Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kl sura 2 kur. 12-22
  • Kitabu Kifunuacho Ujuzi Juu ya Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Kifunuacho Ujuzi Juu ya Mungu
  • Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA BIBLIA
  • JE, WAWEZA KUITUMAINI BIBLIA?
  • SAHIHI NA YENYE KUTEGEMEKA
  • KITABU CHA UNABII
  • ‘FANYIZA HAMU SANA’ YA UJUZI JUU YA MUNGU
  • Mafundisho ya Kweli Yanayompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Biblia​—Kitabu Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Je! Kweli Biblia Ilitoka kwa Mungu?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
kl sura 2 kur. 12-22

Sura 2

Kitabu Kifunuacho Ujuzi Juu ya Mungu

1, 2. Sababu gani tunahitaji mwongozo wa Muumba wetu?

NI JAMBO lenye kupatana na akili tu kwamba Muumba wetu mwenye upendo angewatolea wanadamu kitabu chenye maagizo na mwongozo. Na je, hukubali kwamba wanadamu wanahitaji mwongozo?

2 Miaka zaidi ya 2,500 iliyopita, nabii fulani aliye mwanahistoria aliandika hivi: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Leo, ukweli wa taarifa hiyo ni wa wazi zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Hivyo, mwanahistoria William H. McNeill asema hivi: “Mambo ambayo yamempata mwanadamu katika sayari hii yamekuwa mfululizo karibu usiokatizwa wa misiba na machafuko ya utaratibu uliowekwa wa jamii.”

3, 4. (a) Tunapaswa tulifikieje funzo la Biblia? (b) Tutaanzaje kuichunguza Biblia?

3 Biblia hutimiza mahitaji yetu yote ya kuwa na mwelekezo wenye hekima. Ni kweli, wengi huhisi wamelemewa wanapoichunguza Biblia kwa mara ya kwanza. Ni kitabu kikubwa, na baadhi ya sehemu zayo ni ngumu kuelewa. Lakini ikiwa ungepewa hati ya kisheria inayoonyesha yale uliyohitaji kufanya ili upokee urithi wenye thamani, je, usingechukua wakati wa kuisoma kwa uangalifu? Ikiwa ungeona sehemu fulani za hati hiyo kuwa ngumu kuelewa, yaelekea ungepata msaada wa mtu fulani mwenye uzoefu wa mambo hayo. Sababu gani usiifikie Biblia ukiwa na mtazamo uo huo? (Matendo 17:11) Yanayohusika ni mengi zaidi kuliko urithi wa kimwili tu. Kama vile tulivyojifunza kati­ka sura iliyotangulia, ujuzi juu ya Mungu waweza kuongoza kwenye uhai udumuo milele.

4 Acheni tuchunguze kitabu hiki kifunuacho ujuzi juu ya Mungu. Kwanza tutatoa maelezo mafupi juu ya Biblia yote kwa ujumla. Kisha tutazungumzia sababu gani watu wengi wenye maarifa huamini kwamba hilo ni Neno la Mungu lililopuliziwa.

YALIYOMO KATIKA BIBLIA

5. (a) Ni nini yaliyomo katika Maandiko ya Kiebrania? (b) Ni nini yaliyomo katika Maandiko ya Kigiriki?

5 Biblia ina vitabu 66 katika sehemu mbili, ambazo mara nyingi huitwa Agano la Kale na Agano Jipya. Vitabu 39 vya Biblia viliandikwa hasa katika Kiebrania na 27 katika Kigiriki. Maandiko ya Kiebrania, yaliyo na Mwanzo hadi Malaki, huzungumzia uumbaji na pia ile miaka 3,500 ya kwanza ya historia ya kibinadamu. Tuchunguzapo sehemu hiyo ya Biblia, tunajifunza juu ya shughuli za Mungu pamoja na Waisraeli—tangu kuzaliwa kwao wakiwa taifa katika karne ya 16 K.W.K. hadi katika karne ya 5 K.W.K.a Maandiko ya Kigiriki, yaliyo na vitabu vya Mathayo hadi Ufunuo, hukazia mafundisho na utendaji mbalimbali wa Yesu Kristo na wanafunzi wake wakati wa karne ya kwanza W.K.

6. Sababu gani tunapaswa kujifunza Biblia nzima?

6 Wengine hudai kwamba “Agano la Kale” ni la Wayahudi na “Agano Jipya” ni la Wakristo. Lakini kulingana na 2 Timotheo 3:16, ‘Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa.’ Kwa hiyo, lazima funzo la Maandiko lifaalo litie ndani Biblia nzima. Kwa hakika, zile sehemu mbili za Biblia zinakamilishana, zikichangamana kwa upatano ili kukuza kichwa cha ujumla.

7. Ni nini kilicho kichwa cha Biblia?

7 Labda wewe umehudhuria ibada za kidini kwa miaka mingi na umesikia sehemu ya Biblia ikisomwa kwa sauti. Au huenda ukawa umejisomea sehemu mbalimbali kutoka kwayo. Je, ulijua kwamba Biblia ina jambo moja la ujumla kutoka Mwanzo hadi Ufunuo? Ndiyo, kichwa kimoja chenye upatano chaenea Biblia yote. Kichwa hicho ni nini? Ni utetezi wa haki ya Mungu ya kutawala wanadamu na utimizo wa kusudi lake lenye upendo kupitia Ufalme wake. Baadaye, tutaona jinsi hasa Mungu atakavyotimiza kusudi hili.

8. Biblia hufunua nini juu ya utu wa Mungu?

8 Zaidi ya kusimulia kusudi la Mungu, Biblia hufunua utu wake. Kwa kielelezo, tunajifunza kutoka Biblia kwamba Mungu ana hisia na kwamba anajali machaguo tunayofanya. (Zaburi 78:40, 41; Mithali 27:11; Ezekieli 33:11) Zaburi 103:8-14 yasema kwamba Mungu “amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili.” Yeye hututendea kwa huruma, ‘akikumbuka kwamba sisi tumefanyizwa kwa mavumbi tu’ na hurudi huko wakati wa kifo. (Mwanzo 2:7; 3:19) Yeye huonyesha sifa nzuri ajabu kama nini! Je, huyu siye aina ya Mungu ambaye unataka kumwabudu?

9. Biblia hutuonyeshaje waziwazi viwango vya Mungu, na tunaweza kunufaikaje na ujuzi huo?

9 Biblia hutuonyesha waziwazi viwango vya Mungu. Nyakati nyingine hivyo husemwa kuwa sheria. Hata hivyo, mara nyingi zaidi huonyeshwa katika kanuni zinazofundishwa kupitia mifano. Mungu aliagiza kwamba mambo fulani katika historia ya Israeli la kale yaandikwe kwa manufaa yetu. Masimulizi hayo ya unyoofu wa moyo huonyesha jinsi hali inavyokuwa wakati watu wanapofanya mambo kwa kupatana na kusudi la Mungu, na pia matokeo ya kuhuzunisha wanapojitegemea. (1 Wafalme 5:4; 11:4-6; 2 Mambo ya Nyakati 15:8-15) Kusoma masimulizi hayo ya maisha halisi kutaathiri mioyo yetu bila shaka. Tukijaribu kuona akilini matukio hayo yaliyorekodiwa, tunaweza kujitia katika hali ya wale watu waliohusika katika hayo. Kwa njia hiyo, tunaweza kunufaika kutokana na vielelezo vizuri na kuepuka mitego iliyonasa wakosaji. Hata hivyo, swali hili la muhimu linataka jibu: Tunaweza kuwaje na hakika kwamba yale tunayosoma katika Biblia kwa kweli yamepuliziwa na Mungu?

JE, WAWEZA KUITUMAINI BIBLIA?

10. (a) Sababu gani wengine huhisi kwamba Biblia si ya kisasa? (b) 2 Timotheo 3:16, 17 hutuambia nini juu ya Biblia?

10 Labda umeona kwamba vitabu vingi vinavyotoa shauri huwa vya zamani katika muda wa miaka michache tu. Namna gani Biblia? Hiyo ni ya zamani sana, na karibu miaka 2,000 imepita tangu maneno yayo ya mwisho yalipoandikwa. Kwa hiyo wengine huhisi kwamba si yenye kutumika katika wakati wetu wa kisasa. Lakini ikiwa Biblia imepuliziwa na Mungu, shauri layo linapaswa kuwa la kisasa sikuzote ujapokuwa umri wayo mkubwa. Maandiko yapaswa bado yawe yenye “[ku]faa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

11-13. Sababu gani tunaweza kusema kwamba Biblia ni yenye kutumika kwa siku yetu?

11 Uchunguzi wa karibu unafunua kwamba kanuni za Biblia zinatumika sana leo kadiri ileile ambayo zilitumika zilipoandikwa mara ya kwanza. Kwa mfano, kwa habari ya asili ya kibinadamu, Biblia huonyesha uelewevu mwingi unaotumika kwa kila kizazi cha wanadamu. Tunaweza kuona hilo kwa urahisi katika Mahubiri ya Mlimani ya Yesu, yanayopatikana katika kitabu cha Mathayo, sura ya 5 hadi ya 7. Mahubiri hayo yalimvutia sana yule kiongozi Mhindi aliyekufa Mohandas K. Gandhi hivi kwamba imeripotiwa kwamba alimwambia ofisa fulani wa Uingereza hivi: “Wakati nchi yako na yangu zitakapoungana juu ya mafundisho aliyofundisha Kristo katika haya Mahubiri ya Mlimani, sisi tutakuwa tumetatua matatizo si ya nchi zetu tu bali yale ya ulimwengu mzima.”

12 Si ajabu kwamba watu huvutiwa na mafundisho ya Yesu! Katika Mahubiri ya Mlimani, yeye alituonyesha njia iongozayo kwenye furaha ya kweli. Yeye alieleza jinsi ya kusuluhisha mabishano. Yesu alitoa maagizo juu ya jinsi ya kusali. Alionyesha ule mtazamo wenye hekima zaidi wa kuwa nao kuelekea mahitaji ya kimwili naye akatoa ile Kanuni Bora ili kuwa na mahusiano yafaayo na wengine. Jinsi ya kutambua waongo wa kidini na jinsi ya kuwa na wakati ujao salama yalikuwa pia miongoni mwa mambo yaliyozungumziwa katika mahubiri hayo.

13 Katika Mahubiri ya Mlimani na kotekote katika kurasa zayo nyinginezo, Biblia hutuambia kwa wazi yale ya kufanya na yale ya kuepuka ili kuboresha hali yetu maishani. Shauri layo ni lenye kutumika sana hivi kwamba mwelimishaji mmoja alisukumwa kusema hivi: “Ingawa mimi ni mshauri wa shule ya upili mwenye diploma na digrii na nikiwa nimesoma vitabu vingi juu ya afya ya akilini na saikolojia, niligundua kwamba shauri la Biblia juu ya mambo kama vile ndoa yenye mafanikio, kuzuia uhalifu wa watoto na jinsi ya kupata na kudumisha marafiki ni la hali ya juu zaidi kuliko jambo lolote nililokuwa nimesoma au kujifu­nza chuoni.” Zaidi ya kuwa yenye kutumika na ya kisasa, Biblia ni yenye kutegemeka.

SAHIHI NA YENYE KUTEGEMEKA

14. Ni nini kinachoonyesha kwamba Biblia ni sahihi kwa habari za kisayansi?

14 Ingawa Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi, ni sahihi kwa habari za kisayansi. Kwa kielelezo, katika wakati ambapo watu walio wengi waliamini kwamba dunia ilikuwa tambarare, nabii Isaya aliirejezea kuwa “duara” (Kiebrania, chugh, ambalo hapa lina wazo la “tufe”). (Isaya 40:22) Wazo la dunia la kitufe halikukubaliwa na wengi mpaka maelfu ya miaka baada ya siku ya Isaya. Zaidi ya hayo, maneno ya Ayubu 26:7—yaliyoandikwa miaka zaidi ya 3,000 iliyopita—yasema kwamba Mungu “a[na]ining’iniza dunia pasipo na kitu.” (NW) Msomi mmoja wa Biblia asema hivi: “Jinsi Ayubu alivyojua ukweli, ulioonyeshwa na utaalamu wa nyota, wa kwamba dunia inaning’inia bila utegemezo wowote katika anga isiyo na kitu, ni swali lisilojibiwa kwa urahisi na wale wanaokana kupuliziwa kwa Maandiko Matakatifu.”

15. Uhakika katika Biblia unaimarishwaje na namna yayo ya kuripoti?

15 Namna ya kuripoti inayopatikana katika Biblia inaimarisha pia uhakika wetu katika kitabu hiki cha zamani sana. Tofauti na ngano, mambo yanayozungumziwa katika Biblia yanahusianishwa na watu na tarehe hususa. (1 Wafalme 14:25; Isaya 36:1; Luka 3:1, 2) Na ingawa karibu sikuzote wanahistoria wa kale walitia chumvi juu ya ushindi mbalimbali wa watawala wao na kuficha kushindwa kwao na makosa yao, waandikaji wa Biblia waliandika kwa unyoofu wa moyo na kwa kufuatia haki—hata juu ya dhambi zao wenyewe zilizo nzito.—Hesabu 20:7-13; 2 Samweli 12:7-14; 24:10.

KITABU CHA UNABII

16. Ni nini uthibitisho wenye nguvu zaidi kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu?

16 Unabii uliotimizwa watoa uthibitisho wenye nguvu wa kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu. Biblia ina unabii mwingi ambao umetimizwa kikamili. Kwa wazi, wanadamu duni wasingeweza kufanya hayo. Basi, unabii huo mbalimbali unatokana na nini? Biblia yenyewe husema kwamba “unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na [r]oho [t]akatifu,” au kani ya utendaji ya Mungu. (2 Petro 1:21) Fikiria baadhi ya vielelezo:

17. Ni unabii upi mbalimbali uliotabiri kule kuanguka kwa Babiloni, na huo ulitimizwaje?

17 Kuanguka kwa Babiloni. Isaya na Yeremia wote wawili walitabiri kuanguka kwa Babiloni kupitia Wamedi na Waajemi. Kwa ajabu, unabii wa Isaya juu ya jambo hili ulirekodiwa miaka ipatayo 200 kabla ya Babiloni kushindwa! Sehemu zifuatazo za unabii sasa ni mambo yaliyorekodiwa katika historia: kukauka kwa Mto Frati kwa kugeuza maji yao upande hadi katika ziwa lenye kufanyizwa na watu (Isaya 44:27; Yeremia 50:38); kutokuwa waangalifu kulinda malango ya mtoni ya Babiloni (Isaya 45:1); na ushindi wa mtawala aitwaye Koreshi.—Isaya 44:28.

18. Unabii wa Biblia ulitimizwaje katika kule kuinuka na kuanguka kwa “mfalme wa Ugiriki” (NW)?

18 Kuinuka na kuanguka kwa “mfalme wa Ugiriki.” (NW) Katika ono, Danieli aliona beberu akimpiga na kumwangusha chini kondoo mume, akivunja pembe zake mbili. Kisha, ile pembe kubwa ya beberu ikavunjwa, na pembe nne zikachukua mahali payo. (Danieli 8:1-8) Ilielezwa hivi kwa Danieli: “Yule kondoo mume uliyemwona, mwenye pembe mbili, hizo ndizo wafalme wa Umedi na Uajemi. Na yule beberu, mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani [“Ugiriki,” NW]; na ile pembe kubwa iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza. Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake.” (Danieli 8:20-22) Kulingana na unabii huu, karne mbili hivi baadaye, “mfalme wa Ugiriki,” (NW) Aleksanda Mkubwa, alipindua milki ya Umedi na Uajemi yenye pembe mbili. Aleksanda alikufa katika 323 K.W.K. na hatimaye mahali pake pakachukuliwa na majenerali wake wanne. Hata hivyo, hakuna mmoja wa falme hizo zilizofuata uliolingana na nguvu za milki ya Aleksanda.

19. Ni unabii upi uliotimizwa katika Yesu Kristo?

19 Maisha ya Yesu Kristo. Maandiko ya Kiebrania yana unabii mwingi uliotimizwa katika kuzaliwa, huduma, kifo, na ufufuo wa Yesu. Kwa kielelezo, miaka zaidi ya 700 kimbele, Mika alitabiri kwamba Mesiya, au Kristo, angezaliwa katika Bethlehemu. (Mika 5:2; Luka 2:4-7) Isaya aliyeishi wakati mmoja na Mika alitabiri kwamba Mesiya angepigwa na kutemewa mate. (Isaya 50:6; Mathayo 26:67) Miaka 500 kimbele, Zekaria alitoa unabii kwamba Mesiya angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha. (Zekaria 11:12; Mathayo 26:15) Miaka zaidi ya elfu moja kimbele, Daudi alitabiri hali zilizohusiana na kifo cha Yesu Mesiya. (Zaburi 22:7, 8, 18; Mathayo 27:35, 39-43) Karne tano hivi kimbele, unabii wa Danieli ulifunua wakati ambapo Mesiya angetokea na pia urefu wa huduma yake na wakati wa kifo chake. (Danieli 9:24-27) Hiyo ni mifano tu ya unabii uliotimizwa katika Yesu Kristo. Utaliona kuwa jambo lenye kuthawabisha kusoma mengi zaidi juu yake baadaye.

20. Rekodi kamilifu ya Biblia juu ya unabii uliotimizwa inapaswa itupe sisi uhakika upi?

20 Unabii wa Biblia mwingine mwingi wenye kuchukua muda mrefu umetimizwa tayari. ‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘hilo linaathirije maisha yangu?’ Ikiwa mtu fulani angekuambia kweli kwa muda wa miaka mingi, je, ungemtilia shaka ghafula wakati angekuambia jambo jipya? La! Mungu ameisema kweli kotekote katika Biblia. Je, hilo lisikuze kutumaini kwako katika yale ambayo Biblia inaahidi, kama vile unabii wayo mbalimbali kuhusu paradiso ya kidunia inayokuja? Kwa kweli, tunaweza kuwa na uhakika uleule wa Paulo, mmoja wa wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza, aliyeandika kwamba ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Zaidi ya hayo, tunaposoma Maandiko na kutumia shauri layo, tunadhihirisha hekima ambayo wanadamu hawawezi kutimiza wakiwa peke yao, kwani Biblia ni kitabu kifunuacho ujuzi juu ya Mungu uongozao kwenye uhai udumuo milele.

‘FANYIZA HAMU SANA’ YA UJUZI JUU YA MUNGU

21. Unapaswa kufanya nini ikiwa mambo fulani unayojifunza kutoka katika Biblia yanaonekana kuwa yenye kulemea?

21 Ujifunzapo Biblia, yaelekea utajifunza mambo yanayotofautiana na yale ambayo umefundishwa wakati uliopita. Huenda hata ukagundua kwamba desturi fulani za kidini unazopenda sana hazimpendezi Mungu. Utajifunza kwamba Mungu ana viwango vya mema na mabaya vilivyo juu zaidi kuliko vile vilivyo vya kawaida katika ulimwengu huu wenye uendekevu. Huenda hilo likaonekana kuwa lenye kulemea mwanzoni. Lakini uwe mwenye subira! Chunguza Maandiko kwa uangalifu ili upate ujuzi juu ya Mungu. Jitayarishe kwa uwezekano wa kwamba shauri la Biblia huenda likataka rekebisho katika kufikiri kwako na matendo yako.

22. Sababu gani unajifunza Biblia, na unaweza kusaidiaje wengine waelewe jambo hili?

22 Marafiki na watu wa ukoo wenye nia njema huenda wakapinga funzo lako la Biblia, lakini Yesu alisema hivi: “Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 10:32, 33) Huenda wengine wakahofu kwamba wewe utajihusisha na kidhehebu au utakuwa mshupavu wa dini. Hata hivyo, kwa halisi, unajitahidi tu kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu na juu ya kweli yake. (1 Timotheo 2:3, 4) Ili kusaidia wengine waelewe jambo hilo, uwe mwenye kukubali sababu, si mwenye kubishana, unapoongea nao juu ya yale unayojifunza. (Wafilipi 4:5) Kumbuka kwamba wengi ‘wanavutwa pasipo lile Neno’ wanapoona uthibitisho wa kwamba ujuzi wa Biblia hunufaisha watu kwelikweli.—1 Petro 3:1, 2.

23. Unaweza ‘kufanyizaje hamu sana’ ya ujuzi juu ya Mungu?

23 Biblia hutuhimiza hivi: “Kama watoto wachanga sana waliozaliwa karibuni, fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya lile neno.” (1 Petro 2:2, NW) Kitoto kichanga hutegemea lishe kutoka kwa mama yacho na husisitiza kutimiziwa uhitaji huo. Vivyo hivyo, sisi tunategemea ujuzi kutoka kwa Mungu. ‘Fanyiza hamu sana’ ya Neno lake kwa kuendeleza funzo lako. Ndiyo, fanya lengo lako liwe kusoma Biblia kila siku. (Zaburi 1:1-3) Hilo litakuletea baraka tele, kwani Zaburi 19:11 yasema hivi juu ya sheria za Mungu: “Katika kuzishika kuna thawabu nyingi.”

[Maelezo ya Chini]

a Ufupisho K.W.K. humaanisha “kabla ya Wakati wa Kawaida,” ambao ni sahihi zaidi kuliko K.K. (“kabla ya Kristo”). Ufupisho W.K. humaanisha “Wakati wa Kawaida,” ambao mara nyingi huitwa A.D., kwa anno Domini, ikimaanisha “katika mwaka wa Bwana wetu.”

TAHINI UJUZI WAKO

Ni kwa njia zipi Biblia si kama kitabu kingine chochote?

Sababu gani unaweza kuitumaini Biblia?

Ni nini kinachokuthibitishia kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa?

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

TUMIA BIBLIA YAKO VIZURI

Kuizoelea Biblia hakuhitaji kuwa jambo gumu. Tumia jedwali yayo ya yaliyomo ili ujifunze utaratibu na mahali pa vitabu vya Biblia.

Vitabu vya Biblia vina sura na mistari ili iwe rahisi kufanya marejezeo. Migawanyo ya sura iliongezwa wakati wa karne ya 13 na yaonekana kwamba mpiga-chapa Mfaransa wa karne ya 16 ndiye aliyegawanya Maandiko ya Kigiriki katika mistari. Biblia kamili ya kwanza kuwa na nambari za sura na mistari pia ilikuwa chapa ya Kifaransa iliyochapishwa katika 1553.

Maandiko yanapotajwa katika kitabu hiki, nambari ya kwanza inaonyesha sura na nambari ifuatayo inaonyesha mstari. Kwa kielelezo, mtajo wa “Mithali 2:5” wamaanisha kitabu cha Mithali, sura ya 2, mstari wa 5. Kwa kufungua maandiko yaliyotajwa, upesi utaona ni rahisi kupata maandiko ya Biblia.

Njia bora zaidi ya kuizoelea Biblia ni kuisoma kila siku. Mwanzoni huenda hilo likaonekana kuwa jambo gumu. Lakini ukisoma sura tatu hadi tano tu kwa siku, ikitegemea urefu wazo, utakamilisha usomaji wa Biblia yote kwa mwaka mmoja. Sababu gani usianze leo?

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

BIBLIA—KITABU KISICHO NA KIFANI

• Biblia ni ‘yenye pumzi ya Mungu.’ (2 Timotheo 3:16) Ingawa wanadamu waliyaandika maneno, Mungu alielekeza mawazo yao, hivi kwamba Biblia kwa kweli ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

• Biblia iliandikwa kwa kipindi cha karne 16, na wachangaji wapatao 40 kutoka malezi tofauti. Hata hivyo, Biblia yote ni yenye upatano kutoka mwanzo hadi mwisho.

• Biblia imeokoka ubishi mwingi zaidi kuliko kitabu kingine chochote. Wakati wa Enzi za Kati, wengi waliteketezwa kwenye mti kwa sababu tu ya kuwa na nakala ya Maandiko.

• Biblia ni kitabu maarufu kinachouzwa zaidi ulimwenguni. Imetafsiriwa, ikiwa yote au kwa sehemu, katika lugha zaidi ya 2,000. Maelfu ya mamilioni ya nakala yamechapishwa, na karibu hakuna mahali duniani ambapo nakala haiwezi kupatikana.

• Sehemu ya Biblia iliyo ya zamani zaidi ni ile ya tarehe ya tangu karne ya 16 K.W.K. Hiyo ni kabla ya kutokea kwa Rig-Veda ya Kihindu (katika karibu 1300 K.W.K.), au “Kanuni ya Vikapu Vitatu” ya Kibuddha (karne ya tano K.W.K.), au Qurani ya Kiislamu (karne ya saba W.K.), na pia Nihongi ya Kishinto (720 W.K.).

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 20]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki