Sura ya 24
Ulimwengu Huu Hauna Msaada
1, 2. (a) Kwa nini wakazi wa Yerusalemu wamejaa hofu? (b) Kwa sababu ya hali mbaya ya Yerusalemu, ni maswali gani yanayozuka?
WAKAZI wa Yerusalemu wamejaa hofu—na kuna sababu ya kuhofu! Ashuru, milki yenye nguvu kuliko zote wakati huo, imeshambulia “miji yote ya Yuda yenye maboma, akaitwaa.” Na sasa majeshi ya Ashuru yanatishia jiji kuu la Yuda. (2 Wafalme 18:13, 17) Mfalme Hezekia na wakazi wengine wa Yerusalemu watafanyaje?
2 Kwa kuwa tayari miji mingine nchini mwake imeanguka, Hezekia ajua kuwa Yerusalemu haliwezi kushindana na jeshi la Ashuru lenye nguvu. Isitoshe, Waashuri wajulikana sana kuwa watu wenye ukatili na ujeuri usio na kifani. Jeshi la nchi hiyo ni lenye kutia hofu sana hivi kwamba nyakati nyingine wapinzani wao hukimbia bila hata kupigana! Kwa sababu ya hali mbaya ya Yerusalemu, wakazi wake waweza kupata msaada wapi? Kuna njia yoyote ya kuponyoka jeshi la Ashuru? Na je, watu wa Mungu walipataje kuingia katika hali hiyo? Ili kujibu maswali hayo, twapaswa kutazama nyuma na tuone jinsi Yehova alivyolitendea taifa lake la agano katika miaka ya mapema.
Uasi Katika Israeli
3, 4. (a) Taifa la Israeli liligawanyika kuwa falme mbili lini na jinsi gani? (b) Yeroboamu aliupa ufalme wa kaskazini wa makabila kumi mwanzo gani mbaya?
3 Tangu Israeli ilipotoka Misri hadi kifo cha Solomoni mwana wa Daudi—kipindi cha miaka inayozidi kidogo 500—yale makabila 12 ya Israeli yalikuwa yameungana yakawa taifa moja. Baada ya kifo cha Solomoni, Yeroboamu alifanya makabila kumi ya kaskazini yaasi nyumba ya Daudi, na tangu wakati huo na kuendelea taifa hilo likagawanyika kuwa falme mbili. Hayo yalitukia mwaka wa 997 K.W.K.
4 Yeroboamu alikuwa mfalme wa kwanza wa ufalme wa kaskazini wa Israeli, naye aliwaongoza raia zake kwenye uasi kwa kuondoa ukuhani wa Aroni na ibada halali ya Yehova na badala yake kuweka ukuhani haramu na mfumo wa ibada ya ndama. (1 Wafalme 12:25-33) Hayo yalimchukiza sana Yehova. (Yeremia 32:30, 35) Kwa sababu hiyo na nyinginezo, aliiruhusu Ashuru iitiishe Israeli. (2 Wafalme 15:29) Mfalme Hoshea alijaribu kuvunja nira ya Ashuru kwa kupanga njama na Misri, lakini njama hiyo haikufaulu.—2 Wafalme 17:4.
Israeli Yaendea Kimbilio Lisilo la Kweli
5. Israeli yamwendea nani ili kupata msaada?
5 Yehova ataka kuwafanya Waisraeli warudiwe na fahamu zao.a Kwa hiyo amtuma nabii Isaya atoe onyo hili: “Ole wao watelemkao kwenda Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti BWANA!” (Isaya 31:1) Yahuzunisha kama nini! Israeli yatumaini zaidi farasi na magari ya vita kuliko inavyomtumaini Mungu aliye hai, Yehova. Kwa maoni ya kimwili ya Israeli, farasi za Misri ni wengi na wenye nguvu. Kwa hakika Misri itakuwa mshirika anayefaa dhidi ya jeshi la Ashuru! Hata hivyo, karibuni Waisraeli watatambua kwamba kuungana kwao na Misri hakufai kitu.
6. Kwa nini hatua ya Israeli kuiendea Misri yaonyesha ukosefu mbaya sana wa imani katika Yehova?
6 Wakazi wa Israeli na Yuda wamejiweka wakfu kwa Yehova kupitia agano la Sheria. (Kutoka 24:3-8; 1 Mambo ya Nyakati 16:15-17) Kwa kuiendea Misri kupata msaada, Israeli yaonyesha ukosefu wa imani katika Yehova na upuuzaji wa sheria zilizo sehemu ya agano takatifu. Kwa nini? Sababu ni kwamba ndani ya masharti ya agano hilo mna ahadi ya Yehova ya kuwalinda watu wake iwapo wampa ujitoaji usiohusisha wengine. (Mambo ya Walawi 26:3-8) Kupatana na ahadi hiyo, Yehova amethibitika tena na tena kuwa ‘ngome wakati wa taabu.’ (Zaburi 37:39; 2 Mambo ya Nyakati 14:2, 9-12; 17:3-5, 10) Zaidi ya hayo, kupitia Musa mpatanishi wa agano la Sheria, Yehova aliwaambia wale ambao wangekuwa wafalme wa Israeli wakati ujao wasifanye farasi zao kuwa wengi. (Kumbukumbu la Torati 17:16) Kutii kanuni hiyo kungeonyesha kuwa wafalme hao wanamtegemea “Mtakatifu wa Israeli” awalinde. Kwa kusikitisha, watawala wa Israeli hawana imani ya aina hiyo.
7. Wakristo leo waweza kujifunza nini kutokana na ukosefu wa imani wa Israeli?
7 Hilo ni fundisho kwa Wakristo leo. Israeli ilitafuta utegemezo unaoonekana kutoka Misri badala ya utegemezo wenye nguvu zaidi ambao Yehova huandaa. Vivyo hivyo leo, huenda Wakristo wakashawishiwa kuvitumainia vyanzo vya kimwili vya usalama—akaunti za benki, vyeo vya kijamii, urafiki katika ulimwengu—badala ya kumtumainia Yehova. Ni kweli kwamba vichwa vya familia za Kikristo huchukua kwa uzito wajibu wao wa kuandalia familia zao vitu vya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, hawaweki tumaini lao katika vitu vya kimwili. Nao hujilinda dhidi ya “kila namna ya tamaa.” (Luka 12:13-21) Yehova Mungu peke yake ndiye “ngome kwa nyakati za shida.”—Zaburi 9:9; 54:7.
8, 9. (a) Ingawa huenda mipango ya Israeli ikaonekana kuwa yenye busara, matokeo yatakuwaje, na kwa nini? (b) Kuna tofauti gani kati ya ahadi za binadamu na ahadi za Yehova?
8 Isaya sasa awadhihaki viongozi wa Israeli waliofanya mapatano na Misri, akisema: “Yeye naye ana akili, naye ataleta uovu, wala hatayatangua maneno yake; bali ataondoka juu ya nyumba yao watendao mabaya, na juu ya msaada wa hao watendao maovu.” (Isaya 31:2) Huenda viongozi wa Israeli wakadhani kwamba wana hekima. Lakini je, Muumba wa ulimwengu wote si mwenye hekima kwa njia kuu? Ni kana kwamba njama ya Israeli ya kutafuta msaada kutoka Misri ni yenye busara. Ingawa hivyo, kufanya mwungano wa kisiasa kama huo ni uzinzi wa kiroho machoni pa Yehova. (Ezekieli 23:1-10) Kwa hiyo, Isaya asema kwamba Yehova “ataleta uovu.”
9 Kwa jumla, ahadi za binadamu hazitegemeki, na ulinzi wa binadamu sio hakika. Kwa upande mwingine, Yehova hahitaji ‘kuyatangua maneno yake.’ Bila shaka yeye atafanya mambo anayoahidi. Neno lake halimrudii bure.—Isaya 55:10, 11; 14:24.
10. Ni nini kitakachozipata Misri na Israeli?
10 Je, Wamisri watathibitika kuwa ulinzi unaotegemeka kwa Israeli? La. Isaya aambia Israeli: “Basi Wamisri ni wanadamu wala si Mungu, na farasi zao ni nyama wala si roho; na BWANA atakaponyosha mkono wake, yeye asaidiaye atajikwaa, na yeye asaidiwaye ataanguka, nao wote pamoja watakoma.” (Isaya 31:3) Asaidiaye (Misri) naye asaidiwaye (Israeli) watajikwaa, waanguke, na kukomeshwa wakati Yehova anyoshapo mkono wake ili kutekeleza hukumu yake kwa kutumia Ashuru.
Kuanguka kwa Samaria
11. Israeli imefanya dhambi gani nyingi, na hatimaye matokeo yatakuwa nini?
11 Kutokana na rehema yake, Yehova awatuma manabii wake tena na tena ili waitie moyo Israeli itubu na kurudia ibada safi. (2 Wafalme 17:13) Licha ya hayo, Israeli yaongeza dhambi yake ya ibada ya ndama kwa kushiriki katika uaguzi, ibada ya Baali isiyo ya adili, na utumizi wa nguzo takatifu na mahali pa juu. Waisraeli hata ‘wawapitisha watoto wao, waume na wake, motoni,’ wakidhabihu uzao wao wenyewe kwa miungu ya mashetani. (2 Wafalme 17:14-17; Zaburi 106:36-39; Amosi 2:8) Ili kuukomesha uovu wa Israeli, Yehova aagiza hivi: “Mfalme wa Samaria atachukuliwa, kama kipande cha mti juu ya maji.” (Hosea 10:1, 7, BHN) Majeshi ya Ashuru yashambulia Samaria jiji kuu la Israeli, mwaka wa 742 K.W.K. Baada ya mazingiwa ya miaka mitatu, Samaria laanguka, na mwaka wa 740 K.W.K., ufalme huo wa makabila kumi wakomeshwa.
12. Yehova ametoa utume wa kazi gani leo, na wale wanaopuuza onyo hilo watapatwa na nini?
12 Leo, Yehova ametoa utume wa kazi ya kuhubiri ulimwenguni kote ili kuwaonya “wanadamu kwamba wapaswa wote kila mahali kutubu.” (Matendo 17:30; Mathayo 24:14) Wale wanaoikataa njia ya Mungu ya wokovu watakuwa kama “kipande cha mti,” wataharibiwa kama taifa la Israeli lenye kuasi. Kwa upande mwingine, wale wanaomtumaini Yehova “watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Basi ni jambo lenye hekima kama nini tuepuke makosa ya ufalme wa kale wa Israeli! Na tumtumaini Yehova kwa ukamilifu ili tupate wokovu.
Nguvu ya Yehova ya Kuokoa
13, 14. Yehova aambia Sayuni maneno gani yenye kufariji?
13 Yerusalemu, jiji kuu la Yuda, liko kilometa chache kutoka kwenye mpaka wa kusini wa Israeli. Wakazi wa Yerusalemu wanafahamu vema sana mambo ambayo yameikumba Samaria. Sasa wanajikuta katika hali ya kutishwa na adui yuleyule mwenye kutia hofu aliyekomesha jirani yao wa kaskazini. Je, watajifunza kutokana na maafa ya Samaria?
14 Maneno ya Isaya yanayofuata yawafariji wakazi wa Yerusalemu. Yeye awahakikishia kuwa Yehova bado anawapenda watu wake wa agano, akisema: “BWANA aniambia hivi, Kama vile ilivyo simba angurumapo na mwana-simba juu ya mawindo yake, wachungaji wengi wakiitwa ili kumpiga, lakini hatiwi hofu na sauti zao, wala kufanya woga kwa sababu ya mshindo wao; ndivyo BWANA wa majeshi atakavyoshuka ili kufanya vita juu ya mlima Sayuni, na juu ya kilima chake.” (Isaya 31:4) Kama vile mwana-simba anayesimama juu ya mawindo yake, ndivyo Yehova atakavyolilinda kwa uangalifu jiji lake takatifu, Sayuni. Maneno yoyote yenye majivuno, wala yenye vitisho, wala rabsha nyingine zozote za vikosi vya wanajeshi wa Ashuru hazitamgeuza Yehova asitimize kusudi lake.
15. Yehova awatendeaje wakazi wa Yerusalemu kwa wororo na huruma?
15 Ona sasa jinsi Yehova atakavyowatendea wakazi wa Yerusalemu kwa wororo na huruma: “Kama ndege warukao, BWANA wa majeshi ataulinda Yerusalemu; ataulinda na kuuokoa, atapita juu yake na kuuhifadhi.” (Isaya 31:5) Ndege wa kike huwa mwangalifu nyakati zote kulinda watoto wake. Yeye huruka kwa mbawa zilizonyoshwa juu ya makinda yake, naye hutazama kwa macho makali dalili zozote za hatari. Mwindaji akikaribia, yeye hushuka haraka ili kuyalinda makinda yake. Vivyo hivyo, Yehova atawatunza kwa wororo wakazi wa Yerusalemu kwa sababu ya Waashuri wanaovamia.
“Rudini, Enyi Watu”
16. (a) Yehova awatolea watu wake sihi gani yenye upendo? (b) Uasi wa watu wa Yuda unakuwa wazi zaidi lini? Eleza.
16 Yehova sasa awakumbusha watu wake kwamba wamefanya dhambi naye awatia moyo waache njia zao zenye makosa: “Mwelekeeni yeye [“rudini, enyi watu, kwa Yule,” “NW”] mliyemwasi sana, enyi wana wa Israeli.” (Isaya 31:6) Ufalme wa Israeli wa makabila kumi sio ufalme pekee ulioasi. Watu wa Yuda, ambao pia ni “wana wa Israeli,” ‘wameasi sana.’ Hilo hasa litaonekana waziwazi wakati ambapo, muda mfupi baada ya Isaya kumaliza ujumbe wake wa unabii, Manase mwana wa Hezekia atakapokuwa mfalme. Kulingana na masimulizi ya Biblia, ‘Manase aliwakosesha Yuda na wenyeji wa Yerusalemu, hata wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliowaharibu BWANA mbele ya wana wa Israeli.’ (2 Mambo ya Nyakati 33:9) Hebu wazia hilo! Yehova ayaharibu mataifa ya kipagani kwa sababu yanachukiza kwa uchafu wao, ila wakazi wa Yuda walio katika uhusiano wa agano na Yehova ni wabaya hata zaidi kuliko watu wa mataifa hayo.
17. Hali za leo zafananaje na zile za Yuda chini ya utawala wa Manase?
17 Mwanzoni mwa karne ya 21, hali za ulimwengu zafanana kwa njia nyingi na hali katika nchi ya Yuda wakati wa Manase. Chuki za kidini, kijamii, na kikabila zinazidi kuugawanya ulimwengu. Mauaji yenye kuogopesha, kuteswa, ubakaji, na mauaji ya kikabila yamewapata mamilioni ya watu. Pasipo shaka, watu na mataifa—hasa mataifa ya Jumuiya ya Wakristo—‘wameasi sana.’ Hata hivyo, twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hataruhusu uovu uendelee milele. Kwa nini? Kwa sababu ya mambo yaliyotukia katika siku ya Isaya.
Yerusalemu Lakombolewa
18. Rabshake ampa Hezekia onyo gani?
18 Wafalme wa Ashuru waliisifu miungu yao kutokana na ushindi vitani. Kitabu kiitwacho Ancient Near Eastern Texts kina maandishi ya Ashurbanipali, mtawala Mwashuri aliyedai kuwa aliongozwa “na miungu mikuu iitwayo Ashuru, Beli, Nebo, ambayo ilikuwa mabwana wake, waliotembea kando yake sikuzote, alipowashinda wanajeshi waliozoea vita . . . katika pigano kubwa.” Katika siku ya Isaya, Rabshake, anayewakilisha Mfalme Senakeribu wa Ashuru, aonyesha itikadi hiyo katika hotuba yake kwa Mfalme Hezekia kwamba miungu inahusika katika vita vya binadamu. Amwonya mfalme wa Wayahudi kwamba asiutegemee wokovu wa Yehova naye aeleza kwamba miungu ya mataifa mengine haikuweza kuwalinda watu wake dhidi ya jeshi lenye nguvu la Ashuru.—2 Wafalme 18:33-35, kielezi-chini.
19. Hezekia aitikiaje dhihaka za Rabshake?
19 Mfalme Hezekia aitikiaje? Masimulizi ya Biblia yasema: “Mfalme Hezekia aliposikia hayo, alizirarua nguo zake, akajivika nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya BWANA.” (2 Wafalme 19:1) Hezekia atambua kwamba kuna Mmoja tu awezaye kumsaidia katika hali hiyo yenye kutia woga. Yeye ajinyenyekeza na kuutegemea mwelekezo wa Yehova.
20. Yehova atatendaje kwa niaba ya wakazi wa Yuda, nao wapaswa kujifunza nini kutokana na hilo?
20 Yehova atoa mwelekezo ambao umeombwa. Kupitia nabii Isaya, yeye asema: “Katika siku hiyo kila mtu atatupa sanamu zake za fedha, na sanamu zake za dhahabu, ambazo mikono yenu imezifanya, zikawa dhambi kwenu.” (Isaya 31:7) Yehova awapiganiapo watu wake, miungu ya Senakeribu itathibitishwa kuwa isiyofaa kitu. Wakazi wa Yuda wapaswa kuzingatia fundisho hilo. Licha ya uaminifu wa Mfalme Hezekia, nchi ya Yuda, sawa na Israeli, imejazwa sanamu. (Isaya 2:5-8) Itahitaji wakazi wa Yuda wasitawishe uhusiano wao na Yehova kwa kutubu dhambi zao na kukataa ‘kila mtu sanamu zake.’—Ona Kutoka 34:14.
21. Isaya aelezaje kwa unabii matendo ya hukumu ya Yehova dhidi ya Mwashuri?
21 Isaya sasa aeleza kwa unabii matendo ya hukumu ya Yehova dhidi ya adui ya Yuda mwenye kutia hofu: “Huyo Mwashuri ataanguka kwa upanga ambao si wa mtu; na upanga usio upanga wa mtu utamla; naye ataukimbia upanga, na vijana wake watatoa kodi.” (Isaya 31:8) Wakati wa kupambana ufikapo, wakazi wa Yerusalemu hawatahitaji hata kidogo kuchomoa panga zao kutoka alani mwake. Wanajeshi bora katika jeshi la Ashuru waangamizwa, si kwa panga za binadamu, bali kwa upanga wa Yehova. Mfalme Senakeribu wa Ashuru naye “ataukimbia upanga.” Baada ya wapiganaji wake 185,000 kufa mikononi mwa malaika wa Yehova, yeye arudi nyumbani. Baadaye, wanawe wamwua anapokuwa akiinamia Nisroki mungu wake.—2 Wafalme 19:35-37.
22. Wakristo leo waweza kujifunza nini kutokana na matukio yaliyohusisha Hezekia na jeshi la Ashuru?
22 Hakuna mtu yeyote, akiwemo Hezekia, ambaye angeweza kuona kimbele jinsi ambavyo Yehova angekomboa Yerusalemu kutoka kwa jeshi la Ashuru. Hata hivyo, njia ya Hezekia ya kushughulikia mgogoro huo yaandaa kielelezo bora kwa wale walio na majaribu leo. (2 Wakorintho 4:16-18) Kwa kuzingatia sifa yenye kuogopesha ya Waashuri wanaotishia Yerusalemu, yaeleweka ni kwa nini Hezekia anahofu. (2 Wafalme 19:3) Licha ya hayo, yeye alikuwa na imani katika Yehova, na akatafuta mwongozo Wake, wala si wa mwanadamu. Kufanya hivyo kulikuwa baraka iliyoje kwa Yerusalemu! Huenda Wakristo wenye kumhofu Mungu leo wakapata hisia kali chini ya mkazo. Katika hali nyingi, yaeleweka ni kwa nini watu wanaweza kuhofu. Ingawa hivyo, ‘tukitupa hangaiko letu lote juu ya Yehova,’ atatutunza. (1 Petro 5:7) Atatusaidia tuishinde hofu yetu naye atatuimarisha ili tukabiliane na hali inayoleta mkazo.
23. Senakeribu, wala si Hezekia, aachwaje na hisia zenye hofu?
23 Mwishowe, Senakeribu ndiye anayeachwa na hisia zenye hofu, wala si Hezekia. Amwendee nani? Isaya atabiri: “Mwamba wake utatoweka kwa sababu ya hofu, nao wakuu wake wataionea bendera hofu kuu, asema BWANA, ambaye moto wake u katika Sayuni, na tanuru yake katika Yerusalemu.” (Isaya 31:9) Miungu ya Senakeribu—“mwamba” wake, kimbilio analolitumaini—haimsaidii vyovyote. Ni kana kwamba ‘inatoweka kwa sababu ya hofu.’ Isitoshe, hata wakuu wa Senakeribu hawafai chochote. Wao pia wamejawa na hofu.
24. Twaweza kujifunza habari gani iliyo wazi kutokana na mambo yaliyompata Mwashuri?
24 Sehemu hiyo ya unabii wa Isaya yatoa habari waziwazi kwa yeyote anayenuia kumpinga Mungu. Hakuna silaha yoyote, wala serikali, wala chombo chochote kile kiwezacho kuzuia makusudi ya Yehova. (Isaya 41:11, 12) Na wakati huohuo, wale wanaodai kumtumikia Mungu ilhali wanageuka kutoka kwake ili kutafuta usalama katika mambo ya kimwili watavunjika moyo. Wowote ambao “hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli” watamwona Yehova ‘akileta uovu.’ (Isaya 31:1, 2) Kwa kweli, kimbilio pekee lililo halisi na lenye kudumu ni Yehova Mungu.—Zaburi 37:5.
[Maelezo ya Chini]
a Yaonekana kwamba mistari mitatu ya kwanza ya Isaya sura ya 31 imeelekezwa hasa kwa Israeli. Yaelekea mistari sita ya mwisho yahusu Yuda.
[Picha katika ukurasa wa 319]
Wale wanaovitumainia vitu vya kimwili watavunjika moyo
[Picha katika ukurasa wa 322]
Kama vile simba anayelinda mawindo yake, ndivyo Yehova atakavyolilinda jiji lake takatifu
[Picha katika ukurasa wa 324]
Chuki za kidini, kijamii, na kikabila zimeugawanya ulimwengu
[Picha katika ukurasa wa 326]
Hezekia alienda nyumbani kwa Yehova kutafuta msaada