Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kr sura 20 kur. 209-219
  • Kazi ya Kutoa Msaada

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kazi ya Kutoa Msaada
  • Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Kazi ya Kutoa Msaada Ni “Utumishi Mtakatifu”?
  • Kazi ya Kutoa Msaada Iliyo na Makusudi Hususa
  • Huduma ya Kutoa Msaada Huleta Faida za Kudumu
  • Je, Unaweza Kushiriki?
  • Jinsi ya Kusaidia Baada ya Janga
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Je, Mashahidi wa Yehova Hutoa Misaada Wakati wa Misiba?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Kukua Pamoja Katika Upendo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutoa Msaada Katika 2023—⁠“Tumejionea Wenyewe Upendo wa Yehova”
    Jinsi Michango Yako Inavyotumiwa
Pata Habari Zaidi
Ufalme wa Mungu Unatawala!
kr sura 20 kur. 209-219

SURA YA 20

Kazi ya Kutoa Msaada Humtukuza Yehova

WAZO KUU KATIKA SURA HII

Upendo wa Kikristo unaonyeshwa nyakati za misiba

1, 2. (a) Wakristo huko Yudea walikabili hali gani ngumu? (b) Wakristo walioishi Yudea walionyeshwaje upendo?

NI KARIBU mwaka wa 46 W.K., eneo la Yudea limeathiriwa na njaa kali. Wayahudi ambao ni wanafunzi wa Kristo wanaoishi katika eneo hilo hawana pesa za kununua chakula kinachouzwa ghali kwa sababu ya uhaba wa nafaka. Wanakaribia kufa njaa. Hata hivyo, muda si muda, wataona jinsi ambavyo Yehova atawalinda kwa njia ambayo hajawahi kuwalinda wanafunzi wa Kristo. Ni nini kitakachotokea?

2 Kwa sababu ya kuwahurumia Wakristo Wayahudi wanaoteseka huko Yerusalemu na Yudea, Wakristo Wayahudi na wasio Wayahudi huko Antiokia ya Siria wanakusanya michango ya kuwasaidia waamini wenzao. Kisha wanachagua ndugu wawili wanaotegemeka, Barnaba na Sauli, na kuwatuma wapeleke michango hiyo kwa wazee wa kutaniko huko Yerusalemu. (Soma Matendo 11:27-30; 12:25.) Hebu wazia jinsi ambavyo ndugu wenye uhitaji huko Yudea waliguswa moyo na upendo huo walioonyeshwa na ndugu zao wa Antiokia!

3. (a) Watu wa Mungu leo wanafuataje kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza huko Antiokia? Toa mfano. (Ona pia sanduku “Kazi ya Kwanza Kubwa ya Kutoa Msaada Katika Nyakati za Kisasa.”) (b) Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

3 Tukio hilo lililotukia katika karne ya kwanza W.K., ndilo tukio la kwanza kuandikwa ambalo linataja Wakristo wanaoishi katika sehemu moja ya ulimwengu wakituma msaada kwa Wakristo wanaoishi sehemu nyingine ya ulimwengu. Leo, tunafuata kielelezo kilichowekwa na ndugu zetu wa Antiokia. Tunapojulishwa kwamba waamini wenzetu katika sehemu nyingine wamekumbwa na msiba au hali ngumu, sisi huwasaidia.a Ili kuelewa jinsi kazi ya kutoa msaada inavyohusiana na huduma zetu nyingine, acheni tuchunguze maswali matatu kuhusu huduma ya kutoa msaada: Kwa nini tunaiona kazi ya kutoa msaada kuwa huduma? Kazi yetu ya kutoa msaada inatimiza makusudi gani? Sisi hunufaikaje na huduma ya kutoa msaada?

Kwa Nini Kazi ya Kutoa Msaada Ni “Utumishi Mtakatifu”?

4. Paulo aliwaambia nini Wakorintho kuhusu huduma ya Kikristo?

4 Katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, Paulo alieleza kwamba huduma yetu ya Kikristo ina sehemu mbili. Ingawa Paulo alikuwa akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta, maneno yake yanawahusu pia “kondoo wengine” wa Kristo leo. (Yoh. 10:16) Sehemu moja ya huduma yetu ni “huduma ya upatanisho,” yaani, kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha. (2 Kor. 5:18-20; 1 Tim. 2:3-6) Sehemu ile nyingine inahusu huduma tunayotoa kwa niaba ya waamini wenzetu. Paulo alitaja kihususa “huduma [ya kutoa msaada].” (2 Kor. 8:4) Katika maneno “huduma ya upatanisho” na ‘huduma ya kutoa msaada,’ neno “huduma” linatafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki di·a·ko·niʹa. Kwa nini hilo ni muhimu?

5. Kwa nini ni muhimu Paulo aliita kazi ya kutoa msaada kuwa huduma?

5 Kwa kutumia neno lilelile la Kigiriki kurejelea huduma hizo mbili, Paulo alihusianisha kazi ya kutoa msaada na huduma nyingine zilizofanywa katika kutaniko la Kikristo. Alikuwa amesema hivi awali: “Kuna huduma za namna mbalimbali, na bado kuna Bwana yuleyule; na kuna utendaji wa namna mbalimbali, . . . Lakini ni roho ileile moja inayofanya utendaji huu wote.” (1 Kor. 12: 4-6, 11) Kwa kweli, Paulo alihusianisha huduma mbalimbali zinazofanywa kutanikoni na “utumishi mtakatifu.”b (Rom. 12:1, 6-8) Haishangazi kwamba aliona kuwa jambo linalofaa kutumia wakati wake “ili kuwahudumia watakatifu”!—Rom. 15:25, 26.

6. (a) Kama Paulo alivyoeleza, kwa nini kazi ya kutoa msaada ni sehemu ya ibada yetu? (b) Eleza jinsi ambavyo kazi yetu ya kutoa msaada inafanywa ulimwenguni pote. (Ona sanduku “Msiba Unapotokea!” ukurasa wa 214.)

6 Paulo aliwasaidia Wakorintho kuelewa ni kwa nini kazi ya kutoa msaada ilikuwa sehemu ya huduma na ibada yao kwa Yehova. Ona hoja alizotoa: Wakristo wanaotoa msaada hufanya hivyo kwa sababu ‘wanajitiisha kwenye habari njema juu ya Kristo.’ (2 Kor. 9:13) Hivyo, wakichochewa na tamaa yao ya kufuata mafundisho ya Kristo, Wakristo huwasaidia waamini wenzao. Matendo hayo ya fadhili wanayofanya kwa ajili ya ndugu zao, kwa kweli ni wonyesho wa “fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa za Mungu.” (2 Kor. 9:14; 1 Pet. 4:10) Kwa hiyo, likizungumzia kuhusu kuwatumikia ndugu zetu wenye uhitaji, kutia ndani kazi ya kutoa msaada, gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1975, lilisema hivi kwa kufaa: “Hatupaswi kutilia shaka kamwe kwamba Yehova Mungu na Mwana wake Yesu Kristo wanauona utumishi huo kuwa muhimu sana.” Naam, kazi ya kutoa msaada ni sehemu muhimu ya utumishi mtakatifu.—Rom. 12:1, 7; 2 Kor. 8:7; Ebr. 13:16.

Kazi ya Kutoa Msaada Iliyo na Makusudi Hususa

7, 8. Huduma yetu ya kutoa msaada inatimiza kusudi gani la kwanza? Eleza.

7 Kazi yetu ya kutoa msaada inatimiza makusudi gani? Paulo alijibu swali hilo katika barua yake ya pili kwa Wakorintho. (Soma 2 Wakorintho 9:11-15.) Katika mistari hiyo, Paulo anakazia makusudi au malengo matatu ambayo tunatimiza kwa kushiriki katika “huduma ya utumishi huu wa watu wote,” yaani, kazi ya kutoa msaada. Acheni tuchunguze makusudi hayo, moja baada ya lingine.

8 Kwanza, huduma yetu ya kutoa msaada humletea Yehova utukufu. Ona kwamba katika mistari mitano iliyotajwa hapo juu, Paulo anaelekeza fikira za ndugu zake kwa Yehova Mungu. Mtume huyo anawakumbusha kuhusu “wonyesho wa shukrani kwa Mungu” na kuhusu “maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu.” (Mstari wa 11, 12) Anataja jinsi ambavyo kazi ya kutoa msaada hufanya Wakristo ‘wamtukuze Mungu’ na wasifu “fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa za Mungu.” (Mstari wa 13, 14) Na Paulo anamalizia mazungumzo yake kuhusu huduma ya kutoa msaada kwa kusema hivi: “Mungu apewe shukrani.”—Mstari wa 15; 1 Pet. 4:11.

9. Kazi ya kutoa msaada inaweza kubadilije maoni ya watu? Toa mfano.

9 Kama Paulo, watumishi wa Mungu leo huona kazi za kutoa misaada kuwa fursa za kumletea Yehova utukufu na kupamba mafundisho yake. (1 Kor. 10:31; Tito 2:10) Kwa kweli, kazi ya kutoa msaada huchangia kwa kiasi kikubwa kuondoa maoni mabaya ambayo watu fulani wamekuwa nayo kumhusu Yehova na Mashahidi wake. Kwa mfano: Mwanamke mmoja aliyeishi katika eneo fulani lililokumbwa na kimbunga alikuwa na ishara hii mlangoni pake: “Mashahidi wa Yehova—Msipige Hodi Mlangoni Kwangu.” Kisha siku moja aliona wajitoleaji wakirekebisha nyumba ya jirani yake. Kwa siku nyingi, aliwatazama wafanyakazi hao wenye urafiki, kisha akaamua kwenda kujua walikuwa akina nani. Alipogundua kwamba wajitoleaji hao walikuwa Mashahidi wa Yehova, alivutiwa sana na kusema, “Niliwaelewa vibaya.” Matokeo yakawa nini? Aliondoa ile ishara iliyokuwa mlangoni kwake.

10, 11. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba tunatimiza kusudi letu la pili la kutoa msaada? (b) Ni chapisho gani huwasaidia wale wanaotoa msaada? (Ona sanduku “Kifaa kwa Ajili ya Wafanyakazi wa Kutoa Msaada.”)

10 Pili, tunatoa msaada ili “kukidhi mahitaji” ya waamini wenzetu. (2 Kor. 9:12a, Neno—Biblia Takatifu) Tuna hamu ya kutosheleza mahitaji ya lazima ya ndugu na dada zetu na kusaidia kupunguza mateso yao. Kwa nini? Kwa sababu washiriki wa kutaniko la Kikristo ni “mwili mmoja,” na “kiungo kimoja kikiumia, vile viungo vingine vyote huumia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:20, 26) Kwa hiyo, upendo wa kindugu na huruma huwachochea ndugu na dada wengi leo wabadili ratiba zao mara moja, wachukue vifaa vyao na kwenda kuwasaidia waamini wenzao katika maeneo yaliyokumbwa na msiba. (Yak. 2:15, 16) Kwa mfano, baada ya tsunami kutokea nchini Japani katika mwaka wa 2011, ofisi ya tawi ya Marekani ilituma barua kwa Halmashauri za Ujenzi za Mkoa nchini humo kuomba ikiwa “ndugu wachache wenye ustadi” wanaweza kujitolea kujenga upya Majumba ya Ufalme nchini Japani. Watu waliitikiaje? Baada ya majuma machache tu, karibu wajitoleaji 600 waliomba kwenda kusaidia, na wakakubali kujilipia nauli ya ndege hadi Japani! “Watu wengi sana wamejitolea,” ikasema ofisi ya tawi ya Marekani. Ndugu mmoja nchini Japani alipomuuliza mmoja wa wajitoleaji kwa nini alikuja kuwasaidia, alijibu hivi: “Ndugu zetu nchini Japani ni sehemu ya ‘mwili wetu.’ Tunaumia na kuteseka pamoja nao.” Wakichochewa na upendo wa kujidhabihu, nyakati nyingine wafanyakazi hao wa kutoa msaada wamehatarisha maisha yao ili kuwasaidia waamini wenzao.c—1 Yoh. 3:16.

Mmoja wa Mashahidi wa Yehova akipanga kutoa misaada nchni Uswizi mwaka wa 1946

Uswisi, 1946

KAZI YA KWANZA KUBWA YA KUTOA MSAADA KATIKA NYAKATI ZA KISASA

MNAMO Septemba 1945, miezi michache tu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kumalizika barani Ulaya, Ndugu Knorr alitangaza kuanzishwa kwa kampeni kubwa sana ya kutuma “msaada kwa ndugu wenye uhitaji Ulaya ya kati.”

Majuma machache tu baada ya tangazo hilo, Mashahidi nchini Kanada, Marekani, na nchi nyingine walianza kuchagua na kupakia nguo na kukusanya chakula. Kuanzia Januari 1946 na kuendelea, msaada ulitumwa kwa waamini wenzetu nchini Austria, Bulgaria, Chekoslovakia, China, Denmark, Filipino, Finland, Hungaria, Italia, Norway, Poland, Rumania, Ubelgiji, Ufaransa, Ugiriki, Uholanzi, Uingereza, na Ujerumani.

Programu hiyo ya kutoa msaada haikuwa kazi ya pindi moja tu. Msaada uliendelea kutumwa kwa miaka miwili na nusu! Katika kipindi hicho, ndugu na dada 85,000 hivi walituma kilogramu 300,000 hivi za chakula, kilogramu 450,000 hivi za nguo, na zaidi ya jozi 124,000 za viatu kwa ndugu na dada zao katika maeneo yaliyoharibiwa na vita. Kufikia Agosti 1948, kazi hiyo kubwa ya kutoa msaada ilikamilishwa. Gazeti Mnara wa Mlinzi la mwaka wa 1949 lilisema hivi: “Kwa hakika msaada huo ulionyesha kwamba tunapendana. Tunajua ndugu wote walifanya hivyo ili kumletea sifa Bwana, wakikumbuka kwamba msaada huo wa kimwili ungewasaidia baadhi yao kuendelea na ibada ya kweli; na kwa hiyo waliliona kuwa pendeleo kubwa kuwasaidia ndugu zao kwa njia hiyo.” Kazi hiyo ya kutoa msaada ilimletea Yehova sifa, iliwapa waamini wenzetu kitulizo, na kuimarisha kifungo cha umoja miongoni mwa ndugu ulimwenguni pote.

11 Watu ambao si Mashahidi pia huthamini kazi yetu ya kutoa msaada. Kwa mfano, baada ya msiba kutokea katika jimbo la Arkansas, Marekani, mwaka wa 2013, gazeti moja liliripoti hivi kuhusu jinsi ambavyo wajitoleaji Mashahidi walivyoitikia haraka: “Mashahidi wa Yehova wana utaratibu mzuri wa kutoa msaada hivi kwamba kunapokuwa na msiba, wajitoleaji wao hutoa msaada haraka na kwa ustadi.” Kwa kweli, kama mtume Paulo alivyosema, sisi ‘hukidhi mahitaji’ ya ndugu zetu.

12-14. (a) Kwa nini kutimiza kusudi letu la tatu la kazi yetu ya kutoa msaada ni muhimu sana? (b) Baadhi ya waathiriwa wamesema nini kuhusu umuhimu wa kuendelea na utendaji wa kiroho?

12 Tatu, tunawasaidia walioathiriwa warudie utendaji wao wa kiroho. Kwa nini hilo ni muhimu? Paulo alisema kwamba wale wanaopokea msaada watachochewa kufanya “maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu.” (2 Kor. 9:12b) Kurudia utendaji wao wa kiroho haraka iwezekanavyo ndiyo njia bora kabisa kwa wale walioathiriwa kuonyesha shukrani zao kwa Yehova. (Flp. 1:10) Gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi mwaka wa 1945: “Paulo alikubali . . . michango ikusanywe kwa sababu michango hiyo ilikuwa ikiwasaidia . . . ndugu Wakristo wenye uhitaji kupata msaada wa kimwili ili waweze kushiriki kwa bidii na bila kizuizi chochote katika kazi ya kutoa ushahidi ambayo Yehova amewapa.” Tuna kusudi hilohilo leo. Wanaporudia kazi yao ya kuhubiri, hilo huwaimarisha ndugu zetu walioathiriwa na pia jirani zao waliofadhaika.—Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.

13 Ona baadhi ya maelezo ya wale waliopokea msaada waliohitaji sana, wakaanza kuhubiri tena, na kuimarishwa kwa kufanya hivyo. Ndugu mmoja alisema hivi: “Ilikuwa baraka kwa familia yetu kwenda utumishi wa shambani. Kuwafariji wengine kulitusaidia tusihangaikie sana hali yetu.” Dada mmoja alisema: “Kukazia fikira utendaji wa kiroho kulifanya niache kufikiria kuhusu uharibifu uliotokea. Nilijihisi nikiwa salama.” Dada mwingine alisema: “Ingawa mambo mengi yalipita uwezo wetu, huduma iliisaidia familia yetu. Kuzungumza na wengine kuhusu tumaini letu la ulimwengu mpya kuliimarisha uhakika wetu kwamba vitu vyote vitafanywa kuwa vipya.”

14 Kuhudhuria mikutano ni utendaji mwingine ambao waamini wenzetu walioathiriwa na msiba wanahitaji kurudia haraka iwezekanavyo. Fikiria kisa cha Kiyoko, dada aliyekuwa na umri wa miaka 50 na kitu msiba ulipotokea. Dada huyo hakujua la kufanya kwa kuwa alipoteza kila kitu wakati wa tsunami isipokuwa nguo na viatu alivyokuwa amevaa. Kisha mzee fulani akamwambia kwamba wangefanya mkutano wa Kikristo katika gari lake. Kiyoko anasema hivi: “Mzee huyo, mke wake, mimi, na dada mwingine tuliketi ndani ya gari hilo. Mkutano huo haukuwa na mambo mengi, lakini kama muujiza, nilisahau kabisa kuhusu tsunami. Nilihisi nikiwa na amani ya akili. Mkutano huo ulinionyesha kwamba ushirika wa Kikristo una nguvu.” Akieleza kuhusu mikutano aliyohudhuria baada ya msiba, dada mwingine alisema hivi: “Mikutano hiyo ilinisaidia kuvumilia!”—Rom. 1:11, 12; 12:12.

Huduma ya Kutoa Msaada Huleta Faida za Kudumu

15, 16. (a) Wakristo huko Korintho na kwingineko wangenufaikaje kwa kuunga mkono kazi ya kutoa msaada? (b) Sisi leo tunanufaikaje na kazi ya kutoa msaada?

15 Alipokuwa akizungumza kuhusu huduma ya kutoa msaada, Paulo pia aliwaeleza Wakorintho kuhusu faida ambazo wao na Wakristo wengine wangepata kwa kushiriki katika kazi hiyo. Alisema hivi: “Nao [Wakristo Wayahudi huko Yerusalemu ambao walipokea msaada] kupitia dua kwa ajili yenu wanatamani kuwaona ninyi kwa sababu ya fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa za Mungu juu yenu.” (2 Kor. 9:14) Naam, ukarimu wa Wakorintho ungewachochea Wakristo Wayahudi wasali kwa niaba ya ndugu zao huko Korintho, kutia ndani Watu wa Mataifa, na hilo lingeongeza upendo wao kuwaelekea.

16 Likionyesha kwamba maneno ya Paulo kuhusu manufaa ya kazi ya kutoa msaada yanatuhusu leo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1945, lilisema hivi: “Sehemu moja ya watu wa Mungu waliojiweka wakfu inapochangia mahitaji ya kikundi kingine, hebu wazia jinsi ambavyo jambo hilo huwaunganisha!” Wafanyakazi wa kutoa msaada hujionea jambo hilo leo. Mzee mmoja aliyesaidia kutoa msaada wakati wa mafuriko alisema hivi: “Kufanya kazi ya kutoa msaada kulinifanya nihisi nikiwa na uhusiano wa karibu zaidi na ndugu zangu.” Dada mmoja aliyethamini sana msaada aliopata alisema, “Undugu wetu ndilo jambo linalolingana sana na Paradiso hapa duniani.”—Soma Methali 17:17.

17. (a) Maneno yanayopatikana kwenye Isaya 41:13 yanahusianaje na kazi ya kutoa msaada? (b) Taja mifano inayoonyesha kwamba kazi ya kutoa msaada inamletea Yehova sifa na kuimarisha kifungo chetu cha umoja. (Ona pia sanduku “Wajitoleaji Ulimwenguni Pote Wanaleta Kitulizo.”)

17 Watoaji msaada wanapofika katika eneo lililokumbwa na msiba, ndugu zetu walioathiriwa wanaona kwa njia ya pekee utimizo wa ahadi hii ya Mungu: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’” (Isa. 41:13) Baada ya kuokoka msiba fulani, dada mmoja alisema hivi: “Nilijihisi sina tumaini lolote nilipoona uharibifu mkubwa, lakini Yehova alinishika mkono. Akina ndugu walinisaidia kwa njia kubwa sana.” Baada ya msiba kuharibu eneo lao, wazee wawili waliandika hivi kwa niaba ya kutaniko lao: “Tetemeko la nchi lilisababisha maumivu mengi, lakini tuliona jinsi Yehova alivyotusaidia kupitia ndugu zetu. Tulikuwa tumesoma kuhusu kazi ya kutoa msaada, lakini sasa tulijionea wenyewe msaada ukitolewa.”

Peter Johnson akifanya ujenzi katika majengo ya kitheokrasi

KULIBADILI MAISHA YAKE

KUSHIRIKI katika kazi ya kutoa msaada kuna matokeo gani kwa vijana? Fikiria kisa cha Peter Johnson, ambaye alishiriki kwa mara ya kwanza kazi hiyo alipokuwa na umri wa miaka 18. Anakumbuka hivi: “Kuona jinsi ambavyo ndugu walithamini sana, na shangwe niliyopata kwa sababu ya kutoa kulinigusa sana moyo. Kulizidisha tamaa yangu ya kumtumikia Yehova kikamili katika maisha yangu yote.” Baadaye, Peter alianza upainia. Pia alifanya kazi Betheli, na baadaye akatumikia akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa. Leo Peter anasema hivi: “Kushiriki katika kazi ya kutoa msaada kwa mara ya kwanza mwaka wa 1974 kulibadili maisha yangu.” Je, wewe ni kijana? Je, unaweza kufuata mfano wa Peter? Huenda kufanya hivyo kukabadili maisha yako katika utumishi wa Yehova!

Je, Unaweza Kushiriki?

18. Unaweza kufanya nini ikiwa unataka kushiriki katika kazi ya kutoa msaada? (Ona pia sanduku “Kulibadili Maisha Yake.”)

18 Je, ungependa kuonja shangwe inayotokana na kazi ya kutoa msaada? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba mara nyingi wale wanaofanya kazi ya kutoa msaada huchaguliwa miongoni mwa wale ambao wamejitolea katika miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Kwa hiyo, wajulishe wazee wa kutaniko lako kwamba ungependa kujaza fomu ya kujitolea katika ujenzi. Mzee ambaye amefanya kazi ya kutoa msaada kwa miaka mingi anatoa kikumbusho hiki: “Usiende kwenye eneo lililokumbwa na msiba hadi upokee mwaliko rasmi kutoka kwa Halmashauri ya Kutoa Misaada.” Kwa kutii kikumbusho hicho, kazi ya kutoa msaada itaendeshwa kwa utaratibu.

19. Wafanyakazi wa kutoa msaada wanaonyeshaje kwamba kwa kweli sisi ni wanafunzi wa Kristo?

19 Kwa kweli, kazi ya kutoa msaada ni njia ya pekee ya kuonyesha kwamba tunatii amri ambayo Kristo alitoa kwamba ‘tupendane.’ Kuonyeshana upendo kwa njia hiyo kunathibitisha kwamba kwa kweli sisi ni wanafunzi wa Kristo. (Yoh. 13:34, 35) Ni baraka kubwa sana leo kuwa na wafanyakazi wengi wanaojitoa kwa hiari ambao humletea Yehova utukufu wanapotoa msaada unaohitajiwa kwa wale ambao wanaunga mkono kwa ushikamanifu Ufalme wa Mungu!

a Sura hii inazungumzia msaada ambao hutolewa kwa waamini wenzetu. Hata hivyo, katika visa vingi, kazi yetu ya kutoa msaada huwanufaisha pia watu ambao si Mashahidi.—Gal. 6:10.

b Paulo alitumia neno di·aʹko·nos (mhudumu) katika hali ya wingi alipokuwa akizungumza kuhusu “watumishi wa huduma.”—1 Tim. 3:12.

c Ona makala “Kusaidia Familia Yetu ya Waamini Katika Bosnia,” kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1994, ukurasa wa 23-27.

Ufalme Ni Halisi Kwako Kadiri Gani?

  • Tunajuaje kwamba kazi ya kutoa msaada ni sehemu ya utumishi wetu mtakatifu kwa Yehova?

  • Kazi ya kutoa msaada inatimiza makusudi gani matatu?

  • Kazi ya kutoa msaada huleta manufaa gani ya kudumu?

  • Kazi ya kutoa msaada inahusianaje na amri ambayo Yesu alitoa kwenye Yohana 13:34?

WAJITOLEAJI ULIMWENGUNI POTE WALETA KITULIZO

AFRIKA YA KATI NA YA MAGHARIBI

Katika mwaka wa 1994, watu 800,000 hivi au zaidi waliuawa wakati wa mauaji ya jamii nzima-nzima nchini Rwanda. Baada ya mauaji hayo ya halaiki, ghasia zilienea katika nchi nyingine katika Afrika ya Kati, na kusababisha kuwe na kambi za wakimbizi zilizofurika watu. Ili kuwasaidia waamini wenzao walioathiriwa, Mashahidi wa Yehova nchini Ubelgiji, Ufaransa, na Uswisi walituma kupitia ndege tani 300 hivi za nguo, dawa, mahema, chakula, na vitu vingine. Baada ya majuma machache tu, misaada hiyo iliwafikia ndugu zetu waliokuwa na uhitaji.

Pia barani Afrika, kikundi cha madaktari na wauguzi kumi ambao ni Mashahidi kutoka Ufaransa wamekuwa wakiwasaidia ndugu zetu ambao wanateseka kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, njaa, na magonjwa. Katika kipindi cha miaka miwili tu iliyopita, wataalamu hao wa tiba walitoa ushauri wa kitiba kwa watu zaidi ya 10,000. Kazi yao inamletea sifa Yehova na tengenezo lake. Mmoja wa wauguzi hao anasema: “Tunapowasili katika eneo fulani ili kuwasaidia ndugu na dada zetu, watu husema hivi kwa heshima: ‘Hawa ni Mashahidi wa Yehova. Wamekuja kuwasaidia ndugu zao.’” Baada ya kusaidiwa na muuguzi mmoja, dada mmoja alisema hivi kwa furaha: “Asante sana dada yangu. Asante sana, Yehova!”

Nyakati nyingine, msaada unahitajiwa kunapotokea aksidenti mbaya. Katika mwaka wa 2012, aksidenti ya barabarani nchini Nigeria iliwaua Mashahidi 13 wa kutaniko moja dogo, na wengine 54 wakajeruhiwa vibaya. Halmashauri ya kutoa misaada ilifanya mipango ya kuwasaidia waathiriwa wote mchana na usiku. Alipoona utegemezo mkubwa ambao ndugu na dada waliojeruhiwa walipata, mgonjwa mmoja aliyelazwa hospitalini alimpigia simu kasisi wake na kumwambia hivi: “Hakuna mtu yeyote kutoka katika kanisa letu amenitembelea. Njoo hospitalini na uone jinsi ambavyo Mashahidi wa Yehova wanaonyesha upendo kwa matendo!”

Ingawa ndugu zetu wapendwa katika kutaniko hilo walihuzunika sana kuwapoteza wapendwa wao, walifarijika sana kuona upendo ambao waamini wenzao waliwaonyesha. Isitoshe, walipoona jinsi ambavyo ndugu waliokuja kuwasaidia waliwajali kwa upendo ndugu walioathiriwa, watu wengi katika kutaniko hilo walichochewa kuongeza bidii yao katika huduma. Kabla ya aksidenti hiyo, kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 35. Lakini katika kipindi cha mwaka moja, idadi hiyo iliongezeka hadi 60.

AUSTRALIA

Katika mwaka wa 2013, sehemu fulani za pwani ya Queensland zilikumbwa na mafuriko yaliyowaacha Mashahidi 70 bila makao. Mark na Rhonda pamoja na binti yao waliacha nyumba yao iliyofurika na kukimbilia kwenye kituo cha kuwahamisha watu. Kituo hicho kilikuwa na watu wengi sana. Rhonda anasema, “Hakukuwa na mahali pa kuketi.” Kelele nyingi za helikopta zilizokuwa zikitua na kupaa katika eneo la karibu zilifanya watu wawe na mkazo zaidi. Akiwa na wasiwasi, dada huyo alimuuliza mume wake, “Sasa tutafanya nini?” Mark alisali kwa bidii ili Yehova awasaidie. Rhonda anasema: “Baada ya dakika 30 hivi, gari fulani liliwasili katika kituo hicho, na ndugu watatu wakashuka. Tulipokutana nao, walituambia hivi: ‘Tumekuja kuwachukua. Mtakaa kwenye nyumba ya ndugu fulani.’” Rhonda anaongezea hivi: “Tuliguswa sana moyo na jinsi ambavyo tengenezo la Yehova lilitujali kwa upendo katika pindi hiyo.”

Zaidi ya wajitoleaji 250 walienda haraka kuwasaidia ndugu zetu katika eneo hilo lililokumbwa na msiba. Ndugu mmoja mzee anasema hivi: “Ghafla tuliona kikundi cha Mashahidi ambao walianza kufanya kazi kwa bidii kama siafu ili kuondoa takataka katika nyumba yetu. Mimi na mke wangu hatutasahau kamwe jinsi walivyotusaidia.”

BRAZILI

Katika mwaka wa 2008, kulitokea maporomoko ya matope na mafuriko katika jimbo la Santa Catarina, na watu 80,000 hivi walilazimika kuhama nyumba zao. Mkaaji mmoja alisema kwamba eneo hilo lilikuwa ni kana kwamba limekumbwa na “tsunami ya udongo, matope na miti.” Baadhi ya akina ndugu walipata makao katika Jumba la Kusanyiko. Márcio, mtunzaji wa jumba hilo anasema: “Hawakubeba chochote isipokuwa nguo walizokuwa wamevaa ambazo zilikuwa zimejaa matope.” Dada mmoja anasema: “Nyumba yetu iliporomoka. Iliumiza sana kuona nyumba hiyo ikitokomea ghafla, lakini sitasahau kamwe jinsi ambavyo ndugu na dada zetu walitufariji. Walituonyesha upendo katika njia nyingi! Tukio hilo lilinifundisha kwamba ni jambo la hekima sana kujiwekea hazina ya vitu vya kiroho.”

Mashahidi wa Yehova wakipanga na kugawa misaada wakati wa msiba Brazili

Jumba la Kusanyiko huko Santa Catarina, Brazili, lilitumiwa kama kituo cha kutoa msaada kilichojaa michango, 2009

Maporomoko ya matope yameharibu maeneo yote yaliyokuwa kwenye miteremko ya milima karibu na jiji la Rio de Janeiro. Ili kukabiliana inavyofaa na misiba kama hiyo ambayo hutokea mara kwa mara, akina ndugu walianzisha Halmashauri ya kudumu ya Kutoa Misaada. Kunapotokea tisho la maporomoko ya matope, ndugu walioteuliwa ambao huishi katika eneo lililoathiriwa huitaarifu halmashauri hiyo. Mara moja, wajitoleaji hufika katika eneo hilo wakiwa na magari yaliyoandikwa, “Mashahidi wa Yehova—Msaada wa Kibinadamu.” Kila mshiriki wa kikundi hicho kilichojiandaa vizuri hupewa mgawo hususa mapema. Wafanyakazi hao huvaa fulana zinazowatambulisha wazi kuwa Mashahidi wa Yehova. Wakishirikiana na ndugu wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, wao huwasaidia ndugu na dada waliojeruhiwa. Wafanyakazi wa kutoa msaada huleta chakula, maji, dawa, na vitu vingine vya kitiba, mavazi, na sabuni. Kuondoa matope kutoka ndani ya nyumba ni kazi ngumu. Baada ya maporomoko yaliyotokea hivi karibuni, iliwachukua wajitoleaji 60 kuondoa kwenye nyumba moja tu matope ambayo yangetoshea katika malori manne!

KUJITAYARISHA KWA AJILI YA MSIBA

Baraza Linaloongoza limeelekeza kwamba ofisi za tawi ulimwenguni pote zitoe mwongozo kwa wazee wa kutaniko na waangalizi wanaosafiri kuhusu jinsi ya kujitayarisha na jinsi ya kushughulika na misiba. Kwa mfano, hata kabla msiba haujatokea wazee wanahitaji kuhakikisha kwamba wanajua mahali ambapo kila mshiriki wa kutaniko anaishi na namba zao za simu za karibuni zaidi.

MSIBA UNAPOTOKEA!

Mzee Mkristo akiwatembelea familia ya wahubiri
  1. Wazee wawasiliane na wahubiri wote

  2. Wazee wamjulishe mratibu wa baraza la wazee

  3. Mpango wa kuratibu katika ya waangalizi wanaosafiri, na akina ndugu wakristo na ofisi ya tawi

    Waratibu wamjulishe mwangalizi anayesafiri na ndugu wengine ambao wanawasiliana na ofisi ya tawi

  4. Maji na chakula

    Chakula, maji, malazi, matibabu, na faraja ya kihisia na kiroho inatolewa haraka iwezekanavyo

  5. Ripori ya misaada ya misiba ikikaguliwa

    Ofisi ya tawi inatuma taarifa kuhusu hali na mahitaji ya waathiriwa kwa Halmashauri ya Waratibu ya Baraza Linaloongoza

  6. Kugawanya misaada wakati wa misiba

    Halmashauri ya Kutoa Misaada hupanga kazi ya kutoa msaada na kuwasaidia akina ndugu na dada mpaka wanaporudia hali yao ya kawaida

  7. Ndege ikiwa inapaa

    Halmashauri ya Waratibu inachunguza hali, na ikihitajika, inaidhinisha wajitoleaji kutoka nchi nyingine ili wakasaidie

KIFAA KWA AJILI YA WAFANYAKAZI WA KUTOA MISAADA

jalada la brosha Mashahidi wa Yehova na Kutoa Misaada

MNAMO Juni 2013, broshua Jehovah’s Witnesses and Disaster Relief ilitolewa. Ilitayarishwa hasa kwa ajili ya maofisa wa serikali nchini Marekani ambao wanasimamia shughuli za kukabiliana na hali ya dharura. Broshua hiyo inaelezea kazi ya kutoa misaada ambayo tumefanya tangu katikati ya miaka ya 1940. Pia ina ramani ambayo inaonyesha nchi mbalimbali ambako tumetoa msaada. Mzee mmoja anayefanya kazi ya kutoa msaada anasema hivi: “Akina ndugu wanaotumikia katika Halmashauri za Kutoa Misaada wanatumia broshua hiyo kusitawisha mawasiliano mazuri na maofisa muhimu katika maeneo yanayokumbwa na misiba mara kwa mara kabla ya msiba kutokea. Maofisa hao wanapoifahamu vizuri kazi yetu ya kutoa misaada, inakuwa rahisi kwetu kupata kibali cha kuingia katika maeneo yaliyokumbwa na misiba.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki