Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ip-2 sura 23 kur. 335-348
  • “Jina Jipya”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Jina Jipya”
  • Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Hakai Kimya
  • Wapewa “Jina Jipya” na Yehova
  • ‘Yehova Amekufurahia’
  • “Msiwe na Kimya”
  • Kutumikia Mungu Kutathawabishwa
  • “Wokovu Wako Unakuja”!
  • ‘Imbeni Pamoja kwa Shangwe’!
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa Nuru
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kitabu Cha Biblia Namba 23—Isaya
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
ip-2 sura 23 kur. 335-348

Sura Ya Ishirini Na Tatu

“Jina Jipya”

Isaya 62:1-12

1. Ni uhakikisho gani ambao umeandikwa katika Isaya sura ya 62?

WAYAHUDI walioshuka moyo kule Babiloni wanahitaji hasa kupewa uhakikisho, faraja, na tumaini la kurudishwa. Miongo kadhaa imepita tangu Yerusalemu na hekalu lake ziharibiwe. Umbali wa kilometa 800 hivi kutoka Babiloni, nchi ya Yuda imekaa hali ya ukiwa, na inaonekana ni kama Wayahudi wamesahauliwa na Yehova. Ni nini kinachoweza kuleta maendeleo katika hali yao? Ni ahadi za kwamba Yehova atawarejesha nyumbani na kuwaruhusu warudishe ibada safi. Ndipo mitajo kama vile “Aliyeachwa” na “Ukiwa” zitaondolewa, na badala yake kuweko majina yanayoonyesha ukubali wa Mungu. (Isaya 62:4; Zekaria 2:12) Sura ya 62 ya Isaya imejaa ahadi hizo. Hata hivyo, kama vile unabii mwingine mbalimbali wa kurudishwa, sura hii inagusia masuala mengi sana, wala si kukombolewa tu kwa Wayahudi ili watoke utekwani kule Babiloni. Katika utimizo wake mkubwa, Isaya sura ya 62 inatuhakikishia kwamba wokovu wa taifa la kiroho la Yehova, yule “Israeli wa Mungu,” ni hakika.—Wagalatia 6:16.

Yehova Hakai Kimya

2. Kwa mara nyingine, Yehova anaonyeshaje kwamba anamkubali Sayuni?

2 Babiloni yapinduliwa mwaka wa 539 K.W.K. Baada ya hapo, Mfalme Koreshi wa Uajemi anatoa amri inayowawezesha Wayahudi wanaomhofu Mungu warejee Yerusalemu wakairudishe ibada ya Yehova. (Ezra 1:2-4) Mwaka wa 537 K.W.K., Wayahudi wa kwanza kurudi wamekwisha fikia nchi yao. Kwa mara nyingine Yehova anaonyesha kwamba anamkubali Yerusalemu, kama vile inavyoonyeshwa kwa uchangamfu unaotumiwa kutoa tangazo lake la kiunabii: “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia [“sitakaa kimya,” “NW”], hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo [“mwenge,” “VB”].”—Isaya 62:1.

3. (a) Kwa nini Sayuni wa kidunia anakataliwa na Yehova mwishowe, na ni nani anayechukua mahali pake? (b) Ni ukengeufu gani unaotukia, unatukia wakati gani, nasi tunaishi katika kipindi gani leo?

3 Mwaka wa 537 K.W.K., Yehova alitimiza ahadi yake kuelekea Sayuni, au Yerusalemu, iliyorudishwa. Wakaaji wake waliona akiwapa wokovu, na uadilifu wao ukang’aa sana. Ingawa hivyo, baadaye walipeperuka wakaiacha ibada safi. Mwishowe wakamkataa Mesiya, naye Yehova hatimaye akawaacha kabisa wasiwe taifa lake teule. (Mathayo 21:43; 23:38; Yohana 1:9-13) Yehova alisababisha taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” lizaliwe. Taifa hili jipya likawa watu wake wa pekee, na katika karne ya kwanza, washirika wake wakazihubiri habari njema kwa bidii kotekote katika ulimwengu uliojulikana wakati huo. (Wagalatia 6:16; Wakolosai 1:23) Inahuzunisha kwamba baada ya mitume kufa kulitokea ukengeufu wa kuiacha dini ya kweli. Matokeo ni kwamba, Ukristo wa namna fulani ya uasi-imani ulisitawi, ule unaopatikana katika Jumuiya ya Wakristo leo. (Mathayo 13:24-30, 36-43; Matendo 20:29, 30) Kwa karne nyingi, Jumuiya ya Wakristo ikawa imeruhusiwa kuleta suto kubwa juu ya jina la Yehova. Hata hivyo, mwishowe “mwaka wa nia njema” wa Yehova ukaanza katika mwaka wa 1914, pamoja na utimizo mkubwa wa sehemu hii ya unabii wa Isaya.—Isaya 61:2, NW.

