Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 21 kur. 340-351
  • Yote Hayo Hugharimiwaje?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yote Hayo Hugharimiwaje?
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio”
  • Hutegemezwa kwa Upaji wa Kujitolea
  • Kugharimia Mahalimahali pa Mikutano pa Kwetu
  • Kushughulikia Upanuzi wa Makao Makuu ya Ulimwengu
  • Kugharimia Upanuzi wa Vifaa vya Tawi
  • Je, Kuna Faida Kutokana na Fasihi?
  • Hawatumikii kwa Ajili ya Pato la Kibinafsi
  • Jinsi Kazi za Ufalme Zinavyogharimiwa
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Jinsi Yehova Anafanikisha Kazi Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Hizo Pesa Hutoka Wapi?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 21 kur. 340-351

Sura ya 21

Yote Hayo Hugharimiwaje?

NI WAZI kwamba kazi inayoendeshwa na Mashahidi wa Yehova hutaka fedha. Kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, ofisi za tawi, viwanda, na makao ya Betheli huhusisha fedha, na fedha zaidi huhitajiwa ili kuyadumisha. Inagharimu pia kutangaza na kugawanya fasihi kwa ajili ya funzo la Biblia. Yote hayo hugharimiwaje?

Mawazo yasiyo na msingi kuhusu jambo hilo yameenezwa hadharani na watu wapingao kazi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini mambo ya hakika yanaunga mkono jibu walitoalo Mashahidi wenyewe. Ni jipi hilo? Kazi nyingi hufanywa na watu wenye kujitolea, ambao hawatarajii na hawataki kulipwa fedha kwa ajili ya utumishi wao mbalimbali, na gharama za kitengenezo hulipiwa kwa upaji wa hiari.

“Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio”

Mapema sana kama toleo la pili la Watch Tower, katika Agosti 1879, Ndugu Russell alitaarifu hivi: “Twaamini ‘Zion’s Watch Tower’ lina YEHOVA akiwa mtegemezaji walo, na inapokuwa hivyo halitaombaomba wala kusihi wanadamu walitegemeze. Wakati Yeye asemaye: ‘Dhahabu na fedha zote za milimani ni zangu,’ ashindwapo kuandaa fedha zihitajiwazo, sisi tutaelewa kwamba ni wakati wa kuacha kuchapa.” Kupatana na hilo, fasihi za Mashahidi wa Yehova haziombiombi fedha.

Kama ilivyo kwa fasihi zao ndivyo ilivyo kwa habari ya mikutano yao. Hakuna maombi ya kuchochea hisiamoyo ili kupata fedha katika mikutano yao au kwenye mikusanyiko yao. Hakuna visahani vya michango ambavyo hupitishwa; hakuna bahasha ambazo hugawanywa za kuweka fedha; hakuna barua za kuombaomba fedha ambazo hupelekwa kwa washiriki wa makutaniko. Makutaniko hayachezi kamari au kushindania zawadi ili kupata fedha. Mapema sana kama 1894, wakati Watch Tower Society ilipotuma wasemaji wasafirio, ilitoa tangazo hili kwa manufaa ya kila mtu: “Na ieleweke tokea mwanzo kwamba kukusanya michango au njia nyinginezo za kuombaomba fedha hazikubaliwi wala kukubaliwa na Sosaiti hii.”

Hivyo, tangu mapema sana katika historia yao ya kisasa, vikaratasi vya mwaliko na mialiko mingineyo inayochapwa kwa ajili ya umma ili kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova huwa na shime “Viti Ni vya Bure. Hakuna Viingilio.”

Kuanzia mapema katika 1914, Wanafunzi wa Biblia walikodi majumba ya maonyesho pamoja na majumba mengine ya mikutano na kualika umma ili waje kuona “Photo-Drama of Creation.” Huo ulikuwa utoaji wenye sehemu nne, saa nane kwa ujumla, uliofanyizwa kwa slaidi na sinema zilizoambatanishwa na sauti. Wakati wa mwaka wa kwanza pekee, mamilioni ya watu waliuona katika Amerika Kaskazini, Ulaya, Australia, na New Zealand. Ijapokuwa baadhi ya wenyeji wa majumba ya maonyesho walitoza fedha kwa ajili ya viti vilivyohifadhiwa, Wanafunzi wa Biblia hawakuomba kamwe fedha kwa wenye kuingia ili kutazama. Na hakuna michango iliyokusanywa.

Baadaye, kwa miaka zaidi ya 30, Watch Tower Society iliendesha kituo cha redio WBBR katika New York City. Mashahidi wa Yehova walitumia pia utumishi mbalimbali wa mamia ya vituo vingine ili kutangaza programu za elimu ya Biblia. Lakini hawakutumia kamwe vituo kama hivyo ili kuombaomba fedha.

Basi, ule upaji ambao hugharimia utendaji wao hupatikanaje?

Hutegemezwa kwa Upaji wa Kujitolea

Biblia huweka kigezo. Chini ya Sheria ya Musa, kulikuwa michango fulani iliyotolewa kwa hiari. Mingine watu walitakwa waitoe. Kutoa zaka, au sehemu ya kumi, kulikuwa mojayapo michango ya lazima. (Kut. 25:2; 30:11-16; Hes. 15:17-21; 18:25-32) Lakini Biblia huonyesha pia kwamba Kristo alitimiza ile Sheria, naye Mungu akaikomesha; hivyo Wakristo hawafungwi tena na amri zayo. Wao hawatoi sehemu ya kumi, wala hawako chini ya wajibu wa kutoa michango mingine yoyote ya kiasi hususa au kwa wakati hususa.—Mt. 5:17; Rum. 7:6; Kol. 2:13, 14.

Badala ya hivyo, wao hutiwa moyo wasitawishe roho ya ukarimu na upaji wa hiari kwa kuiga kielelezo kizuri ajabu kilichowekwa na Yehova mwenyewe na Mwana wake, Yesu Kristo. (2 Kor. 8:7, 9; 9:8-15; 1 Yoh. 3:16-18) Hivyo, kwa habari ya kutoa, mtume Paulo aliandikia kutaniko la Kikristo katika Korintho hivi: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” Walipojulishwa juu ya uhitaji fulani, jambo hilo liliwapa ‘jaribu la unyofu wa upendo wao,’ kama vile Paulo alivyoeleza. Yeye alisema pia: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”—2 Kor. 8:8, 12; 9:7, NW.

