Sura ya 20
Kujenga Pamoja Duniani Pote
ILE hisi ya udugu wa kweli miongoni mwa Mashahidi wa Yehova inadhihirika kwa njia nyingi. Wale ambao huhudhuria mikutano yao huona ithibati yayo. Kwenye mikusanyiko yao inaonyeshwa kwa kadiri kubwa zaidi. Pia inaonekana wazi wanapofanya kazi pamoja ili kuandaa mahali pafaapo pa kukutania kwa ajili ya makutaniko yao.
Mwongo wa 1990 ulipokuwa ukianza, kulikuwa zaidi ya makutaniko 60,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wakati wa mwongo uliotangulia, wastani wa makutaniko mapya 1,759 yalikuwa yakiongezwa, kila mwaka. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, mwendo huo ulikuwa umeongezeka kufikia 3,000 kwa mwaka. Kuyaandalia yote mahali pafaapo pa kukutanikia kumekuwa kazi kubwa sana.
Majumba ya Ufalme
Kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, mwanzoni makutaniko mengi ya Mashahidi wa Yehova yalitumia makao ya faragha kwa mikutano yao mingi. Katika Stockholm, Sweden, wale wachache wa kwanza waliofanya mikutano ya ukawaida huko walitumia duka la useremala, ambalo walikodi ili walitumie baada ya kazi ya siku kufanywa. Kwa sababu ya mnyanyaso, kikundi kidogo katika mkoa wa La Coruña, Hispania, kilifanya mikutano yao ya kwanza katika bohari, au ghala ndogo.
Wakati nafasi zaidi ilipohitajiwa, katika nchi zilizokuwa na uhuru wa kufanya hivyo, makutaniko ya mahali ya Mashahidi wa Yehova yangekodi mahali pa mikutano. Hata hivyo, ikiwa jumba hilo lilikuwa likitumiwa pia na matengenezo mengine, ilibidi kusafirisha vifaa au kuviandaa kwa matumizi kwa ajili ya kila mkutano, na mara nyingi kulikuwako harufu ya tumbako iliyobakia. Mahali ilipowezekana, akina ndugu wangekodi duka lisilotumiwa au chumba cha orofa ambacho kingetumiwa na kutaniko pekee. Lakini, baada ya wakati, katika mahali pengi gharama za juu za kukodi na kutopatikana kwa mahali pafaapo kulifanya iwe lazima kufanya mipango mingine. Katika visa fulani majengo yalinunuliwa na kurekebishwa upya.
Kabla ya Vita ya Ulimwengu 2, yalikuwako makutaniko machache yaliyojenga mahali pa kukutana palipokusudiwa hasa kwa matumizi yao. Hata mapema sana kama 1890, kikundi cha Wanafunzi wa Biblia katika Marekani katika Mount Lookout, West Virginia, kilijenga mahali pacho chenyewe pa kukutanikia.a Hata hivyo, ujenzi wa Majumba ya Ufalme wenye kuenea haukuanza mpaka miaka ya 1950.
Jina Jumba la Ufalme lilidokezwa katika 1935 na J. F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Watch Tower Society. Kuhusiana na vifaa vya tawi la Sosaiti katika Honolulu, Hawaii, alipanga ndugu wajenge jumba ambamo mikutano ingefanyiwa. Wakati James Harrub alipouliza Ndugu Rutherford angeliitaje jengo hilo, yeye alijibu: “Waonaje tukiliita kwa jina ‘Jumba la Ufalme,’ kwa kuwa ndivyo tunavyofanya, kuhubiri habari njema za Ufalme?” Baada ya hapo, ilipowezekana, majumba yaliyokuwa yakitumiwa kwa ukawaida na Mashahidi yakaanza hatua kwa hatua kutambulishwa kwa ishara zilizosema “Jumba la Ufalme.” Hivyo, wakati London Tabernacle liliporekebishwa upya katika 1937-1938, lilipewa jina jipya Jumba la Ufalme. Baada ya wakati, mahali pakuu pa mikutano pa makutaniko ulimwenguni pote pakaja kuitwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.
Njia Zaidi ya Moja za Kujenga
Maamuzi juu ya kama watakodi au kujenga Majumba ya Ufalme hufanywa na makutaniko yenyewe mojamoja. Pia hayo hulipia gharama zozote za ujenzi na udumishaji. Ili kuokoa fedha, makutaniko mengi yamejitahidi kufanya kazi nyingi ya ujenzi kadiri inavyowezekana bila kuajiri wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa.
Majumba yenyewe yaweza kujengwa kwa matufali, mawe, na mbao, au vifaa vingine, ikitegemea gharama pamoja na vifaa vinavyopatikana katika eneo. Katika Katima Mulilo, Namibia, nyasi ndefu zilitumiwa kwa ajili ya paa, na udongo kutoka vichuguu (ambao hukauka na kuwa imara sana) ulifinyangwa kuwa ukuta na sakafu. Mashahidi katika Segovia, Kolombia, walitengeneza matufali ya saruji yao wenyewe ya kujengea. Mawe ya volkano kutoka Mlima Lasen yalitumiwa katika Colfax, California.
Hudhurio la mikutano mara nyingi likiwa linazidi 200 katika 1972, kutaniko katika Maseru, Lesotho, lilijua kwamba walihitaji kujenga Jumba la Ufalme lifaalo. Kila mtu alisaidia katika mradi huo. Ndugu wazee-wazee walitembea kufikia kilometa 32 ili kushiriki. Watoto walivingirisha mapipa ya maji kuyaleta kwenye mahali pa ujenzi. Dada waliandaa milo. Pia walitumia nyayo zao kutwanga ardhi, ili kuiimarisha katika kuitayarisha kwa ajili ya kumwagwa kwa bamba la zege, wakati wote wakiimba nyimbo za Ufalme na kukanyagakanyaga chini kwa kufuatana na mwendo wa muziki. Changarawe, iliyogharimu kuisafirisha tu kutoka milima ya karibu, ilitumiwa kwa ajili ya kuta. Tokeo likawa Jumba la Ufalme ambalo lingeweza kutoshea watu kama 250.
Nyakati nyingine, Mashahidi kutoka makutaniko ya karibu walisaidia kazi ya ujenzi. Hivyo, katika 1985, wakati Mashahidi wa Yehova katika Imbali, mji wa weusi katika Afrika Kusini, walipojenga jumba ambalo lingeweza kutoshea watu 400 vizuri, Mashahidi wenzao kutoka majiji ya karibu ya Pietermaritzburg na Durban walikuja kusaidia. Je, waweza kuwazia jinsi majirani walivyoshangaa wakati, katika pindi ya siku hizo za msukosuko wa tofauti za rangi katika Afrika Kusini, walipoona vikundi vya Mashahidi weupe, Machotara, na Wahindi wakimiminika katika mji na kufanya kazi bega kwa bega pamoja na ndugu zao Waafrika weusi? Kama vile meya mwenyeji alivyojulisha: “Laweza kufanywa kwa upendo tu.”
Hata roho ya kupenda iweje, makutaniko yaliona kwamba hali za mahali zilizuia yale ambayo ndugu wangeweza kufanya. Wanaume kutanikoni walikuwa na familia za kuruzuku na kwa kawaida wangeweza kufanya kazi kwenye mradi huo wakati wa miisho-juma tu na labda kidogo jioni. Makutaniko mengi yalikuwa na mafundi wa ujenzi wachache tu. Hata hivyo, jengo ambalo kidogo ni rahisi, lililo wazi kidogo lifaalo hali za tropiki lingeweza kujengwa kwa siku chache au labda majuma machache. Kwa msaada wa Mashahidi katika makutaniko ya karibu, majengo imara zaidi yangeweza kukamilishwa kwa miezi mitano au sita. Katika visa vingine ilitaka mwaka mmoja au miwili.
Hata hivyo, walipokuwa wakisonga kuingia katika miaka ya 1970, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walikuwa wakiongezeka kwa kadiri ya makutaniko mawili au matatu mapya kila siku. Kufikia miaka ya mapema ya 1990, kadiri ya ongezeko ilifikia makutaniko tisa kwa siku. Je, uhitaji wao mkubwa wa Majumba ya Ufalme mapya ungeweza kutimizwa?
Kusitawisha Mbinu za Ujenzi wa Haraka
Mapema katika miaka ya 1970, katika Marekani, Mashahidi zaidi ya 50 kutoka makutaniko ya karibu walikuja pamoja ili kusaidia kujenga Jumba la Ufalme jipya katika Carterville, Missouri, kwa ajili ya kikundi kilichokuwa kikikutana katika Jiji la Webb. Katika mwisho-juma mmoja walijenga kiunzi kikuu na kufanya kazi kubwa kwenye paa. Kulikuwa kungali na mengi ya kufanywa, na ilichukua miezi kadhaa kumaliza kazi; lakini sehemu ya maana yalo ilikuwa imekamilishwa kwa kipindi kifupi.
Wakati wa mwongo uliofuata, kadiri akina ndugu walivyofanya kazi pamoja kujenga majumba kama 60, vizuizi vilishindwa, na njia zenye matokeo zaidi zikasitawishwa. Baada ya wakati, walipata kuona kwamba baada ya kazi ya msingi kufanywa, wangeweza kukaribia kukamilisha Jumba la Ufalme lote kwa mwisho-juma mmoja.
Waangalizi kadhaa wa makutaniko—wote kutoka magharibi-kati mwa Marekani—walianza kujitahidi kufikia mradi huo. Wakati makutaniko yalipoomba msaada wa kujenga Jumba la Ufalme lao, mmoja au zaidi wa akina ndugu hao angezungumzia mradi huo pamoja nao na kuandaa mambo mengi madogomadogo kuhusu matayarisho ambayo lazima yashughulikiwe na wenyeji kabla ya kazi kuanza kufanywa. Miongoni mwa mambo mengine, ilibidi ruhusa za ujenzi zipatikane, ilibidi msingi na bamba la sakafu la zege vimwagwe, ilibidi umeme uwe unafanya kazi, ilibidi mabomba ya maji ya chini ya ardhi yawe yamewekwa mahali payo, na ilibidi ifanywe mipango yenye kutegemeka ya kuleta vifaa vya ujenzi. Kisha tarehe ingeweza kuwekwa ya ujenzi wa Jumba la Ufalme lenyewe. Jengo hilo halingekuwa limetangulia kuundwa; lingejengwa toka chini hadi juu mahali papo hapo pa ujenzi.
Ni nani wangefanya hasa kazi ya ujenzi? Kwa kadiri ilivyowezekana, ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa. Familia nzimanzima mara nyingi zilishiriki. Wale wenye kupanga mradi huo waliwasiliana na Mashahidi waliokuwa mafundi na ambao walikuwa wameeleza nia yao ya kushiriki katika miradi hiyo. Wengi wao walitazamia kwa hamu kila mradi mpya wa ujenzi. Mashahidi wengine waliopata kujua juu ya miradi hiyo walitaka kushiriki; mamia kutoka eneo la karibu—na kutoka sehemu za mbali zaidi—walimiminika kwenye mahali pa ujenzi, wakiwa na hamu ya kutoa utumishi wao mbalimbali katika njia yoyote waliyoweza. Walio wengi wao hawakuwa wajenzi stadi, lakini hakika walitoa ithibati kwamba wao walifaana na maelezo ya wale ambao wangekuwa waungaji mkono wa Mfalme wa Kimesiya wa Yehova kama ilivyoandikwa kwenye Zaburi 110:3, ambalo husema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.”
Alhamisi jioni kabla ya ile jitihada kubwa kuanza, wale waliokuwa wakisimamia ujenzi walikutana ili kupanga mambo madogomadogo ya mwisho. Jioni iliyofuata, wafanyakazi walionyeshwa slaidi juu ya utaratibu ili waelewe jinsi ambavyo kazi ingefanywa. Mkazo ulitiwa juu ya umaana wa sifa za kimungu. Ndugu walitiwa moyo wafanye kazi pamoja kwa upendo, wawe wenye fadhili, na kuonyesha saburi na ufikirio. Kila mtu alitiwa moyo afanye kazi kwa mwendo wa taratibu lakini asiharakishe na asisite kuchukua dakika chache kushiriki pamoja na mwingine jambo lililoonwa lenye kujenga. Mapema asubuhi iliyofuata, ujenzi ulianza.
Katika wakati uliopangwa mapema Jumamosi asubuhi, kila mtu angeacha kufanya alilokuwa akifanya ili kusikiliza mazungumzo ya Andiko la siku. Sala ilitolewa, maana ilifahamiwa vema kwamba fanikio la mradi wote lilitegemea baraka ya Yehova.—Zab. 127:1.
Kazi ilipoanza, hiyo ilisonga mbele kasi. Katika muda wa saa moja kuta zilikuwa zimesimama. Farasi za paa zilifuata. Kufunika kuta kukamalizwa. Mafundi wa umeme wakaanza kuzungusha waya. Vitundu vya visawazishahewa vikawekwa. Kabati zikajengwa pahali pazo. Nyakati nyingine kulinyesha mwisho-juma wote, au halihewa iligeuka kuwa baridi sana au joto sana, lakini kazi ilisonga mbele. Hakukuwa na mashindano au ushindani miongoni mwa mafundi.
Mara nyingi, kabla ya jua kushuka katika siku ya pili, Jumba la Ufalme lilikuwa limekamilishwa—limepambwa vizuri ndani, labda hata kupambwa mandhari ya nje. Ilipofaa zaidi, kazi ziliratibiwa ziendelee kwa siku tatu, au labda miisho-juma miwili. Mwishoni mwa mradi, walio wengi kati ya wafanyakazi wangebaki, wakiwa wamechoka lakini wenye furaha sana, wafurahie mkutano wa kwanza wa kawaida wa kutaniko, funzo la Mnara wa Mlinzi.
Wakitia shaka kwamba kazi nzuri ingeweza kufanywa kwa haraka sana jinsi hiyo, watu kadhaa katika Guymon, Oklahoma, Marekani, waliita mkaguzi wa ujenzi wa jiji. “Niliwaambia kwamba kama walitaka kuona jambo lililofanywa sawasawa, yawapasa kuzuru jumba hilo!” akasema mkaguzi huyo baadaye alipokuwa akisimulia Mashahidi kisa hicho. “Nyinyi watu hata mnafanya sawasawa yale yaliyofichika na yasiyoonekana!”
Kadiri uhitaji wa Majumba ya Ufalme ulivyoongezeka, ndugu waliokuwa wamesitawisha zile njia nyingi za ujenzi wa haraka walizoeza wengine. Ripoti za yale yaliyokuwa yakifanywa zilienea kwenye nchi nyinginezo. Je, njia hizo za ujenzi zingeweza kutumiwa huko pia?
Ujenzi wa Haraka Wafanywa Kuwa wa Kimataifa
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika Kanada ulikuwa ukiachwa nyuma sana na mahitaji ya makutaniko. Mashahidi katika Kanada walialika wale waliokuwa wakipanga miradi ya ujenzi wa haraka katika Marekani waje wawaeleze jinsi walivyoufanya. Mwanzoni, Wakanada walikuwa na shaka kidogo kwamba wangeweza kujenga hivyo katika Kanada, lakini waliamua kujaribu. Jumba la Ufalme la kwanza lililojengwa kwa njia hiyo katika Kanada lilijengwa katika Elmira, Ontario, katika 1982. Kufikia 1992, kulikuwa Majumba ya Ufalme 306 katika Kanada yaliyokuwa yamejengwa kwa njia hiyo.
Mashahidi katika Northampton, Uingereza, walifikiri kuwa wangeweza kufanya hivyo pia. Mradi wao, katika 1983, ulikuwa ndio wa kwanza katika Ulaya. Ndugu wenye ujuzi katika namna hiyo ya ujenzi walisafiri kutoka Marekani na Kanada ili kusimamia mradi huo na kusaidia Mashahidi wenyeji wajifunze jinsi ya kuufanya. Wenye kujitolea wengine walikuwapo kutoka mbali sana kama vile Japani, India, Ufaransa, na Ujerumani. Walikuwapo wakiwa wenye kujitolea, si ili kulipwa. Yote yaliwezekanaje? Kama vile mwangalizi wa kikundi kimoja cha Mashahidi wa Ireland kilichofanya kazi katika mradi kama huo alivyosema, ‘Yanafanikiwa kwa sababu ndugu na dada wote hushirikiana chini ya uvutano wa roho ya Yehova.’
Hata wakati sheria za ujenzi za mahali zinapoonekana zikifanya miradi kama hiyo isiwezekane, Mashahidi wamepata kwamba, mara nyingi, wakati maofisa wa jiji wanapoelezwa mambo kirefu, wanakuwa na furaha kushirikiana.
Baada ya mradi wa ujenzi wa haraka katika Norway, kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki, gazeti Finnmarken lilieleza kwa mshangao hivi: “Ajabu kabisa. Hayo ndiyo maneno pekee tuwezayo kupata ya kuelezea waliyofanya Mashahidi wa Yehova mwisho-juma uliopita.” Vivyo hivyo, wakati Mashahidi katika Kisiwa cha Kaskazini cha New Zealand walipojenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia kwa siku mbili na nusu, kichwa kikuu cha habari kwenye ukurasa wa mbele katika gazeti la mahali hapo kilijulisha: “Mradi Wakaribia Kuwa Muujiza.” Makala hiyo iliongeza: “Labda sehemu ya mradi huo yenye kuduwaza akili zaidi ni upangaji mzuri wa mambo na uendeshaji-mambo wenye utulivu kabisa.”
Umbali wa mahali panapohitaji Jumba la Ufalme hauthibitiki kuwa kizuizi kisichoshindika. Katika Belize mradi wa ujenzi wa haraka ulifanywa, hata ingawa ilimaanisha kusafirisha kila kipande cha kifaa cha ujenzi hadi kwenye kisiwa kilometa 60 kutoka Jiji la Belize. Wakati Jumba la Ufalme lenye kifaa cha kusawazisha hewa lilipojengwa katika Port Hedland, Australia Magharibi, mwisho-juma mmoja, lilijengwa kwa vifaa na wafanyakazi ambao karibu wote walikuja kutoka umbali wa kilometa 1,600 au zaidi. Wafanyakazi wenyewe walijilipia nauli zao wenyewe. Walio wengi kati ya wale walioshiriki sehemu katika mradi huo hawakujua kibinafsi Mashahidi katika Kutaniko la Port Hedland, na ni wachache sana kati yao ambao wangepata kuhudhuria mikutano humo wakati wowote. Lakini hiyo haikuwazuia kuonyesha upendo wao katika njia hiyo.
Hata kukiwa na idadi ndogo ya Mashahidi mahali fulani, hilo halizuii utumizi wa njia hizo za kujenga majumba. Mashahidi kama 800 kutoka Trinidad walijitolea kusafiri hadi Tobago ili kusaidia ndugu na dada zao Wakristo 84 wa huko wajenge jumba katika Scarborough katika 1985. Wale Mashahidi 17 (wengi wao wakiwa wanawake na watoto) katika Goose Bay, Labrador, bila shaka walihitaji msaada ikiwa wangeweza wakati wowote kupata Jumba la Ufalme lao wenyewe. Katika 1985, Mashahidi kutoka sehemu nyingine za Kanada walikodi ndege tatu ili kusafirisha 450 kati yao hadi Goose Bay ili kufanya kazi hiyo. Baada ya siku mbili za kazi ya bidii, walikuwa na programu ya kuwekwa wakfu katika jumba lililokamilika jioni ya Jumapili.
Hiyo haimaanishi kwamba Majumba ya Ufalme yote sasa yanajengwa kwa njia za ujenzi wa haraka, lakini idadi yayo inayozidi kukua yanajengwa hivyo.
Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa
Kufikia katikati ya 1986 kadiri ambayo Majumba ya Ufalme yalihitajiwa ilikuwa imeongezeka sana. Wakati wa mwaka uliotangulia, makutaniko mapya 2,461 yalikuwa yameundwa ulimwenguni pote; 207 kati ya hayo yalikuwa katika Marekani. Baadhi ya Majumba ya Ufalme yalikuwa yakitumiwa na makutaniko matatu, manne, au hata matano. Kama vile Maandiko yalivyokuwa yametabiri, kwelikweli Yehova alikuwa akiharakisha kazi ya kukusanya kuleta ndani.—Isa. 60:22.
Ili kuhakikisha utumizi bora zaidi wa wafanyakazi na kuwezesha wote waliokuwa wakijenga Majumba ya Ufalme wanufaike kutokana na ujuzi uliokuwa umepatikana, Sosaiti ilianza kuratibu utendaji wao. Ukiwa mwanzo, katika 1987 Marekani iligawanywa miongoni mwa Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa 60. Kulikuwa mengi ya kufanywa na hizo zote; upesi baadhi yazo zilikuwa na miradi iliyopangwa kwa mwaka mmoja au zaidi. Wale waliowekwa kutumikia kwenye halmashauri hizo walikuwa wanaume ambao, kwanza kabisa, walikuwa wamestahili kiroho, wazee katika makutaniko, walio vielelezo vizuri katika kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Wengi wao pia walikuwa na ujuzi katika kushughulikia mambo ya mashamba na nyumba, uhandisi, ujenzi, usimamizi wa biashara, usalama, na nyanja zinazohusiana.
Makutaniko yalitiwa moyo yashauriane na Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa kabla ya kuchagua mahali pa kujenga Jumba la Ufalme jipya. Mahali mlimokuwa na zaidi ya kutaniko moja jijini, walihimizwa pia kushauriana na mwangalizi au waangalizi wa mizunguko, mwangalizi wa jiji, na wazee kutoka makutaniko ya karibu. Makutaniko yaliyokuwa yakipanga urekebishaji mkubwa wa jengo la zamani au ujenzi wa Jumba la Ufalme jipya yalishauriwa yanufaike na ujuzi wa ndugu wa Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ya eneo lao na kwa miongozo ambayo Sosaiti ilikuwa imewatolea. Kupitia halmashauri hiyo, mipango ingeratibiwa ili kukusanya wafanyakazi stadi waliohitajiwa kutoka miongoni mwa ndugu na dada katika kazi za ufundi 65 waliokuwa tayari wamejitolea kusaidia kwenye miradi hiyo.
Kadiri taratibu zilivyofanywa kuwa bora zaidi, iliwezekana kupunguza idadi ya wafanyakazi waliohusika katika ujenzi wowote ule mmoja. Badala ya kuwa na maelfu penye ujenzi ama wakitazama ama wakitoa utumishi wao mbalimbali, ni mara chache sana walipokuwapo zaidi ya 200 penye ujenzi kwa wakati wowote ule mmoja. Badala ya kutumia mwisho-juma wote pale, wafanyakazi walikuwapo wakati tu stadi zao hususa zilipohitajiwa. Hivyo walikuwa na wakati zaidi wa kutumia pamoja na familia zao na wa kufanya utendaji pamoja na makutaniko ya kwao. Wakati ndugu wenyeji walipokuwa wanaweza kufanya kazi fulani kwa wakati mzuri, mara nyingi ilionekana kuwa yafaa zaidi kuleta kikundi cha ujenzi wa haraka wakati tu wa zile kazi ambazo walihitajiwa sana kufanya.
Ijapokuwa kazi yote ilisonga mbele kwa mwendo wenye kushangaza, hilo halikuwa ndilo jambo muhimu. Jambo muhimu zaidi lilikuwa kuandaa ujenzi bora wa Majumba ya Ufalme yenye kiasi yaliyokusudiwa kutimiza mahitaji ya mahali. Upangaji-mambo wa uangalifu ulifanywa ili kutimiza jambo hilo huku gharama zikiwa chini iwezekanavyo. Hatua zilichukuliwa kuhakikisha kwamba usalama ulifikiriwa zaidi—usalama wa wafanyakazi, majirani, wapita njia, na watumiaji wa wakati ujao wa Jumba la Ufalme.
Ripoti kuhusu mpango huo wa kujenga Majumba ya Ufalme zilipofikia nchi nyinginezo, ofisi za tawi za Sosaiti ambazo ziliamini kwamba ungekuwa wenye kufaidi katika maeneo yazo ziliandaliwa habari kamili zilizohitaji. Kufikia 1992, Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa zilizowekwa rasmi na Sosaiti zilikuwa zikisaidia ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika nchi kama vile Afrika Kusini, Argentina, Australia, Japani, Kanada, Mexico, Ufaransa, Hispania, Uingereza, na Ujerumani. Njia za ujenzi zilipatanishwa na hali za mahali. Msaada ulipohitajiwa kutoka kwa tawi jingine kwa ajili ya ujenzi wa Jumba la Ufalme, huo ulipangwa kupitia ofisi ya makao makuu ya Sosaiti. Katika sehemu fulani za ulimwengu, majumba mapya yalikuwa yakijengwa kwa siku kadhaa; kwingineko, kwa majuma kadhaa au labda miezi michache. Kwa kupanga mambo kwa uangalifu na jitihada zilizoratibiwa, bila shaka wakati uliotakwa ili kuandaa Jumba la Ufalme jipya ulikuwa ukipunguzwa.
Utendaji wa ujenzi wa Mashahidi wa Yehova haukuwa wa Majumba ya Ufalme tu. Vifaa vikubwa zaidi huhitajiwa wakati vikundi vya makutaniko vikutanapo kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko na siku za kusanyiko la pekee za kila mwaka.
Kutimiza Uhitaji wa Majumba ya Kusanyiko
Kwa muda wa miaka iliyopita, vifaa vya aina nyingi vimetumiwa kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko. Mashahidi wa Yehova wamekodi mahali kama vile majumba ya umma, shule, majumba ya maonyesho, mabohari ya silaha, viwanja vya michezo, na viwanja vya maonyesho. Katika sehemu chache, vifaa bora sana vilipatikana kwa bei nafuu. Mara nyingi zaidi, wakati na jitihada nyingi vilitakwa ili kusafisha mahali, kuandaa vikuza-sauti, kujenga jukwaa, na kusafirisha viti. Nyakati nyingine mapatano yalifutwa dakika ya mwisho. Kadiri idadi ya makutaniko ilivyoongezeka, ikawa vigumu zaidi na zaidi kupata mahalimahali pafaapo pa kutosha. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?
Kwa mara nyingine tena, suluhisho lilikuwa kwamba Mashahidi wa Yehova wawe na mahali pao wenyewe. Hiyo ingehusisha kurekebisha upya majengo yenye kufaa na kujenga mapya. La kwanza la Majumba ya Kusanyiko kama hayo katika Marekani lilikuwa jumba la maonyesho katika Long Island City, New York, lililorekebishwa upya na likaanza kutumiwa na Mashahidi wa Yehova mwishoni-mwishoni mwa 1965.
Karibu wakati uleule, Mashahidi kwenye kisiwa cha Guadeloupe cha Karibea walikuwa wakichora ramani ya Jumba la Kusanyiko la kutimiza mahitaji yao. Walihisi kwamba ingefaidi ikiwa wangekuwa na makusanyiko ya mzunguko katika sehemu nyingi tofauti-tofauti. Lakini miji iliyo mingi haikuwa na vifaa vilivyokuwa vikubwa vya kutosha. Kwa hiyo Mashahidi walijenga muundo uwezao kubebeka uliofanyizwa kwa vyuma na paa ya aluminiamu, kitu ambacho kingetosha kwa watu 700 na ambacho kingeweza kujengwa popote palipokuwa na ardhi iliyokuwa tambarare kidogo. Walilazimika kuongezea ukubwa wa jumba hilo tena na tena, mpaka lilipofikia kuweza kutoshea watu 5,000. Ebu fikiria kusafirisha, kujenga, na kubomoa tani 30 za vifaa kwa kila kusanyiko! Hilo Jumba la Kusanyiko lilijengwa na kubomolewa mara kadhaa kwa mwaka kwa muda wa miaka 13, mpaka ilipokuwa vigumu kupata ardhi kwa ajili ya jumba lenye kubebeka, ikawa lazima kununua ardhi na kujenga Jumba la Kusanyiko la kudumu, ambalo sasa hutumika kwa ajili ya makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya.
Katika sehemu chache, miradi ya Jumba la Kusanyiko ilitumia majengo yaliyokuwako. Katika Uingereza, katika Hays Bridge, Surrey, shule yenye majengo mengi ya miaka 50 ilinunuliwa na kurekebishwa upya. Iko katika uwanja wa hektari 11 katika sehemu nzuri ya mashambani. Yaliyokuwa hapo zamani majengo ya sinema na bohari la bidhaa za viwanda yalijengwa yakiwa na umbo jipya na kuanza kutumiwa katika Hispania; kiwanda cha nguo kisichotumika katika Australia; jumba la dansi katika Quebec, Kanada; jumba la michezo ya kuvingirisha matufe katika Japani; bohari la bidhaa katika Jamhuri ya Korea. Yote hayo yalijengwa upya na kuwa Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia ambayo yangeweza kutumika vyema kuwa vitovu vikubwa vya elimu ya Biblia.
Majumba ya Kusanyiko mengine yalikuwa mapya kabisa, yakiwa yamejengwa toka chini hadi juu. Lile umbo la pembenane la aina yalo la jumba katika Hellaby, South Yorkshire, Uingereza, pamoja na uhakika wa kwamba kazi iliyo nyingi ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea lilitokeza makala katika jarida la Taasisi ya Uhandisi wa Ujenzi. Jumba la Kusanyiko katika Saskatoon, Saskatchewan, katika Kanada, lilikusudiwa litoshee watu 1,200; lakini wakati kuta za ndani zinaposimamishwa mahali pazo, jengo hilo laweza kutumiwa likiwa Majumba ya Ufalme manne yakiwa upande kwa upande. Jumba la Kusanyiko la Haiti (lililotangulia kujengwa na kusafirishwa kutoka Marekani) lilikuwa wazi katika pande mbili ili wale walioketi ndani waweze kupashwa baridi daima na pepo zilizoko—kitulizo chenye kukaribishwa katika jua kali la Haiti. Jumba katika Port Moresby, Papua New Guinea, lilibuniwa kwa njia ya kwamba sehemu za kuta zingeweza kufunguka kama milango ili kuweza kutoshea umati mkubwa kuliko ule ambao ungeweza kutoshea ndani.
Uamuzi wa kujenga Jumba la Kusanyiko haufanywi na kikundi cha waangalizi ambao baada ya hapo hutarajia kila mtu mwingine auunge mkono. Kabla ya Jumba la Kusanyiko jipya lolote kujengwa, Sosaiti huhakikisha kwamba uchanganuzi wa uangalifu umefanywa kuhusu uhitaji walo na ni mara ngapi litatumiwa. Ufikirio hutolewa si kwa idili ya wenyeji kwa ajili ya mradi bali pia mahitaji ya ujumla shambani. Jambo hilo huzungumzwa pamoja na makutaniko yote yatakayohusika, ili kuhakikisha tamaa na uwezo wa akina ndugu wa kuutegemeza.
Hivyo, kazi ianzapo, Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanaiunga mkono kabisa. Pesa za kila mradi hutolewa na Mashahidi wenyewe. Mahitaji ya kifedha huelezwa, lakini michango ni ya kujitolea na watoaji hawajulikani ni kina nani. Mipango ya uangalifu hutangulia kufanywa, na ujenzi hunufaika kutokana na ujuzi uliokwisha kupatikana katika kujenga Majumba ya Ufalme na, mara nyingi, kutoka kwa miradi ya Majumba ya Kusanyiko katika sehemu nyingine. Inapohitajiwa, pande fulani za kazi zinaweza kupewa wafanyakazi wa mkataba wa kulipwa, lakini kazi iliyo nyingi kwa kawaida hufanywa na Mashahidi wenye idili. Hiyo inaweza kupunguza nusu ya gharama.
Kukiwa na jamii ya wafanyakazi wenye stadi na wengine ambao hutoa wakati na vipawa vyao, kwa kawaida ujenzi wote husonga mbele kwa haraka. Ujenzi fulani waweza kuhitaji zaidi ya mwaka. Lakini kwenye Kisiwa cha Vancouver katika Kanada, katika 1985, wenye kujitolea kama 4,500 walikamilisha Jumba la Kusanyiko la meta za mraba 2,300 kwa siku tisa tu. Jengo hilo latia ndani pia Jumba la Ufalme liwezalo kutoshea watu 200 kwa matumizi ya makutaniko ya mahali hapo. Katika New Caledonia, kafyu iliwekwa na serikali katika 1984 kwa sababu ya msukosuko wa kisiasa, hata hivyo wenye kujitolea kama 400 walifanya kazi kwenye Jumba la Kusanyiko wakati ule, na lilikamilishwa kwa miezi minne tu. Karibu na Stockholm, Sweden, Jumba la Kusanyiko zuri, lenye kufaa, likiwa na viti 900 vya mbao za oki vyenye matakia, lilijengwa kwa miezi saba.
Nyakati nyingine jitihada zenye kuendelea katika mahakama zimehitajiwa ili kupata ruhusa ya kujenga hayo Majumba ya Kusanyiko. Ndivyo ilivyokuwa katika Kanada katika Surrey, British Columbia. Wakati uwanja uliponunuliwa, matakwa ya kisheria ya eneo yaliruhusu ujenzi wa mahali kama hapo pa ibada. Lakini wakati ramani zilipopelekwa kwenye baraza, katika 1974, Baraza la Wilaya ya Surrey lilipitisha sheria ikisema kwamba makanisa na majumba ya kusanyiko yangeweza kujengwa tu katika Eneo la P-3—eneo lisilokuwako! Hata hivyo, makanisa 79 yalikuwa yamejengwa katika manispaa hiyo katika wakati uliopita bila matata. Jambo hilo lilipelekwa mahakamani. Maamuzi mengi yenye kupendelea Mashahidi wa Yehova yalitolewa. Wakati kizuizi cha maofisa wenye chuki zisizo na msingi kilipoondolewa hatimaye, wafanyakazi wa kujitolea walifuatia ujenzi huo kwa idili kubwa hivi kwamba waliukamilisha kwa miezi kama saba. Kama ilivyokuwa kwa habari ya Nehemia katika jitihada zake za kujenga upya kuta za Yerusalemu la kale, walihisi kwamba ‘mkono wa Mungu ulikuwa juu yao’ ili wakamilishe kazi hiyo.—Neh. 2:18.
Wakati Mashahidi wa Yehova katika Marekani waliponunua Stanley Theater katika Jersey City, New Jersey, jengo hilo lilikuwa katika daftari ya mkoa ya mahali pa kihistoria. Ijapokuwa jumba hilo lilikuwa katika hali mbaya yenye kuhitaji marekebisho, lilikuwa na uwezekano mzuri sana wa kutumika likiwa Jumba la Kusanyiko. Hata hivyo, wakati Mashahidi walipotaka kufanya marekebisho yaliyohitajiwa, maofisa wa jiji walikataa kutoa ruhusa. Meya hakutaka Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo; yeye alikuwa na mipango mingine kwa ajili ya jengo hilo. Hatua ya kisheria ilihitajiwa ili kuzuia maofisa wasitumie mamlaka yao kinyume cha sheria. Mahakama ilitoa uamuzi wenye kupendelea Mashahidi. Upesi baada ya hapo, wakazi wa eneo hilo walipiga kura kumwondoa meya huyo katika cheo chake. Kazi kwenye jumba ilisonga mbele kwa haraka. Tokeo lilikuwa Jumba la Kusanyiko zuri sana lililotoshea watu zaidi ya 4,000. Ni mahali ambapo wanabiashara na wakazi wa jiji hilo pia huonea fahari.
Wakati wa miaka 27 iliyopita, katika sehemu nyingi za dunia, Majumba ya Kusanyiko yenye kuvutia na yenye kufaa yamejengwa na Mashahidi wa Yehova ili kutumika kuwa vitovu vya elimu ya Biblia. Majumba kama hayo yanapatikana kwa hesabu zenye kuongezeka katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, na nch za Mashariki, pamoja na visiwa vingi. Katika nchi fulani—kwa kielelezo, Nigeria, Italia, na Denmark—Mashahidi wa Yehova wamejenga hata vifaa vya kudumu vilivyo vikubwa zaidi katika mahali peupe ambavyo vinaweza kutumiwa kwa ajili ya mikusanyiko yao ya wilaya.
Hata hivyo, Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme siyo miradi ya ujenzi pekee ambayo Mashahidi wa Yehova huhusika nayo ili kuendeleza kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu.
Ofisi, Matbaa, na Makao ya Betheli Ulimwenguni Pote
Ulimwenguni pote katika 1992, kulikuwa ofisi za tawi 99 za Watch Tower Society, kila moja yazo ilitumika katika kuratibu utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika sehemu yalo ya shamba la ulimwengu. Zaidi ya nusu ya matawi hayo hufanya uchapaji wa aina tofauti-tofauti ili kusogeza mbele kazi ya elimu ya Biblia. Wengi wa wale wanaofanya kazi katika matawi, huishi wakiwa familia kubwa katika makao yaitwayo Betheli, kumaanisha “Nyumba ya Mungu.” Kwa sababu ya mpanuko wa idadi ya Mashahidi wa Yehova na utendaji wao wa kuhubiri, imekuwa lazima kuongeza ukubwa wa makao hayo na kujenga mapya.
Ukuzi wa tengenezo umekuwa wa kasi sana hivi kwamba mara nyingi kumekuwa programu za upanuzi wa tawi 20 hadi 40 zikiendelea kwa wakati mmoja. Hiyo imetaka programu kubwa mno ya ujenzi wa kimataifa.
Kwa sababu ya kazi kubwa mno ya ujenzi inayofanywa ulimwenguni pote, Watch Tower Society ina Idara ya Uhandisi na Uchoraji-ramani yayo yenyewe kwenye makao makuu yayo ya New York. Wahandisi wenye miaka mingi ya ujuzi wameacha kazi zao za kimwili wakajitolea ili kusaidia kwa wakati wote kwenye miradi ya ujenzi inayohusiana moja kwa moja na utendaji wa Ufalme. Kwa kuongezea, wale ambao wana ujuzi wamefundisha wanaume na wanawake wengine katika kazi ya uhandisi, ubuni, na uchoraji-ramani. Kwa kuratibu kazi kupitia idara hii, ujuzi unaopatikana katika ujenzi wa tawi katika sehemu yoyote ya ulimwengu unaweza kunufaisha wale wanaofanya kazi kwenye miradi katika nchi nyinginezo.
Baada ya wakati, kiasi kikubwa cha kazi inayofanywa kilitokeza uhitaji wa kufungua Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa katika Japani ili kusaidia kufanya uchoraji-ramani kwa ajili ya miradi katika nchi za Mashariki. Ofisi za Uhandisi za Kimkoa nyingine huendesha kazi katika Ulaya na Australia, wafanyakazi wakiwa wametoka katika nchi mbalimbali. Ofisi hizo hufanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na ofisi ya makao makuu, na utumishi wazo, pamoja na utumizi wa tekinolojia ya kompyuta, hupunguza idadi ya wafanyakazi wa uchoraji-ramani wenye kuhitajiwa kwenye mahali popote pale pa ujenzi.
Baadhi ya miradi, kidogo ni ya ukubwa wa kiasi. Ndivyo ilivyokuwa kuhusu ofisi ya tawi iliyojengwa katika Tahiti katika 1983. Ilitia ndani nafasi ya ofisi, ghala kadhaa, na makao kwa ajili ya wafanyakazi wanane wa kujitolea. Na ndivyo ilivyokuwa pia kuhusu lile jengo la tawi lenye orofa nne lililojengwa kwenye kisiwa cha Karibea cha Martinique wakati wa miaka ya 1982 hadi 1984. Majengo hayo huenda yasionekane kuwa yenye kutokeza kwa wakazi wa majiji makubwa katika nchi nyinginezo, lakini yalivuta uangalifu wa umma. Gazeti France-Antilles lilijulisha kwamba jengo la tawi katika Martinique lilikuwa “ujenzi wa ustadi mkubwa” ulioonyesha “upendo mkubwa wa kazi iliyofanywa vizuri.”
Kwa kutofautisha, kuhusu ukubwa, majengo yaliyokamilishwa katika Kanada katika 1981 yalitia ndani matbaa, au kiwanda, kikiwa na nafasi ya meta za mraba zaidi ya 9,300 na jengo la makazi kwa ajili ya wenye kujitolea 250. Katika Cesario Lange, katika Brazili, majengo mengi ya Watch Tower yaliyokamilishwa mwaka uo huo yalitia ndani majengo manane, yenye nafasi ya sakafu ya meta za mraba 46,000. Yalihitaji malori 10,000 yaliyojaa saruji, mawe, na mchanga, pamoja na vizingiti vyenye mkorogo wa saruji na kokoto vinavyofika mara mbili ya urefu wa Mlima Everest! Katika 1991, matbaa kubwa mpya ilipokamilishwa katika Filipino, ilihitajiwa pia kuandaa jengo la makazi la orofa 11.
Ili kutimiza mahitaji ya idadi yenye kukua ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Nigeria, mradi mkubwa wa ujenzi ulianzishwa katika Igieduma katika 1984. Ungetia ndani kiwanda, jengo la ofisi lenye nafasi kubwa, majengo manne yaliyounganishwa ya makazi, na vifaa vingine. Mipango ilifanywa kwamba kuta za kiwanda zitangulie kufanyizwa kabisa na kusafirishwa kutoka Marekani. Lakini ndugu walikabiliwa na masharti magumu ya kuingiza vitu nchini yaliyoonekana kuwa hayawezekani. Wakati masharti hayo yalipotimizwa na kila kitu kikawasili salama kwenye mahali pa ujenzi, Mashahidi hawakujipa sifa wenyewe bali walimshukuru Yehova kwa baraka yake.
Upanuzi wa Kasi Duniani Pote
Hata hivyo, ukuzi wa kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme umekuwa wa kasi sana hivi kwamba, hata baada ya upanuzi mkubwa wa vifaa vya tawi katika nchi, mara nyingi imekuwa lazima kuanza kujenga tena kwa muda mfupi. Fikiria vielelezo vichache.
Katika Peru tawi jipya zuri—lenye nafasi ya ofisi, vyumba 22 vya kulala pamoja na vifaa vingine vya msingi kwa ajili ya washiriki wa familia ya Betheli, na Jumba la Ufalme moja—vilikamilishwa mwishoni mwa 1984. Lakini itikio kwa ujumbe wa Ufalme katika nchi hiyo ya Amerika Kusini lilikuwa kubwa zaidi ya ilivyotarajiwa. Miaka minne baadaye ilikuwa lazima kurudufisha majengo yaliyokuwako, wakati huu kwa kutumia ubuni unaohimili tetemeko la dunia.
Majengo mapya ya tawi yenye nafasi kubwa yalikamilishwa katika Kolombia katika 1979. Ilionekana kwamba yangeandaa nafasi ya kutosha kwa miaka mingi ijayo. Hata hivyo, katika muda wa miaka saba idadi ya Mashahidi katika Kolombia ilikuwa karibu imerudufika, na sasa tawi lilikuwa likichapa magazeti La Atalaya (Mnara wa Mlinzi) na ¡Despertad! (Amkeni!) si kwa ajili ya Kolombia tu bali pia kwa ajili ya nchi nne jirani. Walilazimika kuanza kujenga tena katika 1987—wakati huu mahali ambapo palikuwa na nafasi zaidi kwa ajili ya upanuzi.
Wakati wa 1980, Mashahidi wa Yehova katika Brazili walitumia saa 14,000,000 hivi kwa kazi ya kuhubiri hadharani ujumbe wa Ufalme. Tarakimu hiyo ilipanda kufikia karibu 50,000,000 katika 1989. Watu wengi zaidi walikuwa wakionyesha tamaa ya kutaka njaa yao ya kiroho itoshelezwe. Yale majengo ya tawi yaliyokuwa yamewekwa wakfu katika 1981 hayakutosha tena. Tayari kufikia Septemba 1988, uchimbuzi kwa ajili ya kiwanda kipya ulikuwa ukiendelea. Hicho kingeandaa asilimia 80 ya nafasi zaidi ya sakafu kuliko iliyokuwako katika kiwanda kilichoko, na bila shaka, makazi ya kutunza familia ya Betheli iliyoongezeka yangehitajiwa pia.
Katika Selters/Taunus, Ujerumani, jengo kubwa la kuchapia la pili kwa ukubwa kati ya viwanda vya kuchapia vya Watch Tower Society liliwekwa wakfu katika 1984. Miaka mitano baadaye, kwa sababu ya maongezeko katika Ujerumani na pia fursa za kupanua kazi ya kutoa ushahidi katika nchi ambazo tawi hilo huchapia fasihi, mipango ilikuwa ikiendelea kuongeza ukubwa wa kiwanda kufikia zaidi ya asilimia 85 na kuongeza vifaa vingine vya utegemezo.
Tawi la Japani lilikuwa limehamia Numazu kutoka Tokyo kwenye makao makubwa mapya katika 1972. Upanuzi zaidi uliokuwa mkubwa ulifanywa katika 1975. Kufikia 1978 mahali pengine palikuwa pamenunuliwa, katika Ebina; na kazi ya kujenga kiwanda kilichozidi ukubwa wa kile kilicho Numazu kwa mara tatu ilianza haraka. Hicho kilikamilishwa katika 1982. Bado hakikutosha; majengo zaidi yaliongezwa kufikia 1989. Je, haingewezekana kujenga mara moja tu na kukifanya kiwe kikubwa vya kutosha? La. Idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika Japani imerudufika tena na tena kwa njia ambayo hakuna mtu angeweza kutazamia. Kuanzia 14,199 katika 1972, idadi yao imepanda hadi 137,941 katika 1989, na walio wengi wao walikuwa katika huduma ya wakati wote.
Kiolezo icho hicho kinaonwa katika sehemu nyingine za dunia. Katika muda wa mwongo mmoja—na nyakati nyingine miaka michache—baada ya kujenga matawi makubwa yenye vifaa vya kuchapia, ilikuwa lazima kuanza upanuzi mkubwa. Ilikuwa hivyo katika Mexico, Kanada, Afrika Kusini, na Jamhuri ya Korea, miongoni mwa mengine.
Ni nani ambao hasa hufanya kazi ya ujenzi? Hiyo hutimizwaje?
Maelfu Mengi Wana Hamu ya Kusaidia
Katika Sweden, kati ya Mashahidi 17,000 katika nchi wakati ule wa ujenzi wa tawi lao katika Arboga, 5,000 hivi walijitolea kusaidia kazi. Wengi walikuwa tu wasaidizi wenye moyo wa kupenda, lakini kulikuwa pia wafanyakazi wenye ustadi wa hali ya juu wa kutosha kuhakikisha kwamba kazi ilifanywa sawasawa. Msukumo wao ni nini? Kumpenda Yehova.
Wakati mkuu kwenye ofisi ya upimaji-ardhi katika Denmark aliposikia kwamba kazi kwenye tawi jipya katika Holbæk ingefanywa na Mashahidi wa Yehova, alionyesha kutia shaka. Hata hivyo, miongoni mwa Mashahidi waliojitolea kusaidia, wote wenye ujuzi uliohitajiwa walipatikana. Hata hivyo, je, ingekuwa afadhali kama wafanyakazi wa mkataba wa kibiashara wangalilipwa wafanye kazi hiyo? Baada ya ujenzi huo kukamilishwa, wastadi kutoka idara ya ujenzi ya mji walizuru makao hayo na kueleza juu ya kazi yenye ustadi iliyofanywa—jambo ambalo wao huliona mara chache sana kwenye kazi zilizofanywa na watu wa kulipwa siku hizi. Kwa habari ya yule mkuu aliyetia shaka mapema kidogo, yeye alitabasamu na kusema: “Angalia, wakati ule sikujua nyinyi watu mna tengenezo la aina gani.”
Miji na majiji katika Australia yametawanyika sehemu zilizo mbali; hivyo, wengi kati ya wale 3,000 waliojitolea kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi katika Ingleburn kati ya 1978 na 1983 walilazimika kusafiri angalau kilometa 1,600. Hata hivyo, safari za basi za vikundi vya wenye kujitolea ziliratibiwa, na makutaniko njiani yalijitolea kutoa milo na ushirika kwa ukaribishaji-wageni kwa ajili ya akina ndugu kwenye vituo vya kupumzikia. Baadhi ya ndugu waliuza makao yao, wakafunga biashara zao, wakachukua likizo, na kutoa dhabihu nyingine ili kushiriki katika ujenzi. Vikundi vya mafundi stadi vilikuja—baadhi yavyo zaidi ya mara moja—kumwaga kokoto, kuangika dari, na kujenga ua. Wengine walitoa upaji wa vifaa vya ujenzi.
Walio wengi kati ya wenye kujitolea kwenye miradi hiyo walikuwa bila ustadi, lakini kwa kuzoezwa kidogo, baadhi yao walitwaa madaraka makubwa wakafanya kazi bora sana. Walijifunza jinsi ya kutengeneza madirisha, kuendesha matrekta, kuchanganya kokoto, na kujenga matufali. Walifurahia mambo yasiyofurahiwa na wasio-Mashahidi wafanyao aina ileile ya kazi ili kulipwa. Kwa njia gani? Wenye ujuzi walikuwa tayari kushiriki maarifa yao. Hapana yeyote aliyehisi kwamba mtu mwingine angechukua kazi yake; kulikuwa kazi nyingi kwa kila mtu kufanya. Na kulikuwa na msukumo wenye nguvu wa kufanya kazi ya hali ya juu, kwa sababu ilifanywa ikiwa wonyesho wa kumpenda Mungu.
Kwenye mahali pa ujenzi, baadhi ya Mashahidi hufanyiza kiini cha “familia” ya ujenzi. Wakati wa kazi katika Selters/Taunus, Ujerumani, tokea 1979 hadi 1984, mamia kadhaa kwa kawaida walifanyiza kiini hicho cha wafanyakazi. Maelfu wengine walijiunga nao kwa vipindi tofauti-tofauti vya wakati, wengi katika miisho-juma. Kulikuwa mpango wa uangalifu hivi kwamba wenye kujitolea walipowasili, walikuwa na kazi tele ya kufanya.
Maadamu watu si wakamilifu, kutakuwako matatizo, lakini wale ambao hufanya kazi kwenye ujenzi huo hujaribu kutatua matatizo kwa msingi wa kanuni za Biblia. Wanajua kwamba kufanya mambo katika njia ya Kikristo ni jambo la maana zaidi ya kuwa na matokeo. Kikiwa kikumbusho, kwenye mahali pa ujenzi katika Ebina, Japani, kulikuwa ishara kubwa zenye picha za wafanyakazi wenye kuvalia kofia ngumu, na juu ya kila kofia ngumu liliandikwa kwa herufi za Kijapani moja la matunda ya roho ya Mungu: upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti. (Gal. 5:22, 23, NW) Wale ambao hutembelea mahali pa kazi wanaweza kuona na kusikia ile tofauti. Akieleza maoni yake mwenyewe, mwandishi mmoja wa habari aliyetembelea mahali pa ujenzi wa tawi katika Brazili alisema hivi: “Hapana machafuko au ukosefu wa ushirikiano . . . Mazingira haya ya Kikristo huifanya iwe tofauti hapa na yale ambayo huonwa kwa kawaida katika ujenzi wa kulipwa katika Brazili.”
Ukuzi Wenye Kuendelea Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu
Wakati matawi ya Watch Tower Society yamekuwa yakikua, imehitajiwa pia kupanua vifaa vya makao makuu ya ulimwengu. Kumekuwa maongezeko makubwa kwenye makao ya kiwanda na ofisi zayo katika Brooklyn na katika mahali pengine katika Jimbo la New York zaidi ya mara kumi tangu Vita ya Ulimwengu 2. Ili kuwapa makao wafanyakazi, imekuwa lazima kujenga au kununua na kurekebisha majengo mengi, makubwa na madogo pia. Upanuzi mwingine mkubwa katika Brooklyn ulitangazwa katika Agosti 1990 na katika Januari 1991—hata ingawa kaskazini mwa New York City ujenzi mkubwa ulioanza katika 1989 ulikuwa ukiendelea kwenye Kitovu cha Elimu cha Watchtower, ambacho kilikusudiwa kuwapa makao watu 1,200, kutia na wafanyakazi na wanafunzi.
Tangu 1972, kazi ya ujenzi haijaacha kufanywa kwenye makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn na vifaa vyayo vinavyohusiana karibukaribu katika sehemu nyingine za New York na katika New Jersey. Baada ya muda, ilipata kuwa wazi kwamba hata ingawa idadi yao ilifikia mamia, wafanyakazi wa ujenzi wa kawaida walishindwa kuiweza kazi. Kwa hiyo, katika 1984 programu yenye kuendelea ya wafanyakazi wa muda ilianzishwa. Barua zilipelekwa kwa yale ambayo wakati huo yalikuwa makutaniko 8,000 katika Marekani kualika ndugu wenye kustahili waje wasaidie kwa juma moja au zaidi. (Programu kama hiyo ilikuwa tayari imefanya kazi vizuri katika baadhi ya yale matawi, kutia na Australia, ambako wale walioweza kukaa majuma mawili walialikwa wajitolee.) Wafanyakazi wangepewa makao na chakula lakini wangelipia gharama zao za usafiri na hawangepokea mishahara. Ni nani wangeitikia?
Kufikia 1992, maombi zaidi ya 24,000 yalikuwa yameshughulikiwa! Angalau 3,900 kati ya hawa walikuwa watu waliokuwa wakirudi kwa mara ya 2, ya 3, hata ya 10 au ya 20. Walio wengi wao walikuwa wazee, watumishi wa huduma, au mapainia—watu binafsi wenye sifa nzuri za kiroho. Wote walikuwa wakijitolea kufanya lolote lililohitajiwa, iwe hiyo iliwataka watumie ufundi wao au la. Mara nyingi kazi ilikuwa nzito na chafu. Lakini walilihesabu kuwa pendeleo kuchanga katika njia hiyo kusogeza mbele masilahi ya Ufalme. Baadhi yao walihisi hiyo iliwasaidia kuthamini vizuri zaidi ile roho ya kujidhabihu inayoonyesha aina ya kazi ifanywayo kwenye makao makuu ya ulimwengu. Wote walihisi kuwa walithawabishwa sana kwa sababu ya kuwapo kwa ajili ya programu ya familia ya Betheli ya ibada ya asubuhi na funzo la Mnara wa Mlinzi la familia lifanywalo kila juma.
Wenye Kujitolea wa Kimataifa
Kadiri uhitaji wa upanuzi wa kasi ulivyokua, mpango wa wenye kujitolea wa kimataifa ulianzishwa katika 1985. Hiyo kwa vyovyote haikuwa ndiyo mara ya kwanza kuwa na ushirikiano wa kimataifa katika ujenzi, lakini sasa mpango huo uliratibiwa kwa uangalifu kutoka makao makuu. Wote ambao hushiriki ni Mashahidi ambao hujitolea kusaidia kazi ya ujenzi nje ya nchi zao wenyewe. Wao ni wafanyakazi stadi, pamoja na wenzi wa ndoa ambao huenda pamoja na waume zao kusaidia kwa njia yoyote wawezayo. Walio wengi wao hulipia nauli zao wenyewe; hakuna wanaopewa mshahara kwa ajili ya kile wafanyacho. Baadhi yao huenda kwa muda mfupi, kwa kawaida wakikaa kuanzia majuma mawili hadi miezi mitatu. Wengine ni wenye kujitolea wa muda mrefu, wakikaa kwa mwaka au zaidi, labda mpaka ujenzi unapokamilika. Mashahidi wa Yehova zaidi ya 3,000 kutoka nchi mbalimbali 30 walishiriki sehemu katika kazi hiyo wakati wa miaka mitano ya kwanza, na wengi zaidi walikuwa na hamu ya kushiriki kadiri stadi zao zilivyohitajiwa. Wao hulihesabu kuwa pendeleo kujitoa wenyewe na mali zao ili kusogeza mbele masilahi ya Ufalme wa Mungu kwa njia hiyo.
Wafanyakazi wa kujitolea wa kimataifa huandaliwa makao na milo. Mara nyingi starehe ni ndogo kabisa. Mashahidi wenyeji huthamini sana yale yanayofanywa na ndugu zao wenye kuzuru, na inapowezekana, wao huwakaribisha nyumbani mwao, hata iwe sahili namna gani. Mara nyingi sana milo huliwa kwenye mahali pa kazi.
Ndugu wa kutoka ng’ambo hawawi hapo ili kufanya kazi yote. Lengo lao ni kufanya kazi pamoja na kikundi cha ujenzi cha wenyeji. Na mamia, hata maelfu, ya wengine katika nchi huenda pia wakaja kusaidia wakati wa miisho-juma au kwa juma moja au zaidi kwa wakati mmoja. Katika Argentina, wenye kujitolea 259 kutoka nchi nyingine walifanya kazi pamoja na maelfu kadhaa ya ndugu wenyeji, baadhi yao walikuwapo kwa ajili ya kazi kila siku, wengine kwa majuma machache, na wengine zaidi wakati wa miisho-juma. Katika Kolombia, wenye kujitolea wa kimataifa zaidi ya 830 walisaidia kwa vipindi mbalimbali vya wakati. Kulikuwa pia wenye kujitolea wenyeji zaidi ya 200 walioshiriki katika mradi huo kwa wakati wote, na wasaidizi wengine 250 au zaidi kila mwisho-juma. Jumla ya zaidi ya watu mmoja-mmoja tofauti 3,600 walishiriki.
Tofauti ya lugha yaweza kutokeza matatizo, lakini haizuii vikundi vya kimataifa visifanye kazi pamoja. Lugha ya ishara, ishara za uso, ucheshi, na tamaa ya kuona kazi itakayomheshimu Yehova ikikamilishwa husaidia kazi ifanywe.
Ukuzi wa tengenezo wenye kutokeza—ukitokeza uhitaji wa makao makubwa ya tawi—nyakati nyingine hutokea katika nchi ambako idadi ya watu wenye stadi katika ufundi wa ujenzi ni ndogo. Lakini hicho si kizuizi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, ambao husaidiana kwa furaha. Wao hufanya kazi pamoja wakiwa sehemu ya familia ya duniani pote ambayo haigawanywi na taifa, rangi ya ngozi, au lugha.
Katika Papua New Guinea, wenye kujitolea waliotoka Australia na New Zealand kila mmoja alizoeza raia wa Papua New Guinea kazi yake ya kiufundi, kupatana na ombi la Idara ya Wafanyakazi ya Serikali. Katika njia hiyo, huku wakijitoa wenyewe, Mashahidi wenyeji walijifunza kazi za ufundi ambazo zingeweza kuwasaidia kutosheleza mahitaji yao wenyewe na ya familia zao.
Wakati tawi jipya lilipohitajiwa katika El Salvador, wenye kujitolea 326 kutoka ng’ambo walijiunga na ndugu wenyeji. Kwa ajili ya mradi wa ujenzi katika Ekuado, Mashahidi 270 kutoka nchi 14 walifanya kazi pamoja na ndugu na dada Waekuado. Baadhi ya wenye kujitolea wa kimataifa walisaidia katika miradi kadhaa ya ujenzi iliyokuwa ikiendelea wakati uleule mmoja. Walifanya kazi kwa zamu katika mahali pa ujenzi katika Ulaya na Afrika, kulingana na uhitaji wa stadi zao za kiufundi.
Kufikia 1992, wenye kujitolea wa kimataifa walikuwa wamepelekwa sehemu 49 za matawi ili kusaidia vikundi vya ujenzi vya wenyeji. Katika visa fulani wale waliopokea msaada kutokana na programu hii waliweza pia kuandaa usaidizi kwa wengine. Hivyo, wakiwa wamenufaika na kazi za bidii za watumishi wa muda mrefu wa kimataifa kama 60 waliosaidia na ujenzi wa mradi wa tawi katika Filipino, pamoja na wenye kujitolea zaidi ya 230 kutoka ng’ambo waliosaidia kwa vipindi vifupi zaidi, baadhi ya Wafilipino walijitoa wenyewe ili kusaidia kujenga vifaa katika sehemu nyingine za Kusini-Mashariki mwa Asia.
Kazi ya ujenzi inafanywa na Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya mahitaji yaliyoko sasa kuhusiana na kazi ya kuhubiri habari njema. Kwa msaada wa roho ya Yehova, wanataka kutoa ushahidi ulio mkubwa zaidi iwezekanavyo katika pindi ya wakati unaobaki kabla ya Har–Magedoni. Wanasadiki kwamba ulimwengu mpya wa Mungu u karibu sana, na wana imani kwamba wataokoka wakiwa watu waliofanywa tengenezo waingie katika huo ulimwengu mpya, chini ya utawala wa Ufalme wa Kimesiya wa Mungu. Pia ni tumaini lao kwamba labda vingi kati ya vifaa vizuri ambavyo wamejenga na kuviweka wakfu kwa Yehova vitaendelea kutumiwa baada ya Har–Magedoni vikiwa vitovu vya kueneza ujuzi wa yule Mungu wa kweli peke yake mpaka ujuzi huo ujaze dunia kwelikweli.—Isa. 11:9.
[Maelezo ya Chini]
a Liliitwa Kanisa la “Nuru Mpya” kwa sababu wale walioshirikiana humo walihisi kwamba kama tokeo la kusoma vichapo vya Watch Tower, walikuwa na nuru mpya ya uelewevu juu ya Biblia.
[Blabu katika ukurasa wa 322]
Mashahidi kutoka makutaniko ya karibu walisaidia kazi
[Blabu katika ukurasa wa 323]
Kazi ya ujenzi ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa
[Blabu katika ukurasa wa 324]
Mkazo ulitiwa juu ya sifa za kiroho
[Blabu katika ukurasa wa 326]
Ujenzi bora, usalama, gharama ndogo sana, uharaka
[Blabu katika ukurasa wa 328]
Jumba la Kusanyiko lenye kubebeka!
[Blabu katika ukurasa wa 331]
Kwenda mahakamani
[Blabu katika ukurasa wa 332]
Upanuzi wa kimataifa wa kadiri kubwa
[Blabu katika ukurasa wa 333]
Wafanyakazi walitoa sifa kwa Yehova, si kwao wenyewe
[Blabu katika ukurasa wa 334]
Ukuzi kwa kadiri ambayo hakuna binadamu angeweza kubashiri
[Blabu katika ukurasa wa 336]
Walikuhesabu kuwa pendeleo kusaidia kujenga kwenye makao makuu
[Blabu katika ukurasa wa 339]
Wao hufanya kazi wakiwa familia ya duniani pote, ambayo haigawanywi na taifa, rangi ya ngozi, au lugha
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 320, 321]
Kufanya Kazi Pamoja ili Kujenga Haraka Majumba ya Ufalme
Maelfu ya makutaniko mapya huundwa kila mwaka. Katika visa vingi, Majumba ya Ufalme mapya hujengwa na Mashahidi wenyewe. Picha hizi zilipigwa wakati wa ujenzi wa Jumba la Ufalme katika Connecticut, Marekani, katika 1991
Ijumaa, saa 1:40 asubuhi
Ijumaa, saa 6 adhuhuri
Jumamosi, saa 1:41 jioni
Kazi kubwa yakamilika, Jumapili, saa 12:10 jioni
Wamtegemea Yehova kwa baraka yake, na huchukua wakati kuzungumzia shauri kutoka Neno lake
Wote ni wenye kujitolea wasiolipwa, wenye furaha kufanya kazi mmoja kando ya mwenzake
[Picha katika ukurasa wa 327]
Majumba ya Ufalme Katika Nchi Mbalimbali
Mahali pa mikutano patumiwapo na Mashahidi wa Yehova kwa kawaida huwa penye kiasi. Ni safi, penye starehe, katika mazingira yenye kuvutia
Peru
Filipino
Ufaransa
Jamhuri ya Korea
Japani
Papua New Guinea
Ireland
Kolombia
Norway
Lesotho
[Picha katika ukurasa wa 330]
Majumba ya Kusanyiko ya Mashahidi wa Yehova
Ili kuwa na mahali pa makusanyiko yao ya pindi kwa pindi, Mashahidi wa Yehova katika baadhi ya maeneo wameona kuwa jambo lenye kufaa kujenga Majumba ya Kusanyiko yao wenyewe. Kazi iliyo nyingi hufanywa na Mashahidi wenyeji. Hapa pana machache tu ya majumba hayo yaliyokuwa yakitumiwa katika miaka ya mapema ya 1990
Uingereza
Venezuela
Italia
Ujerumani
Kanada
Japani
[Picha katika ukurasa wa 338]
Programu ya Ujenzi wa Kimataifa Hutimiza Mahitaji ya Haraka
Ukuzi wa kasi wa tengenezo umetaka upanuzi wenye kuendelea wa ofisi, viwanda, na makao ya Betheli duniani pote
Wenye kujitolea wa kimataifa hutoa usaidizi kwa Mashahidi wenyeji
Hispania
Njia za ujenzi zitumiwazo hufanya wenye kujitolea wengi wasiokuwa na ujuzi waweze kufanya kazi yenye thamani
Puerto Riko
Wafanyakazi stadi hutoa huduma zao kwa furaha
New Zealand
Ugiriki
Brazili
Matumizi ya vifaa vyenye kudumu husaidia kupunguza gharama za muda mrefu za udumishaji
Uingereza
Kazi bora sana hutokana na kupendezwa kwa binafsi kwa upande wa wenye kuifanya; hiyo ni wonyesho wa upendo wao kwa Yehova
Kanada
Ujenzi huo mbalimbali ni pindi za shangwe; urafiki mwingi wenye kudumu hufanyizwa
Kolombia
Ishara katika Japani zilikumbusha wafanyakazi juu ya hatua za usalama, pia juu ya uhitaji wa kuonyesha matunda ya roho ya Mungu
[Picha katika ukurasa wa 318]
Jengo la kwanza lililoitwa Jumba la Ufalme, katika Hawaii
[Picha katika ukurasa wa 319]
Majumba ya Ufalme mengi ya mapema yalikuwa majengo yaliyokodiwa au yalikuwa vyumba tu vilivyokuwa juu ya maduka; machache yalijengwa na Mashahidi
[Picha katika ukurasa wa 329]
Mawili ya Majumba ya Kusanyiko ya kwanza
New York City
Guadeloupe
[Picha katika ukurasa wa 337]
Wafanyakazi wa muda wa ujenzi waliotoka tu kuwasili kwenye makao makuu katika New York
Kila kikundi hukumbushwa kwamba kuwa mtu wa kiroho na kufanya kazi bora hutangulizwa juu ya kufanya kazi haraka