SEHEMU YA 5
Mungu Ambariki Abrahamu na Familia Yake
Wazao wa Abrahamu wapata ufanisi. Mungu amlinda Yosefu nchini Misri
YEHOVA alijua kwamba kuna wakati ambapo mwana wake mpendwa atateseka na kufa. Unabii uliorekodiwa katika Mwanzo 3:15 ulidokeza hilo. Je, Mungu angeweza kuwasaidia wanadamu waelewe jinsi kifo cha mwana wake kingemhuzunisha? Biblia ina mfano halisi uliotokea. Mungu alimwagiza Abrahamu amtoe dhabihu Isaka mwana wake mpendwa.
Abrahamu alikuwa na imani kubwa. Kumbuka kwamba Mungu alikuwa ameahidi kwamba Mkombozi, au Uzao ulioahidiwa, angetokea katika ukoo wa Isaka. Akiwa na imani kwamba Mungu atamfufua Isaka ikihitajika, Abrahamu alikuwa tayari kutii na kumtoa mwana wake mwenyewe awe dhabihu. Lakini malaika wa Mungu akamzuia Abrahamu dakika ya mwisho. Akimsifu Abrahamu kwa nia yake ya kumtolea Mungu kitu kilichokuwa na thamani zaidi kwake, Mungu alirudia ahadi Yake aliyokuwa amemtolea.
Baadaye, Isaka alipata wana wawili, Esau na Yakobo. Tofauti na Esau, Yakobo alithamini mambo ya kiroho naye akathawabishwa. Mungu alibadili jina la Yakobo likawa Israeli, na wana 12 wa Israeli wakawa vichwa vya makabila ya Israeli. Lakini familia hiyo ilipataje kuwa taifa kubwa?
Mambo yalianza wakati ambapo wengi kati ya wana hao walianza kumwonea kijicho Yosefu, ndugu yao mdogo. Walimuuza utumwani, naye akapelekwa Misri. Hata hivyo Mungu alimbariki kijana huyo mwenye ujasiri. Ijapokuwa alikabili hali ngumu, Yosefu aliteuliwa na Farao, mtawala wa Misri, na kupewa mamlaka kubwa. Hilo lilitokea wakati barabara, kwa kuwa njaa kali ilimfanya Yakobo awatume baadhi ya wana wake waende Misri kununua vyakula—naye Yosefu ndiye aliyekuwa akisimamia ugawanyaji wa chakula! Baada ya kuungana tena na ndugu zake wenye toba, Yosefu aliwasamehe na kupanga familia nzima ihamie Misri. Walipewa eneo zuri sana, ambapo wangeweza kukaa na kupata ufanisi. Yosefu alielewa kwamba Mungu alikuwa ameelekeza mambo hivyo ili atimize ahadi Zake.
Yakobo alimalizia maisha yake huko Misri, akiwa na familia yake iliyokuwa ikizidi kuongezeka. Alipokuwa akikaribia kufa, alitabiri kwamba Mkombozi, au Uzao ulioahidiwa, angekuwa Mtawala mwenye nguvu ambaye angezaliwa katika ukoo wa mwana wake Yuda. Kabla hajafa miaka kadhaa baadaye, Yosefu alitabiri kwamba siku moja, Mungu angeitoa familia ya Yakobo nchini Misri.
—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 20 hadi 50; Waebrania 11:17-22.