Habari za Ufalme Na. 37
Ujumbe kwa Ulimwengu Wote
Mwisho Wa Dini Ya Uwongo Unakaribia!
▪ Dini ya uwongo ni nini?
▪ Itakomeshwaje?
▪ Je, utaokoka itakapokomeshwa?
Dini ya Uwongo Ni Nini?
Je, wewe huhangaishwa na mambo mabaya yanayofanywa na dini? Je, wewe huudhiwa na matendo yasiyo ya haki kama vile vita, ugaidi, na ufisadi unaofanywa na watu wanaodai kumtumikia Mungu? Kwa nini inaonekana kwamba dini ndiyo chanzo cha matatizo mengi?
Si dini zote zinazopaswa kulaumiwa, bali ni dini ya uwongo. Yesu Kristo, ambaye anaheshimiwa na dini nyingi alisema kwamba dini ya uwongo hufanya watu watende maovu, kama vile “mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.” (Mathayo 7:15-17) Dini ya uwongo huzaa matunda gani?
Dini ya Uwongo . . .
◼ HUJIINGIZA KATIKA VITA NA SIASA: Gazeti Asiaweek linasema: “Barani Asia na sehemu nyingine, viongozi wenye kujitakia makuu huongoza kwa hila maoni ya watu kuhusu dini kwa faida yao wenyewe.” Kwa sababu hiyo, gazeti hilo linaonya: “Ni kana kwamba ulimwengu unaelekea kushikwa na kichaa.” Kiongozi mmoja mashuhuri wa kidini nchini Marekani alisema hivi: “Lazima uwaue magaidi ili kukomesha mauaji.” Anapendekeza suluhisho gani? “Walipue wote katika jina la Bwana.” Kinyume cha hilo, Biblia inasema: “Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo.” (1 Yohana 4:20) Hata Yesu alisema: “Endeleeni kuwapenda adui zenu.” (Mathayo 5:44) Karibu wafuasi wa dini zote hujiingiza katika vita!
◼ HUENEZA MAFUNDISHO YA UWONGO: Dini nyingi hufundisha kwamba mwanadamu ana nafsi au roho isiyoonekana ambayo huendelea kuishi mwili unapokufa. Kwa kutumia fundisho hilo, dini nyingihupunja washiriki wake kwa kuwatoza pesa ili kuombea nafsi za waliokufa. Hata hivyo, Biblia inafundisha jambo tofauti. “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4) “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Yesu alifundisha kwamba wafu watafufuliwa. Ufufuo haungekuwa wa lazima ikiwa wanadamu wangekuwa na nafsi isiyoweza kufa. (Yohana 11:11-25) Je, dini yako inafundisha kwamba nafsi haifi?
◼ HAISHUTUMU NGONO ZISIZO ZA ADILI: Katika nchi za Magharibi, vikundi vya kidini huwatawaza wanaume wanaolala na wanaume na wanawake wanaolala na wanawake kuwa makasisi na kuhimiza serikali zitambue ndoa kati ya watu wa jinsia moja. Hata dini ambazo hushutumu uasherati zimewavumilia viongozi wa kidini ambao wamewatendea watoto vibaya kingono. Lakini Biblia inafundisha nini? Inasema hivi waziwazi: “Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume . . . hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Je, unajua dini ambazo huvumilia ngono zisizo za adili?
Dini zinazozaa matunda yaliyooza zitapatwa na nini? Yesu alionya hivi: “Kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa ndani ya moto.” (Mathayo 7:19) Kwa hakika, dini ya uwongo itakatwa na kuharibiwa! Lakini itaharibiwaje na hilo litatukia lini? Maono ya kinabii yaliyoandikwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, sura ya 17 na 18 yanatoa jibu.
Dini ya uwongo itakomeshwaje?
Hebu wazia. Kahaba ameketi juu ya mgongo wa mnyama mwenye kutisha. Mnyama huyo ana vichwa saba na pembe kumi. (Ufunuo 17:1-4) Kahaba huyo anawakilisha nani? Ana uvutano “juu ya wafalme wa dunia.” Amevaa mavazi ya zambarau, anatumia uvumba, na ana mali nyingi sana. Pia, ‘mataifa yote yamepotoshwa’ kwa mazoea yake ya kuwasiliana na pepo. (Ufunuo 17:18; 18:12, 13, 23) Biblia inatusaidia kutambua kwamba kahaba huyo anawakilisha dini zote za uwongo ulimwenguni. Hawakilishi dini moja tu bali dini zote zinazozaa matunda yaliyooza.
Mnyama ambaye kahaba huyo amempanda anawakilisha serikali za kisiasa za ulimwengu.a (Ufunuo 17:10-13) Dini ya uwongo imepanda juu ya mgongo wa mnyama huyo wa kisiasa, ikijaribu kuathiri maamuzi yake na kumwongoza.
Hata hivyo, hivi karibuni jambo lenye kushangaza litatukia. “Zile pembe kumi ulizoona, na yule mnyama-mwitu, hawa watamchukia yule kahaba na kumfanya kuwa ukiwa na uchi, nao watakula sehemu zake zenye nyama na kumteketeza kabisa kwa moto.” (Ufunuo 17:16) Ghafula bin vuu, serikali za kisiasa za ulimwengu zitashambulia dini ya uwongo na kuiangamiza kabisa! Ni nini kitakachozichochea kuchukua hatua hiyo? Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinajibu: “Mungu alitia hilo ndani ya mioyo yao ili kutekeleza wazo lake.” (Ufunuo 17:17) Naam, Mungu atatoza dini ya uwongo hesabu kwa sababu ya mambo yenye kuchukiza ambayo imefanya katika jina lake. Akitenda kupatana na haki yake, ataangamiza dini ya uwongo akitumia serikali za kisiasa ambazo ni rafiki za dini hizo.
Unapaswa kufanya nini ikiwa hutaki kuharibiwa pamoja na dini ya uwongo? Mjumbe wa Mungu anatuhimiza hivi: “Tokeni kwake, watu wangu.” (Ufunuo 18:4) Kwa kweli, sasa ndio wakati wa kukimbia kutoka katika dini ya uwongo! Lakini utakimbilia wapi? Si kwa watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu kwa kuwa wao pia hawana tumaini lolote la wakati ujao. (2 Wathesalonike 1:6-9) Kimbilio pekee ni katika dini ya kweli. Unaweza kuitambuaje dini ya kweli?
Jinsi ya kuitambua dini ya kweli
Dini ya kweli inapaswa kuzaa matunda gani mazuri?—Mathayo 7:17.
Dini ya Kweli . . .
◼ INATAMBULISHWA KWA UPENDO: Waabudu wa kweli “si sehemu ya ulimwengu,” hawana migawanyiko ya kijamii au kitamaduni, nao wana ‘upendo kati yao wenyewe.’ (Yohana 13:35; 17:16; Matendo 10:34, 35) Badala ya kuuana, kila mmoja yuko tayari kufa kwa ajili ya mwenzake.—1 Yohana 3:16.
◼ INATUMAINI NENO LA MUNGU: Badala ya kufundisha “mapokeo” na “amri za wanadamu kuwa mafundisho,” dini ya kweli hufundisha mambo yanayotegemea Neno la Mungu, Biblia. (Mathayo 15:6-9) Kwa nini? Kwa sababu “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.
◼ INAIMARISHA FAMILIA NA KUFUATA KANUNI ZA JUU ZA MAADILI: Dini ya kweli huwafundisha ‘waume kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe,’ huwasaidia wake ‘kuwaheshimu sana waume zao,’ na huwafundisha watoto ‘kuwatii wazazi wao.’ (Waefeso 5:28, 33; 6:1) Kwa kuongezea, wale walio na madaraka wanapaswa kuwa na maadili mazuri.—1 Timotheo 3:1-10.
Je, kuna dini inayotimiza viwango hivyo? Kitabu Holocaust Politics, kilichochapishwa mwaka wa 2001, kinasema: “Ikiwa watu wengi zaidi wangefuata mafundisho na mwenendo wa Mashahidi wa Yehova, yale Maangamizi Makubwa ya Wayahudi hayangalitukia wala hakungalikuwa tena na mauaji ya jamii nzima-nzima ulimwenguni.”
Kwa kweli, katika nchi 235, Mashahidi wa Yehova hawahubiri tu kuhusu viwango vya maadili vya Biblia, bali pia wanafuata viwango hivyo maishani. Tunakuhimiza uwaulize Mashahidi wa Yehova wakusaidie kujifunza matakwa ya Mungu ili uweze kumwabudu kwa njia anayoikubali. Unahitaji kuchukua hatua sasa. Usikawie. Mwisho wa dini ya uwongo unakaribia!—Sefania 2:2, 3.
Ikiwa ungependa habari zaidi kuhusu ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova huhubiri, wasiliana nao kwa kutumia anwani iliyoonyeshwa hapa.
□ Ningependa kupokea broshua Endeleeni Kukesha! bila malipo.
□ Ningependa kujifunza Biblia nyumbani kwangu bila malipo.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi kuhusu habari hii, ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Dini ya uwongo ina uvutano “juu ya wafalme wa dunia”
[Blabu katika ukurasa wa 3]
“Tokeni kwake, watu wangu”