4, 5. (a) Sayuni na watoto wake wanafananisha nani leo? (b) Yehova ametumiaje Sayuni ili kufanya ‘wokovu wake uwe kama taa iwakayo’?

4 Leo ahadi ya Yehova ya kurudisha Sayuni imetimizwa kuhusiana na tengenezo lake la kimbingu, “Yerusalemu la juu,” kama vile linavyowakilishwa duniani na watoto wake, Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. (Wagalatia 4:26) Tengenezo la Yehova la kimbingu ni msaidiaji mwenye moyo wa kujitoa—ni mlinzi aliye macho, mwenye upendo, na mwenye bidii. Mwaka wa 1914 ulikuwa pindi ya kusisimua kama nini wakati tengenezo hilo lilipozaa Ufalme wa Kimesiya! (Ufunuo 12:1-5) Kuanzia 1919 hasa, watoto wake wa kidunia wamehubiria mataifa kuhusu haki na wokovu wa tengenezo hilo. Kama vile Isaya alivyotabiri, watoto hawa wamelimulika giza kama mwenge, wakiacha nuru yao ing’ae.—Mathayo 5:15, 16; Wafilipi 2:15.

5 Yehova anapendezwa sana na waabudu wake na hatapumzika, wala kukaa kimya, mpaka atimize ahadi zote alizomtolea Sayuni na watoto wake. Hata mabaki ya watiwa-mafuta pamoja na waandamani wao walio “kondoo wengine” wanakataa kukaa kimya. (Yohana 10:16) Wanatoa sauti kweli kweli wakiwaonyesha watu njia pekee ya kupata wokovu.—Waroma 10:10.

Wapewa “Jina Jipya” na Yehova

6. Yehova ana lengo gani kuhusu Sayuni?

6 Yehova ana lengo gani kuhusu Sayuni, “mwanamke” wake wa kimbingu, aliyewakilishwa na Yerusalemu la kale? Anasema hivi: “Mataifa wataiona haki yako [“Ee mwanamke,” “NW”], na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha BWANA.” (Isaya 62:2) Wakati Waisraeli wanapotenda uadilifu, mataifa yanalazimika kuangalia kwa makini. Hata wafalme wanalazimika kukubali kwamba Yehova anatumia Yerusalemu na kwamba utawala wowote walio nao si kitu ukilinganishwa na Ufalme wa Yehova.—Isaya 49:23.

7. Jina jipya la Sayuni linamaanisha nini?

7 Sasa Yehova anampa Sayuni jina jipya ili kuthibitisha kwamba hali yake imebadilika. Jina hilo jipya linamaanisha hali yenye baraka na cheo chenye heshima kinachofurahiwa na watoto wa kidunia wa Sayuni kuanzia mwaka wa 537 K.W.K.a Linaonyesha kwamba Yehova anamkubali Sayuni kuwa mali yake. Leo, Israeli wa Mungu wanasisimuka kuwa kipenzi cha Yehova kwa njia hiyo, na wale kondoo wengine wanashangilia pamoja nao.

8. Yehova amemheshimu Sayuni kwa njia zipi?

8 Akiisha kumpa Sayuni jina jipya, sasa Yehova anaahidi hivi: “Utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa BWANA, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.” (Isaya 62:3) Yehova anamwinua mke wake wa mfano, Sayuni wa kimbingu, atazamwe kwa mshangao kwa sababu anavutia. (Zaburi 48:2; 50:2) Taji la uzuri na “kilemba cha kifalme” zinaonyesha kwamba mke huyo amevikwa heshima na mamlaka. (Zekaria 9:16) Israeli wa Mungu, ambaye anawakilisha Sayuni wa kimbingu, au “Yerusalemu la juu,” ametokea kwa kufanyizwa vizuri ajabu na mkono wa Mungu, yaani nguvu zake zikiwa katika hali ya kutumika. (Wagalatia 4:26) Kwa msaada wa Yehova, taifa hilo la kiroho limeweka kumbukumbu zuri ajabu la uaminifu wa maadili na moyo wa kujitoa kwa muda mrefu. Mamilioni ya watu, kutia na watiwa-mafuta na kondoo wengine, wanaimarishwa kuonyesha imani na upendo wa kutokeza. Wakati wa Utawala wa Milenia ya Kristo, watiwa-mafuta, wakiisha kufikia thawabu yao tukufu ya kimbingu, watatumiwa kama vyombo mkononi mwa Yehova ili kuinua uumbaji unaougua ufikie kiwango cha uhai wa milele.—Waroma 8:21, 22; Ufunuo 22:2.

‘Yehova Amekufurahia’

9. Eleza jinsi hali ya Sayuni inavyogeuzwa.

9 Upaji wa jina jipya ni sehemu ya kumgeuza Sayuni wa kimbingu, anayewakilishwa na watoto wake wa kidunia, ili awe na hali ya kupendeza. Tunasoma hivi: “Hutaitwa tena Aliyeachwa, wala nchi yako haitaitwa tena, Ukiwa; bali utaitwa Hefsiba [Namfurahia]; na nchi yako Beula [Ameolewa]; kwa kuwa BWANA anakufurahia, na nchi yako itaolewa.” (Isaya 62:4) Sayuni wa kidunia amekuwa ukiwa tangu alipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Hata hivyo, maneno ya Yehova yanamhakikishia kwamba nchi yake itarudishiwa hali yake ya kwanza na kujazwa wakaaji tena. Sayuni aliyeteketezwa wakati mmoja hatakuwa tena mwanamke aliyeachwa pweke, wala nchi yake haitakuwa ukiwa tena. Kurudishwa kwa Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. kunamaanisha kwamba atapata hali mpya, inayotofautiana kabisa na hali yake ya kwanza ya kuwa magofu. Yehova anatangaza kwamba Sayuni ataitwa “Namfurahia,” na nchi yake itaitwa “Ameolewa.”—Isaya 54:1, 5, 6; 66:8; Yeremia 23:5-8; 30:17; Wagalatia 4:27-31.

10. (a) Hali ya Israeli wa Mungu iligeuzwaje? (b) “Nchi” ya Israeli wa Mungu ni nini?

10 Kuanzia mwaka wa 1919 badiliko kama hilo lilipata Israeli wa Mungu. Wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, Wakristo watiwa-mafuta walionekana ni kama wamekataliwa na Mungu. Lakini mwaka wa 1919 walirudishiwa hali ya kukubalika, na njia yao ya kuabudu ikatakaswa. Jambo hilo liligeuza mafundisho yao, tengenezo lao, na utendaji wao. Taifa la Israeli wa Mungu liliingia katika “nchi” yake, miliki yake ya kiroho, au makao ya utendaji.—Isaya 66:7, 8, 20-22.

11. Wayahudi wanamwoaje mama yao?

11 Yehova anazidi kukazia hali mpya ya kukubalika kwa watu wake, anapotangaza hivi: “Kama vile kijana amwoavyo mwanamwali, ndivyo wana wako watakavyokuoa wewe; na kama vile bwana arusi amafurahiavyo bibi arusi, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe.” (Isaya 62:5) Wayahudi, wale “wana” wa Sayuni, wanawezaje kumwoa mama yao? Katika maana ya kwamba wana wa Sayuni wanaorudi baada ya kufunguliwa watoke uhamishoni Babiloni wanamiliki jiji lao kuu la zamani na kukaa humo tena. Inapokuwa hivyo, Sayuni si mkiwa tena, bali ana wana chungu nzima.—Yeremia 3:14.

12. (a) Yehova amejulishaje wazi kwamba Wakristo watiwa-mafuta ni sehemu ya tengenezo ambalo limeungana naye katika ndoa? (b) Shughuli za Yehova pamoja na watu wake zinatoaje kielelezo cha ndoa ya hali ya juu leo? (Ona sanduku katika ukurasa wa 342.)

