Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wt sura 2 kur. 14-22
  • Mtukuze Yehova—Mungu wa Pekee wa Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtukuze Yehova—Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mungu Ni Upendo”
  • Kuwaonyesha Wengine Upendo
  • ‘Tembea Katika Jina la Yehova’
  • Upendo wa Kikristo Wenye Msingi wa Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Mpende Mungu Anayekupenda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • “Katika Hayo Lililo Kuu ni Upendo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Mjengwe na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
wt sura 2 kur. 14-22

Sura Ya Pili

Mtukuze Yehova—Mungu wa Pekee wa Kweli

1. Mungu pekee wa kweli ni nani?

BIBLIA inasema kwamba ijapokuwa kuna wengi wanaoitwa miungu, “kwetu kuna Mungu mmoja Baba.” (1 Wakorintho 8:5, 6) ‘Mungu huyo mmoja’ ni Yehova, Muumba wa vitu vyote. (Kumbukumbu la Torati 6:4; Ufunuo 4:11) Yesu alimwita “Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Alikubaliana na Musa, ambaye alikuwa amesema hivi awali: “Yehova ndiye Mungu wa kweli; hapana mwingine ila yeye.” (Kumbukumbu la Torati 4:35, NW) Yehova hawezi kamwe kulinganishwa na vitu vingine vinavyoabudiwa, kama vile sanamu, wanadamu, au adui yake Shetani Ibilisi, ambaye ni “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Kinyume chake, Yehova ni “Mungu pekee wa kweli” kama Yesu alivyomwita.—Yohana 17:3.

2. Kujifunza kumhusu Mungu kunapasa kuwa na matokeo gani maishani mwetu?

2 Watu wengi wanaomthamini Mungu wanachochewa kumkaribia wanapojifunza sifa zake zenye kuvutia, mambo ambayo tayari ametufanyia na yale ambayo atatufanyia. Upendo wao kwa Yehova unapozidi kuongezeka, wanachochewa kumtukuza. Jinsi gani? Njia moja ni kuwaambia wengine kumhusu. Andiko la Waroma 10:10 lasema: “Kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” Njia nyingine ni kumwiga kwa maneno na kwa matendo. Andiko la Waefeso 5:1 lasema: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” Ili kufanya hivyo kikamili, ni lazima tumjue Yehova vyema.

3. Taja sifa kuu za Mungu.

3 Maandiko mengi ya Biblia yanafunua sifa kuu za Mungu. Sifa zake kuu nne ni hekima, haki, nguvu, na upendo. ‘Hekima ina yeye.’ (Ayubu 12:13) “Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4, italiki ni zetu.) Yeye ni “hodari kwa nguvu.” (Isaya 40:26, italiki ni zetu.) “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hata hivyo, ni sifa gani iliyo kuu zaidi kati ya hizo sifa nne, inayoonyesha utu wa Mungu kwa njia ya pekee?

“Mungu Ni Upendo”

4. Ni sifa gani ya Mungu iliyomchochea kuumba ulimwengu na viumbe wote?

4 Fikiria sababu iliyomchochea Yehova aumbe ulimwengu na viumbe wote wenye akili—malaika na wanadamu. Je, ni hekima yake au ni nguvu zake? La, ingawa Mungu alitumia sifa hizo, hazikumchochea kuumba, wala hakuwajibika kuwapa wengine zawadi ya uhai kwa sababu ya haki yake. Badala yake, upendo wa Mungu usio na kifani ndio uliomchochea kuumba viumbe wenye akili ili nao wafurahie uhai. Kwa upendo, alikusudia wanadamu watiifu waishi milele katika Paradiso. (Mwanzo 1:28; 2:15) Kwa upendo, alifanya mpango wa kuondoa laana ambayo dhambi ya Adamu iliwaletea wanadamu.

5. Kulingana na Biblia, Yehova ni mfano halisi wa sifa gani, na kwa nini?

5 Hivyo basi, upendo ndiyo sifa kuu zaidi ya Mungu. Upendo ni utu wake. Ingawa sifa ya hekima, haki na nguvu ni muhimu, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mojawapo ya sifa hizo. Lakini inasema kwamba yeye ni upendo. Naam, Yehova ndiye mfano halisi wa upendo. Upendo wake unategemea kanuni, si hisia. Upendo wa Mungu unategemea kanuni za kweli na za uadilifu. Huu ni upendo wa hali ya juu sana na Yehova Mungu hana kifani katika kuonyesha upendo huo. Upendo huo si wa ubinafsi na sikuzote huonyeshwa kwa matendo.

6. Ni nini kinachotuwezesha kumwiga Mungu tujapokuwa wanadamu wa hali ya chini?

6 Sifa hii nzuri sana ya upendo ndiyo inayotuwezesha kumwiga Mungu. Tukiwa wanadamu wa hali ya chini, wasiokamilika na wanaokosea mara nyingi, huenda tukafikiri kwamba hatuwezi kamwe kumwiga Mungu. Lakini Yehova anaonyesha upendo wake usio na kifani kwa njia nyingine: Anatambua udhaifu wetu naye hatarajii tutende mambo kwa ukamilifu. Anajua kwamba sisi si wakamilifu. (Zaburi 51:5) Ndiyo sababu Zaburi 130:3, 4 inasema: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha.” Naam, Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema.” (Kutoka 34:6) “Wewe, Bwana, U mwema, umekuwa tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Maandiko hayo yanatia moyo sana. Inaburudisha kama nini kumtumikia Mungu huyo asiye na kifani na kutunzwa naye kwa upendo na rehema!

7. Uumbaji wa Yehova unaonyeshaje kwamba ana upendo?

7 Uumbaji wa Yehova unaonyesha pia kwamba ana upendo. Fikiria vitu vyote vizuri ambavyo Yehova ameumba ili tuvifurahie, kama vile milima, misitu, maziwa, na bahari zenye kuvutia. Ametupatia vyakula vingi vyenye ladha za kupendeza na vinavyoendeleza uhai wetu. Yehova ameumba pia maua maridadi sana na yenye harufu ya kupendeza na wanyama wenye kustaajabisha. Aliumba vitu vya kuwafurahisha wanadamu, hata ingawa si vya lazima. Ni kweli kwamba tukiwa wenye dhambi hatuwezi kufurahia uumbaji wake kikamili katika ulimwengu huu mwovu. (Waroma 8:22) Lakini hebu wazia mambo ambayo Yehova atatufanyia katika Paradiso! Mtunga-zaburi anatuhakikishia hivi: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake [yanayofaa].”—Zaburi 145:16.

8. Wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Yehova kwa wanadamu ni upi?

8 Wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Yehova kwa wanadamu ni upi? Biblia inasema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Je, Yehova alimtoa mwana wake kwa sababu wanadamu ni wema? Andiko la Waroma 5:8 lajibu: “Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” Naam, Mungu alimtuma Mwanaye mkamilifu duniani ili atoe uhai wake kuwa dhabihu ya fidia ili kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. (Mathayo 20:28) Dhabihu hiyo iliwaandalia watu wanaompenda Mungu uwezekano wa kuishi milele. Inapendeza kwamba Mungu anawapenda wote wanaotaka kufanya mapenzi yake, kwa kuwa Biblia inatuambia hivi: “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

9. Kwa kuwa Yehova alimtoa Mwanaye awe fidia kwa ajili yetu, tunapaswa kutumiaje maisha yetu?

9 Basi kwa kuwa Yehova alimtoa Mwanaye awe fidia kwa ajili yetu, na hivyo akatupatia fursa ya kuishi milele, tunapaswa kutumiaje maisha yetu leo? Tunapaswa kumpenda sana Yehova, Mungu wa kweli. Vilevile, tunapaswa kuwa tayari kumsikiliza Yesu, ambaye ni mwakilishi wa Mungu. “[Yesu] alikufa kwa ajili ya wote ili wale waishio wapate kuishi si kwa ajili yao wenyewe tena, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao.” (2 Wakorintho 5:15) Inafurahisha sana kufuata hatua za Yesu, kwa sababu aliiga kikamili upendo na rehema ya Yehova. Jambo hilo linaonyeshwa na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanyenyekevu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.

Kuwaonyesha Wengine Upendo

10. Taja baadhi ya njia tunazoweza kuwaonyesha Wakristo wenzetu upendo?

10 Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawapenda Wakristo wenzetu jinsi Yehova na Yesu wanavyotupenda? Tunaweza kuonyesha upendo kwa njia nyingi sana: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujitutumui, haujiendeshi bila adabu, hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:4-8; 1 Yohana 3:14-18; 4:7-12.

11. Tunapaswa kuwapenda nani wengine, na kwa njia gani?

11 Tunapaswa kuwapenda nani wengine, na kwa njia gani? Yesu alisema: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hilo lamaanisha kuwahubiria wale ambao si Wakristo wenzetu habari njema za ulimwengu mpya wa Mungu ambao unakuja. Yesu alionyesha waziwazi kwamba hatupaswi kuwapenda waumini wenzetu tu, aliposema hivi: “Mkipenda [tu] wale wanaowapenda nyinyi, mna thawabu gani? Je, wakusanya-kodi pia hawafanyi jambo hilohilo? Na mkisalimu ndugu zenu tu, ni jambo gani lizidilo la kawaida mnalofanya? Je, watu wa mataifa pia hawafanyi jambo hilohilo?”—Mathayo 5:46, 47; 24:14; Wagalatia 6:10.

‘Tembea Katika Jina la Yehova’

12. Kwa nini jina la Mungu linamfaa yeye peke yake?

12 Jambo jingine muhimu katika kumtukuza Mungu wa kweli ni kujua, kutumia, na kuwafundisha wengine jina lake la pekee, Yehova. Mtunga-zaburi alitamani sana: “[Watu] wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zaburi 83:18) Jina Yehova lamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Yeye ndiye Mkusudiaji Mkuu, sikuzote yeye hutimiza makusudi yake kwa mafanikio. Jina hilo linamfaa Mungu wa pekee wa kweli tu, kwa sababu wanadamu hawawezi kamwe kuwa na hakika kwamba jitihada zao zitafanikiwa. (Yakobo 4:13, 14) Ni Yehova peke yake anayeweza kusema kwamba neno lake “litafanikiwa” katika mambo yale aliyolituma. (Isaya 55:11) Watu wengi huchangamka sana wanapoona kwa mara ya kwanza jina la Mungu katika Biblia zao na wanapojifunza maana ya jina hilo. (Kutoka 6:3) Lakini watafaidika tu ikiwa ‘watatembea katika jina la Yehova milele.’—Mika 4:5, NW.

13. Kujua jina la Yehova na kutembea katika jina hilo kunamaanisha nini?

13 Zaburi 9:10 yasema hivi kuhusu jina la Mungu: “Wakujuao jina lako wakutumaini Wewe.” Ili kumtumaini Yehova, mengi yanahusika kuliko tu kujua jina lake. Kujua jina la Mungu kunamaanisha kumfahamu vyema Yehova Mungu, kuheshimu mamlaka yake, kutii amri zake, na kumtumaini katika mambo yote. (Mithali 3:5, 6) Vivyo hivyo, kutembea katika jina la Yehova kunamaanisha kujiweka wakfu kwake na kumwakilisha ukiwa mmoja wa waabudu wake, na kuishi kikweli kupatana na mapenzi ya Mungu. (Luka 10:27) Je, unafanya hivyo?

14. Ikiwa tunataka kumtumikia Yehova milele, ni nini kinachohitajiwa mbali na kutimiza tu wajibu?

14 Ikiwa tunataka kumtumikia Yehova milele, hatupaswi kufanya hivyo ili kutimiza wajibu tu. Mtume Paulo alimhimiza hivi Timotheo ambaye alikuwa tayari amemtumikia Yehova kwa miaka mingi: “Uwe ukijizoeza mwenyewe ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha yako.” (1 Timotheo 4:7) Ujitoaji unatokana na kumthamini sana yule unayejitoa kwake. “Ujitoaji-kimungu” ni heshima nyingi na staha anayopewa Yehova peke yake. Unamaanisha kushikamana naye kwa upendo kwa sababu ya kumthamini yeye na njia zake. Hutufanya tuwe na hamu ya kuona jina lake likiheshimiwa na kila mtu. Ni lazima tukuze ujitoaji-kimungu maishani mwetu ikiwa twataka kutembea milele katika jina la Yehova, Mungu wa pekee wa kweli.—Zaburi 37:4; 2 Petro 3:11.

15. Tunawezaje kumpa Mungu ujitoaji wa pekee?

15 Ili Mungu akubali utumishi wetu, ni lazima tumwabudu yeye peke yake, kwa maana yeye ni “Mungu anayetaka ujitoaji wa pekee.” (Kutoka 20:5, NW) Hatuwezi kumpenda Mungu na wakati uleule kuupenda ulimwengu mwovu ambao Shetani ni mungu wake. (Yakobo 4:4; 1 Yohana 2:15-17) Yehova anajua vizuri sifa ambazo kila mmoja wetu anajaribu kukuza. (Yeremia 17:10) Anaona ikiwa kwa kweli tunapenda uadilifu, naye atatusaidia kuvumilia majaribu tunayopata kila siku. Atatutegemeza pia na roho yake takatifu yenye nguvu, ili itusaidie kushinda uovu ulioenea sana ulimwenguni leo. (2 Wakorintho 4:7) Atatusaidia pia kudumisha tumaini lenye nguvu la kuishi milele katika paradiso duniani. Hilo ni tumaini tukufu sana! Tunapaswa kumthamini kabisa na kumtumikia kwa hiari Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, ambaye ametuahidi uhai huo wa milele.

16. Unapaswa ujiunge na mamilioni ya watu wengine kufanya nini?

16 Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wamekubali kwa furaha mwaliko huu wa mtunga-zaburi: “Mtukuzeni BWANA pamoja nami, na tuliadhimishe jina lake pamoja.” (Zaburi 34:3) Yehova anakualika ujiunge na umati mkubwa unaomtukuza katika mataifa yote.

Mazungumzo ya Kurudia

• Yehova ana utu wa aina gani? Tunapata faida gani tunapofahamu vizuri sifa zake?

• Tunawezaje kuwasaidia wengine wajifunze kweli kumhusu Mungu?

• Kujua jina la Yehova na kutembea katika jina hilo kunamaanisha nini?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Yehova ataonyesha upendo wake usio na kifani kwa ‘kuufumbua mkono wake, na kukishibisha kila kilicho hai matakwa yake’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki