Somo la 9
Ni Lazima Watumishi wa Mungu Wawe Safi
Kwa nini tuwe safi katika kila njia? (1)
Inamaanisha nini kuwa safi kiroho? (2) safi kiadili? (3) safi kiakili? (4) safi kimwili? (5)
Ni usemi wa aina gani usio safi tupaswao kuepuka? (6)
1. Yehova Mungu ni safi na mtakatifu. Yeye huwatazamia waabudu wake waendelee kuwa safi—kiroho, kiadili, kiakili, na kimwili. (1 Petro 1:16) Jitihada nyingi yatakiwa ili tuendelee tukiwa safi machoni pa Mungu. Twaishi katika ulimwengu usio safi. Pia tuna shindano dhidi ya mielekeo yetu wenyewe ya kufanya mabaya. Lakini ni lazima tusife moyo.
2. Usafi wa Kiroho: Ikiwa twataka kumtumikia Yehova, hatuwezi kuendelea kushikamana na mafundisho au desturi zozote za dini bandia. Ni lazima tutoke katika dini bandia na tusiiunge mkono kwa njia yoyote ile. (2 Wakorintho 6:14-18; Ufunuo 18:4) Mara tujifunzapo kweli kumhusu Mungu, ni lazima tuwe waangalifu tusije tukaongozwa vibaya na watu wafundishao uwongo.—2 Yohana 10, 11.
3. Usafi wa Kiadili: Yehova awataka waabudu wake wajiendeshe wakiwa Wakristo wa kweli nyakati zote. (1 Petro 2:12) Yeye huona kila jambo tufanyalo, hata sirini. (Waebrania 4:13) Twapaswa kuepuka ukosefu wa adili katika ngono na mazoea mengine yasiyo safi ya ulimwengu huu.—1 Wakorintho 6:9-11.
4. Usafi wa Kiakili: Tukizijaza akili zetu mawazo yaliyo safi, yaliyotakata, mwenendo wetu utakuwa safi pia. (Wafilipi 4:8) Lakini tukifikiria mambo yasiyo safi, hilo litatokeza matendo maovu. (Mathayo 15:18-20) Twapaswa kuepuka namna za vitumbuizo ambazo zingeweza kuzichafua akili zetu. Twaweza kujaza akili zetu mawazo yaliyo safi kwa kujifunza Neno la Mungu.
5. Usafi wa Kimwili: Kwa sababu wanamwakilisha Mungu, Wakristo wapaswa waweke miili na mavazi yao yakiwa safi. Twapaswa kuosha mikono yetu baada ya kutumia choo, na twapaswa kuiosha kabla ya kula milo au kushika chakula. Ikiwa huna bomba lifaalo la kuondoshea uchafu, kinyesi kutoka chooni chapasa kuzikwa. (Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Kudumisha usafi kimwili huchangia afya njema. Nyumba ya Mkristo yapaswa iwe nadhifu na safi ndani na nje pia. Yapaswa itokeze katika jumuiya ikiwa kielelezo chema.
6. Usemi Ulio Safi: Ni lazima watumishi wa Mungu waseme kweli sikuzote. Waongo hawatauingia Ufalme wa Mungu. (Waefeso 4:25; Ufunuo 21:8) Wakristo hawatumii lugha mbaya. Hawasikilizi wala kusimulia ucheshi mchafu au hadithi zisizo safi. Kwa sababu ya usemi wao ulio safi, wao hutokeza kuwa tofauti kazini au shuleni na katika ujirani.—Waefeso 4:29, 31; 5:3.
[Picha katika ukurasa wa 18, 19]
Ni lazima watumishi wa Mungu wawe safi katika mambo yote