12 Kwa njia ya ulinganifu, tangu mwaka wa 1919 watoto wa Sayuni wa kimbingu wamemiliki nchi yao, miliki yao ya kiroho, iliyo na jina la kiunabii “Ameolewa.” Utendaji wao wa Kikristo katika nchi hiyo umeonyesha wazi kwamba Wakristo hawa watiwa-mafuta ni “watu kwa ajili ya jina lake” Yehova. (Matendo 15:14) Kuzaa kwao matunda ya Ufalme na kutangaza jina la Yehova kumeonyesha wazi kwamba Yehova huwafurahia sana Wakristo hawa. Yeye ameonyesha wazi kwamba wao ni sehemu ya tengenezo ambalo limeungana naye katika umoja usiovunjika. Kwa kuwatia mafuta Wakristo hawa kwa roho takatifu, kuwakomboa watoke katika utekwa wa kiroho, na kuwatumia ili wahubirie jamii yote ya wanadamu tumaini la Ufalme, Yehova ameonyesha kwamba anawashangilia kwa shangwe ya bwana-arusi kumwelekea bibi-arusi.—Yeremia 32:41.

“Msiwe na Kimya”

13, 14. (a) Nyakati za kale, Yerusalemu linakuwaje jiji lenye usalama? (b) Nyakati za kisasa, Sayuni amekuwaje “sifa duniani”?

13 Jina jipya la mfano ambalo Yehova amewapa watu wake huwafanya wahisi usalama. Wanajua kwamba yeye huwakubali na kwamba wao ni miliki yake. Sasa Yehova anatumia mfano tofauti na kuongea na watu wake kana kwamba anaongea na jiji lenye kuta: “Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Ee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye kumkumbusha [“kumtaja,” “NW”] BWANA, msiwe na kimya; wala msimwache akae kimya, mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa duniani.” (Isaya 62:6, 7) Katika wakati wa Yehova, baada ya mabaki waaminifu kutoka Babiloni, Yerusalemu linakuwa “sifa duniani”—jiji lenye kuta za kuwapa wakaaji wake usalama. Mchana na usiku, walinzi katika kuta hizo wako macho kuhakikisha kwamba jiji lina usalama, na kuwapasha wakaaji wake habari za kuwaonya.—Nehemia 6:15; 7:3; Isaya 52:8.

14 Nyakati za kisasa Yehova amewatumia walinzi wake watiwa-mafuta kuwaonyesha watu watiifu njia ya kupata uhuru kutoka kwenye utumwa wa dini ya uwongo. Watu hao wamealikwa waje ndani ya tengenezo lake, ambamo wanalindwa wasipatwe na uchafu wa kiroho, mavutano ya kutomhofu Mungu, na ili wasichukiwe na Yehova. (Yeremia 33:9; Sefania 3:19) Jamii ya mlinzi, yaani yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” inatimiza fungu muhimu sana la kutoa ulinzi huo, kwani inaandaa ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ (Mathayo 24:45-47) Kwa kufanya kazi na jamii ya mlinzi, ule “umati mkubwa” pia hushiriki sehemu ya maana katika kufanya Sayuni awe “sifa duniani.”—Ufunuo 7:9.

15. Jamii ya mlinzi na waandamani wao wanamtumikiaje Yehova daima?

15 Jamii ya mlinzi na waandamani wake inaendelea kutoa utumishi! Mtazamo wao wa kujitoa kwa nafsi yote unaonekana katika utendaji wenye bidii unaofanywa na mamilioni ya watu mmoja-mmoja walio waaminifu, huku wakiungwa mkono na waangalizi wanaosafiri na wake zao; watu waliojitolea katika makao mbalimbali ya Betheli na katika sehemu za uchapaji za Mashahidi wa Yehova; mishonari; na mapainia wa pekee, wa kawaida, na wasaidizi. Zaidi ya hilo, wanajibidiisha kujenga Majumba mapya ya Ufalme, kutembelea wagonjwa, kusaidia watu mmoja-mmoja wanaokabili hali ngumu za kitiba, na kuwapa msaada wa wakati wake wale wanaopatwa na majanga na misiba. Mara nyingi, wengi wa watu hawa wenye kujidhabihu hutumikia kihalisi “mchana na usiku”!—Ufunuo 7:14, 15.

16. Ni jinsi gani watumishi wa Yehova ‘wasivyomwacha akae kimya’?

16 Watumishi wa Yehova wanatiwa moyo kusali bila kukoma, kumwomba Mungu ‘mapenzi yake yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.’ (Mathayo 6:9, 10; 1 Wathesalonike 5:17) Wanahimizwa hivi: “Msimwache [Yehova] akae kimya” mpaka awatimizie tamaa zenu na matumaini yanayohusiana na kurudishwa kwa ibada ya kweli. Yesu alikazia uhitaji wa kusali daima, akawahimiza wafuasi wake ‘kumpaazia Mungu kilio mchana na usiku.’—Luka 18:1-8.

Kutumikia Mungu Kutathawabishwa

17, 18. (a) Wakaaji wa Sayuni wanaweza kutazamiaje kufurahia matunda ya kazi yao? (b) Watu wa Yehova leo wanafurahiaje matunda ya kazi yao?

17 Jina jipya ambalo Yehova anawapa watu wake linawahakikishia kwamba jitihada zao si za bure. “BWANA ameapa kwa mkono wake wa kuume, na kwa mkono wa nguvu zake, Hakika sitawapa adui zako nafaka yako tena kuwa chakula chao; wala wageni hawatakunywa divai yako, uliyoifanyia kazi. Lakini walioivuna, ndio watakaoila, na kumhimidi BWANA; na walioichuma, ndio watakaoinywa, ndani ya nyua za patakatifu pangu.” (Isaya 62:8, 9) Mkono wa kuume wa Yehova na mkono wa nguvu zake ni ishara za kuonyesha uwezo wake na nguvu zake. (Kumbukumbu la Torati 32:40; Ezekieli 20:5) Anapoapa kwa mkono wake wa kuume na kwa mkono wa nguvu zake, hiyo inaonyesha kwamba amepiga moyo konde kuibadili hali ya Sayuni. Mwaka wa 607 K.W.K., Yehova anaruhusu adui za Sayuni wamnyang’anye mali zake na kuzipora. (Kumbukumbu la Torati 28:33, 51) Lakini sasa, mali za Sayuni zitafurahiwa na wale tu walio na haki ya kuzigusa.—Kumbukumbu la Torati 14:22-27.

18 Katika utimizo wa kisasa wa ahadi hiyo, watu wa Yehova waliorudishwa wanapata ufanisi mkubwa wa kiroho. Wanayafurahia kikamili matunda ya kazi yao, yaani idadi iliyoongezeka ya wanafunzi Wakristo na wingi wa chakula cha kiroho. (Isaya 55:1, 2; 65:14) Kwa sababu watu wake ni waaminifu, Yehova haachi adui zake wavuruge ufanisi wao wa kiroho wala wawanyang’anye matokeo ya utumishi wao wa nafsi yote. Hakuna kazi inayofanywa katika utumishi wa Yehova iliyo ya bure.—Malaki 3:10-12; Waebrania 6:10.

19, 20. (a) Vikwazo vinaondolewaje njiani ili Wayahudi warudi Yerusalemu? (b) Katika nyakati za kisasa, vikwazo vimeondolewaje njiani ili watu watiifu waingie katika tengenezo la Yehova?

19 Vilevile lile jina jipya linafanya tengenezo la Yehova liwavutie watu wenye mioyo ya kupenda haki. Makundi ya watu yanalimiminikia, na njia inaachwa wazi ili waendelee kuingia. Unabii wa Isaya unasema hivi: “Piteni, piteni, katika malango; itengenezeni njia ya watu; tutieni, tutieni barabara [“kuu,” “NW”]; toeni mawe yake; twekeni bendera kwa ajili ya kabila za watu.” (Isaya 62:10) Katika kisa cha kwanza, inaelekea kuwa mwito huu unamaanisha kupita na kutoka nje ya malango ya jiji ya Babilonia ili kurudi Yerusalemu. Hao wenye kurudi wanapaswa kuondoa mawe njiani ili kurahisisha safari na kuinua ishara ya kuonyesha njia ya kupitia.—Isaya 11:12.

20 Tangu mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wamewekwa kando kwa ajili ya utumishi wa kimungu na wanasafiri katika ile “Njia ya utakatifu.” (Isaya 35:8) Walikuwa wa kwanza kutembea katika barabara kuu ya kiroho kutoka katika Babiloni Mkubwa. (Isaya 40:3; 48:20) Mungu aliwapa pendeleo la kuongoza katika kutangaza kazi zake hodari na kuwaonyesha wengine njia ya kuingia katika ile barabara kuu. Wao wenyewe ndio wangefaidika kwa kuondolea mbali mawe— kuondoa vikwazo njiani. (Isaya 57:14) Walihitaji kuyaona makusudi na mafundisho ya Mungu waziwazi. Imani za uwongo ni mawe ya kukwaza katika njia ya uhai, lakini Neno la Mungu ni “kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande.” Wakiwa nayo, Wakristo watiwa-mafuta walivunja-vunja mawe ya kukwaza ambayo yangeweza kuwatega wale waliotaka kumtumikia Yehova.—Yeremia 23:29.

21, 22. Yehova amesimamisha ishara gani ili iwaongoze wale wanaotoka katika dini ya uwongo, nasi tunajuaje?

21 Mwaka wa 537 K.W.K., jiji la Yerusalemu likawa ishara iliyowavutia mabaki Wayahudi ili warudi wakajenge hekalu upya. (Isaya 49:22) Mwaka wa 1919, mabaki watiwa-mafuta walipokombolewa kutoka kwenye utumwa wa dini ya uwongo, hawakutanga-tanga ovyo-ovyo. Walijua pa kwenda, kwa maana Yehova alikuwa amesimamisha ishara kwa ajili yao. Ishara gani? Ishara ile ile iliyotabiriwa kwenye Isaya 11:10, inayosema hivi: ‘Itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese litasimama kuwa ishara kwa kabila za watu.’ Mtume Paulo anatumia maneno hayo kumhusu Yesu. (Waroma 15:8, 12) Ndiyo, ile ishara ni Kristo Yesu, anayetawala akiwa Mfalme juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu!—Waebrania 12:22; Ufunuo 14:1.

22 Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine pia wamekusanyika kumzunguka Yesu Kristo ili wajihusishe katika ibada ya Mungu Aliye Juu Zaidi inayounganisha watu. Utawala wake unasaidia kutetea enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu mzima na kubariki watu wa mataifa yote ya dunia ambao ni wanyofu moyoni. Je, hiyo si sababu ya kumfanya kila mmoja wetu ajiunge katika kumtukuza kwa kumpa sifa?

“Wokovu Wako Unakuja”!

23, 24. Wale walio na imani katika Mungu wanaletewaje wokovu?

23 Jina jipya ambalo Yehova anapatia tengenezo lake lililo kama mke linahusiana na wokovu wa milele wa watoto wake. Isaya anaandika hivi: “Tazama, BWANA ametangaza habari mpaka mwisho wa dunia, Mwambieni binti Sayuni, Tazama, wokovu wako unakuja; tazama, thawabu yake i pamoja naye, na malipo yake yako mbele zake.” (Isaya 62:11) Wokovu uliwajia Wayahudi wakati Babiloni ilipoanguka, nao wakarudia nchi yao. Lakini maneno haya yanaelekeza kwenye jambo kubwa zaidi. Tangazo la Yehova linatokeza kikumbusha cha unabii huu wa Zekaria unaohusu Yerusalemu: “Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; tazama, mfalme wako anakuja kwako; ni mwenye haki, naye ana wokovu; ni mnyenyekevu, amepanda punda, naam, mwana-punda, mtoto wa punda.”—Zekaria 9:9.

24 Miaka mitatu na nusu baada ya Yesu kubatizwa katika maji na kutiwa mafuta kwa roho ya Mungu, alipanda punda akaingia Yerusalemu na kulisafisha hekalu la jiji hilo. (Mathayo 21:1-5; Yohana 12:14-16) Leo, Yesu Kristo ndiye anayewaletea wokovu wa Yehova wale wote wanaomwamini Mungu. Tangu atawazwe mwaka wa 1914, Yesu pia ndiye Hakimu na Mfishaji aliyewekwa na Yehova. Mwaka wa 1918, miaka mitatu na nusu baada ya yeye kutawazwa, alisafisha hekalu la kiroho la Yehova, kama linavyowakilishwa duniani na kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. (Malaki 3:1-5) Alipoinuliwa awe ishara, hapo ndipo watu wa sehemu zote za dunia walipoanza kukusanywa ili kuunga mkono Ufalme wa Kimesiya. Kwa kufuata kielelezo cha kale, “wokovu” uliwajia Israeli wa Mungu walipofunguliwa kutoka Babiloni Mkubwa mwaka wa 1919. Wafanyakazi wa mavuno wenye roho ya kujidhabihu wanapata “thawabu” au “malipo” ya uhai wa mbinguni usioweza kufa ama uhai wa milele duniani. Wote wale wanaobaki wakiwa waaminifu wanaweza kuwa na hakika kwamba ‘kazi yao ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.’—1 Wakorintho 15:58.

25. Watu wa Yehova wanahakikishiwa nini?

25 Lo, kuna matazamio mazuri kama nini kwa ajili ya tengenezo la Yehova la kimbingu, kwa wawakilishi wake watiwa-mafuta hapa duniani, na kwa ajili ya kila mtu anayeshirikiana nao kwa bidii! (Kumbukumbu la Torati 26:19) Isaya alitoa unabii huu: “Nao watawaita, Watu watakatifu, waliokombolewa na BWANA; nawe utaitwa, Aliyetafutwa, Mji usioachwa.” (Isaya 62:12) Wakati mmoja “Yerusalemu la juu,” anayewakilishwa na Israeli wa Mungu, alihisi kuwa ameachwa. Hatahisi hivyo tena. Yehova atafurahi sana kuwalinda watu wake milele, huku wao pia wakifurahia kukubaliwa naye daima.

[Maelezo ya Chini]

a Katika unabii wa Biblia, “jina jipya” linaweza kumaanisha cheo kipya au pendeleo jipya.—Ufunuo 2:17; 3:12.

[Sanduku katika ukurasa wa 342]

Kielelezo cha Ndoa ya Hali ya Juu

Watu wanapofunga ndoa, kila mmoja wao hutazamia mambo fulani katika muungano huo wa ndoa. Lakini Mungu ana matazamio gani? Ni yeye aliyeanzisha muungano wa ndoa. Alikusudia iwe namna gani?

Jambo moja la kuonyesha maoni ya Mungu kuhusu ndoa linatokana na uhusiano wake na taifa la Israeli katika mambo mbalimbali. Isaya anauonyesha uhusiano huo kuwa kama ndoa. (Isaya 62:1-5) Angalia mambo ambayo Yehova Mungu akiwa kama “mume” anamfanyia “bibi-arusi” wake. Anamlinda na kumtakasa. (Isaya 62:6, 7, 12) Anamheshimu na kumthamini. (Isaya 62:3, 8, 9) Na anamfurahia sana huyo mke, kama vile inavyoonyeshwa na majina mapya anayompa.—Isaya 62:4, 5, 12.

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Paulo anayarudia maelezo ya Isaya juu ya uhusiano ulio kati ya Yehova na Israeli wakati anapoulinganisha uhusiano wa mume na mke na ule wa Kristo na kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta.—Waefeso 5:21-27.

Paulo aliwatia moyo Wakristo waige uhusiano ulio kati ya Yesu na kutaniko katika ndoa zao. Hakuwezi kuwako upendo mkubwa kuliko ule ulioonyeshwa na Yehova kuelekea Israeli na ule unaoonyeshwa na Kristo kuelekea kutaniko. Visa hivyo vya uhusiano wa kimfano vinaandaa kielelezo cha ndoa ya hali ya juu, yenye mafanikio na furaha kati ya Wakristo.—Waefeso 5:28-33.

[Picha katika ukurasa wa 339]

Yehova atamwita Sayuni wa kimbingu kwa jina jipya

[Picha katika ukurasa wa 347]

Nyakati za kisasa, jamii ya mlinzi wa Yehova haijakaa kimya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki