Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kp kur. 9-11
  • Maisha Yako Yanaelekea Wapi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maisha Yako Yanaelekea Wapi?
  • Endeleeni Kukesha!
  • Habari Zinazolingana
  • Ungejibuje?
    Amkeni!—2007
  • Ungejibuje?
    Amkeni!—2007
  • Mazungumzo ya Familia
    Amkeni!—2010
  • Ungejibuje?
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Endeleeni Kukesha!
kp kur. 9-11

Maisha Yako Yanaelekea Wapi?

• Watu wengi hujishughulisha mno na maisha ya kila siku hivi kwamba hawafikirii wanakoelekea.

• Biblia inatujulisha matukio mazuri yaliyo mbele. Pia inatuonya kuhusu mabadiliko makubwa yatakayokumba mashirika ya wanadamu ulimwenguni pote. Ili tupate faida na kuepuka msiba, tunahitaji kuchukua hatua inayofaa haraka.

• Watu fulani wanajua yale ambayo Biblia inasema na wanajaribu kuyafuata lakini wanaacha mahangaiko ya maisha yawakengeushe.

• Je, wewe unaridhika na mwelekeo wa maisha yako? Unapopanga mambo, je, wewe hufikiria jinsi mambo hayo yanavyoweza kuathiri miradi yako ya wakati ujao?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Ni Nini Kilicho Muhimu Sana Kwako?

Mambo yafuatayo ni muhimu kwako kadiri gani? Yaorodheshe ukianza na lililo muhimu zaidi.

Mengi ya mambo haya ni muhimu maishani, lakini inapokuwa lazima uchague, utaweka jambo gani kwanza? pili? na kadhalika.

․․․ Vitumbuizo/tafrija

․․․ Kazi yangu

․․․ Afya yangu

․․․ Furaha yangu

․․․ Mwenzi wangu wa ndoa

․․․ Wazazi wangu

․․․ Watoto wangu

․․․ Nyumba nzuri, nguo nzuri

․․․ Kufanikiwa kabisa katika lolote nifanyalo

․․․ Kumwabudu Mungu

[Sanduku katika ukurasa wa 10, 11]

Je, Maamuzi Yako Yanakuelekeza Unakotaka Kwenda?

FIKIRIA MASWALI HAYA

VITUMBUIZO/TAFRIJA: Je, tafrija ninayochagua huniburudisha? Je, ninashiriki michezo inayosisimua ambayo inaweza kuhatarisha uhai wangu au hata kunilemaza kabisa? Je, ni “raha” inayosisimua kwa saa chache tu lakini inayoweza kuleta madhara ya kudumu? Hata kama vitumbuizo ninavyochagua vinafaa, je, vinachukua wakati mwingi hivi kwamba sipati wakati wa kufanya mambo yaliyo muhimu zaidi?

KAZI YANGU: Je, inanisaidia kupata mahitaji ya lazima, au nimekuwa mtumwa wake? Je, inahitaji nguvu na wakati mwingi hivi kwamba inahatarisha afya yangu? Je, mimi huchagua kufanya kazi saa za ziada badala ya kuwa pamoja na mwenzi wangu au watoto wangu? Mwajiri wangu akitaka nifanye kazi ambayo inasumbua dhamiri yangu au ambayo mara nyingi huchukua wakati wa shughuli za kiroho, je, nitaifanya ili nisifutwe?

AFYA YANGU: Je, mimi hupuuza afya yangu au huitunza kwa uangalifu sikuzote? Je, mimi huongea juu ya afya yangu kila wakati? Je, ninaitunza afya yangu kwa njia inayoonyesha kwamba ninaijali familia yangu?

FURAHA YANGU: Je, furaha yangu ndilo jambo la kwanza maishani? Je, ninatanguliza furaha yangu badala ya furaha ya mwenzi wangu au ya familia yangu? Je, ninatafuta furaha kwa njia inayoonyesha kwamba mimi ni mwabudu wa Mungu wa kweli?

MWENZI WANGU WA NDOA: Je, mimi humwona mwenzi wangu kuwa rafiki yangu wakati tu kufanya hivyo kunanifurahisha? Je, mimi humheshimu mwenzi wangu na kuona kuwa anastahili heshima? Je, imani yangu katika Mungu inaongoza jinsi ninavyomwona mwenzi wangu?

WAZAZI WANGU: Ikiwa mimi ni mtoto, je, ninawatii wazazi wangu—ninawajibu kwa heshima, ninafanya kazi za nyumbani wanazonipa, ninarudi nyumbani saa walizoweka, ninaepuka mashirika na mambo wanayokataza? Ikiwa mimi ni mtu mzima, je, mimi huwasikiliza wazazi wangu kwa heshima na kuwapa msaada unaofaa wanapouhitaji? Je, ninashughulika nao nitakavyo au ninaongozwa na shauri la Neno la Mungu?

WATOTO WANGU: Je, ninahisi kwamba nina daraka la kuwafundisha watoto wangu maadili yanayofaa au ninawaachia walimu daraka hilo? Je, mimi hutumia wakati pamoja na watoto wangu au huwaacha watumie wakati mwingi wakicheza na vitu vya kuchezea, wakitazama televisheni au kutumia kompyuta? Je, mimi huwatia nidhamu watoto wangu kila mara wanapopuuza vikumbusho vya Mungu, au mimi huwatia nidhamu wanaponikasirisha tu?

NYUMBA NZURI, NGUO NZURI: Ni nini kinachoamua jinsi ninavyovaa na kujipamba na vitu ninavyonunua? Je, ni kutaka kuwavutia jirani zangu? Je, ni mahitaji ya familia yangu? Je, ni kwa sababu mimi ni mwabudu wa Mungu?

KUFANIKIWA KABISA KATIKA LOLOTE NIFANYALO: Je, ninaona ni muhimu kufanya mambo vyema kabisa? Je, ninajitahidi kufanya mambo kwa njia bora kuliko mtu mwingine yeyote? Je, ninafadhaika mtu mwingine akifanya jambo kwa njia bora kuliko mimi?

IBADA YA MUNGU: Je, kupata kibali cha Mungu ni muhimu kwangu kuliko kupata kibali cha mwenzi wangu, watoto wangu, wazazi wangu, au mwajiri wangu? Je, ningeacha maisha ya raha yachukue mahali pa utumishi wangu kwa Mungu?

FIKIRIA KWA MAKINI SHAURI LA BIBLIA

Ibada ya Mungu ni muhimu kwako kadiri gani?

Mhubiri 12:13: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”

JIULIZE: Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba ninafuata andiko hilo? Je, ninatii amri za Mungu kwa kutekeleza madaraka yangu nyumbani, kazini, au shuleni? Au je, mambo mengine au mikazo ya maisha huamua ikiwa nitapata wakati wa kumtumikia Mungu?

Una uhusiano gani na Mungu?

Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

Mathayo 4:10: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”

JIULIZE: Je, ninahisi hivyo kumhusu Mungu? Je, shughuli zangu za kila siku na jinsi ninavyokabiliana na matatizo kunaonyesha kwamba nimejitoa kwa Mungu na ninamtumaini?

Kusoma na kujifunza Biblia ni muhimu kwako kadiri gani?

Yohana 17:3: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”

JIULIZE: Je, ninaonyesha kwamba ninaamini maneno hayo kwa kusoma Neno la Mungu na kulitafakari kwa bidii?

Kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya kutaniko ni muhimu kwako kadiri gani?

Waebrania 10:24, 25: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, . . . na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.”

Zaburi 122:1: “Nilishangilia walipokuwa wakiniambia: ‘Na twende katika nyumba ya Yehova.’”

JIULIZE: Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba ninathamini mwongozo huo unaopatikana katika Neno la Mungu? Je, nilikosa kuhudhuria mkutano wowote wa Kikristo mwezi uliopita kwa sababu ya kutanguliza mambo mengine?

Je, unawahubiria wengine kwa bidii kumhusu Mungu na kusudi lake?

Mathayo 24:14: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi . . . , na ndipo ule mwisho utakapokuja.”

Mathayo 28:19, 20: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”

Zaburi 96:2: “Mwimbieni Yehova, libarikini jina lake. Tangazeni habari njema za wokovu wake siku baada ya siku.”

JIULIZE: Je, utendaji huu ni muhimu maishani mwangu? Je, jitihada zangu katika utendaji huu zinaonyesha kwamba ninasadiki kuwa tunaishi nyakati za hatari?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki