Sura 133
Yesu Amaliza Yote Ambayo Mungu Amwomba Afanye
WAKATI Mwanavita Mfalme Yesu Kristo aondoshapo Shetani na ulimwengu wake usio mwadilifu, kutakuwa na sababu nzuri kama nini ya kushangilia! Mwishowe waja ule Utawala wa Miaka Elfu wenye amani wa Yesu!
Chini ya mwelekezo wa Yesu na wafalme washirika wake, waokokaji wa Har–Magedoni wataondolea mbali magofu yalioachwa na vita hiyo ya uadilifu. Yaelekea waokokaji wa kidunia watazaa watoto pia kwa muda fulani, na hao watashiriki katika ile kazi yenye kupendeza ya kuilima dunia na kuigeuza iwe shamba lenye kupendeza sana mfano wa bustani.
Baada ya wakati fulani Yesu atatoa kutoka makaburi yao mamilioni yasiyojulikana waifurahie Paradiso hiyo nzuri. Atafanya hivyo katika kutimiza uhakikishio huu wake mwenyewe: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini . . . watatoka.”
Miongoni mwa hao wafufuliwao na Yesu atakuwamo yule aliyekuwa hapo kwanza mtenda maovu aliyekufa kando yake juu ya mti wa mateso. Kumbuka kwamba Yesu alimwahidi hivi: “Kweli kweli mimi nakuambia wewe leo, Wewe utakuwa na mimi katika Paradiso.” Hapana, mtu huyo hatachukuliwa mbinguni akatawale akiwa mfalme pamoja na Yesu, wala Yesu hatakuja tena awe binadamu na kuishi katika Paradiso hiyo duniani pamoja naye. Badala ya hivyo, Yesu atakuwa pamoja na huyo aliyekuwa hapo kwanza mtenda maovu katika maana ya kwamba Yeye atamfufua aishi katika Paradiso na kuhakikisha kwamba atimiziwa mahitaji yake, ya kimwili na ya kiroho, kama picha inavyoonyesha katika ukurasa unaofuata.
Ebu fikiria hilo! Chini ya uangalizi wenye upendo wa Yesu, familia yote ya kibinadamu—waokokaji wa Har–Magedoni, wazao wao, na wale maelfu ya mamilioni ya wafu waliofufuliwa na wanaomtii—watakua kuelekea ukamilifu wa kibinadamu. Yehova, kwa njia ya Mwana wake wa kifalme, Yesu Kristo, atakaa kiroho pamoja na aina ya kibinadamu. “Naye,” kama ile sauti aliyosikia Yohana isemavyo, “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” Hakuna mtu duniani atakayeteseka au kuwa mgonjwa.
Kufikia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu, hali itakuwa kama vile Mungu alivyokusudia mwanzoni wakati alipowaambia watu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, waongezeke na kuijaza dunia. Ndiyo, dunia itajawa na jamii yenye uadilifu ya binadamu wakamilifu. Hiyo ni kwa sababu faida za dhabihu ya ukombozi ya Yesu zitakuwa zimetumiwa kwa kila mmoja. Kifo kwa sababu ya dhambi ya Adamu hakitakuwako tena!
Hivyo, Yesu atakuwa amekwisha timiza yote ambayo Yehova alimwomba afanye. Kwa hiyo, mwishoni mwa ile miaka elfu, atampa Baba yake Ufalme na familia ya kibinadamu iliyofanywa kuwa kamilifu. Ndipo Mungu atakapowaachilia Shetani na roho wake waovu watoke katika abiso ya kutotenda iliyo mfano wa kifo. Kwa kusudi gani?
Basi, kufikia mwishoni mwa ile miaka elfu, walio wengi wa wale wanaoishi katika Paradiso watakuwa wale waliofufuliwa ambao imani yao haijapata kujaribiwa kamwe. Kabla ya kufa, hawakuwa wamejua kamwe juu ya ahadi za Mungu na hivyo hawangeweza kuonyesha imani yao katika ahadi hizo. Halafu, baada ya kufufuliwa na kufundishwa kweli za Biblia, ilikuwa rahisi kwao kumtumikia Mungu katika Paradiso, bila upinzani wowote. Lakini Shetani akipewa fursa ajaribu kuwazuia wasiendelee kumtumikia Mungu, je! wangethibitisha ushikamanifu wao chini ya jaribu? Ili kuamua swali hilo, Shetani ataachiliwa.
Ufunuo aliopewa Yohana hufunua kwamba baada ya Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu, Shetani atafaulu katika kugeuza hesabu ya watu isiyojulikana waache kumtumikia Mungu. Kisha, jaribu la mwisho likiisha malizika, Shetani, roho wake waovu, na wale wote ambao atafaulu kuwapotosha wataharibiwa milele. Kwa upande mwingine, waokokaji washikamanifu waliojaribiwa kikamili wataendelea kuishi waonee shangwe baraka za Baba yao wa kimbingu kwa umilele wote.
Kwa wazi, Yesu ametimiza, na ataendelea kutimiza, fungu muhimu katika kutimiza makusudi matukufu ya Mungu. Lo! ni wakati ujao mtukufu kama nini tunaoweza kuonea shangwe kama tokeo la yote atimizayo akiwa Mfalme mkuu wa kimbingu wa Mungu. Hata hivyo, sisi hatuwezi kusahau yote ambayo alifanya alipokuwa duniani akiwa binadamu.
Kwa moyo wa kupenda Yesu alikuja duniani na kutufundisha juu ya Baba yake. Zaidi ya hilo yeye alitoa kielelezo cha sifa zenye thamani kubwa za Mungu. Mioyo yetu inasukumwa wakati tunapofikiria ujasiri wake mwingi sana na sifa zake za kiume, hekima yake isiyolinganika, uwezo wake mwingi sana akiwa mwalimu, uongozi wake wa ujasiri, huruma zake nyororo na hisia zenye kusikitikia wengine. Tukumbukapo jinsi alivyoteseka kwa njia isiyoweza kuelezeka alipokuwa akitoa ukombozi, ambao kwa huo pekee twaweza kupata uhai, hakika mioyo yetu inasukumwa imthamini!
Kweli kweli, ni mtu wa namna gani tumeona katika funzo hili la maisha ya Yesu! Ukuu wake waonekana wazi nao ni mkubwa mno. Twasukumwa turudishe sauti ya maneno haya ya gavana Mroma Pontio Pilato: “Tazama, mtu huyu!” Ndiyo, kweli kweli, “Mtu huyu,” yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi!
Tukikubali uandalizi wa dhabihu yake ya ukombozi, ule mzigo wenye kulemea wa dhambi na kifo tulivyorithi kutoka kwa Adamu waweza kuondolewa kwetu, na Yesu aweza kuwa “Baba wa Milele” wetu. Wale wote ambao wangependa kupata uhai wa milele ni lazima watwae maarifa ya kumjua si Mungu tu bali pia Mwana wake, Yesu Kristo. Kusoma na kujifunza kwako kitabu hiki na kukusaidie utwae maarifa hayo yenye kutoa uhai! 1 Yohana 2:17; 1:7; Yohana 5:28, 29; 3:16; 17:3; 19:5; Luka 23:43, NW; Mwanzo 1:28; 1 Wakorintho 15:24-28; Ufunuo 20:1-3, 6-10; 21:3, 4; Isaya 9:6.
▪ Ni nini litakalokuwa pendeleo lenye furaha la waokokaji wa Har–Magedoni na watoto wao?
▪ Zaidi ya waokokaji wa Har–Magedoni na watoto wao, ni nani wengine wataonea shangwe Paradiso na ni katika maana gani Yesu atakuwa pamoja nao?
▪ Hali itakuwaje mwishoni mwa ile miaka elfu, na Yesu atafanya nini wakati huo?
▪ Ni kwa nini Shetani ataachiliwa kutoka katika abiso, na mwishowe yeye na wale wote wamfuatao watapatwa na nini?
▪ Yesu awezaje kuwa “Baba wa Milele” wetu?