Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • od sura 13 kur. 130-140
  • “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”
  • Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • USAFI WA KIROHO NA WA MAADILI
  • USAFI WA KIMWILI
  • TAFRIJA NA BURUDANI ZINAZOFAA
  • KAZI ZA SHULENI
  • KAZI NA WATU TUNAOSHIRIKIANA NAO
  • KUKAA KATIKA UMOJA WA KIKRISTO
  • Mungu Anawapenda Watu Walio Safi
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Tafrija Zinazofaa na Zinazoburudisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je, Tafrija Unayochagua Inakujenga?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Uwe Safi Katika Akili na Mwili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
od sura 13 kur. 130-140

SURA YA 13

“Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”

TUKIWA watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova. Mtume Paulo alitoa kanuni inayotuongoza alipoandika hivi: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Hilo linatia ndani kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova vinavyoonyesha utu wake mkamilifu. (Kol. 3:10) Ni lazima tumwige Mungu tukiwa watu watakatifu.—Efe. 5:1, 2.

2 Akikazia umuhimu wa Wakristo kuwa watakatifu, mtume Petro aliandika hivi: “Kama watoto watiifu, acheni kufinyangwa na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika hali yenu ya kutojua, lakini iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote kama Yule Mtakatifu aliyewaita ninyi, kwa maana imeandikwa: ‘Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Pet. 1:14-16) Kama Waisraeli wa kale, wote katika kutaniko la Kikristo wanapaswa kudumisha utakatifu. Hilo linamaanisha kwamba wanapaswa kubaki safi na kuepuka kuchafuliwa na dhambi na mambo yasiyofaa ya ulimwengu. Hivyo wanatakaswa kwa ajili ya utumishi wa Yehova.—Kut. 20:5.

3 Utakatifu unadumishwa kwa kufuata sheria na kanuni za Yehova zinazotajwa waziwazi katika Maandiko Matakatifu. (2 Tim. 3:16) Tulipojifunza Maandiko, tulifundishwa kumhusu Yehova na njia zake, na tukachochewa kumkaribia. Kujifunza Biblia kulitusadikisha kwamba tulihitaji kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwetu. (Mt. 6:33; Rom. 12:2) Ili kufanya hivyo, ilitubidi tuvae utu mpya.—Efe. 4:22-24.

USAFI WA KIROHO NA WA MAADILI

4 Si rahisi kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova nyakati zote. Adui yetu, Shetani Ibilisi, anajaribu kutukengeusha kutoka kwenye kweli. Pindi fulani ushawishi mbaya wa ulimwengu huu na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi hufanya mambo yawe magumu. Ili tuishi kulingana na wakfu wetu tunahitaji kupigana vita vya kiroho. Maandiko yanatuambia kwamba tusishangae tunapopingwa au kujaribiwa. Tutateseka kwa ajili ya uadilifu. (2 Tim. 3:12) Tunaweza kufurahi tunapokuwa chini ya majaribu, tukijua kwamba majaribu hayo yanathibitisha kuwa tunafanya mapenzi ya Mungu.—1 Pet. 3:14-16; 4:12, 14-16.

5 Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alijifunza utii kutokana na mateso yaliyompata. Hakukubali kamwe kushindwa na vishawishi vya Shetani au kujitakia mambo makuu ya ulimwengu. (Mt. 4:1-11; Yoh. 6:15) Yesu hakufikiria kamwe kulegeza msimamo wake. Ingawa ulimwengu ulimchukia kwa sababu ya uaminifu wake, sikuzote alishikamana na viwango vya uadilifu vya Yehova. Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwatahadharisha wanafunzi wake kwamba ulimwengu ungewachukia wao pia. Tangu wakati huo, wafuasi wa Yesu wamepata dhiki nyingi, lakini wamejipa moyo kwa kujua kwamba Mwana wa Mungu aliushinda ulimwengu.—Yoh. 15:19; 16:33; 17:16.

6 Ili tusiwe sehemu ya ulimwengu, tunahitaji kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova kama alivyofanya Bwana wetu. Mbali na kuepuka mambo ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu huu, tunapaswa kupinga maadili yake mapotovu. Tunapaswa kutii ushauri wa andiko la Yakobo 1:21: “Ondoeni uchafu wote na ubaya wote, na pokeeni kwa upole kupandwa kwa lile neno linaloweza kuwaokoa.” Tunapojifunza na kuhudhuria mikutano, ‘tunapanda lile neno’ la kweli akilini na mioyoni mwetu, na hatutatamani hata kidogo mambo ya ulimwengu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Yak. 4:4) Kwa sababu hiyo, Biblia inatuhimiza kwa uthabiti tufuate viwango vya uadilifu vya Yehova na kujitenga na ulimwengu.

