Sura 90
Tumaini la Ufufuo
MWISHOWE Yesu anawasili kwenye viunga vya Bethania, kijiji kilicho karibu kilometa 3 kutoka Yerusalemu. Ni siku chache tu zimepita tangu Lazaro afe na kuzikwa. Mariamu na Martha dada zake wangali wanaomboleza, na wengi wamekuja nyumbani kwao kuwaliwaza.
Wanapokuwa wakiomboleza, mtu fulani anampasha Martha habari kwamba Yesu yuko njiani. Kwa hiyo yeye anaondoka na kufanya haraka akamlaki, inaonekana bila ya kumwambia dada yake. Akimjia Yesu, Martha anarudia maneno ambayo ni lazima yeye na dada yake wawe wameyasema mara nyingi siku nne zilizopita: “Kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa.”
Hata hivyo, Martha anaonyesha tumaini, akidokeza kwamba huenda bado Yesu akaweza kumfanyia ndugu yake jambo fulani. “Najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Martha anasema.
“Ndugu yako atafufuka,” Yesu anaahidi.
Martha anaelewa kuwa Yesu ananena juu ya ufufuo wa kidunia wa wakati ujao, ambao Abrahamu na watumishi wengine pia wa Mungu waliutazamia. Kwa hiyo anajibu hivi: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”
Hata hivyo, Yesu anatoa tumaini la kitulizo cha mara hiyo, akijibu hivi: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima.” Anakumbusha Martha kwamba Mungu amempa uwezo juu ya kifo, akisema: “Yeye aniaminiye [anayejizoeza imani katika, NW] mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; na kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”
Yesu hamdokezei Martha kwamba waaminifu walio hai wakati huo hawatakufa kamwe. Sivyo, bali wazo analotokeza ni kwamba kujizoeza imani katika yeye kunaweza kuongoza kwenye uhai wa milele. Uhai huo utaonewa shangwe na walio wengi kutokana na kufufuliwa kwao siku ya mwisho. Lakini wengine walio waaminifu wataokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo duniani, na kwa hao maneno ya Yesu yatakuwa kweli katika maana halisi sana. Wao hawatakufa kamwe kamwe! Baada ya taarifa hiyo ya kustaajabisha, Yesu anauliza Martha, “Je! unayasadiki hayo?”
“Naam, Bwana,” anajibu. “Mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.”
Halafu Martha anafanya haraka kuita dada yake, akimwambia faraghani: “Mwalimu yupo anakuita.” Mara hiyo Mariamu anaondoka nyumbani. Wengine wanapomwona akienda, wanafuata, wakidhani kwamba anaenda kwenye ziara la ukumbusho.
Akimjia Yesu, Mariamu anaanguka kwenye nyayo zake akilia machozi. “Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu, hangalikufa,” anasema. Yesu anaguswa moyo sana anapoona kwamba Mariamu na umati wa watu wanaomfuata wanalia. “Mmemweka wapi?” anauliza.
“Bwana, njoo utazame,” wanajibu.
Yesu pia anaruhusu machozi yamtoke, ikisababisha Wayahudi kusema: “Angalieni jinsi alivyompenda.”
Baadhi yao wanakumbuka kwamba wakati wa Sikukuu ya Mahema miezi michache iliyotangulia, Yesu alikuwa ameponya kijana mwanamume aliyezaliwa kipofu, nao wanauliza: “Je! huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?” Yohana 5:21; 6:40; 9:1-7; 11:17-37.
▪ Ni wakati gani Yesu anawasili mwishowe karibu na Bethania, na hali ikoje huko?
▪ Martha ana msingi gani wa kuamini katika ufufuo?
▪ Yesu anaathiriwaje na kifo cha Lazaro?