Kwa kufikiria hayo, maelezo yaliyotolewa na Tertuliano kuhusu mikutano iliyofanywa na watu waliojitahidi kuzoea Ukristo katika siku zake (karibu 155–baada ya 220 W.K.) lapendeza. Yeye aliandika hivi: “Hata ingawa kuna kisanduku cha aina fulani, hakikufanyizwa kwa fedha zilizolipwa zikiwa viingilio, kana kwamba dini ilikuwa jambo la mkataba. Mara moja kwa mwezi kila mtu huleta sarafu ndogo—au wakati wowote atakapo, na ikiwa tu ataka, na ikiwa aweza; maana hapana mtu alazimishwaye; ni toleo la hiari.” (Apology, 39, 5) Hata hivyo, wakati wa karne nyingi tangu hapo, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamejitia katika kila aina ya mbinu ya kujipatia fedha ili kugharimia shughuli zayo.

Charles Taze Russell alikataa kuiga makanisa. Yeye aliandika hivi: “Ni maoni yetu kwamba fedha zinazopatikana kwa zile mbinu mbalimbali za kuombaomba katika jina la Bwana wetu ni zenye kumchukiza, hazikubaliki kwake, nazo hazileti baraka yake ama juu ya wapaji ama juu ya kazi itimizwayo.”

Badala ya kujaribu kupata upendeleo wa wale waliokuwa na mali, Ndugu Russell alitaarifu waziwazi, kupatana na Maandiko, kwamba wengi wa watu wa Bwana wangekuwa maskini katika mali za ulimwengu huu lakini tajiri katika imani. (Mt. 19:23, 24; 1 Kor. 1:26-29; Yak. 2:5) Badala ya kukazia uhitaji wa fedha ili kueneza kweli ya Biblia, yeye alikazia fikira umaana wa kusitawisha roho ya upendo, tamaa ya kutoa, na tamaa ya kusaidia wengine, hasa kwa kushiriki kweli pamoja nao. Kwa wale waliokuwa na uwezo wa kuchuma fedha na ambao walidokeza kwamba kwa kujitoa wenyewe sana kwa mambo ya kibiashara wangekuwa na vingi zaidi vya kuchanga kifedha, yeye alisema kwamba ingekuwa afadhali wapunguze utendaji huo na kujitoa wenyewe na wakati wao katika kueneza kweli. Huo ungali ndio msimamo uchukuliwao na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.a

Kihalisi, watu hutoa kiasi gani? Yale wanayofanya ni uamuzi wao binafsi. Hata hivyo, kwa habari ya kutoa, yapasa kuangaliwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawafikiri tu juu ya kutoa mali za kimwili. Kwenye mikusanyiko yao ya wilaya katika 1985-1986, walizungumza juu ya kichwa cha habari “Kumheshimu Yehova kwa Vitu Vyetu vya Thamani.” (Mit. 3:9) Ilikaziwa kwamba vitu hivyo vya thamani hutia ndani si mali za kimwili tu bali pia nguvu zetu za kimwili, za kiakili, na za kiroho.

Huko nyuma katika 1904, Ndugu Russell alitaja kwamba mtu ambaye amejitakasa kabisa (au, kujiweka wakfu, kama tusemavyo sasa) kwa Mungu “amekwisha toa vyote alivyo navyo kwa Bwana.” Hivyo, apaswa sasa “kujifikiria mwenyewe kuwa amewekwa na Bwana kuwa msimamizi wa wakati wake mwenyewe, uvutano, fedha, n.k., na kila mmoja atatafuta kutumia talanta hizo kwa kadiri awezavyo, kwa utukufu wa Bwana-Mkubwa.” Yeye aliongeza kwamba, kwa kuongozwa na hekima kutoka juu, “kwa kadiri upendo na bidii yake vinavyokua kwa ajili ya Bwana siku kwa siku kupitia ujuzi wa Kweli na kupata roho yayo, atajikuta akitoa wakati zaidi na zaidi, na uvutano wake zaidi na zaidi, na mali alizo nazo zaidi na zaidi, kwa ajili ya utumishi wa Kweli.”—Studies in the Scriptures, “The New Creation,” kur. 344-345.

Wakati wa miaka hiyo ya mapema, Watch Tower Society ilikuwa na ile iliyoitwa Hazina ya Tower Tract. Hiyo ilikuwa nini? Habari hii yenye kupendeza iliandikwa upande wa nyuma wa karatasi na bahasha zilizotumiwa nyakati nyingine na Ndugu Russell: “Hazina hii huwa na matoleo ya hiari ya wale ambao wamelishwa na kuimarishwa na ‘nyama kwa wakati wake’ ambayo vichapo vilivyo juu [vitolewavyo na Watch Tower Society], vikiwa vyombo vya Mungu, vinatolea sasa watakatifu waliojitakasa, ulimwenguni pote.

“Hazina hii hutumiwa daima katika kupeleka nje, bila malipo, maelfu ya nakala za ZION’S WATCH TOWER na OLD THEOLOGY TRACTS ziwafaazo sana wasomaji wapya. Husaidia pia katika kueneza vitabu vilivyojalidiwa kwa karatasi vya mfululizo wa DAWN, kwa kusaidia wale walio tayari kuzieneza—makolpota na wengine. Pia huandalia ‘hazina ya maskini’ ambayo yeyote wa watoto wa Bwana ambaye, kwa sababu ya uzee, au ugonjwa, au kwa sababu nyingine, hawawezi kuandikisha WATCH TOWER wanapewa ugavi bila malipo, kwa sharti la kwamba wapeleka barua au kadi mwanzoni mwa kila mwaka, wakitaarifu tamaa na kutoweza kwao.

“Hapana mtu aulizwaye wakati wowote achangie hazina hii: upaji wote lazima uwe wa hiari. Sisi hukumbusha wasomaji wetu maneno ya Mtume (1 Kor. 16:1, 2) na huyathibitisha kwa kusema kwamba wale wanaoweza kutoa na wanaotoa ili kueneza kweli hakika watalipwa kwa mapendeleo ya kiroho.”

Utendaji wa duniani pote wa Mashahidi wa Yehova katika kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu huendelea kutegemezwa kwa upaji wa hiari. Kuongezea Mashahidi wenyewe, watu wengi wenye kupendezwa wenye uthamini hulihesabu kuwa pendeleo kutegemeza kazi ya Kikristo kwa michango yao ya kutoa kwa hiari.

Kugharimia Mahalimahali pa Mikutano pa Kwetu

Kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova lina visanduku vya mchango vifaavyo mahali ambapo watu waweza kuweka upaji wowote watakao—wapendapo kufanya hivyo na ikiwa wanaweza. Hushughulikiwa kwa njia ya faragha hivi kwamba kwa kawaida wengine huwa hawajui kiasi ambacho mtu anatoa. Ni jambo ambalo ni yeye na Mungu tu hujua.

Hakuna mishahara ya kulipwa, lakini inagharimu fedha kudumisha mahali pa mikutano. Ili kutimiza uhitaji huo, washiriki wa kutaniko lazima waarifiwe. Hata hivyo, zaidi ya miaka 70 iliyopita, The Watch Tower lilijulisha wazi kwamba kwa habari ya michango, hakupasi kuwe na kusihisihi au kuhimiza—ni taarifa tu iliyo wazi, ya unyoofu juu ya mambo ya hakika. Kupatana na maoni hayo, mikutano ya kutaniko haitii ndani mazungumzo ya mara kwa mara ya mambo ya kifedha.

Hata hivyo, nyakati nyingine, kunakuwa na mahitaji ya pekee. Huenda ikawa kwamba mipango inafanywa ya kurekebisha upya au kuongeza ukubwa wa Jumba la Ufalme au labda kujenga jipya. Ili kuhakikisha ni kiasi gani cha fedha kitakachopatikana, wazee waweza kuuliza wale walio kutanikoni waandike juu ya vikaratasi kiasi wanachotarajia kuchangia mradi huo au, ikiwezekana, kufanya kipatikane kwa miaka kadhaa. Kwa kuongezea, wazee waweza kuuliza kwamba watu mmoja-mmoja au familia waandike kwenye vikaratasi kiasi wanachohisi wataweza kuchanga kila juma au kila mwezi, kwa baraka za Yehova. Hakuna majina yanayoandikwa. Hivi si hati za kuahidi kulipa, bali huandaa msingi wa kupanga mambo kwa njia yenye akili.—Luka 14:28-30.

Katika Tarma, Liberia, kutaniko lilipata fedha lilizohitaji kwa njia iliyo tofauti kidogo. Wengine kutanikoni walikuza mpunga kwa ajili ya Shahidi mmoja katika shamba lake huku yeye akijitoa kwa mwaka mzima kwa kazi ya kukata miti na kupasua mbao, ambazo ziliuzwa ili kupata fedha kwa ajili ya mradi wa ujenzi. Katika Paramaribo, Suriname, ijapokuwa vifaa vilihitaji kununuliwa, kutaniko halikuhitaji fedha ili kununua ardhi kwa sababu Shahidi mmoja alichanga ardhi yake kwa ajili ya Jumba la Ufalme, akaomba tu kwamba nyumba yake ihamishiwe nyuma ya kiwanja. Bei kubwa mno ya shamba na nyumba katika Tokyo, Japani, ilifanya iwe vigumu kwa makutaniko ya huko kupata ardhi ya kujengea Majumba ya Ufalme. Ili kusaidia kutatua tatizo hilo, familia kadhaa zilitoa matumizi ya ardhi ambayo juu yayo makao yao wenyewe yalijengwa. Waliomba tu kwamba baada ya Jumba la Ufalme jipya kujengwa mahali makao yao yalipokuwa, waandaliwe chumba juu ya jumba.

Kadiri makutaniko yalivyokua na kugawanywa, wale waliokuwa katika eneo lolote lile walijaribu kusaidiana ili kuandaa Majumba ya Ufalme yafaayo. Ijapokuwa hiyo roho ya ukarimu, jambo jingine lilihitajiwa. Bei za viwanja na gharama za ujenzi ziliongezeka sana, na mara nyingi makutaniko moja moja yaliliona kuwa jambo lisilowezekana kulipa gharama hizo. Ni jambo gani lingeweza kufanywa?

Kwenye “Umoja wa Ufalme” Mikusanyiko ya Wilaya katika 1983, Baraza Linaloongoza lilieleza mpango uliotaka kutumiwa kwa kanuni iliyoandikwa kwenye 2 Wakorintho 8:14, 15 (NW), ambayo hutia moyo kuruhusu ziada ya wale waliyo nayo isawazishe upungufu wa wale wengine ili “usawazisho upate kutukia.” Hivyo wale walio na vichache hawatakuwa na vichache mno hivi kwamba wazuiwe katika jitihada za kumtumikia Yehova.

Kila kutaniko lilialikwa kupanga kuwe na kisanduku kilichoandikwa “Michango kwa Ajili ya Hazina ya Sosaiti ya Jumba la Ufalme.” Kila kitu kilichotiwa humo kingetumiwa kwa kusudi hilo tu. Hivyo, fedha zilizochangwa kotekote nchini zingetumiwa kusawazisha upungufu wa makutaniko yaliyohitaji sana Jumba la Ufalme lakini ambayo hayangeweza kupanga kuwa nalo kwa sababu ya masharti yaliyowekwa na benki za mahali. Baada ya uchunguzi wa uangalifu ili kuhakikisha ni wapi uhitaji ulikokuwa mkubwa kwelikweli, Sosaiti ilianza kufanya fedha hizo zipatikane ili kuwezesha makutaniko yajenge au yajipatie Majumba ya Ufalme mapya. Kadiri michango zaidi ilivyopokewa na (katika nchi ambako ingeweza kufanywa) mikopo ikalipwa, bado makutaniko zaidi yangeweza kusaidiwa.

Mpango huo ulianza kutumiwa kwanza katika Marekani na Kanada, na tangu hapo umeenea kwenye zaidi ya nchi 30 katika Ulaya, Afrika, Amerika ya Latin, na Mashariki ya Mbali. Kufikia 1992, katika nane tu kati ya nchi hizo, fedha zilikuwa zimekwisha tolewa kusaidia kuandaa Majumba ya Ufalme 2,737, yakitumiwa na makutaniko 3,840.

Hata katika nchi ambako mpango huo haukuwa ukitenda, lakini ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme ambayo hayangeweza kugharimiwa na wenyeji, Baraza Linaloongoza lilijitahidi kufanya mipango mingine ili kuhakikisha kwamba msaada uliandaliwa. Hivyo usawaziko ulitukia, hivi kwamba wale waliokuwa na vichache hawakuwa na vichache mno.

Kushughulikia Upanuzi wa Makao Makuu ya Ulimwengu

Uendeshaji wa makao makuu ya ulimwengu umehitaji fedha pia. Kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, wakati Watch Tower Bible and Tract Society ilipoliona kuwa jambo lenye kunufaisha kuchapa na kujalidi vitabu vyayo yenyewe, mpango ulifanywa ambao kwao mashine zilizohitajiwa zilinunuliwa kwa majina ya watu binafsi—watumishi wenzi wa Yehova. Badala ya kulipa faida kwa kampuni za kibiashara kwa kutengeneza vitabu, Sosaiti ilitumia kiasi hicho kila mwezi ili kupunguza deni la vifaa. Kadiri manufaa za kufanya hivyo zilivyopatikana, bei ya fasihi kwa umma ilipunguzwa kwa karibu nusu. Jambo lililokuwa likifanywa lilikuwa kusongeza mbele kazi ya kuhubiri habari njema, si kutajirisha Watch Tower Society.

Katika muda wa miaka michache, ilikuwa wazi kwamba vifaa vikubwa zaidi vilihitajiwa kwenye makao makuu ya ulimwengu ili kushughulikia kazi ya duniani pote ya kuhubiri Ufalme. Tena na tena, kadiri ambavyo tengenezo limekua na utendaji wa kuhubiri umeongezwa, imekuwa lazima kuongeza vifaa hivyo. Badala ya kuendea mabenki kupata fedha zilizohitajiwa ili kuongeza na kuzipa vifaa ofisi na viwanda vya makao makuu pamoja na vifaa vya ziada katika New York na viunga vyalo, Sosaiti imeeleza akina ndugu uhitaji huo. Jambo hilo limefanywa, si mara nyingi, bali mara 12 kwa kipindi cha miaka 65.

Hakujapata kamwe kuwa na kuombaomba. Wowote waliotaka kutoa upaji walialikwa kufanya hivyo. Wale waliochagua kutoa fedha walihakikishiwa kwamba kukitokea uhitaji usiotazamiwa na wa haraka, mkopo wao ungelipwa ombi lao lipokewapo. Hivyo katika kushughulikia mambo, Sosaiti ilijitahidi kuepuka kusababisha magumu kwa watu mmoja-mmoja na kwa makutaniko ambayo yalitoa fedha kwa fadhili. Utegemezo uliotolewa na Mashahidi wa Yehova kwa njia ya michango yao umewezesha Sosaiti kulipa mikopo yote sikuzote. Michango hiyo iliyopelekwa kwa Sosaiti haipokewi bila shukrani. Kwa kadiri iwezekanavyo, hiyo hushukuriwa kwa njia ya barua na taarifa nyinginezo za uthamini.

Kazi ya tengenezo haitegemezwi kwa upaji wa kikundi cha wapaji matajiri. Michango mingi hutoka kwa watu mmoja-mmoja ambao wana mali kidogo tu—wengi wao, wakiwa na mali kidogo sana za ulimwengu huu. Wanaotiwa ndani ni watoto wachanga ambao hutaka kushiriki kwa njia hiyo katika kuunga mkono kazi ya Ufalme. Mioyo ya wapaji hao wote husukumwa na uthamini mwingi wa wema wa Yehova na tamaa ya kusaidia wengine wajifunze juu ya maandalizi yake yenye neema.—Linganisha Marko 12:42-44.

Kugharimia Upanuzi wa Vifaa vya Tawi

Kwa kuwa kazi ya kuhubiri Ufalme imeongezeka zaidi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu, imehitajika kuongeza ukubwa wa vifaa vya tawi vya tengenezo. Hiyo hufanywa chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza.

Hivyo, baada ya kupitia mapendekezo kutoka tawi la Ujerumani, mielekezo ilitolewa katika 1978 ya kupata ardhi ifaayo, kisha kujenga majengo makubwa mapya kabisa. Je, Mashahidi Wajerumani wangeweza kushughulikia gharama zilizohusika? Fursa ilitolewa kwao. Wakati wa kukamilishwa kwa mradi huo katika 1984, katika Selters, kwenye ukingo wa magharibi wa Milima Taunus, ofisi ya tawi iliripoti hivi: “Makumi ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova—matajiri kwa maskini, vijana kwa wazee—walichanga mamilioni ya dola ili kusaidia kulipia vile vifaa vipya. Kwa sababu ya ukarimu wao, mradi wote ungeweza kukamilishwa bila uhitaji wa kukopa fedha kutoka mashirika ya kilimwengu au kuingia katika deni.” Kwa kuongezea, karibu 1 kati ya kila Mashahidi 7 katika Jamhuri ya Muungano ya Ujerumani alikuwa ameshiriki kazi yenyewe ya ujenzi katika Selters/Taunus.

Katika nchi fulani, uchumi wa nchi au hali ya kifedha ya Mashahidi wa Yehova imefanya iwe vigumu sana, hata isiwezekane, kwao kujenga ofisi za tawi zilizohitajiwa ili kusimamia kazi au viwanda vya kutangazia fasihi za Biblia kwa lugha za wenyeji. Mashahidi katika nchi wamepewa fursa ya kufanya wawezavyo. (2 Kor. 8:11, 12) Lakini ukosefu wa fedha katika nchi hauruhusiwi uzuie kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme huko ikiwa fedha zilizohitajiwa zapatikana kwingineko.

Hivyo, ingawa Mashahidi wenyeji hufanya wawezayo, katika sehemu kubwa ya ulimwengu kiasi kikubwa cha fedha zinazohitajiwa kwa majengo ya tawi huandaliwa na upaji unaofanywa na Mashahidi wa Yehova katika nchi nyinginezo. Ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na ujenzi wa majengo makubwa yaliyokamilishwa katika Afrika Kusini katika 1987, Nigeria katika 1990, na Filipino katika 1991. Ndivyo pia ilivyokuwa kuhusu Zambia, ambako vilivyotazamiwa kuwa vifaa vya kuchapia vilikuwa vingali vinajengwa katika 1992. Hali kadhalika imekuwa hivyo kuhusu miradi mingi ya kadiri ndogo zaidi, kama ile iliyokamilishwa katika India katika 1985; Chile katika 1986; Kosta Rika, Ekuado, Guyana, Haiti, na Papua New Guinea katika 1987; Ghana katika 1988; na Honduras katika 1989.

Hata hivyo, katika nchi fulani, ndugu wameshangaa kuona yale ambayo wangeweza kutimiza nchini mwao kwa baraka ya Yehova juu ya jitihada zao za pamoja. Kwa kielelezo, katika miaka ya mapema ya 1980 tawi katika Hispania lilikuwa likifanya mipango ya nyongeza kubwa kwa vifaa vyalo. Tawi liliomba Baraza Linaloongoza liandae fedha zilizohitajiwa. Lakini kwa sababu ya matumizi makubwa katika pande nyinginezo katika wakati ule, msaada huo haukupatikana wakati ule. Wakipewa fursa, je, Mashahidi Wahispania, wangeweza, kwa mishahara yao ambayo kidogo ni ya chini, kuandaa fedha za kutosha kwa mradi kama huo?

Walielezwa hali. Kwa furaha walitoa vito vyao, pete, na vikuku ili viuzwe na fedha zipatikane. Wakati Shahidi mmoja wa kike mzee-mzee alipoulizwa kama alikuwa na hakika kwamba alitaka kutoa upaji wa kikuku kizito cha dhahabu alichokuwa amechanga, alijibu: “Ndugu, kitatimiza mema mengi zaidi kikilipia Betheli mpya kuliko vile kitatimiza kikiwa katika kiwiko changu!” Dada mmoja wa umri mkubwa zaidi alifukua rundo la manoti yaliyochakaa ambayo alikuwa amefukia chini ya sakafu ya kao lake kwa muda wa miaka mingi iliyopita. Waume na wake walichanga fedha walizokuwa wamehifadhi ili kufunga safari. Watoto walipeleka fedha walizohifadhi. Kijana mmoja aliyekuwa akipanga kununua gitaa alitoa upaji wa fedha hizo kwa ajili ya mradi wa tawi badala ya kununua gitaa. Kama vile Waisraeli wakati tabenakulo lilipojengwa jangwani, Mashahidi Wahispania walithibitika kuwa wachangaji wakarimu na wenye moyo wa kupenda wa vyote vilivyohitajiwa katika vitu vya kimwili. (Kut. 35:4-9, 21, 22) Halafu wakajitolea wenyewe—kwa wakati wote, wakati wa likizo, wakati wa miisho-juma—kufanya kazi yenyewe. Kutoka pande zote za Hispania walikuja—maelfu yao. Mashahidi wengine kutoka Ujerumani, Sweden, Uingereza, Ugiriki, na Marekani, kutaja nchi chache, walijiunga nao ili kukamilisha ile ambayo mwanzoni ilionekana kuwa kazi isiyowezekana.

Je, Kuna Faida Kutokana na Fasihi?

Kufikia 1992, fasihi za Biblia zilikuwa zikichapwa kwenye makao makuu ya ulimwengu na kwenye matawi 32 ulimwenguni pote. Kiasi kikubwa kilikuwa kikitolewa ili kugawanywa na Mashahidi wa Yehova. Lakini hapana yoyote yayo iliyofanywa kwa ajili ya pato la kibiashara. Maamuzi kwa habari ya lugha ambazo katika hizo fasihi zingechapwa na nchi ambako zingesafirishwa yalifanywa si kwa sababu ya faida yoyote ya kibiashara bali kwa sababu tu ya kukamilisha kazi ambayo Yesu Kristo aligawia wafuasi wake.

Mapema kama Julai 1879, wakati toleo la kwanza kabisa la Watch Tower lilipotangazwa, lilikuwa na taarifa ikisema kwamba wale waliokuwa maskini sana wasiweze kulipia uandikishaji (wakati huo ukiwa tu senti 50 za Marekani, kwa mwaka) wangeweza kuupata bila malipo ikiwa wangeandika tu na kutoa ombi. Lengo kuu lilikuwa kusaidia watu wajifunze juu ya kusudi kuu la Yehova.

Kwa kusudi hilo, tangu 1879 kiasi kikubwa cha fasihi za Biblia kimegawanywa miongoni mwa umma bila malipo. Katika 1881 na baada ya hapo, karibu nakala 1,200,000 za Food for Thinking Christians ziligawanywa bila malipo. Nyingi za hizo zilikuwa kwa namna ya kitabu cha kurasa 162; nyingine, katika umbo la gazeti. Trakti nyingi za ukubwa tofauti-tofauti zilitangazwa wakati wa miaka iliyofuata. Kiasi kikubwa cha hizo (kihalisi mamia ya mamilioni ya nakala) kiligawanywa bila malipo. Hesabu ya trakti na vichapo vingine vilivyotolewa bila malipo ilizidi kukua. Katika 1915 pekee, ripoti ilionyesha kwamba nakala 50,000,000 za trakti katika lugha kama 30 zilitolewa ili kugawanywa ulimwenguni pote bila malipo. Fedha za yote hayo zilikuwa zikitoka wapi? Sanasana zilitoka kwa upaji wa hiari kwa Hazina ya Tract Society.

Kulikuwa pia fasihi iliyotolewa kwa mchango wakati wa miongo ya mapema ya historia ya Sosaiti, lakini mchango uliodokezwa uliwekwa ukiwa mdogo sana kadiri ilivyowezekana. Fasihi hiyo ilitia ndani vitabu vilivyojalidiwa vya kurasa 350 hadi 744. Wakati makolpota (kama wahubiri wa wakati wote walivyojulikana wakati ule) wa Sosaiti walipovitoa kwa umma, walitaarifu kiasi kilichodokezwa kuwa mchango. Hata hivyo, lengo lao halikuwa kuchuma fedha bali kutia mikononi mwa watu kweli muhimu za Biblia. Walitaka watu wasome fasihi ili iwanufaishe.

Walikuwa na nia sana ya kumpa mtu fasihi (wakilipia mchango wao wenyewe) ikiwa mwenye nyumba alikuwa maskini sana. Lakini ilikuwa imeonwa kwamba watu wengi walielekea zaidi kusoma kichapo ambacho walikuwa wamelipia kitu fulani, na bila shaka, kile walichochanga kingeweza kutumiwa kuchapa fasihi zaidi. Hata hivyo, kikikazia kwamba Wanafunzi wa Biblia hawakuwa wakitafuta pato la kifedha, kikaratasi cha maagizo ya utumishi cha Sosaiti, Bulletin, cha Oktoba 1, 1920, kilisema hivi: “Siku kumi baada ya kuwa umepeleka kijitabu [kilichokuwa na kurasa 128], watembelee tena watu na kuhakikisha kama wamekisoma. Ikiwa hawajakisoma, waombe wakirudishe na kuwarudishia fedha zao. Waambie kwamba wewe si mwakilishi wa [kampuni ya] vitabu, bali kwamba unapendezwa na kutoa ujumbe huo wa faraja na uchangamfu kwa kila mtu, na kwamba ikiwa wao hawapendezwi vya kutosha na jambo la hakika linalowahusu sana kadiri hiyo . . . , wataka kutia kitabu hicho mikononi mwa mtu mwingine atakayependezwa.” Mashahidi wa Yehova hawakuendelea kutumia njia hiyo, kwa sababu wameona kwamba washiriki wengine wa familia mara nyingi huchukua fasihi na kunufaishwa nayo; lakini jambo lililofanywa huko nyuma hukazia lengo halisi la Mashahidi.

Kwa miaka mingi walirejezea ugawanyaji wao wa fasihi kuwa “kuuza.” Lakini usemi huo ulisababisha mvurugo, na kwa hiyo kuanzia na 1929, uliacha kutumiwa hatua kwa hatua. Usemi huo haukufaana kwelikweli na utendaji wao, kwa kuwa kazi yao haikuwa ya kibiashara. Lengo lao halikuwa kuchuma fedha. Kusudio lao lote lilikuwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, katika 1943 Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani iliamua kwamba Mashahidi wa Yehova hawakutakwa kupata leseni ya kuchuuza kibiashara kabla ya kugawanya fasihi zao. Na mahakama ya Kanada baada ya hapo ilinukuu kwa kupendelea kutoa sababu kulikofanywa na Mahakama Kuu Zaidi ya Marekani katika uamuzi huo.b

Katika nchi nyingi Mashahidi wa Yehova wametoa kwa ukawaida fasihi zao kwa msingi wa mchango. Mchango udokezwao umekuwa chini sana, ukilinganishwa na vitabu na magazeti mengine, hivi kwamba watu wengi wamejitolea kuchanga zaidi. Lakini jitihada kubwa imefanywa kwa upande wa tengenezo kuendeleza michango idokezwayo ikiwa chini ili iwe katika kiwango cha pato la mamilioni mengi ya watu walio na mali kidogo sana za ulimwengu huu lakini ambao hushukuru kupokea Biblia au fasihi za Biblia. Hata hivyo, lengo katika kudokeza mchango limekuwa si kutajirisha tengenezo la Mashahidi wa Yehova.

Mahali ambako sheria hueleza ugawanyaji wowote wa fasihi za Biblia kuwa biashara ikiwa mgawanyaji hudokeza mchango kwa ajili ya fasihi, Mashahidi wa Yehova humwachia kwa furaha yeyote aonyeshaye kupendezwa kwa moyo mweupe na ambaye huahidi kuisoma. Wale ambao hutaka kuchanga kitu fulani kwa ajili ya kusogeza mbele kazi ya elimu ya Biblia waweza kutoa chochote watakacho. Kwa kielelezo, jambo hilo hufanywa katika Japani. Katika Uswisi, kufikia karibuni, michango ya kutoa kwa hiari yalikubaliwa, lakini kufikia kiasi kilichotaarifiwa tu kwa ajili ya kichapo; hivyo ikiwa wenye nyumba walitaka kutoa zaidi, Mashahidi walimrudishia tu au kumwandalia mwenye nyumba fasihi zaidi. Tamaa yao ilikuwa, si kukusanya fedha, bali kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu.

Katika 1990, kwa sababu ya kashfa za kifedha katika baadhi ya dini za Jumuiya ya Wakristo ambazo zilitangazwa sana kwa umma, pamoja na mwelekeo wenye kuongezeka wa serikali wa kuainisha utendaji wa kidini kuwa shughuli za kibiashara, Mashahidi wa Yehova walifanya marekebisho fulani katika utendaji wao ili kuepuka kueleweka vibaya kwa vyovyote. Baraza Linaloongoza lilielekeza kwamba katika Marekani, fasihi zote ambazo hugawanywa na Mashahidi—Biblia, pamoja na trakti, vijitabu, magazeti, na vitabu vilivyojalidiwa vyenye kuelezea Biblia—vitolewe kwa watu kwa sharti tu la kwamba watavisoma, bila kudokeza mchango. Utendaji wa Mashahidi wa Yehova si wa kibiashara hata kidogo, na mpango huo ulitumika kuwatofautisha zaidi na vikundi vya kidini ambavyo hufanya dini kuwa ya kibiashara. Bila shaka, watu wengi wanajua kwamba inagharimu kuchapa fasihi kama hiyo, na wale ambao huthamini utumishi unaofanywa na Mashahidi waweza kutaka kutoa upaji wa kitu fulani kusaidia kazi. Watu hao wanaelezwa kwamba kazi ya ulimwenguni pote ya elimu ya Biblia iongozwayo na Mashahidi wa Yehova hutegemezwa kwa upaji wa hiari. Upaji hukubaliwa kwa furaha, lakini hauombwiombwi.

Wale ambao hushiriki huduma ya shambani hawaifanyi kwa pato la kifedha. Wao hutoa upaji wa wakati wao, na hulipia usafiri wao wenyewe. Ikiwa mtu aonyesha kupendezwa, wao hupanga kurudi kila juma, bila malipo hata kidogo, ili kutoa maagizo ya kibinafsi katika Biblia. Ni upendo tu kwa Mungu na wanadamu wenzao ndio ungeweza kuwasukuma kuendelea kushiriki katika utendaji huo, mara nyingi kwa kukabiliwa na ubaridi na upinzani wa moja kwa moja.

Fedha zipokewazo kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova au kwenye ofisi zayo za tawi hutumiwa, si kutajirisha tengenezo au mtu yeyote, bali kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema. Huko nyuma katika 1922, The Watch Tower liliripoti kwamba kwa sababu ya hali ya kiuchumi katika Ulaya, vitabu vilivyochapwa huko kwa ajili ya Sosaiti vilikuwa vikilipiwa sanasana na ofisi ya Amerika na mara nyingi vilikuwa vikiachwa kwa watu kwa bei iliyo chini ya gharama ya kuchapisha. Ingawa sasa Mashahidi wa Yehova huendesha mashirika ya kuchapia katika nchi nyingi, baadhi ya nchi ambako fasihi husafirishwa haziwezi kupeleka fedha zozote nje ya nchi ili kulipia bei. Upaji wa ukarimu wa kutoa kwa hiari wa Mashahidi wa Yehova katika nchi ambazo zina mali ya kutosha ndiyo husaidia kusawazisha upungufu katika nchi ambazo zina mali kidogo.

Sikuzote Watch Tower Society imejitahidi kutumia mali yote iliyo nayo kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema. Katika 1915, akiwa msimamizi wa Sosaiti, Charles Taze Russell alisema: “Sosaiti yetu haikutafuta kuweka akiba ya mali za kilimwengu kwa ajili ya wakati ujao, bali, imekuwa shirika lenye kutumia mali ili kutimiza mambo. Chochote ambacho mwelekezo wa Mungu ulituletea bila kuombaomba tumetafuta kutumia kwa hekima kadiri ilivyowezekana kupatana na Neno na Roho ya Bwana. Muda mrefu uliopita tulitangaza kwamba wakati fedha zingekoma, utendaji wa Sosaiti ungekoma kwa kadiri iyo hiyo; na kwa kadiri fedha zingeongezeka, utendaji wa Sosaiti ungeongezeka.” Sosaiti imeendelea kufanya vivyo hivyo.

Hadi sasa, tengenezo hutumia fedha zipatikanazo kutuma waangalizi wasafirio ili wakaimarishe makutaniko na kuyatia moyo katika huduma ya hadharani. Yaendelea kutuma wamishonari na wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kwenye nchi ambako kuna uhitaji wa pekee. Hutumia pia fedha zozote zipatikanazo kutuma mapainia wa pekee kwenye maeneo ambako ni kazi ndogo sana imefanywa au hakuna kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ambayo imepata kufanywa. Kama ilivyoripotiwa katika Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1993, (Kiingereza) wakati wa mwaka wa utumishi uliotangulia huo, dola 45,218,257.56 (Marekani) zilitumiwa katika njia hizo.

Hawatumikii kwa Ajili ya Pato la Kibinafsi

Hakuna mshiriki yeyote wa Baraza Linaloongoza, maofisa wa mashirika yao halali, au watu wengine mashuhuri wanaoshirikiana na tengenezo ambaye hupata faida ya kifedha kutokana na kazi ya Mashahidi wa Yehova.

Kuhusu C. T. Russell, aliyetumikia akiwa msimamizi wa Watch Tower Society kwa zaidi ya miaka 30, mmojawapo washirika wake aliandika hivi: “Ikiwa njia ya kuamulia kama mwendo wake ulipatana na Maandiko, na pia ikiwa njia ya kuonyesha weupe wake mwenyewe wa moyo, yeye aliamua kutahini kibali cha Bwana kama ifuatavyo: (1) Atoe maisha yake kabisa kwa imani aliyotetea; (2) Atumie mali yake katika kuendeleza kazi; (3) Akataze kukusanywa kwa fedha kwenye mikutano yote; (4) Ategemee michango isiyo ya kuombaomba (ya kutoa kwa hiari kabisa) ili kuendeleza kazi baada ya mali yake kumalizika.”

Badala ya kutumia utendaji wa kidini ili kujipatia utajiri wa vitu vya kimwili, Ndugu Russell alitumia rasilimali zake zote katika kazi ya Bwana. Baada ya kifo chake iliripotiwa hivi katika The Watch Tower: “Alitumia mali yake binafsi kabisakabisa katika imani ambayo alitolea maisha yake. Alipokea kiasi kidogo cha dola 11.00 (Marekani) kwa mwezi kwa ajili ya matumizi ya binafsi. Alikufa, asiache mali yoyote hata kidogo.”

Kuhusu wale ambao wangeendesha kazi ya Sosaiti, Ndugu Russell alitoa sharti katika wasia wake kwamba: “Kwa habari ya kulipia gharama, nafikiri ni jambo la hekima kudumisha mwendo wa Sosaiti wa wakati uliopita kwa habari ya mishahara—kwamba yeyote asilipwe; kwamba matumizi ya kiasi tu yaruhusiwe kwa wale ambao hutumikia Sosaiti au kazi yayo kwa njia yoyote.” Wale ambao wangetumikia kwenye makao ya Betheli, ofisi, na viwanda vya Sosaiti, pamoja na wawakilishi wa Sosaiti wasafirio, wangeandaliwa tu chakula, makao, na kiasi kidogo kwa ajili ya gharama—kutosha mahitaji ya wakati uliopo lakini “bila uandalizi . . . wa kuweka akiba ya fedha kwa wakati ujao.” Kiwango icho hicho chatumika leo.

Wale ambao hukubaliwa kwa ajili ya utumishi wa pekee wa wakati wote kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova wote hukubali nadhiri ya umaskini, kama ilivyo kwa washiriki wote wa Baraza Linaloongoza na washiriki wengine wote wa familia ya Betheli kule. Hiyo haimaanishi kwamba wanaishi maisha yasiyo na furaha, bila starehe yoyote. Lakini yamaanisha kwamba wanashiriki, bila upendeleo, maandalizi ya kiasi ya chakula, makao, na rudishio la gharama vinavyoandaliwa kwa wote walio katika utumishi huo.

Hivyo ndivyo tengenezo huendesha kazi yalo kwa kutegemea kabisa msaada ambao Mungu hutoa. Bila kulazimishwa bali kama udugu halisi wa kiroho ambao hufika sehemu zote za dunia, Mashahidi wa Yehova hutumia kwa furaha rasilimali zao ili kutimiza kazi ambayo Yehova, Baba yao mtukufu wa kimbingu, amewapa wafanye.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Septemba 1, 1944, ukurasa 269; Desemba 15, 1987, kurasa 19-20.

b Murdock v. Commonwealth of Pennsylvania, 319 U.S. 105 (1943); Odell v. Trepanier, 95 C.C.C. 241 (1949).

[Blabu katika ukurasa wa 340]

‘Kuombaomba fedha hakuruhusiwi wala hakukubaliwi na Sosaiti hii’

[Blabu katika ukurasa wa 342]

Mkazo mkubwa u juu ya ubora wa kushiriki kweli pamoja na wengine

[Blabu katika ukurasa wa 343]

Taarifa iliyo wazi, ya unyoofu juu ya mambo ya hakika

[Blabu katika ukurasa wa 344]

Makutaniko husaidiana yapate Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa

[Blabu katika ukurasa wa 345]

Michango mingi hutoka kwa watu mmoja-mmoja ambao wana mali kidogo tu

[Blabu katika ukurasa wa 348]

Fasihi nyingi hugawanywa bila malipo—ni nani huilipia?

[Blabu katika ukurasa wa 349]

Kwa furaha wao huachia fasihi yao yeyote anayeonyesha kupendezwa kwa moyo mweupe na ambaye aahidi kuisoma

[Blabu katika ukurasa wa 350]

Ni jambo gani hufanywa na fedha zinazochangwa?

[Blabu katika ukurasa wa 351]

“Alitumia mali yake binafsi kabisakabisa katika imani ambayo alitolea maisha yake”

[Sanduku katika ukurasa wa 341]

Mungu Haombiombi

“Yeye aliyesema, ‘Kama ningekuwa na njaa singekuambia, maana ulimwengu ni wangu, navyo viujazavyo. . . . Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako, wala beberu katika mazizi yako; maana kila hayawani wa msitu ni wangu, na makundi ya ng’ombe juu ya milima elfu’ (Zab. 50:12, 9, 10), aweza kuendesha kazi yake kuu bila kuombaomba fedha ama kutoka kwa ulimwengu ama kutoka kwa watoto wake. Wala hatashurutisha watoto wake kutoa dhabihu au chochote katika utumishi wake, wala hatakubali chochote kutoka kwao isipokuwa toleo changamfu, la hiari.”—“Zion’s Watch Tower,” Septemba 1886, uku. 6.

[Sanduku katika ukurasa wa 347]

Sikuzote Upaji Haukuwa kwa Namna ya Fedha

Mashahidi katika kaskazini ya mbali katika Queensland walitayarisha na kupeleka kwenye ujenzi wa Watch Tower katika Sydney, Australia, malori manne makubwa yenye kujaa shehena ya mbao bora kabisa ambazo wakati ule zilikadiriwa kuwa na thamani ya dola kati ya 60,000 na 70,000 za Australia.

Wakati kiwanda cha Watch Tower katika Elandsfontein, Afrika Kusini, kilipokuwa kikiongezewa ukubwa, ndugu Mhindi alipiga simu na kuomba kwamba waje tafadhali wachukue upaji wa mifuko 500 (kilo 50 kila mmoja) ya saruji—wakati kulipokuwa na uhaba wayo nchini. Wengine walitoa malori yao yatumiwe na Sosaiti. Dada Mwafrika alilipa kampuni moja ili ipeleke meta za kyubiki 15 za mchanga wa kujengea.

Katika Uholanzi wakati vifaa vipya vya tawi vilipokuwa vikijengwa katika Emmeni, kiasi kikubwa cha vyombo na mavazi ya kujengea vilichangwa. Dada mmoja, ajapokuwa mgonjwa sana, alifuma jozi ya soksi ndefu kwa kila mmoja wa wafanyakazi wakati wa pindi hiyo ya majira ya baridi.

Ili kujenga ofisi ya tawi mpya na kile kilichotazamiwa kuwa kiwanda cha uchapaji katika Lusaka, Zambia, vifaa vya ujenzi vilinunuliwa na fedha zilizotolewa na Mashahidi katika nchi nyinginezo. Vifaa na vyombo ambavyo havikupatikana nchini vilipelekwa Zambia kwa malori vikiwa upaji kwa ajili ya kazi kule.

Shahidi katika Ekuado, katika 1977, alitoa upaji wa kisehemu cha ardhi cha hekta 34. Hapo lilijengwa Jumba la Kusanyiko na majengo ya tawi jipya.

Mashahidi wenyeji katika Panama waliwakaribisha na kuwapa makao wafanyakazi wa kujitolea; baadhi yao waliokuwa na mabasi waliandaa usafiri; wengine walishiriki kuandaa milo 30,000 iliyoandaliwa mahali penye ujenzi.

Kwa ajili ya wafanyakazi kwenye mradi katika Arboga Sweden, kutaniko moja lilioka na kupeleka vitumbua 4,500. Wengine walipeleka asali, matunda, na jemu. Mkulima mmoja karibu na ujenzi, ajapokuwa si Shahidi, aliandaa tani mbili za karoti.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki