Sura 93
Wakati Mwana wa Binadamu Anapofunuliwa
YESU akiwa angali kaskazini (ama katika Samaria ama katika Galilaya), Mafarisayo wanamuuliza juu ya kufika kwa Ufalme. Wao wanaamini kwamba utakuja kwa fahari ya kujionyesha sana na kwa sherehe, lakini Yesu anasema: “Ufalme wa Mungu hauji kwa njia ya kuonekana yenye kustaajabisha sana, wala watu hawatakuwa wakisema, ‘Oneni hapa!’ au ‘Pale!’ Kwa maana tazama! ufalme wa Mungu umo katikati yenu.”
Maneno ya Yesu “katikati yenu,” nyakati fulani yametafsiriwa “ndani yenu.” Wengine wamefikiri kwamba Yesu alimaanisha kwamba Ufalme wa Mungu hutawala katika mioyo ya watumishi wa Mungu. Lakini, kwa wazi, Ufalme wa Mungu haumo ndani ya mioyo ya Mafarisayo hawa wasioamini ambao Yesu ananena nao. Hata hivyo, umo katikati yao, kwa kuwa Mfalme mkusudiwa wa Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo, yumo mle mle miongoni mwao.
Labda ni baada ya Mafarisayo kwenda zao kwamba Yesu anazidi kuongea na wanafunzi wake juu ya kuja kwa Ufalme. Yeye anafikiria hasa kuwapo kwake kwa wakati ujao katika mamlaka ya Ufalme wakati anapoonya hivi: “Watu watasema kwenu nyinyi, ‘Oneni pale!’ au ‘Oneni hapa!’ Msiende nje wala msiende mbio kutafuta [Mesiya hawa bandia]. Kwa maana hata kama vile umeme, kwa kuwaka kwao, unavyong’aa kutoka sehemu moja chini ya mbingu hadi sehemu nyingine chini ya mbingu, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa.” Kwa sababu hiyo, Yesu anaonyesha kwamba kama vile umeme unavyoonwa katika eneo pana, ushuhuda wa kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme utakuwa wenye kuonekana wazi kwa wote wanaotaka kuuona.
Ndipo Yesu anapofanya ulinganisho wa matukio ya kale kuonyesha vile mielekeo ya watu itakavyokuwa katika pindi ya kuwapo kwake wakati ujao. Anaeleza hivi: “Zaidi ya hilo, kama vile ilivyotukia katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa pia katika siku za Mwana wa binadamu . . . Vilevile, kama vile ilivyotukia katika siku za Loti: walikuwa wanakula, walikuwa wanakunywa, walikuwa wananunua, walikuwa wanauza, walikuwa wanapanda, walikuwa wanajenga. Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma ilikunya moto na salfa kutoka mbinguni na kuharibu wote. Itakuwa vivyo hivyo katika siku hiyo wakati Mwana wa binadamu atapaswa kufunuliwa.”
Yesu hasemi kwamba watu katika siku za Noa na siku za Loti waliharibiwa kwa sababu tu walifuatia utendaji wa kikawaida wa kula, kunywa, kununua, kuuza, kupanda, na kujenga. Hata Noa na Loti na jamaa zao walifanya mambo hayo. Lakini wale wengine walifanya utendaji huo wa kila siku bila kuelekeza usikizi wowote kwenye mapenzi ya Mungu, na hii ndiyo sababu waliharibiwa. Kwa sababu iyo hiyo, watu wataharibiwa wakati Kristo atakapofunuliwa katika pindi ya dhiki kubwa itakayokuwa juu ya mfumo huu wa mambo.
Akikazia umaana wa kuitikia upesi ushuhuda wa kuwapo kwake wakati ujao katika mamlaka ya Ufalme, Yesu anaongezea hivi: “Siku hiyo acheni mtu ambaye yuko juu ya nyumba lakini ambaye vitu vyake vyenye kuchukulika vimo ndani ya nyumba asije chini kuvichukua, na mtu aliye nje katika shamba, acheni yeye vilevile asirudi kwenye vitu vilivyo nyuma. Kumbukeni mke wa Loti.”
Ushuhuda wa kuwapo kwa Kristo unapotokea, watu hawawezi kuacha ufungamano kwa mali za kimwili uwazuie kuchukua hatua ya haraka. Alipokuwa njiani kutoka Sodoma, inaonekana wazi kuwa mke wa Loti alitazama nyuma kwa kutamani vitu alivyoacha nyuma, naye akawa nguzo ya chumvi.
Akiendelea na uelezaji wake wa hali ambayo ingekuwako katika pindi ya kuwapo kwake wakati ujao, Yesu anawaambia wanafunzi wake hivi: “Katika usiku huo wanaume wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja yule atachukuliwa, lakini yule mwingine ataachwa. Watakuwako wanawake wawili wakisaga kwenye kinu kile kile; mmoja yule atachukuliwa, lakini yule mwingine ataachwa.”
Kuchukuliwa kunalingana na vile Noa pamoja na jamaa yake walivyoingia ndani ya safina na vile malaika walivyoondoa Loti na jamaa yake katika Sodoma. Kunamaanisha wokovu. Kwa upande mwingine, kuachwa kunamaanisha kupatwa na uharibifu.
Kufikia hapo, wanafunzi wanauliza: “Wapi, Bwana?”
“Mahali ulipo mwili, hapo pia ndipo tai watakuwa wamekusanyika pamoja,” Yesu anajibu. Wale ‘wanaochukuliwa’ wakapate wokovu ni kama tai wenye kuona mbali katika maana ya kwamba wanakusanyika pamoja kwenye “mwili.” Mwili huo unamaanisha Kristo aliye wa kweli wakati wa kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme na kwenye karamu ya kiroho ambayo Yehova anaandaa. Luka 17:20-37; Mwanzo 19:26, NW.
▪ Ufalme ulikuwaje kati ya Mafarisayo?
▪ Ni katika njia gani kuwapo kwa Kristo ni kama umeme?
▪ Kwa nini watu wataharibiwa kwa sababu ya vitendo vyao katika pindi ya kuwapo kwa Kristo?
▪ Inamaanisha nini kuchukuliwa, na kuachwa?