Sura Ya Nne
Yule Ambaye Manabii Wote Walimshuhudia
1. Maisha ya Yesu kabla hajawa mwanadamu yanaonyesha nini kuhusu uhusiano wake na Yehova?
“BABA ana shauku na Mwana na humwonyesha mambo yote afanyayo.” (Yohana 5:20) Mwana huyo alikuwa na uhusiano mzuri sana na Yehova, Baba yake. Uhusiano wao ulianza wakati alipoumbwa, muda mrefu sana kabla ya Mwana huyo kuzaliwa akiwa mwanadamu. Alikuwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu kwa sababu yeye peke yake ndiye aliyeumbwa na Yehova moja kwa moja. Vitu vingine vyote mbinguni na duniani viliumbwa kupitia Mwana huyo mzaliwa wa kwanza aliyependwa sana. (Wakolosai 1:15, 16) Alikuwa pia Neno au Msemaji wa Mungu, kwa sababu Ndiye aliyewajulisha wengine mapenzi ya Mungu. Mwana huyo, ambaye Mungu alimpenda sana akaja kuwa mwanadamu Yesu Kristo.—Mithali 8:22-30; Yohana 1:14, 18; 12:49, 50.
2. Unabii wa Biblia umemtaja Yesu kwa kadiri gani?
2 Unabii mwingi sana ulioandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ulieleza kumhusu Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu kabla hajazaliwa kimuujiza akiwa mwanadamu. Mtume Petro alithibitisha jambo hilo alipomwambia hivi Kornelio: “Kwake yeye manabii wote hutoa ushahidi.” (Matendo 10:43) Daraka la Yesu lilikaziwa sana katika Biblia hivi kwamba malaika alimwambia hivi mtume Yohana: “Kutoa ushahidi kuhusu Yesu ndiko hupulizia kutoa unabii.” (Ufunuo 19:10) Unabii huo mbalimbali ulimtambulisha waziwazi kuwa ndiye Mesiya. Unabii huo ulikazia njia mbalimbali ambazo angetimiza makusudi ya Mungu. Twapaswa kupendezwa sana na mambo hayo leo.
Mambo Yaliyofunuliwa na Unabii
3. (a) Katika unabii wa Mwanzo 3:15, ni nani anayewakilishwa na nyoka, “mwanamke,” na ‘mbegu ya nyoka’? (b) Kwa nini ‘kupondwa kwa kichwa cha nyoka’ kungewapendeza sana watumishi wa Yehova?
3 Unabii wa kwanza ulitolewa baada ya uasi katika Edeni. Yehova alimwambia nyoka hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako [“mbegu yako,” NW] na uzao wake [“mbegu yake,” NW]; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Unabii huo ulielekezwa hasa kwa Shetani, ambaye aliwakilishwa na nyoka. “Mwanamke” ni tengenezo la Yehova la mbinguni lenye uaminifu, analoliona kama mke mwaminifu. ‘Mbegu ya nyoka’ yatia ndani malaika na wanadamu wote ambao wanaonyesha roho ya Shetani, wale wanaompinga Yehova na watu Wake. ‘Kupondwa kwa kichwa cha nyoka’ kwamaanisha kuangamizwa kwa yule mwasi Shetani, ambaye alimchongea Yehova na kuwaletea wanadamu huzuni kubwa sana. Lakini ni nani aliye sehemu kuu ya ile “mbegu” ambayo ingemponda nyoka? Hiyo ilikuwa “siri takatifu” kwa miaka mingi.—Waroma 16:20, 25, 26.
4. Ukoo wa Yesu ulimtambulishaje kuwa Mbegu aliyeahidiwa?
4 Baada ya miaka 2,000 ya historia ya wanadamu, Yehova alitoa maelezo zaidi. Alisema kwamba Mbegu huyo angezaliwa katika ukoo wa Abrahamu. (Mwanzo 22:15-18) Hata hivyo, ukoo wa Mbegu huyo haungetegemea urithi bali ungechaguliwa na Mungu. Ijapokuwa Abrahamu alimpenda mwanaye Ishmaeli aliyezaliwa na Hagari, Yehova alisema hivi: “Agano langu nitalifanya imara kwa Isaka, ambaye Sara atakuzalia.” (Mwanzo 17:18-21) Baadaye agano hilo lilirudiwa tena, si kwa mwana-mzaliwa wa kwanza wa Isaka, Esau, bali kwa Yakobo, aliyetokeza yale makabila 12 ya Israeli. (Mwanzo 28:10-14) Baada ya muda, ilithibitishwa kwamba Mbegu huyo angezaliwa katika kabila la Yuda, la ukoo wa Daudi.—Mwanzo 49:10; 1 Mambo ya Nyakati 17:3, 4, 11-14.
5. Yesu alipoanza huduma yake duniani, ni nini kilichothibitisha kwamba alikuwa Mesiya?
5 Ni mambo gani mengine yangemtambulisha Mbegu huyo? Zaidi ya miaka 700 mapema, Biblia ilisema kwamba Mbegu aliyeahidiwa angezaliwa huko Bethlehemu. Ilisema pia kwamba Mbegu huyo tayari alikuwapo “tangu milele,” tangu alipoumbwa huko mbinguni. (Mika 5:2) Pia nabii Danieli alitabiri wakati hususa ambapo huyo Mesiya angetokea duniani. (Danieli 9:24-26) Na Yesu alipotiwa mafuta kwa roho takatifu na kuwa Mtiwa-Mafuta wa Yehova, Mungu mwenyewe aliongea kutoka mbinguni na kumtambulisha kuwa Mwanaye. (Mathayo 3:16, 17) Mbegu alikuwa amefunuliwa! Ndiyo sababu Filipo alisema hivi kwa uhakika: “Tumempata yeye ambaye Musa, katika Sheria, na Manabii waliandika juu yake, Yesu.”—Yohana 1:45.
6. (a) Kulingana na Luka 24:27, baadaye wafuasi wa Yesu walifahamu nini? (b) Ni nani aliye sehemu kuu ya ‘mbegu ya mwanamke,’ na kule kumponda nyoka kichwa kunamaanisha nini?
6 Baadaye, wafuasi wa Yesu walifahamu kwamba Maandiko yaliyoongozwa na Mungu yalikuwa na unabii chungu nzima kumhusu. (Luka 24:27) Hata ikawa wazi kwamba Yesu ndiye sehemu kuu ya ‘mbegu ya mwanamke,’ ambayo ingemponda nyoka kichwa, na hivyo kumwangamiza kabisa Shetani. Kupitia Yesu, Mungu atatimiza ahadi zote ambazo amewaahidi wanadamu na mambo yote ambayo tumekuwa tukitamani.—2 Wakorintho 1:20.
7. Licha ya kumjua Yule anayetajwa na unabii mbalimbali, ni muhimu kutambua nini?
7 Tunapaswa tutendeje baada ya kujua mambo hayo? Biblia inasimulia kisa cha towashi Mwethiopia ambaye alikuwa amesoma baadhi ya unabii kumhusu Mesiya, Mkombozi ambaye angekuja. Akiwa ametatanika, alimwuliza hivi mweneza-evanjeli Filipo: “Ni juu ya nani nabii asema hili?” Lakini towashi huyo hakutosheka tu na jibu alilopewa. Baada ya kusikiliza kwa makini maelezo ya Filipo, mtu huyo alitambua kuwa alihitaji kuchukua hatua fulani ili kuonyesha kwamba anathamini unabii huo. Alitambua kwamba alihitaji kubatizwa. (Matendo 8:32-38; Isaya 53:3-9) Je, tunatenda vivyo hivyo?
8. (a) Tendo la Abrahamu kujaribu kumtoa Isaka lilionyesha nini kimbele? (b) Kwa nini Yehova alimwambia Abrahamu kwamba mataifa yote wangejibarikia kupitia Mbegu yake, na hilo linatufunza nini leo?
8 Fikiria pia kisa chenye kugusa moyo cha Abrahamu akijaribu kumtoa Isaka, mwanaye pekee aliyezaliwa na Sara. (Mwanzo 22:1-18) Tendo hilo lilionyesha kimbele jambo ambalo Yehova angefanya—angemtoa Mwanaye mzaliwa-pekee: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Jambo hilo linatuhakikishia kwamba Yehova ambaye alitimiza kusudi Lake kwa kumtoa Mwanaye mzaliwa-pekee, ‘Atatupatia kwa fadhili vitu vingine vyote.’ (Waroma 8:32) Tunapaswa kufanya nini? Andiko la Mwanzo 22:18 linasema Yehova alimwambia Abrahamu kwamba mataifa yote wangejibarikia kupitia Mbegu yake kwa sababu ‘Abrahamu alitii sauti ya Mungu.’ Sisi pia tunapaswa kumtii Yehova na Mwanaye: “Yeye ambaye hudhihirisha imani katika Mwana ana uhai udumuo milele; yeye ambaye hukosa kutii Mwana hataona uhai, bali hasira ya kisasi ya Mungu hukaa juu yake.”—Yohana 3:36.
9. Ikiwa tunathamini tumaini la kuishi milele linalotegemea dhabihu ya Yesu, tutafanya nini?
9 Ikiwa tunathamini tumaini la kuishi milele ambalo linategemea dhabihu ya Yesu, tutakuwa tayari kutii maagizo ambayo Yehova ametoa kupitia Yesu. Maagizo hayo yanahusu kumpenda Mungu na jirani zetu. (Mathayo 22:37-39) Yesu alisema kwamba upendo wetu kwa Yehova unapaswa kutuchochea tuwafundishe wengine ‘kushika mambo yote ambayo Yesu ametuamuru.’ (Mathayo 28:19, 20) Na tunataka kuwaonyesha upendo watumishi wenzetu wa Yehova kwa “kukusanyika pamoja” nao kwa ukawaida. (Waebrania 10:25; Wagalatia 6:10) Vilevile, tunapomsikiliza Mungu na Mwanaye, tusifikiri kwamba wanatutarajia tuwe wakamilifu. Andiko la Waebrania 4:15 linasema kwamba Yesu, akiwa Kuhani wetu wa Cheo cha Juu, anaweza ‘kushiriki hisia za udhaifu wetu.’ Hilo ni jambo lenye kutia moyo sana, hasa tunaposali kwa Mungu kupitia Kristo na kumwomba msaada ili tushinde udhaifu wetu.—Mathayo 6:12.
Dhihirisha Imani Katika Kristo
10. Kwa nini Yesu Kristo peke yake ndiye anayeweza kutuokoa?
10 Baada ya kuiambia mahakama kuu ya Kiyahudi huko Yerusalemu kwamba Yesu alitimiza unabii wa Biblia, mtume Petro alikata kauli hii thabiti: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina jingine chini ya mbingu ambalo limepewa miongoni mwa watu ambalo kwalo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Matendo 4:12) Kwa kuwa wazao wote wa Adamu ni watenda-dhambi, hakuna yeyote kati yao anaweza kufa na kuwa fidia kwa ajili ya mwenzake. Lakini Yesu alikuwa mkamilifu, na uhai wake ungeweza kutolewa kuwa dhabihu. (Zaburi 49:6-9; Waebrania 2:9) Alimpa Mungu fidia ambayo ililingana kabisa na uhai mkamilifu ambao Adamu alipoteza. (1 Timotheo 2:5, 6) Fidia hiyo imetupatia fursa ya kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu.
11. Eleza jinsi ambavyo dhabihu ya Yesu inaweza kutufaidi sana.
11 Fidia hiyo inatufaidi kwa njia nyingine hata sasa. Kwa mfano, tujapokuwa watenda-dhambi, dhabihu ya Yesu inatuwezesha kuwa na dhamiri safi kwa sababu ya kusamehewa dhambi zetu. Dhabihu za wanyama ambazo Waisraeli walitoa kulingana na Sheria ya Musa hazingeweza kufanya hivyo. (Matendo 13:38, 39; Waebrania 9:13, 14; 10:22) Lakini ili tusamehewe, ni lazima tutambue kwa unyofu kwamba tunahitaji sana dhabihu ya Kristo: “Ikiwa twatoa taarifa: ‘Sisi hatuna dhambi yoyote,’ tunajiongoza wenyewe vibaya na kweli haimo katika sisi. Ikiwa twaungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata kutusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu.”—1 Yohana 1:8, 9.
12. Kwa nini kuzamishwa katika maji ni muhimu ili kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu?
12 Watenda-dhambi wanawezaje kudhihirisha imani katika Kristo na dhabihu yake? Watu katika karne ya kwanza walipokuwa waamini, walionyesha jambo hilo hadharani. Jinsi gani? Walibatizwa. Kwa nini? Kwa sababu Yesu aliamuru kwamba wanafunzi wake wote wabatizwe. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 8:12; 18:8) Mtu anapoguswa moyo na uandalizi wenye upendo ambao Yehova amefanya kupitia Yesu, hatasita kubatizwa. Atafanya mabadiliko yoyote yanayohitajika, na kujiweka wakfu kwa Mungu kupitia sala, na kuonyesha wakfu huo kwa kuzamishwa katika maji. Anapodhihirisha imani katika njia hiyo anatoa ‘ombi kwa Mungu ili kupata dhamiri njema.’—1 Petro 3:21.
13. Tunapaswa kufanya nini tukitambua kwamba tumetenda dhambi, na kwa nini?
13 Bila shaka, bado tutakuwa na tabia fulani zenye dhambi hata baada ya kubatizwa. Tufanye nini? Mtume Yohana alisema: “Nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi. Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi, tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu. Na yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 2:1, 2) Je, hilo linamaanisha kwamba hata tukifanya dhambi gani, Mungu atatusamehe tukimwomba msamaha? Si lazima. Msamaha unategemea toba ya kweli. Huenda pia tukahitaji msaada wa Wakristo wakomavu wenye uzoefu kutanikoni. Ni lazima tukubali kosa letu na kujuta kikweli ili tuweze kujitahidi kabisa kutolirudia tena. (Matendo 3:19; Yakobo 5:13-16) Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu atatusaidia na tutapata tena kibali cha Yehova.
14. (a) Eleza jinsi ambavyo dhabihu ya Yesu imetufaidi sana. (b) Ikiwa tuna imani kwelikweli, tutafanya nini?
14 Dhabihu ya Yesu imewapa wale wa “kundi dogo” yaani, ile sehemu ya pili ya mbegu inayotajwa kwenye Mwanzo 3:15, fursa ya kuishi milele mbinguni. (Luka 12:32; Wagalatia 3:26-29) Dhabihu hiyo pia imewapa mabilioni ya wanadamu nafasi ya kuishi milele katika paradiso duniani. (Zaburi 37:29; Ufunuo 20:11, 12; 21:3, 4) Uhai wa milele ni ‘zawadi ambayo Mungu hutoa kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.’ (Waroma 6:23; Waefeso 2:8-10) Maisha yetu yataonyesha wazi ikiwa tuna imani katika dhabihu hiyo na ikiwa tunauthamini mpango huo. Tukifahamu jinsi ambavyo Yehova amemtumia Yesu kwa njia ya ajabu ili atimize mapenzi Yake, na tukifahamu kwamba tunapaswa kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu, huduma ya Kikristo itakuwa mojawapo ya mambo muhimu zaidi maishani mwetu. Imani yetu itaonekana wazi tunapowaeleza wengine kwa usadikisho kuhusu zawadi hiyo ya pekee kutoka kwa Mungu.—Matendo 20:24.
15. Imani katika Yesu Kristo inaletaje umoja?
15 Lo, imani kama hiyo inaleta umoja ulioje! Imani hiyo inatusaidia kuwa na uhusiano mzuri na Yehova, Mwanaye, na Wakristo wenzetu kutanikoni. (1 Yohana 3:23, 24) Kwa hivyo, tunashangalia kwa sababu kwa fadhili, Yehova amempa Mwanaye “jina lililo juu ya kila jina jingine [isipokuwa jina la Mungu], ili katika jina la Yesu kila goti likunjwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:9-11.
Mazungumzo ya Kurudia
• Kwa nini wale walioliamini kabisa Neno la Mungu walimtambua waziwazi Mesiya alipotokea?
• Tunapaswa kufanya mambo gani ili kuonyesha kwamba tunathamini dhabihu ya Yesu?
• Dhabihu ya Yesu imetufaidi katika njia zipi kufikia sasa? Na inatusaidiaje tunapomwomba Yehova atusamehe dhambi zetu?
[Picha katika ukurasa wa 36]
Yesu aliwaambia wafuasi wake wawafundishe wengine kushika amri za Mungu