Sura 74
Shauri kwa Martha, na Fundisho Juu ya Sala
WAKATI wa mwendo wa huduma ya Yesu ya Kiyudea, yeye anaingia katika kijiji cha Bethania. Hapa ndipo Martha, Mariamu, na Lazaro ndugu yao wanaishi. Labda Yesu alikuta hawa watatu mapema kidogo katika huduma yake na kwa hiyo tayari ni rafiki yao wa karibu. Vyoyote iwavyo, sasa Yesu anaenda kwenye makao ya Martha na anakaribishwa naye.
Martha ana hamu nyingi ya kuandalia Yesu kilicho bora kabisa alicho nacho. Kweli kweli, ni heshima kubwa mmoja kufanyiwa ziara na Mesiya aliyeahidiwa kwenye makao yake! Kwa hiyo Martha anajihusisha katika kutayarisha mlo wenye madoido mengi na kuhakikisha vijambo vingine vingi ili kufanya kukaa kwa Yesu kuwe kwenye kufurahika na kustareheka zaidi.
Kwa upande mwingine, Mariamu dada ya Martha anaketi chini kwenye nyayo za Yesu na kumsikiliza. Baada ya kitambo, Martha anakaribia na kusema kwa Yesu hivi: “Bwana, si kitu kwako wewe kwamba dada yangu ameniacha mimi peke yangu nishughulikie mambo? Kwa hiyo, mwambie ajiunge nami na kunisaidia.”
Lakini Yesu anakataa kusema lolote kwa Mariamu. Badala ya hivyo, yeye anashauri Martha kwa kuhangaikia mno vitu vya kimwili. “Martha, Martha,” yeye anakaripia kwa fadhili, “wewe unahangaikia na kusumbukia mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache yahitajiwa, au moja tu.” Yesu anasema kwamba si jambo la lazima kabisa kutumia wakati mwingi kutayarisha vyakula vingi kwa ajili ya mlo mmoja. Vyakula vichache tu, au hata chakula kimoja tu, chatosha.
Makusudio ya Martha ni mema; yeye anataka kuwa mwanamke mwenye ukaribishaji-wageni mzuri. Hata hivyo, kwa hangaikio lake la kuelekeza fikira kwenye maandalizi ya kimwili, yeye anakosa ile fursa ya kupokea fundisho la kibinafsi kutoka kwa Mwana wa Mungu mwenyewe! Kwa hiyo Yesu anamalizia hivi: “Kwa sehemu yake, Mariamu alichagua fungu jema, na hilo halitatwaliwa kutoka kwake.”
Baadaye, katika pindi nyingine, mwanafunzi mmoja anauliza Yesu: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali, kama vile Yohana alivyofundisha pia wanafunzi wake.” Inawezekana mwanafunzi huyu hakuwapo wapata mwaka mmoja na nusu mapema zaidi wakati Yesu alipoandaa ile sala ya kiolezo katika Mahubiri yake ya Mlimani. Kwa hiyo Yesu anarudia maagizo yake lakini ndipo anapotoa kielezi kukazia uhitaji wa kudumu katika sala.
“Ni nani wa nyinyi atakuwa na rafiki,” Yesu anaanza, “na atamwendea usiku wa manane na kusema kwake, ‘Rafiki, nikopeshe mikate mitatu, kwa sababu rafiki yangu mmoja amekuja sasa hivi akiwa safarini na mimi sina kitu cha kuweka mbele yake’? Na huyo akiwa ndani asema katika kujibu, ‘Acha kunifanyia matata. Mlango tayari umefungwa kufuli, na watoto wangu wachanga wamo pamoja nami kitandani; mimi siwezi kuinuka na kukupa wewe kitu chochote.’ Mimi nawaambia nyinyi, Ingawa yeye hatainuka na kumpa kitu chochote kwa sababu ya kuwa rafiki yake, kwa uhakika kwa sababu ya udumifu wake wa kijasiri yeye ataamka na kumpa vitu ambavyo yeye anahitaji.”
Kwa ulinganisho huu Yesu hamaanishi kwamba Yehova Mungu hana nia ya kujibu maombi-rasmi, kama vile alivyokuwa yule rafiki katika hadithi yake. Sivyo, bali yeye anatoa kielezi cha kwamba ikiwa rafiki asiye na nia atajibu maombi yenye kufanywa kwa udumifu, ni zaidi kama nini Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo atafanya hivyo! Kwa hiyo Yesu anaendelea hivi: “Kwa hiyo mimi nasema kwenu nyinyi, Fulizeni kuomba, na nyinyi mtapewa; fulizeni kutafuta, na nyinyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, na nyinyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mmoja ambaye anaomba hupokea, na kila mmoja ambaye anatafuta hupata, na kila mmoja ambaye anabisha hodi atafunguliwa.”
Ndipo Yesu anaporejezea mababa wa kibinadamu wasiokamilika, wenye dhambi, akisema: “Kweli kweli, ni baba yupi aliye miongoni mwenu nyinyi ambaye, ikiwa mwana wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa yeye anaomba yai pia, atampa nge? Kwa hiyo, ikiwa nyinyi, ingawa ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu vipaji vyema, ni zaidi kama nini yule Baba wa mbinguni atawapa roho takatifu wale ambao wanamwomba!” Kweli kweli, ni kitia-moyo chenye kusukuma kama nini ambacho Yesu anaandaa ili kuwa na udumifu katika sala. Luka 10:38–11:13, NW.
▪ Kwa nini Martha anafanya matayarisho mengi sana hivyo kwa ajili ya Yesu?
▪ Mariamu afanya nini, na kwa nini Yesu apongeza yeye badala ya Martha?
▪ Ni jambo gani lasukuma Yesu arudie mafundisho yake juu ya sala?
▪Yesu aonyeshaje uhitaji wa kudumu katika sala?