Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jy sura 121 uku. 278-uku. 279 fu. 2
  • “Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”
  • Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Habari Zinazolingana
  • Shauri Zaidi Wakati wa Kuachana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kuwatayarisha Mitume kwa Ajili ya Kuondoka Kwake
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Yesu​—Njia, Kweli, na Uzima
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Shauri la Wakati wa Kuachana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
jy sura 121 uku. 278-uku. 279 fu. 2
Mitume wana wasiwasi Yesu anapowapatia onyo

SURA YA 121

“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

YOHANA 16:1-33

  • BAADA YA MUDA MFUPI MITUME HAWATAMWONA TENA YESU

  • HUZUNI YA MITUME ITAGEUKA KUWA SHANGWE

Yesu na mitume wake wanakaribia kuondoka kwenye chumba cha juu ambapo walikula mlo wa Pasaka. Baada ya kuwahimiza vya kutosha, Yesu anaongezea hivi: “Nimewaambia mambo haya ili msikwazike.” Kwa nini ushauri huo uliwafaa? Anawaambia hivi: “Watu watawafukuza katika masinagogi. Kwa kweli, saa inakuja ambayo kila mtu atakayewaua atafikiri kwamba amemtolea Mungu utumishi mtakatifu.”—Yohana 16:1, 2.

Huenda habari hizo zinafanya mitume wawe na wasiwasi. Ingawa hapo awali Yesu alikuwa amesema kwamba ulimwengu utawachukia, hakuwa amewaambia moja kwa moja kwamba watauawa. Kwa nini? Yesu anasema: “Sikuwaambia mambo haya mwanzoni, kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi.” (Yohana 16:4) Sasa anawaonya kabla hajaondoka. Jambo hilo litawasaidia wasikwazike baadaye.

Yesu anaendelea kusema: “Ninaenda kwa Yule aliyenituma; na bado hakuna hata mmoja wenu anayeniuliza, ‘Unaenda wapi?’” Mapema jioni hiyo walikuwa wameuliza mahali anakoenda. (Yohana 13:36; 14:5; 16:5) Lakini sasa, wakiwa wameogopa kwa sababu alitaja kuhusu kuteswa, wanalemewa na huzuni. Hivyo, hawaulizi zaidi kuhusu utukufu atakaopata au jambo hilo litamaanisha nini kwa waabudu wa kweli. Yesu anasema hivi: “Kwa sababu nimewaambia mambo haya, mioyo yenu imejaa huzuni.”—Yohana 16:6.

Kisha Yesu anaeleza hivi: “Ninaenda zangu kwa faida yenu. Kwa maana nisipoenda, msaidizi hatakuja kwenu; lakini nikienda, nitamtuma kwenu.” (Yohana 16:7) Yesu akifa na kwenda mbinguni ndipo wanafunzi wake watakapopokea roho takatifu, ambayo ataituma kama msaidizi wa watu wake mahali popote duniani.

Roho takatifu “[itauthibitishia] waziwazi ulimwengu kuhusu dhambi na kuhusu uadilifu na kuhusu hukumu.” (Yohana 16:8) Naam, kosa la ulimwengu la kutomwamini Mwana wa Mungu litafunuliwa. Yesu atakapopaa mbinguni atatoa uthibitisho hakika wa uadilifu wake na ataonyesha kwa nini Shetani, “mtawala wa ulimwengu,” anastahili kuhukumiwa.—Yohana 16:11.

Yesu anaendelea kusema: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa.” Atakapomimina roho takatifu, itawaongoza kwenye “kweli yote,” nao wataweza kuishi kulingana na kweli hiyo.—Yohana 16:12, 13.

Mitume wanashangaa Yesu anaposema hivi: “Baada ya muda kidogo hamtaniona tena, na baada ya muda kidogo mtaniona.” Wanaulizana anamaanisha nini. Yesu anatambua kwamba wanataka kumuuliza kuhusu jambo hilo, basi anaeleza hivi: “Kwa kweli ninawaambia, mtalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utashangilia; mtahuzunika, lakini huzuni yenu itageuka kuwa shangwe.” (Yohana 16:16, 20) Yesu anapouawa siku inayofuata alasiri, viongozi wa kidini wanashangilia, lakini wanafunzi wanaomboleza. Kisha huzuni yao inageuka kuwa shangwe Yesu anapofufuliwa! Nao wanazidi kuwa na shangwe anapomimina juu yao roho takatifu ya Mungu.

Akilinganisha hali ya mitume na mwanamke aliye na uchungu wa kuzaa, Yesu anasema: “Mwanamke anapokuwa akizaa anahisi huzuni kwa sababu saa yake imefika, lakini baada ya kumzaa mtoto hakumbuki tena dhiki hiyo kwa sababu anashangilia kwamba mtu amezaliwa ulimwenguni.” Yesu anawatia moyo mitume wake kwa kusema: “Ninyi pia mnahuzunika sasa; lakini nitawaona tena na mioyo yenu itashangilia na hakuna mtu atakayeondoa shangwe yenu.”—Yohana 16:21, 22.

Kufikia sasa, mitume hawajatoa ombi lolote kamwe katika jina la Yesu. Sasa anasema: “Siku hiyo mtamwomba Baba katika jina langu.” Kwa nini watafanya hivyo? Si kwa sababu Baba hataki kujibu. Kwa kweli, Yesu anasema: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda . . . nikiwa mwakilishi wa Mungu.”—Yohana 16:26, 27.

Huenda maneno ya Yesu yenye kutia moyo yamewapa mitume ujasiri wa kusema hivi: “Kwa hiyo, tunaamini kwamba ulitoka kwa Mungu.” Hivi karibuni uhakika huo utajaribiwa. Kwa kweli, Yesu anafafanua jambo litakalotokea: “Tazama! Saa inakuja, na kwa kweli imefika, wakati kila mmoja wenu atatawanyika na kwenda nyumbani kwake, nanyi mtaniacha peke yangu.” Lakini anawahakikishia hivi: “Nimewaambia mambo haya ili kupitia kwangu muwe na amani. Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:30-33) Si kwamba Yesu anawakimbia. Ana uhakika kwamba wao pia wanaweza kuushinda ulimwengu, kama yeye alivyofanya, kwa kutimiza kwa uaminifu mapenzi ya Mungu licha ya jitihada za Shetani na ulimwengu wake za kuvunja utimilifu wao.

  • Mitume wanakuwa na wasiwasi Yesu anapotoa onyo gani?

  • Kwa nini mitume wanaacha kumuuliza Yesu maswali?

  • Yesu anatumia mfano gani ili kufafanua jinsi huzuni ya mitume itakavyogeuka kuwa shangwe?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki