Sura 69
Lile Swali la Ubaba
WAKATI wa sikukuu ile, mazungumzo ya Yesu pamoja na viongozi wa kidini Wayahudi yanakuwa makali sana. “Mimi najua kwamba nyinyi ni wazao wa Abrahamu,” Yesu anakiri, “lakini nyinyi mnatafuta kuniua, kwa sababu neno langu halifanyi maendeleo miongoni mwenu. Mambo ambayo mimi nimeona pamoja na Baba yangu ninayanena; na nyinyi, basi, mnafanya mambo ambayo nyinyi mmesikia kutoka kwa baba yenu.”
Ingawa hatambulishi baba yao ni nani, Yesu anaelewesha wazi kwamba baba yao ni tofauti na yule wake. Bila kuwa na habari Yesu anamaanisha nani, viongozi wa kidini Wayahudi wanaitikia hivi: “Baba yetu ni Abrahamu.” Wao wanahisi kwamba wana imani ile ile kama ya Abrahamu, aliyekuwa rafiki ya Mungu.
Hata hivyo, Yesu anawashtua kwa jibu hili: “Ikiwa nyinyi ni watoto wa Abrahamu, fanyeni kazi za Abrahamu.” Kweli kweli, mwana halisi huiga baba yake. “Lakini sasa nyinyi mnatafuta kuniua,” Yesu anasema, “mwanamume ambaye amewaambia nyinyi ukweli ambao mimi nilisikia kutoka kwa Mungu. Abrahamu hakufanya hivyo.” Kwa hiyo Yesu anasema tena: “Nyinyi mnafanya kazi za baba yenu.”
Bado akili zao hazishiki Yesu anaongea juu ya nani. Wanashikilia kwamba wao ni wana halali wa Abrahamu, wakisema: “Sisi hatukuzaliwa kutokana na uasherati.” Kwa sababu hiyo, kwa kudai kwamba wao ni waabudu wa kweli kama Abrahamu, wanakazania hivi: “Sisi tuna Baba mmoja, Mungu.”
Lakini je! kweli Mungu ndiye Baba yao? “Kama Mungu angekuwa ndiye Baba yenu,” Yesu anajibu, “nyinyi mngenipenda, kwa maana mimi nilitoka kwa Mungu nami nipo hapa. Wala mimi sikuja kwa kujianzishia mwenyewe hata kidogo, bali huyo Mmoja ndiye aliyenituma. Kwa nini nyinyi hamjui ninalonena?”
Yesu amejaribu kuonyesha hawa viongozi wa kidini matokeo yao ya kumkataa. Lakini sasa anasema hivi kwa kutoboa wazi: “Nyinyi ni wa kutoka kwa baba yenu Ibilisi, na nyinyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu.” Ibilisi ni baba wa aina gani? Yesu alimtambulisha kuwa muuaji na pia akasema: “Yeye ni mwongo na baba ya ule uwongo.” Kwa hiyo Yesu anamalizia hivi: “Yeye ambaye ni wa kutoka kwa Mungu husikiliza semi za Mungu. Hii ndiyo sababu nyinyi hamsikilizi, kwa sababu nyinyi si wa kutoka kwa Mungu.”
Kwa kukasirishwa na shutumu kali la Yesu, Wayahudi wanajibu hivi: “Je! sisi hatusemi kwa kufaa, Wewe ni Msamaria na una roho mwovu?” Mtajo huo “Msamaria” unatumiwa kama usemi wa dharau na suto, Wasamaria wakiwa ni kikundi cha watu wanaochukiwa na Wayahudi.
Akipuuza suto hilo la dharau kwamba ni Msamaria, Yesu anajibu hivi: “Mimi sina roho mwovu, lakini mimi naheshimu Baba yangu, na nyinyi mnanivunjia heshima.” Akiendelea, Yesu anatoa ahadi hii ya kugutusha: “Ikiwa mtu yeyote anashika neno langu, yeye hataona kifo kamwe, hata kidogo.” Bila shaka, Yesu hamaanishi kwamba wote wanaomfuata hawataona kifo kamwe kwa uhalisi. Bali, anamaanisha kwamba wao hawataona kamwe uharibifu wa milele, au “kifo cha pili,” ambacho hakina ufufuo.
Hata hivyo, Wayahudi wanachukua maneno ya Yesu kihalisi. Kwa sababu hiyo, wao wanasema: “Sasa sisi tunajua wewe una roho mwovu. Abrahamu alikufa, pia manabii; lakini wewe wasema, ‘Ikiwa mtu yeyote anashika neno langu, yeye hataonja kifo kamwe hata kidogo.’ Wewe si mkuu zaidi ya Abrahamu baba yetu, ambaye alikufa, sivyo? Pia manabii walikufa. Wewe unadai kuwa nani?”
Katika mazungumzo haya yote, ni wazi kwamba Yesu anaonyesha wanaume hawa uhakika wa kwamba yeye ndiye Mesiya aliyeahidiwa. Lakini badala ya kujibu swali lao moja kwa moja juu ya yeye ni nani, Yesu anasema: “Kama mimi najitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ndiye anitukuzaye mimi, yeye ambaye nyinyi mwasema ndiye Mungu wenu; na bado nyinyi mmekuwa hammjui. Lakini mimi namjua. Na kama mimi ningesema simjui ingenipasa kuwa kama nyinyi, mwongo.”
Akiendelea, Yesu anarejeza tena kwenye Abrahamu mwaminifu, akisema: “Abrahamu baba yenu alishangilia sana katika tazamio la kuona siku yangu, naye aliiona na kushangilia.” Ndiyo, kwa macho ya imani Abrahamu alitazama mbele katika kuwasili kwa Mesiya aliyeahidiwa. Kwa kukataa kuamini, Wayahudi wanajibu hivi: “Wewe hujafika bado miaka hamsini, na bado wewe umeona Abrahamu?”
“Kweli kweli kabisa mimi nawaambia nyinyi,” Yesu akajibu, “kabla Abrahamu hajapata kuwako, mimi nimekuwako.” Bila shaka, Yesu anarejeza kwenye kuwako kwake kabla ya kuwa binadamu akiwa mtu wa roho mwenye uweza mbinguni.
Kwa kukasirishwa na dai la Yesu la kwamba alikuwako kabla ya Abrahamu, Wayahudi wanaokota mawe wamvurumishie. Lakini yeye anajificha na kwenda nje ya hekalu bila kuumizwa. Yohana 8:37-59; Ufunuo 3:14; 21:8, NW.
▪ Yesu anaonyeshaje kwamba yeye na maadui wake wana mababa tofauti?
▪ Ni nini maana ya Wayahudi kumwita Yesu Msamaria?
▪ Ni katika maana gani Yesu anamaanisha kwamba wafuasi wake hawataona kifo kamwe?