7 Neno la Mungu linatuonya kwamba tusishiriki katika mwenendo wa aibu na mpotovu. Linasema hivi: “Uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi au pupa visitajwe kamwe miongoni mwenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.” (Efe. 5:3) Kwa hiyo, hatutaruhusu kamwe akili yetu iendelee kufikiria mambo machafu ya aibu au yaliyopotoka, wala hatutaruhusu kamwe mambo hayo yaingie katika mazungumzo yetu. Kwa kufanya hivyo, tunathibitisha kwamba tunataka kufuata viwango safi na vya uadilifu vya Yehova kuhusu maadili.

USAFI WA KIMWILI

8 Mbali na usafi wa kiroho na wa maadili, Wakristo hutambua umuhimu wa kuwa safi kimwili. Katika Israeli la kale, Mungu mtakatifu aliwaagiza wadumishe usafi kambini. Sisi pia tunapaswa kuwa safi ili Yehova “asione kitu chochote kichafu” ndani yetu.—Kum. 23:14.

9 Katika Biblia, utakatifu unahusianishwa na usafi wa kimwili. Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Wapendwa . . . acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Kor. 7:1) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kujitahidi kuwa safi kimwili kwa kuoga na kufua nguo zao kwa ukawaida. Ijapokuwa hali hutofautiana katika nchi mbalimbali, kwa kawaida tunaweza kupata sabuni na maji ya kutosha kuoga na kuhakikisha kwamba watoto wetu ni wasafi.

10 Tunajulikana sana katika jamii kwa sababu ya kazi yetu ya kutoa ushahidi. Kudumisha mpangilio mzuri na usafi, ndani na nje ya nyumba, ni njia mojawapo ya kuwatolea ushahidi jirani zetu. Familia nzima inaweza kushiriki kufanya hivyo. Akina ndugu wanapaswa kuzingatia usafi wa nyumba na mazingira yake, wakijua kwamba mazingira mazuri ya nyumbani huwavutia wengine. Kuzingatia usafi na pia kuongoza katika mambo ya kiroho, huonyesha kwamba wanasimamia vyema nyumba zao. (1 Tim. 3:4, 12) Akina dada pia wana jukumu la kudumisha usafi, hasa ndani ya nyumba. (Tito 2:4, 5) Watoto waliozoezwa vizuri hutimiza jukumu lao kwa kuwa wasafi na kudumisha mpangilio mzuri na usafi wa vyumba vyao. Hivyo, familia hushirikiana kusitawisha utaratibu wa usafi ambao tutafuata katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu.

11 Watumishi wengi wa Yehova leo hutumia magari kwenda kwenye mikutano. Katika maeneo fulani, inalazimu kuwa na gari katika huduma. Gari hilo linapaswa kuwa safi na kudumishwa vizuri. Nyumba na magari yetu yanapaswa kuonyesha kwamba sisi ni watu wa Yehova walio safi na watakatifu. Kanuni hiyo inahusu pia mikoba na Biblia tunazotumia katika utumishi wa shambani.

12 Mavazi na mapambo yetu yanapaswa kupatana na kanuni za Mungu. Hatuwezi kwenda mbele ya watu mashuhuri tukiwa tumevaa isivyofaa au ovyoovyo. Je, hatupaswi kuvaa vizuri hata zaidi tunapomwakilisha Yehova katika utumishi wa shambani au jukwaani? Mavazi na mapambo yetu yanaweza kuathiri jinsi wengine wanavyoiona ibada ya Yehova. Bila shaka haingefaa kuvaa kwa njia isiyo na kiasi au bila kuwajali wengine. (Mika 6:8; 1 Kor. 10:31-33; 1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, tunapojitayarisha kwenda utumishi wa shambani, mikutanoni au makusanyikoni, tunapaswa kukumbuka yale ambayo Biblia husema kuhusu usafi wa kimwili, mavazi na mwonekano wetu. Sikuzote tunataka kumheshimu na kumtukuza Yehova.

Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova

13 Tunapaswa kufuata kanuni hiyo pia tunapotembelea makao makuu au ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Kumbuka kwamba jina Betheli linamaanisha “Nyumba ya Mungu.” Kwa hiyo, tunapaswa kuvaa, kujipamba, na kujiendesha kama tunavyofanya tunapohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme.

14 Hata tunapokuwa katika tafrija na burudani, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na mapambo yetu. Tunaweza kujiuliza, ‘je, mavazi na mapambo yangu yatanifanya nione aibu kutoa ushahidi isivyo rasmi?’

TAFRIJA NA BURUDANI ZINAZOFAA

15 Tunahitaji kupumzika na kujiburudisha kwa ajili afya. Wakati fulani Yesu aliwaambia wanafunzi wake waende naye mahali patulivu ili ‘wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Vipindi vya mapumziko, tafrija au burudani inayofaa zinaweza kustarehesha. Vinaweza kutupa nguvu za kuendelea na shughuli zetu za kawaida.

16 Kwa sababu kuna aina nyingi za tafrija, Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu na kutumia hekima ya Mungu katika kila jambo wanalofanya. Ingawa tafrija ni muhimu, haipaswi kuwa jambo kuu maishani. Tunaonywa kwamba katika “siku za mwisho,” watu ‘watapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Tim. 3:1, 4) Tafrija na burudani nyingi leo haziwafai wale wanaotamani kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova.

17 Wakristo wa mapema walikataa mtazamo usiofaa wa ulimwengu uliofuatia sana raha. Wakati wa michezo ya Waroma, watazamaji walitumbuizwa kwa kuwatazama wengine wakiteseka. Watu wengi waliburudishwa kwa kutazama jeuri, umwagaji wa damu, na upotovu wa maadili kingono, lakini Wakristo wa mapema hawakujihusisha na mambo hayo. Leo, burudani nyingi ulimwenguni zina mambo kama hayo ambayo yamekusudiwa kutosheleza tamaa zisizofaa za wanadamu. Tunahitaji ‘kuendelea kuangalia sana’ jinsi tunavyotembea, tukiepuka burudani zinazopotosha maadili. (Efe. 5:15, 16; Zab. 11:5) Hata ingawa huenda burudani isiwe mbaya, mara nyingi kuwepo kwa watu wa ulimwengu na ushawishi wao unaweza kutuathiri.—1 Pet. 4:1-4.

18 Kuna tafrija na burudani zinazofaa ambazo Wakristo wanaweza kufurahia. Wengi wamefaidika kwa kufuata ushauri wa Maandiko na mapendekezo mazuri yanayopatikana katika machapisho yetu.

19 Nyakati nyingine, huenda familia kadhaa zikaalikwa katika nyumba fulani kufurahia ushirika wa Kikristo. Au ndugu na dada wanaweza kualikwa harusini au kwenye matukio mengine kama hayo. (Yoh. 2:2) Wale wanaoalika wageni wanapaswa kutambua kuwa watawajibika kwa mambo yote yatakayotokea. Kwa kweli, ni muhimu kuwa waangalifu ikiwa kutakuwa na watu wengi. Hali ya starehe katika vikusanyiko kama hivyo imewafanya wengine wavuke mipaka ya mwenendo unaowafaa Wakristo, na hivyo kula na kunywa kupita kiasi na hata kutumbukia katika dhambi nyingine nzito. Wakristo wenye utambuzi wanaona ni jambo la hekima kuweka idadi hususa ya watu watakaohudhuria na muda wa vikusanyiko hivyo. Ikiwa kutakuwa na pombe, inapaswa kutumiwa kwa kiasi. (Flp. 4:5) Wakristo wakijitahidi kuhakikisha kwamba tafrija zao zinajenga na kuburudisha kiroho, vyakula na vinywaji havitakuwa jambo kuu katika pindi hizo.

20 Ni vizuri kuwa wakaribishaji wageni. (1 Pet. 4:9) Tunapowaalika Wakristo wengine nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula, viburudisho, starehe, na ushirika, tunapaswa kuwakumbuka wale wenye uhitaji. (Luka 14:12-14) Tunapoalikwa, mwenendo wetu unapaswa kupatana na ushauri unaopatikana kwenye Marko 12:31. Sikuzote ni vizuri kuthamini fadhili tunazotendewa na wengine.

21 Wakristo hufurahia zawadi nyingi kutoka kwa Mungu na wanajua kwamba wanaweza “kula na kunywa na kufurahia kazi [yao] yote ngumu.” (Mhu. 3:12, 13) Tunapofanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu,” wale walioandaa tafrija na vilevile wageni watakumbuka jinsi walivyoburudishwa kiroho.

KAZI ZA SHULENI

22 Watoto wa Mashahidi wa Yehova hunufaishwa na elimu ya msingi. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi kujifunza kusoma na kuandika vizuri. Mambo mengine ambayo vijana husoma shuleni yanaweza kuwasaidia wanapojitahidi kufikia malengo yao ya kiroho. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi sana ‘kumkumbuka Muumba wao’ kwa kutanguliza mambo ya kiroho.—Mhu. 12:1.

23 Ikiwa wewe ni kijana Mkristo uliye shuleni, uwe mwangalifu sana ili usishirikiane isivyo lazima na vijana wa ulimwengu. (2 Tim. 3:1, 2) Kwa kuwa Yehova hukupa ulinzi unaohitaji, una mengi ya kufanya yanayoweza kukusaidia kuepuka vishawishi vya ulimwengu. (Zab. 23:4; 91:1, 2) Hivyo, ili ujilinde, tumia kikamili maandalizi ya Yehova.—Zab. 23:5.

24 Ili kujitenga na ulimwengu wakiwa wangali shuleni, vijana wengi Mashahidi huamua kutojihusisha katika shughuli za baada ya masomo. Huenda wanafunzi wenzako na walimu wasielewe msimamo wako. Hata hivyo, jambo muhimu ni kumpendeza Mungu. Ili kufanya hivyo, unahitaji kufuata dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia na kuazimia kabisa kutohusika katika mashindano ya kilimwengu au mambo ya kizalendo. (Gal. 5:19, 26) Mkisikiliza ushauri wa Maandiko kutoka kwa wazazi wenu Wakristo, na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko, ninyi vijana mtashika viwango vya uadilifu vya Yehova.

KAZI NA WATU TUNAOSHIRIKIANA NAO

25 Vichwa vya familia wana wajibu wa Kimaandiko wa kuandalia mahitaji watu wa nyumbani mwao. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, wakiwa wahudumu wanatambua kwamba kuutafuta Ufalme ni muhimu zaidi kuliko kazi ya kimwili. (Mt. 6:33; Rom. 11:13) Wanaepuka mahangaiko na mitego ya kufuatilia vitu vya kimwili kwa kumtumikia Mungu kwa bidii na kuridhika na chakula na mavazi.—1 Tim. 6:6-10.

26 Wakristo wote waliojiweka wakfu wanapaswa kukumbuka kanuni za Maandiko katika kazi zao za kimwili. Tunapaswa kuwa wanyofu tunapotafuta riziki, na hivyo kuepuka mambo yanayovunja sheria za Mungu au sheria za nchi. (Rom. 13:1, 2; 1 Kor. 6:9, 10) Tukumbuke hatari ya kushirikiana na marafiki wabaya. Tukiwa wanajeshi wa Kristo, tunaepuka kufanya biashara zinazovunja viwango vya Mungu, zinazoweza kulegeza msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, au zinazohatarisha hali yetu ya kiroho. (Isa. 2:4; 2 Tim. 2:4) Pia, hatushirikiani na “Babiloni Mkubwa,” adui wa kidini wa Mungu.—Ufu. 18:2, 4; 2 Kor. 6:14-17.

27 Kufuata viwango vya uadilifu vya Mungu, kutatuepusha kutumia vibaya ushirika wetu wa Kikristo ili kuendeleza biashara au faida zetu za kibinafsi. Kusudi la kushirikiana na wenzetu kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo ni kumwabudu Yehova. Tunalishwa katika meza yake ya kiroho na tunafurahia ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12; Ebr. 10:24, 25) Kwenye ushirika huo tunapaswa kuzungumzia mambo ya kiroho.

KUKAA KATIKA UMOJA WA KIKRISTO

28 Ili watu wa Yehova wafuate viwango vyake vya uadilifu wanahitaji “kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:1-3) Badala ya kujifikiria wenyewe, kila mmoja hujitahidi kufanya mambo yanayowapendeza wengine. (1 The. 5:15) Bila shaka umejionea roho hiyo katika kutaniko lako. Bila kujali kabila, taifa, jamii, hali yetu ya kiuchumi au elimu yetu, sote tunaongozwa na viwango vilevile vya uadilifu. Hata watu wasio Mashahidi wameona sifa hiyo ya pekee ya watu wa Yehova.—1 Pet. 2:12.

29 Akikazia msingi wa umoja, mtume Paulo aliandika hivi: “Kuna mwili mmoja, na roho moja, kama mlivyoitwa kwenye tumaini moja; Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja ambaye ni Baba wa wote, aliye juu ya wote, na kupitia wote na katika wote.” (Efe. 4:4-6) Maneno hayo yanatuchochea tuwe na ufahamu uleule wa mafundisho ya msingi na pia mafundisho yenye kina ya Biblia ili tuonyeshe kwamba tunatambua mamlaka kuu ya Yehova. Kwa kweli, Yehova amewapa watu wake lugha safi ya kweli inayowawezesha wamtumikie bega kwa bega.—Sef. 3:9.

30 Umoja na amani ya kutaniko la Kikristo huwaburudisha wote wanaomwabudu Yehova. Tumeshuhudia utimizo wa ahadi hii ya Yehova: “Kwa umoja nitawaweka kama kondoo zizini.” (Mika 2:12) Tunataka kudumisha umoja na amani hiyo kwa kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova.

31 Wenye furaha ni wale waliokubaliwa katika kutaniko safi la Yehova! Tunapaswa kujidhabihu kwa njia yoyote ile ili tuitwe kwa jina la Yehova. Tunapodumisha uhusiano wetu wenye thamani na Yehova, tutajitahidi sana kufuata viwango vyake vya uadilifu na kuwafundisha wengine kufanya hivyo.—2 Kor. 3:18.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki