Tumaini Hakika
“Tangu wakati wa kuzaliwa kuna ule uwezekano usiobadilika kwamba mwanadamu huenda akafa wakati wowote ule; na kwa njia isiyoepukika uwezekano huo unakuja kuwa jambo lenye kutimia.”—ARNOLD TOYNBEE, MWANAHISTORIA MUINGEREZA.
1. Wanadamu wamelazimika kukubali uhakika gani, na huo ukitokeza maulizo gani?
NANI awezaye kubishana na kweli ya kihistoria isiyotiliwa shaka inayotajwa hapo juu? Sikuzote wanadamu wamelazimika kukubali uhakika wenye kutia hofu wa kifo. Na wakati mtu fulani tumpendaye anapokufa tunajisikia kuwa wasioweza kufanya lolote ili kusaidia! Kupoteza huko kunaonekana kusikobadilishwa kabisa. Je! yawezekana kuungana tena na wapendwa wetu waliokufa? Biblia hutoa tumaini gani kwa wafu? Tazama habari inayofuata.
‘Rafiki Yetu Amekufa’
2-5. (a) Rafiki yake Lazaro alipokufa, namna gani Yesu alionyesha kutaka kwake na uwezo wa kumfufua? (b) Zaidi ya kumrudisha Lazaro kwenye uhai, muujiza wa ufufuo ulitimiza nini?
2 Ulikuwa ni mwaka 32 W.K. Katika mji mdogo wa Bethania, kilomita 3 nje ya Yerusalemu, waliishi Lazaro pamoja na dada zake Martha na Maria. Walikuwa marafiki wa karibu wa Yesu. Siku moja, Lazaro akawa mgonjwa sana. Bila kukawia, dada zake wenye kusikitishwa wakatuma habari hiyo kwa Yesu, akiwa ngambo ya Mto Yordani. Yesu alikuwa na shauku kuelekea Lazaro na dada zake, hivyo baadaye akaondoka kuelekea Bethania. Wakiwa njiani, Yesu akawambia wanafunzi wake: “Lazaro rafiki yetu ameenda kupumzika, lakini ninafunga safari huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” Kwa kuwa wanafunzi hawakufahamu mara moja maana ya habari hiyo, Yesu akawaambia waziwazi: “Lazaro amekufa.”—Yohana 11:1-15.
3 Waliposikia kwamba Yesu alikuwa akija Bethania, Martha alienda mbio nje kukutana naye. Akiguswa na sikitiko lake, Yesu akamhakikishia: “Ndugu yako atainuka.” Martha akamjibu: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” Basi Yesu akamwambia: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.”—Yohana 11:20-25.
4 Ndipo Yesu akaenda kwenye kaburi na akaagiza kwamba jiwe lililofunga kiingilio liondolewe mbali. Kisha kusali kwa sauti kubwa, akaamuru: “Lazaro, njoo huku nje!” Na macho ya wote yakiwa yamekaziwa kwenye kaburi, Lazaro kwa kweli akaja nje. Yesu alimfufua Lazaro—akirudisha uhai kwa mwanamume aliyekuwa amekuwa mfu kwa siku nne!—Yohana 11:38-44.
5 Tayari Martha alikuwa na imani katika ahadi ya ufufuo. (Yohana 5:28, 29; 11:23, 24) Muujiza wa kurudishwa kwa Lazaro kwenye uhai ulisaidia kutia nguvu imani yake na kuingiza imani katika wengine. (Yohana 11:45) Lakini, kwa usahihi neno “ufufuo” lamaanisha nini?
“Atainuka”
6. Neno “ufufuo” lamaanisha nini?
6 Neno “ufufuo” latafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki a·naʹsta·sis, ambalo kwa njia halisi lamaanisha “kusimama wima tena.” Watafsiri Waebrania wa Kigiriki walitafsiri a·naʹsta·sis wakitumia maneno ya Kiebrania techi·yathʹ ham·me·thimʹ, yanayomaanisha “kuamka kwa wafu.”a Hivyo, ufufuo hutia ndani kuinua mtu kutoka katika hali isiyo ya uhai ya kifo—kurudisha tena kigezo cha uhai cha mtu.
7. Kwa nini ufufuo wa watu hautatokeza tatizo hata moja kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo?
7 Akiwa mwenye hekima isiyo na mwisho na mkamilifu katika kumbukumbu, Yehova Mungu aweza kwa urahisi kumfufua mtu. Kukumbuka kigezo cha uhai wa watu waliokufa—tabia za nyutu zao, historia ya maisha yao, na mambo yote yanayowatambulisha—si tatizo kwake. (Yobu 12:13; linganisha Isaya 40:26.) Yehova pia ndiye Chanzo cha uhai. Kwa hiyo, yeye aweza kwa urahisi kurudisha kwenye uhai mtu yuleyule, akimpa utu uleule katika mwili wenye muundo mpya. Tena, kama inavyoonyeshwa na jambo lililompata Lazaro, Yesu Kristo ni mwenye kutaka na mwenye uwezo wa kufufua wafu.—Linganisha Luka 7:11-17; 8:40-56.
8, 9. (a) Kwa nini ufufuo haupatani na wazo la kutoweza kufa kwa nafsi? (b) Ni nini dawa ya kifo?
8 Hata hivyo, fundisho la Kimaandiko kuhusu ufufuo ni lisilopatana na fundisho la kutoweza kufa kwa nafsi. Ikiwa nafsi isiyoweza kufa inaokoka kifo, hakuna yeyote angehitaji kufufuliwa au kurudishwa kwenye uhai. Kwa kweli, Martha hakuonyesha wazo lolote kuhusu nafsi isiyoweza kufa ambayo ilikuwa ikiendelea kuishi mahali fulani baada ya kifo. Yeye hakuamini kwamba Lazaro alikuwa tayari amekwenda kwenye makao fulani ya kiroho na kuendelea kuishi huko. Tofauti na hilo, alionyesha imani yake katika kusudi la Mungu la kupindua matokeo ya kifo. Yeye alisema: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Vivyo hivyo, Lazaro mwenyewe hakueleza kuwa amewahi kuona jambo lolote katika maisha ya baada ya kifo. Hakukuwa jambo lolote la kuripoti.
9 Hakuna shaka, kulingana na Biblia, nafsi hufa na dawa kwa kifo ni ufufuo. Lakini maelfu ya mamilioni ya watu wamekuwa wakikufa tangu kuwako duniani kwa mtu wa kwanza, Adamu. Basi, ni nani atakayefufuliwa na wapi?
‘Wote Waliomo Ndani ya Makaburi ya Ukumbusho’
10. Ni ahadi gani Yesu alitoa kuhusiana na wale walio katika makaburi ya ukumbusho?
10 Yesu Kristo alisema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ndiyo, Yesu Kristo aliahidi kwamba wote wale walio katika kumbukumbu la Yehova watafufuliwa. Maelfu ya mamilioni ya watu wameishi na kufa. Nani kati yao aliye katika kumbukumbu la Mungu, akingojea ufufuo?
11. Nani watakaofufuliwa?
11 Wale ambao wamefuatilia mwendo wa uadilifu kama watumishi wa Yehova watafufuliwa. Lakini mamilioni ya watu wengine wamekufa bila kuonyesha ikiwa wangeweza kukubali viwango vya uadilifu vya Mungu. Walikuwa ama wasiojua matakwa ya Yehova, ama walikosa wakati wa kutosha kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa. Hawa pia wamo katika kumbukumbu la Mungu na kwa hiyo watafufuliwa, kwa kuwa Biblia yaahidi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.
12. (a) Ni mwono gani mtume Yohana alipata kuhusu ufufuo? (b) Nini “huvurumishwa katika ziwa la moto,” na usemi huo unamaanisha nini?
12 Mtume Yohana alipata ono lenye kusisimua la waliofufuliwa wakisimama mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu. Akieleza jambo hilo, yeye aliandika: “Nayo bahari ikawatoa hao wafu waliokuwa ndani yayo, na kifo na Hadesi vikawatoa wafu ndani yavyo, nao walihukumiwa mmoja-mmoja kulingana na vitendo vyao. Na kifo na Hadesi vikavurumishwa ndani ya ziwa la moto. Hili humaanisha kifo cha pili, ziwa la moto.” (Ufunuo 20:12-14) Fikiria kile ambacho jambo hilo humaanisha! Wafu wote walio katika kumbukumbu la Mungu watafunguliwa kutoka katika Hadesi, au Sheoli, kaburi la kawaida la wanadamu. (Zaburi 16:10; Matendo 2:31) Ndipo “kifo na Hadesi” vitavurumishwa ndani ya kile kinachoitwa “ziwa la moto,” likimaanisha uharibifu kamili. Kaburi la kawaida la wanadamu litakoma kuwapo.
Kufufuliwa Wapi?
13. Kwa nini Mungu alipangia wengine kwamba wafufuliwe kwenda mbinguni, na Yehova atawapatia mwili wa aina gani?
13 Hesabu ndogo ya wanaume na wanawake watafuliwa kwenye uzima mbinguni. Hao watatawala pamoja na Kristo wakiwa wafalme na makuhani na watashiriki katika kuangamiza matokeo yote ya kifo ambacho wanadamu walirithi kutoka mtu wa kwanza, Adamu. (Waroma 5:12; Ufunuo 5:9, 10) Kulingana na Biblia, wahesabiwa kuwa 144,000 tu na wamechaguliwa kutoka miongoni mwa wafuasi wa Kristo, kuanzia mitume waaminifu. (Luka 22:28-30; Yohana 14:2, 3; Ufunuo 7:4; 14:1, 3) Yehova atapatia kila mmoja wa hao watakaofufuliwa mwili wa kiroho hivi kwamba waweze kuishi mbinguni.—1 Wakorintho 15:35, 38, 42-45; 1 Petro 3:18.
14, 15. (a) Walio wengi zaidi kati ya hao waliokufa watafufuliwa kwenye uhai wa aina gani? (b) Wanadamu watiifu wataziona baraka gani?
14 Lakini, walio wengi zaidi ya wale waliokufa watafufuliwa kwenye uhai duniani. (Zaburi 37:29; Mathayo 6:10) Dunia ya aina gani? Leo dunia inajaa ugomvi, umwagaji-damu, uharibifu wa mazingira, na jeuri. Ikiwa wafu wangepaswa kurudi kwenye uhai katika dunia kama hiyo, hakika furaha yoyote ingekuwa ya muda mfupi tu. Lakini Muumba ameahidi kwamba karibuni ataleta kwenye mwisho jamii ya ulimwengu ya sasa ambayo ni chini ya uongozi wa Shetani. (Mezali 2:21, 22; Danieli 2:44) Jamii mpya ya watu yenye uadilifu—“dunia mpya”— itakuwa hivyo jambo halisi. (2 Petro 3:13) Wakati huo “hapana mwenyeji atakayesema, mimi ni mugonjwa.” (Isaya 33:24) Hata uchungu wa kifo utaondolewa, kwa sababu Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.
15 Katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu, wapole “watajifurahisha katika wingi wa salama.” (Zaburi 37:11) Serikali ya kimbinguni ya Kristo Yesu na washiriki wenzake 144,000 watarudisha polepole wanadamu watiifu kwenye ukamilifu ambao wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walipoteza. Kati ya wakaaji wa dunia mtakuwamo pia wale watakaofufuliwa.—Luka 23:42, 43.
16-18. Ufufuo utaletea familia shangwe gani?
16 Biblia yatoa mwono mdogo wa furaha ambayo ufufuo utaletea familia. Fikiria furaha aliyohisi yule mjane wa Naini wakati Yesu aliposimamisha andamano la mazishi na kumfufua mwana wake pekee! (Luka 7:11-17) Baadaye, karibu na Ziwa la Galilaya, wakati Yesu alipomrudisha binti mwenye umri wa miaka 12 kwenye uhai, wazazi wake “wakapigwa na bumbuazi ya upeo wa shangwe kubwa.”—Marko 5:21-24, 35-42; tazama pia 1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37.
17 Kuhusu mamilioni wanaolala sasa katika kifo, ufufuo utamaanisha uhai katika ulimwengu mpya wenye amani. Fikiri kidogo juu ya tazamio lenye kusisimua ambalo jambo hilo hufungulia Tommy na mfanyabiashara, waliotajwa katika sehemu ya kwanza ya broshua hii! Tommy aamkapo kwenye uhai katika Paradiso duniani, atakuwa ni Tommy yuleyule ambaye mamaye alijua—lakini pasipo magonjwa. Atakuwa na uwezekano wa kumgusa, kumshika katika mikono yake, na kumpenda. Vilevile, pahali pa kunaswa katika karibu duara isiyo na mwisho ya kuzaliwa upya tena na tena, yule mfanyabiashara kutoka India analo tazamio la ajabu la kufungua macho yake akiwa katika ulimwengu mpya wa Mungu na kuwatazama wana wake.
18 Kujua kweli kuhusu nafsi, kuhusu jambo linalotufikia tunapokufa, na kuhusu tumaini la ufufuo kunaweza pia kuwa na matokeo yenye kina juu ya wale wanaoishi sasa. Acheni tuone namna hilo linavyokuwa na matokeo hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Huku neno “ufufuo” likiwa halipatikani katika Maandiko ya Kiebrania, tumaini la ufufuo linaonyeshwa wazi kwenye Yobu 14:13, Danieli 12:13, na Hosea 13:14.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Ufufuo utaleta shangwe yenye kudumu