Sura ya Tano
Uhuru Unaofurahiwa na Waabudu wa Yehova
1, 2. (a) Mungu alimpa mwanamume na mwanamke wa kwanza uhuru wa aina gani? (b) Taja baadhi ya sheria ambazo ziliongoza utendaji wa Adamu na Hawa.
YEHOVA alipomuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, walifurahia uhuru bora sana kuliko uhuru ambao wanadamu wanao leo. Waliishi katika Paradiso, Bustani maridadi ya Edeni. Walifurahia maisha kabisa kwa sababu hawakupatwa na magonjwa yoyote kwa kuwa walikuwa na akili na miili mikamilifu. Hawakutarajia kufa kama wanadamu walioishi baada yao. Isitoshe, hawakufanya mambo kwa kulazimishwa bali walikuwa na zawadi ya pekee—uhuru wa kujifanyia maamuzi. Hata hivyo, ili kuendelea kufurahia uhuru huo mzuri, walihitaji kuheshimu sheria za Mungu.
2 Kwa mfano, fikiria sheria za asili ambazo Mungu ameweka. Bila shaka sheria hizo hazikuandikwa popote, lakini Adamu na Hawa waliumbwa kwa njia ya kwamba walizitii kiasili. Walipohisi njaa walijua kwamba wanahitaji kula; walipohisi kiu walijua kwamba wanahitaji kunywa; walipoona jua likitua walijua ni wakati wa kulala usingizi. Yehova aliwapa pia kazi ya kufanya. Kazi waliyopewa ilikuwa kama sheria, kwa sababu utendaji wao ulitegemea kazi hiyo. Walipaswa kuzaa watoto, kutawala viumbe wote walio duniani, na kuieneza Paradiso duniani pote. (Mwanzo 1:28; 2:15) Sheria hiyo ilikuwa nzuri na yenye manufaa sana. Iliwapa kazi yenye kufurahisha ambayo iliwawezesha kutumia akili yao kikamili na kwa njia inayonufaisha. Walikuwa pia na uhuru wa kutosha wa kuamua jinsi ambavyo wangetimiza kazi yao. Yehova alitimiza mahitaji yao yote.
3. Adamu na Hawa wangejifunzaje kutumia kwa hekima uhuru wao wa kufanya maamuzi?
3 Bila shaka, Adamu na Hawa walipopewa uhuru wa kufanya maamuzi, haikumaanisha kwamba uamuzi wowote ambao wangefanya ungefaa. Walipaswa kufanya maamuzi kulingana na sheria na kanuni za Mungu. Wangejifunzaje sheria na kanuni za Mungu? Kwa kumsikiliza Muumba wao na kwa kuchunguza kazi zake. Mungu aliwapa Adamu na Hawa akili ya kutumia mambo waliyojifunza. Wangekuwa na mwelekeo wa kuonyesha sifa za Mungu wanapofanya maamuzi kwa sababu waliumbwa wakiwa wakamilifu. Kwa kweli, wangejitahidi kufanya hivyo iwapo walithamini kwelikweli mambo ambayo Mungu aliwafanyia na iwapo walitaka kumpendeza.—Mwanzo 1:26, 27; Yohana 8:29.
4. (a) Je, amri ambayo Adamu na Hawa walipewa ya kutokula matunda ya mti mmoja iliwanyima uhuru? (b) Kwa nini sheria hiyo ilifaa?
4 Kwa kufaa, Mungu aliamua kujaribu ujitoaji wao kwake akiwa Mpaji-Uhai na kujua kama wangevuka mipaka ambayo aliwawekea. Yehova alimwamuru Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Hawa pia alijulishwa sheria hiyo baada ya kuumbwa. (Mwanzo 3:2, 3) Je, sheria hiyo iliwanyima uhuru? La hasha. Hawakuhitaji kula matunda ya ule mti mmoja kwa sababu walikuwa na chakula chenye kupendeza cha kila aina. (Mwanzo 2:8, 9) Walipaswa kutambua kwamba dunia ni mali ya Mungu kwa kuwa ndiye aliyeiumba. Kwa hiyo ana haki ya kutunga sheria ambazo zinafaa kusudi lake na zinazowafaidi wanadamu.—Zaburi 24:1, 10.
5. (a) Adamu na Hawa walipotezaje uhuru wao mtukufu? (b) Badala ya kufurahia uhuru, Adamu na Hawa walitumbukia katika hali gani, na hali hiyo imetuathirije?
5 Lakini ni nini kilichotukia? Malaika mmoja alichochewa na tamaa ya makuu, akatumia vibaya uhuru wake hivyo akawa Shetani, yaani, “Mpinzani.” Alimdanganya Hawa kwa kumpa ahadi ambayo ilikuwa kinyume cha mapenzi ya Mungu. (Mwanzo 3:4, 5) Adamu alijiunga na Hawa wakavunja sheria ya Mungu. Walipoteza uhuru wao mtukufu walipochukua kitu ambacho hakikuwa chao. Walitumbukia katika dhambi na mwishowe wakafa kama Mungu alivyokuwa amewaonya. Wazao wao walirithi dhambi, na mwelekeo wao wa kufanya makosa unathibitisha jambo hilo. Dhambi ilitokeza pia udhaifu ambao unasababisha magonjwa, uzee, na kifo. Mwelekeo wa kufanya makosa, ukichochewa na uvutano wa Shetani, umetokeza jamii iliyojaa chuki, uhalifu, ukandamizaji, na vita ambavyo vimesababisha vifo vya mamilioni ya watu. Hali hiyo ni tofauti kabisa na uhuru ambao Mungu aliwapa wanadamu mwanzoni.—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Ayubu 14:1, 2; Waroma 5:12; Ufunuo 12:9.
Mahali Ambapo Uhuru Unaweza Kupatikana
6. (a) Uhuru wa kweli unaweza kupatikana wapi? (b) Yesu alikuwa akizungumzia uhuru wa aina gani?
6 Haishangazi kwamba watu wanatamani kupata uhuru zaidi kwa sababu ya hali mbaya zilizoenea leo. Lakini uhuru wa kweli unaweza kupatikana wapi? Yesu alisema hivi: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:31, 32) Huu si uhuru ambao wanadamu hutafuta wanapomkataa mtawala mmoja au serikali moja na kumchagua mtawala mpya au serikali mpya. Badala yake, uhuru huu unafikia kiini cha matatizo ya wanadamu. Yesu alikuwa akizungumzia uhuru kutoka katika utumwa wa dhambi. (Yohana 8:24, 34-36) Kwa hiyo, mtu anapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, maisha yake yanabadilika, anakuwa huru!
7. (a) Tunaweza kuwa huru kutokana na dhambi sasa katika maana gani? (b) Ni lazima tufanye nini ili tuwe huru kutokana na dhambi?
7 Hilo halimaanishi kwamba hivi sasa Wakristo wa kweli hawaathiriwi na mwelekeo wa kutenda dhambi ambao wamerithi. Bado wanapambana na dhambi ambayo wamerithi. (Waroma 7:21-25) Hata hivyo, mtu akifuata kabisa mafundisho ya Yesu maishani mwake, hatakuwa tena mtumwa wa dhambi. Dhambi haitamtawala tena kama mtawala katili anayewalazimisha watu kufuata amri zake. Hataishi tena maisha yasiyo na kusudi yanayochafua dhamiri yake. Atakuwa na dhamiri safi mbele za Mungu kwa sababu dhambi zake za zamani zitakuwa zimesamehewa kwa msingi wa imani katika dhabihu ya Kristo. Huenda akashawishiwa na mielekeo ya dhambi, lakini anaonyesha kwamba hatawaliwi na dhambi kwa kukataa kufuata mielekeo hiyo anapokumbuka mafundisho safi ya Kristo.—Waroma 6:12-17.
8. (a) Ukristo wa kweli unatuweka huru kutokana na mambo gani? (b) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu watawala wa serikali?
8 Fikiria uhuru ambao sisi Wakristo tunafurahia. Tumewekwa huru kutokana na mafundisho ya uwongo, utumwa wa dhambi na ushirikina. Kweli bora sana kuhusu hali ya wafu na ufufuo zimetuweka huru kutokana na hofu isiyofaa ya kifo. Hatukati tamaa kwa sababu tunajua kwamba Ufalme mwadilifu wa Mungu utaondoa serikali za wanadamu wasio wakamilifu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Hata hivyo, hiyo si sababu ya kutoheshimu serikali za wanadamu na sheria zake.—Tito 3:1, 2; 1 Petro 2:16, 17.
9. (a) Yehova anatusaidiaje kwa upendo tufurahie kadiri kubwa zaidi ya uhuru ambao wanadamu wanaweza kuwa nao sasa? (b) Tunawezaje kufanya maamuzi yenye hekima?
9 Yehova hatuachi tujitafutie njia bora ya maisha kwa kukisia-kisia. Anajua maumbile yetu, anajua mambo yanayotuletea furaha ya kweli, na mambo yanayoweza kutufaidi milele. Anajua mawazo na mwenendo unaoweza kuharibu uhusiano wetu pamoja Naye na pia pamoja na wanadamu wenzetu, au hata mwenendo unaoweza kumzuia mtu asiingie katika ulimwengu mpya. Kwa upendo, Yehova anatumia Biblia na tengenezo lake linaloonekana kutujulisha mambo hayo yote. (Marko 13:10; Wagalatia 5:19-23; 1 Timotheo 1:12, 13) Halafu ni juu yetu kutumia uhuru wetu wa kufanya maamuzi ambao Mungu ametupatia kuamua hatua tutakayochukua. Tukitii maagizo ya Biblia tutafanya maamuzi yenye hekima tofauti na Adamu aliyefanya maamuzi yasiyofaa. Tutaonyesha kwamba jambo muhimu maishani mwetu ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova.
Watu Wengine Hutamani Uhuru wa Aina Nyingine
10. Baadhi ya Mashahidi wa Yehova wametamani uhuru wa aina gani?
10 Nyakati nyingine vijana na vilevile watu fulani wazima ambao ni Mashahidi wa Yehova hutamani uhuru wa aina nyingine. Huenda ulimwengu ukaonekana kuwa wenye kuvutia sana, na kadiri wanavyozidi kufikiria mambo yake ndivyo wanavyozidi kutamani kufanya mambo yanayovunja kanuni za Kikristo ambayo yanapendwa ulimwenguni. Huenda wasiwe na nia ya kutumia dawa za kulevya, kulewa, au kufanya uasherati. Lakini wanaanza kushirikiana na watu ambao si Wakristo wa kweli ili wapendwe nao. Wanaweza hata kuanza kuiga usemi na mwenendo wao.—3 Yohana 11.
11. Nyakati nyingine ni nani wanaowashawishi wengine watende maovu?
11 Nyakati nyingine yule anayewashawishi wengine watende maovu ni mtu anayedai kuwa mtumishi wa Yehova. Ndivyo ilivyotukia kwa Wakristo fulani wa mapema, na inaweza kutukia hivyo siku zetu. Mara nyingi watu hao hutaka kufanya mambo ambayo wanafikiri yatawaletea raha, mambo ambayo ni kinyume cha sheria za Mungu. Wanawahimiza wengine waponde “raha.” ‘Wanawaahidi uhuru, na wao wenyewe ni watumwa wa ufisadi.’—2 Petro 2:19.
12. Mwenendo ulio kinyume cha sheria na kanuni za Mungu husababisha matokeo gani yenye kuhuzunisha?
12 Uhuru huo usiofaa huwa na matokeo mabaya sikuzote, kwa sababu unavunja sheria za Mungu. Kwa mfano, mtu anayefanya uasherati anaweza kufadhaika sana, kuambukizwa ugonjwa, kufa, kupata mimba haramu, na ndoa yake inaweza kuvunjika. (1 Wakorintho 6:18; 1 Wathesalonike 4:3-8) Mtu anayetumia dawa za kulevya anaweza kuwa na matatizo ya kuudhika-udhika, kuzungumza kwa shida, kutoona vizuri, kizunguzungu, kutopumua vizuri, kupumbaa kiakili, na hata anaweza kufa. Dawa za kulevya zinaweza kumtawala mtu na kumlazimisha afanye uhalifu ili apate fedha za kununua dawa hizo. Ulevi pia huwa na matokeo hayohayo. (Mithali 23:29-35) Wale wanaotenda mambo hayo wanaweza kufikiri kwamba wako huru, lakini wanajuta baadaye wanapokuwa watumwa wa dhambi. Na watumwa wa dhambi huona cha mtema kuni! Kufikiria jambo hilo kwa uzito sasa kwaweza kutulinda tusiumie.—Wagalatia 6:7, 8.
Chanzo cha Matatizo
13. (a) Mara nyingi, tamaa zinazosababisha matatizo huchochewa na nini? (b) Ili kuelewa maana ya “mashirika mabaya,” tunahitaji kufahamu maoni ya nani kuhusu jambo hilo? (c) Unapojibu maswali yaliyoorodheshwa kwenye fungu la 13, kazia maoni ya Yehova.
13 Hebu fikiria chanzo kikuu cha matatizo hayo. Biblia inaeleza: “Kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi; nayo, dhambi, wakati imetimilika, hutokeza kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Ni nini kinachoichochea tamaa hiyo? Mambo yanayoingia akilini. Mara nyingi ni kwa sababu ya kushirikiana na watu wasiofuata kanuni za Biblia. Bila shaka sote tunajua kwamba tunapaswa kuepuka “mashirika mabaya.” (1 Wakorintho 15:33) Lakini ni nani walio mashirika mabaya? Yehova ana maoni gani kuhusu mashirika mabaya? Tutapata majibu yanayofaa kwa kutafakari maswali yafuatayo na kusoma maandiko yaliyotajwa.
Hata ingawa watu fulani wanaonekana kuwa wenye kuheshimika, je, hilo linawafanya wawe mashirika mazuri? (Mwanzo 34:1, 2, 18, 19)
Je, tunaweza kujua iwapo wao ni mashirika mazuri kupitia mazungumzo yao au mizaha yao? (Waefeso 5:3, 4)
Yehova anahisije tunaposhirikiana na watu ambao hawampendi? (2 Mambo ya Nyakati 19:1, 2)
Ingawa tunafanya kazi na watu ambao si waamini wenzetu au kusoma pamoja nao shuleni, kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu? (1 Petro 4:3, 4)
Tunaweza kushirikiana na watu wengine kwa kutazama televisheni na sinema, kutumia Internet, na kwa kusoma vitabu na magazeti. Tunahitaji kuepuka habari zipi katika vyombo hivyo vya habari? (Mithali 3:31; Isaya 8:19; Waefeso 4:17-19)
Yehova anatuona tukiwa watu wa aina gani anapoangalia mashirika yetu? (Zaburi 26:1, 4, 5; 97:10)
14. Wale wanaofuata mashauri ya Neno la Mungu kwa uaminifu sasa watapata uhuru gani mtukufu?
14 Ulimwengu mpya wa Mungu utakuja hivi karibuni. Serikali ya Mungu ya Ufalme wa mbinguni itawaweka wanadamu huru kutokana na ushawishi wa Shetani na ulimwengu wake mwovu. Matokeo yote ya dhambi yataondolewa hatua kwa hatua, na wanadamu watiifu watakuwa wakamilifu kiakili na kimwili, na hivyo basi kuweza kufurahia kuishi milele katika Paradiso. Hatimaye, viumbe wote watafurahia uhuru ambao unapatana kabisa na “roho ya Yehova.” (2 Wakorintho 3:17) Je, lingekuwa jambo la busara kukosa mambo hayo yote kwa sababu ya kupuuza mashauri ya Neno la Mungu sasa? Na tuonyeshe sote kwamba kwa kweli tunataka “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu,” kwa kutumia kwa hekima uhuru wetu wa Kikristo leo.—Waroma 8:21.
Mazungumzo ya Kurudia
• Wenzi wawili wa kwanza walifurahia uhuru gani? Na hali ya wanadamu leo ikoje inapolinganishwa na hali waliyokuwa nayo?
• Wakristo wa kweli wana uhuru gani? Na uhuru huo unatofautianaje na uhuru wa ulimwengu?
• Kwa nini ni muhimu sana kuepuka mashirika mabaya? Tofauti na Adamu, tunafuata uamuzi wa nani kuhusu yaliyo mabaya?
[Picha katika ukurasa wa 46]
Neno la Mungu linaonya hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa”