Somo la 6
Ufalme wa Mungu Ni Nini?
Ufalme wa Mungu uko wapi? (1)
Mfalme wao ni nani? (2)
Je, wengine hushiriki katika kutawala pamoja na Mfalme? Ikiwa ndivyo, ni wangapi? (3)
Ni nini kionyeshacho kwamba tunaishi katika siku za mwisho? (4)
Ufalme wa Mungu utawafanyia nini wanadamu wakati ujao? (5-7)
1. Alipokuwa duniani, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake waombe Ufalme wa Mungu uje. Ufalme ni serikali iongozwayo na mfalme. Ufalme wa Mungu ni serikali ya pekee. Umesimamishwa mbinguni nao utatawala juu ya dunia hii. Utatakasa, au kulifanya takatifu, jina la Mungu. Utasababisha mapenzi ya Mungu yafanywe duniani kama yalivyofanywa mbinguni.—Mathayo 6:9, 10.
2. Mungu aliahidi kwamba Yesu angekuwa Mfalme wa Ufalme Wake. (Luka 1:30-33) Yesu alipokuwa duniani, alithibitisha kwamba angekuwa Mtawala mwenye fadhili, mwenye haki, na mkamilifu. Aliporudi mbinguni, yeye hakutawazwa awe Mfalme wa Ufalme wa Mungu mara moja. (Waebrania 10:12, 13) Katika 1914, Yehova alimpa Yesu mamlaka ambayo Yeye alikuwa amemwahidi. Tangu wakati huo, Yesu ametawala mbinguni akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova.—Danieli 7:13, 14.
3. Yehova ameteua pia baadhi ya wanaume na wanawake waaminifu kutoka duniani ili waende mbinguni. Wao watatawala pamoja na Yesu wakiwa wafalme, mahakimu, na makuhani juu ya wanadamu. (Luka 22:28-30; Ufunuo 5:9, 10) Yesu aliwaita hao watawala wenzake katika Ufalme wake “kundi dogo.” Hesabu yao ni 144,000.—Luka 12:32; Ufunuo 14:1-3.
4. Mara Yesu alipokuwa Mfalme, alimtupa Shetani na malaika wake waovu kutoka mbinguni na chini kwenye eneo la dunia. Hiyo ndiyo sababu kwa nini mambo yamekuwa mabaya sana hapa duniani tangu 1914. (Ufunuo 12:9, 12) Vita, njaa kuu, magonjwa ya kuambukiza, uasi-sheria wenye kuongezeka—yote haya ni sehemu ya “ishara” ionyeshayo kwamba Yesu anatawala na kwamba mfumo huu umo katika siku zao za mwisho.—Mathayo 24:3, 7, 8, 12; Luka 21:10, 11; 2 Timotheo 3:1-5.
5. Karibuni Yesu atahukumu watu, akiwatenganisha kama vile mchungaji hutenganisha kondoo kutoka kwa mbuzi. “Kondoo” ni wale watakaokuwa wamejithibitisha wenyewe kuwa raia zake waaminifu-washikamanifu. Watapokea uhai udumuo milele duniani. “Mbuzi” ni wale watakaokuwa wameukataa katakata Ufalme wa Mungu. (Mathayo 25:31-34, 46) Karibuni sana, Yesu ataharibu wote wenye mfano wa mbuzi. (2 Wathesalonike 1:6-9) Ikiwa wewe wataka kuwa mmoja wa “kondoo” wa Yesu, ni lazima usikilize ujumbe wa Ufalme na kutenda kulingana na yale unayojifunza.—Mathayo 24:14.
6. Sasa dunia imegawanywa-gawanywa kuwa nchi nyingi. Kila moja ina serikali yayo yenyewe. Mara nyingi mataifa haya hupigana. Lakini Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. Utatawala ukiwa serikali pekee juu ya dunia nzima. (Danieli 2:44) Kisha hakutakuwa tena na vita, uhalifu, na jeuri. Watu wote wataishi pamoja katika amani na muungano.—Mika 4:3, 4.
7. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu, wanadamu waaminifu watakuwa wakamilifu, na dunia nzima itakuwa paradiso. Kufikia mwisho wa miaka elfu, Yesu atakuwa amefanya kila jambo ambalo Mungu amemwomba afanye. Kisha ataurudisha Ufalme kwa Baba yake. (1 Wakorintho 15:24) Kwa nini usiwaambie marafiki na wapendwa wako juu ya yale ambayo Ufalme wa Mungu utafanya?
[Picha katika ukurasa wa 13]
Chini ya utawala wa Yesu, hakutakuwa tena na chuki wala ubaguzi