Sura 75
Chanzo cha Furaha
WAKATI wa huduma yake katika Galilaya, Yesu alifanya miujiza, na sasa yeye anairudia katika Yudea. Mathalani, yeye anafukuza kutoka kwa mwanamume mmoja roho mwovu ambaye amemzuia kunena. Umati unastaajabu, lakini wachambuzi wanatokeza kipingamizi kama kile kile kilichotokezwa katika Galilaya. “Yeye hufukuza roho waovu kwa njia ya Beelzebuli yule mtawala wa roho waovu,” wao wanadai. Wengine wanataka uthibitisho mkubwa zaidi kutoka kwa Yesu wa kumtambulisha yeye ni nani, na wanajaribu kumshawishi kwa kuomba ishara moja kutoka mbinguni.
Akijua jambo wanalofikiria, Yesu anawapa wachambuzi wake katika Yudea jibu lile lile alilowapa wale waliokuwa katika Galilaya. Yeye anaonelea kwamba kila ufalme uliogawanyika dhidi yao wenyewe utaanguka. “Kwa hiyo,” yeye anauliza, “ikiwa Shetani pia amegawanyika dhidi yake mwenyewe, ufalme wake utasimamaje?” Yeye anaonyesha msimamo hatari wa wachambuzi wake kwa kusema: “Ikiwa ni kwa njia ya kidole cha Mungu mimi hufukuza roho waovu, ufalme wa Mungu umewapita nyinyi kweli kweli.”
Wale wanaotazama miujiza ya Yesu wanapaswa kuiitikia jinsi ile ile walivyoitikia wale ambao karne zilizotangulia walimwona Musa akifanya mwujiza. Wao walipaaza sauti ya mshangao wakisema: “Ni kidole cha Mungu!” Pia “kidole cha Mungu” ndicho kilichongelea zile Amri Kumi juu ya mbao-mawe. Na “kidole cha Mungu”—roho takatifu yake, au kani ya utendaji—ndicho kinachomwezesha Yesu kufukuza roho waovu na kuponya magonjwa. Kwa hiyo Ufalme wa Mungu umewapita wachambuzi hawa kweli kweli, kwa kuwa Yesu, aliye Mfalme mkusudiwa wa ule Ufalme, yupo pale pale katikati yao.
Ndipo Yesu anapotoa kielezi cha kuonyesha kwamba uwezo wake wa kufukuza roho waovu ni uthibitisho wa nguvu zake juu ya Shetani, hata kama vile ilivyo wakati mwanamume mwenye nguvu zaidi anapokuja na kumshinda nguvu mwanamume mwenye silaha za kutosha anayelinda jumba lake la kifalme. Pia anarudia kielezi kile alichosimulia katika Galilaya kuhusu roho asiye safi. Roho huyo anaondoka katika mwanamume fulani, lakini wakati mwanamume huyo anapokosa kujazia utupu huo kwa mambo mema, roho huyo anarudi pamoja na wengine saba, na hali ya mwanamume huyo inakuwa mbaya kuliko hapo kwanza.
Anapokuwa akisikiliza mafundisho hayo, mwanamke mmoja kutoka kwenye ule umati anasukumwa kupaaza sauti ya mshangao hivi: “Ni lenye furaha tumbo-uzazi ambalo lilikuchukua na matiti ambayo ulinyonya!” Kwa kuwa tamaa ya kila mwanamke Myahudi ni kuwa mama ya nabii na hasa yule Mesiya, inaeleweka kwamba mwanamke huyu angesema hivyo. Inaonekana alifikiri Mariamu angeweza kuwa mwenye furaha hususa kwa sababu ya kuwa ndiye mama ya Yesu.
Hata hivyo, Yesu anamsahihisha haraka mwanamke huyo kuhusu chanzo cha kweli cha furaha. “Sivyo,” yeye ajibu, “bali, Wenye furaha ni wale ambao wanasikia neno la Mungu na kulishika!” Yesu hakudokeza kamwe kwamba Mariamu, mama yake, apaswa kupewa heshima ya pekee. Badala ya hivyo, yeye alionyesha kwamba furaha ya kweli inapatikana kwa kuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, si katika mahusiano wala matimizo yoyote ya kimwili.
Kama alivyofanya katika Galilaya, Yesu anaendelea pia kuwakemea watu katika Yudea kwa kuomba ishara kutoka mbinguni. Yeye anawaambia kwamba hakuna ishara itakayotolewa isipokuwa ile ishara ya Yona. Yona alikuja kuwa ishara kwa kuwamo kwake siku tatu katika yule samaki na pia kwa kuhubiri kwake kijasiri, na tokeo likawa ni kuwasukuma Waninawi kwenye toba. “Lakini, tazameni!” Yesu asema, “kitu fulani kilicho zaidi ya Yona kipo hapa.” Vilevile, malkia wa Sheba aliona ajabu kuhusu hekima ya Solomoni. “Lakini, tazameni!” Yesu anasema pia, “kitu fulani kilicho zaidi ya Solomoni kipo hapa.”
Yesu anaeleza kwamba wakati mtu anapowasha taa, yeye haitii katika chumba cha chini ya sakafu au chini ya kikapu bali juu ya kinara cha taa ili kwamba watu waweze kuiona nuru. Labda yeye anadokeza kwamba kufundisha na kufanya miujiza mbele ya watu hawa wenye mioyo migumu katika wasikilizaji wake kunalinganika na kuficha nuru ya taa. Macho ya watazamaji kama hao si rahisi, au hayakazwi mahali pale panapofaa, kwa hiyo madhumuni yaliyokusudiwa ya miujiza yake hayatimizwi.
Yesu amefukuza sasa hivi roho mwovu na kusababisha mwanamume bubu anene. Hilo lapasa kusukuma watu wenye macho rahisi, au yaliyokazwa mahali panapofaa, wasifu kitendo hiki hodari kilicho kitukufu na kutangaza habari njema hizo! Na bado, wachambuzi hawa hawafanyi hivyo. Kwa hiyo Yesu anamalizia hivi: “Kwa hiyo, uwe chonjo. Labda ile nuru ambayo imo ndani yako wewe ni giza. Kwa hiyo, ikiwa mwili wako mzima ni mwangavu bila hata sehemu yoyote kuwa giza, wote utakuwa mwangavu kama wakati ambapo taa inakupa wewe nuru kwa mionzi yayo.” Luka 11:14-36; Kutoka 8:18, 19; 31:18; Mathayo 12:22, 28, NW.
▪ Ni nini itikio la kuponya kwa Yesu yule mwanamume?
▪ “Kidole cha Mungu” ni nini, na Ufalme wa Mungu ulikuwa umewapitaje wasikilizaji wa Yesu?
▪ Ni nini chanzo cha furaha ya kweli?
▪ Mtu anawezaje kuwa na jicho rahisi?