katika sala, na kuizoea sheria ya kifalme, “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Yak. 1:22; 2:24; 1:2, 5; 4:8; 5:13-18; 2:8) Maonyo yake ni yenye nguvu ya kuzuia kufundisha makosa, kutumia ulimi kwa kuumiza, kufanya tofauti za kitabaka (vikundi-vikundi) katika kundi, kutamani anasa ya kuamsha nyege, na kutumainia mali zenye kuharibika. (3:1, 8; 2:4; 4:3; 5:1, 5) Yakobo ajulisha wazi sana kwamba urafiki pamoja na ulimwengu ni sawa na uzinzi wa kiroho na uadui pamoja na Mungu, naye atoa ufafanuzi wa namna ya ibada yenye matokeo iliyo safi machoni pa Mungu: “kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (4:4; 1:27) Mashauri yote haya, yenye matokeo sana na rahisi kueleweka, ndicho kitu hasa ambacho kingeweza kutarajiwa kutoka kwa “nguzo” huyu wa kundi la mapema la Kikristo. (Gal. 2:9) Ujumbe wacho wenye fadhili waendelea kuwa kielekezi kwa Wakristo katika nyakati zetu zenye msukosuko, kwa maana ni “hekima itokayo juu,” ambayo huzaa “tunda la haki.”—3:17, 18.

17. Ni sababu gani yenye nguvu ambayo yatokezwa kwa kuvumilia katika kazi za uaminifu?

17 Yakobo alikuwa na hamu ya kusaidia ndugu zake wafikie mradi wao wa uhai katika Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo awahimiza hivi: “Nanyi vumilieni, mthibitishe mioyo yenu, kwa maana kuja kwake Bwana kunakaribia.” Wao ni wenye furaha ikiwa wataendelea kuvumilia jaribu kwa sababu kibali cha Mungu humaanisha kupokea “taji ya uzima, Bwana [Yehova, NW] aliyowaahidia wampendao.” (5:8; 1:12) Hivyo ahadi ya Mungu ya taji la uhai—ama uhai usiokufa katika mbingu au uhai wa milele duniani—yakaziwa kuwa sababu yenye nguvu ya kuvumilia katika matendo ya uaminifu. Hakika barua hii iliyo nzuri ajabu itawatia wote moyo wajitahidi kufikia mradi wa uhai wa milele ama mbinguni ama katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye kutawalwa na Mbegu ya Ufalme, Bwana wetu Yesu Kristo.—2:5.

[Maelezo ya Chini]

a Jewish Antiquities, XX, 197-200 (ix, 1); Webster’s New Biographical Dictionary, 1983, ukurasa wa 350.

b Ona chati, ukurasa wa 303.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki